Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Fedha za Ofisi ya Waziri Mkuu na taasisi zilizo chini yake pamoja na Mfuko wa Bunge kwa mwaka 2017/2018.

Hon. Dr. Raphael Masunga Chegeni

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Busega

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Fedha za Ofisi ya Waziri Mkuu na taasisi zilizo chini yake pamoja na Mfuko wa Bunge kwa mwaka 2017/2018.

MHE. DKT. RAPHAEL M. CHEGENI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana nami napenda kuunga mkono hotuba ya Mheshimiwa Waziri Mkuu jinsi ambavyo ameweza kuiwasilisha nikiangalia inakidhi kwa kiwango kikubwa mahitaji ya Watanzania.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ni rahisi sana kukosoa lakini naomba niwarejeshe Watanzania na Waheshimiwa Wabunge wenzangu kwamba ukiangalia Serikali ya Awamu ya Tano, kwa muda mfupi imefanya mambo mengi na makubwa kwa Watanzania. Tukikumbuka kwamba Serikali
ya Awamu ya tano imeingia ikirithi madeni ya awamu iliyopita kitu ambacho ukikiangalia na hata katika maelezo ya mpango wa Waziri wa fedha, sasa hivi tunalipia karibu trilioni moja, deni la Taifa kwa kila mwezi. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa ukiangalia kwamba Mheshimiwa Rais pamoja na ubinadamu wake hebu tumpe sifa kwa kile anachokifanya kwa ajili ya Watanzania na tumuunge mkono kama Watanzania na kama Waheshimiwa Wabunge ndani ya Bunge hili. Nchi hii tunaiongoza sisi sote, sitegemei kwamba kwa vile uko upande mmoja wewe ni kusema mabaya siku zote. Hebu tuwajenge Watanzania wajue kwamba chombo hiki kinafanya kazi kama mhimili mmojawapo wa utawala hapa nchini. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, ningependa ku-register kidogo kwamba kwa kipindi ambacho tumeanza kipindi cha bajeti kuna dosari zimejitokeza lazima tuzikubali. Mhimili huu una heshima yake na heshima yake hii lazima ilindwe na Mhimili wenyewe. Vile vile kwa mujibu wa kanuni za Mabunge ya Jumuiya ya Madola, mimi kama Mwenyekiti wa CPA kwa tawi la Tanzania ningeomba sana Mheshimiwa Spika na kiti chake walinde maslahi ya Bunge hili na mustakabali wa Bunge hili kwa sababu haiwezekani tukawa kila siku tunatupa lawama kwa Serikali, tujiulize sisi Kama mhimili tumefanya nini? Haiwezekani kila siku tunasema Serikali, Serikali, Serikali. Bajeti ya Bunge inawezesha Bunge hili lifanye kazi zake kuisimamia Serikali. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kazi za Mbunge ni tatu; ya kwanza ni kutunga Sheria, ya pili ni kuwawakilisha watu waliomchagua kwenye chombo hiki na tatu ni kusimamia na kuishauri Serikali, haya ndiyo majukumu ya msingi ya Mbunge ndani ya Bunge hili. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kumejitokeza maneno yanazungumza hayatii afya kwa Bunge hili. Tunahitaji kauli za Serikali zitoke zikieleza bayana kama kuna tatizo liainishwe. Sitarajii kwamba yamezungumzwa hapa na Waheshimiwa Wabunge wa pande zote mbili lakini kuna Mawaziri wenye dhamana wamekaa kimya. Huku ni kutokuwajibika ndani ya chombo hiki lazima watoe kauli wawaondolee hofu Watanzania ili wajue kwamba Serikali yao wanachofanya ndicho hicho Watanzania wanachokitaka lakini tunapokaa kimya tunaleta a lot of speculations, watu wanakuwa hawaelewi sisi kama Wabunge tunafanya nini. Wananchi wanalalamika, Wabunge wanalalamika, Serikali inalalamika tunakwenda wapi? Kwa hiyo ningeomba sana hii sintofahamu hii, niiombe Serikali, Mheshimiwa Waziri Mkuu kama Kiongozi wa Shughuli za Serikali ndani ya Bunge ni vyema ukatusaidia kuondoa sintofahamu hii. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na hayo nikiangalia kwamba Serikali ya Awamu ya Tano imefanya mambo mazuri sana na lazima tujenge msingi wa uchumi ili tuweze kuendelea. Huku nyuma ukiangalia watu wanalalamika uchumi umebadilika, mdororo wa uchumi siyo kwa Tanzania peke yake, dunia nzima sasa iko kwenye mdororo wa kiuchumi. Tusipofikiria nje ya box nadhani sisi Watanzania ni kama kisiwa ndani ya dunia haiwezekani lakini yanayofanyika tuyapongeze na tuyape jitihada kubwa zaidi ya kuya-support, angalia miundombinu inayofanyika.
Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa hivi, ndani ya muda mfupi tumeona uanzishwaji wa ujenzi wa reli ya kati kwa standard gauge, historia, miradi ya maji inayoendelea ni historia. Upande wa elimu nawasikitikia ambao wanabeza kwamba eti hakuna elimu bure, jamani nawasikitikia sana,
labda hawajui wanachosema. Haijatokea katika historia ya nchi hii kwamba kila mwezi zaidi ya bilioni 18.7 zinatengwa kwa ajili ya elimu bure kwa mtoto wa Kitanzania. Haya tunapaswa kuyapongeza na Mheshimiwa Rais ukiangalia anachokifanya na naomba Watanzania tujue kwamba dhamira yake ni nyeupe, dhamira yake ni kwa ajili ya kuwatumikia Watanzania, tumpeni support hii tusimdiscourage.
Mheshimiwa Mwenyekiti, sijaona kiongozi, mimi ni mgeni ndani ya Bunge lakini ni mwenyeji kidogo. Kazi inayofanyika sasa hivi ni kazi nzuri sana lakini kuna vitu vya kushauriana. Mfano; katika suala zima la kiuchumi, kweli fedha ndani ya uchumi imepungua, ni suala la Waziri wa
Fedha. Hii ni issue ya Micro-economics, mambo ya Monetary Policy na mambo ya Fiscal Policy atusaidie namna gani ya kurudisha fedha katika mzunguko na leo nimesikia kwamba Benki Kuu wameamua kushusha riba ile ya kuwekeza unajua kuna Central Mineral Reserves ambayo ni asilimia 10 ya Mabenki kuwekeza na Benki Kuu wameshusha mpaka asilimia nane. Hii italeta msukumo wa fedha ndani ya mzunguko wa uchumi, nakushukuru Mheshimiwa Waziri wa Fedha kwa kuchukua Monetary Policy ya namna hii. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini tukumbuke kwamba jamani tunasafiri kwenye ngalawa moja. Sisi Wabunge bila kujali vyama vyetu nchi hii ni ya kwetu sote, uchumi huu ni wa kwetu wote tufanye kazi kwa pamoja.
Mheshimiwa Mwenyekiti, namalizia, naipongeza Serikali. Huko Busega mimi nasema kwamba nina mradi wa maji mkubwa umeshaanza kutekelezwa, sasa niseme nini zaidi ya hili jamani. Umeme wa REA keshokutwa tunaenda kuzindua, mafanikio makubwa ya Serikali ya Awamu ya Tano kwa nini niikosoe kwa kitu ambacho naona kuna faida kwa Watanzania? (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini kama haitoshi leo hii watoto wameongezeka katika kusajiliwa darasa la kwanza ni historia katika nchi hii. Hivi wewe unayelalamika kwamba Serikali haijafanya kitu unataka ikufanyie nini? Ikuletee Kitanda nyumbani kwako?
Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru sana.