Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Fedha za Ofisi ya Waziri Mkuu na taasisi zilizo chini yake pamoja na Mfuko wa Bunge kwa mwaka 2017/2018.

Hon. Amina Nassoro Makilagi

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Fedha za Ofisi ya Waziri Mkuu na taasisi zilizo chini yake pamoja na Mfuko wa Bunge kwa mwaka 2017/2018.

MHE. AMINA N. MAKILAGI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipa nafasi. Vilevile nimshukuru Mwenyezi Mungu muweza wa yote, aliyenipa fursa na mimi kuweza kusimama kutoa mchango wangu katika hoja yetu hii iliyo muhimu ya makadirio ya mapato na matumizi ya fedha Ofisi ya Waziri Mkuu na Ofisi ya Bunge kwa mwaka wa fedha 2017/2018. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nianze kuunga mkono hoja na sababu ninazo. Sababu ya kwanza ni kwamba, tangu Serikali imeingia madarakani imefanya kazi kubwa sana yenye kutukuka. Kama kura zingepigwa leo, ushindi wa CCM ungekuwa 99.999%. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, ni ukweli usiopingika kama tutamaliza miaka 10 na Rais huyu Mheshimiwa Dkt. John Pombe Magufuli, makofi tuliyompigia juzi Mheshimiwa Dkt. Jakaya Mrisho Kikwete, Wabunge tutasimama juu ya meza kwa kazi anazozifanya. Hongera sana Mheshimiwa Dkt. John Pombe Magufuli kwa kazi nzuri sana unayoifanya.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kwa mwaka mmoja Rais umethubutu kutununulia ndege. Ni Bunge hilihili na Wabunge hawahawa walikuwa wanasema na ndiyo maana mimi wakati mwingine huwa nashangaa watu wanakuwa na ndimi mbili; leo wanasema Tanzania haina ndege tunazidiwa na Rwanda, Rais ananunua ndege wanabeza. Waswahili wanasema akutukanaye hakuchagulii tusi na ukiwa kwenye maji unaoga akija mwendawazimu haumkimbizi. Mheshimiwa Rais chapa kazi, tuko pamoja, kazi ni nzuri sana. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, ni Rais huyuhuyu Mheshimiwa Dkt. John Magufuli amefanya uamuzi wa busara akasema elimu iwe bila malipo kwa watoto wetu. Ni ukweli usiopingika watoto walioandikishwa wamevuka kiwango cha miaka yote iliyopita. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, ni Rais huyuhuyu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Dkt. John Pombe Magufuli, amethubutu. Kwa miaka mingi tangu nchi yetu imeanza, dhamira ya kuhamia Dodoma ilikuwepo, lakini Mheshimiwa Dkt. John Pombe Magufuli ndiyo ameweza.
Hongera sana Rais wetu, chapa kazi, panga Mji wetu wa Dodoma, maendeleo yaendelee na Watanzania wanakuthamini, endelea baba na usiwe na wasiwasi. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, ni Rais wetu huyuhuyu aliyesikiliza kilio cha Wabunge cha muda mrefu kwamba, mapato mengi ya Tanzania yanapotea, akaziba mianya yote ya upotevu wa mapato. Si Rais mwingine ni Rais Mheshimiwa Dkt. John Pombe Magufuli. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, ni Rais huyuhuyu ambaye Wabunge na wengine nawaona wako humu ndani, tulipaza sauti tukasema Rais apunguze safari za kwenda nje ya nchi. Mheshimiwa Dkt. John Pombe Magufuli amepunguza, Wabunge hatuendi nje ya nchi, Rais haendi nje ya nchi,
watumishi tuko humu ndani, gharama za kuendesha Serikali zimepungua. Ni Wabunge ndio tulioshauri ndio maana mimi wakati mwingine nashangaa kuona watu wenye ndimi mbili. Hongera sana Mheshimiwa Dkt. John Pombe Magufuli kwa kazi nzuri sana unayofanya. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, ni Rais huyuhuyu ambaye tulimtaka aangalie mishahara hewa. Amedhibiti na leo tunashuhudia jinsi anavyokabiliana na mishahara hewa, wakiwemo watumishi hewa. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nikianza kueleza mafanikio ya Serikali hii ya Awamu ya Tano tutalala hapa. Kama tungeanza kuandika kitabu, Mheshimiwa Rais kwa mwaka huu mmoja ameshafanya mengi ambayo kwa kweli Watanzania na hasa wanawake ambao mimi nawawakilisha, zaidi ya milioni 50 wanawake walioko hapa wamenituma nije kusema wanamshukuru sana Rais, achape kazi na timu yake akiwemo Makamu wa Rais Mheshimiwa Mama Samia, kijana Mheshimiwa Waziri wetu Mkuu, Mheshimiwa Jenista na Baraza lote la Mawaziri na Watendaji wote wa Serikali msirudi nyuma, songeni mbele. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, ukweli unabaki palepale ndiyo maana watu sasa wamekosa hoja, tunaanza sasa kuzungumza watu, hatuna cha kusema. Ndiyo maana kila mtu anayesimama anazungumza mtu badala ya kuzungumza maendeleo ya wananchi kwa sababu Mheshimwa Dkt. John Magufuli amefuta na hakuna mtu mwenye swali kwa Serikali ya CCM. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, ninapoona Wabunge sasa wanaacha kujadili matatizo ya wananchi, binafsi nafurahia kwamba Serikali sasa inasonga mbele, kero zimeisha na ndiyo maana tunaanza kuzungumza mtu mmoja mmoja badala ya kuzungumzia matatizo ya wananchi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba niendelee na mchango wangu, nizungumze mambo machache ambayo nimejielekeza kuyachangia kama ifuatavyo.
Taarifa...
MHE. AMINA N. MAKILAGI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa taarifa nzuri, ndege zinahitaji television. Si jambo baya, ndege zijazo tutakazozinunua miaka ijayo tutaweka television ili Wabunge mfurahie matunda yenu. Mheshimiwa Mwenyekiti, zile nyingine zinazokuja tutaweka television mtembee raha mustarehe kwa sababu Mheshimiwa Dkt. John Magufuli amedhamiria. Ahsante sana kwa taarifa nzuri. Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Ndio maana mimi nasema watu wenye ndimi mbili. Ni Mheshimiwa Kikwete huyuhuyu walisema alikuwa hafanyi kitu, leo hapa mtu anasema haya yalifanywa na Mheshimiwa Kikwete. Ahsante sana kwa kutambua kwamba na Mheshimiwa Kikwete alitoa hayo mawazo ya elimu bure. Ahsante Mheshimiwa Waitara. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba sasa nijielekeze katika mambo matatu ambayo nimeyapanga kuyatilia mkazo. La kwanza, nimejipanga kuelezea uwezeshaji wa wananchi na la pili, masuala ya maji, sekta ya afya na kama muda utaniruhusu nitazungumzia kidogo elimu na kilimo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika ukurasa wa 15 - 17 Mheshimiwa Waziri Mkuu ameeleza kwa kina jinsi ambavyo Serikali ya CCM ina dhamira nzuri sana ya kuwawezesha wananchi. Hapa naomba nishauri katika maeneo machache ambayo nimeyaona.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nijielekeze katika kuwawezesha uchumi wanawake na vijana. Naomba nitoe ushauri kwa Serikali, nimejaribu kupekua kwenye hivi vitabu, sijaona ile milioni 50 katika kila kijiji. Ningependa kumwomba Waziri Mkuu, atakapokuja kusimama hapa mbele yetu hebu atuambie hii milioni 50 iko wapi? Maana Bunge lililopita tulipitisha zaidi ya bilioni 50 kwa ajili ya kupeleka kwenye vikundi vya wananchi vya kiuchumi. Napenda Mheshimiwa Waziri Mkuu atakapokuja hapa atuambie ziko wapi na zinatoka lini na utaratibu wa kutoa mikopo hii utakuwa ni nini na wanawake na vijana na wananchi kwa ujumla waweze kushiriki. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini pia nimepekua katika vitabu vyote ambavyo tumepewa, sijaona ule Mfuko wa Maendeleo ya Wanawake. Ni ukweli usiopingika kwamba wanawake ndiyo wazalishaji wa Taifa hili, ndiyo nguvu kazi, ndiyo wenye vikundi, ndiyo walezi wa familia, ndiyo
wajasiriamali, lakini kwa bahati mbaya sana ule mfuko ambao ulikuwa ndiyo ukombozi kwa wanawake siuoni katika vitabu hivi. Napenda kumwomba Waziri Mkuu atakapokuja atuambie hivi mpango ni nini katika suala zima la kuwakomboa wanawake? (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kama mfuko haujawekwa, hatujachelewa. Bajeti ya Wizara ya Maendeleo ya Jamii, Jinsia na Watoto itakuja. Turejee Mheshimiwa na Kamati ya Bajeti itusaidie fedha hizi ziingie kwa ajili ya wanawake. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo lingine ni 5% ya Vijana na Wanawake inayotokana na Halmashauri zetu. Kwa bahati njema mimi niko kwenye Kamati ya LAAC, nimejionea kwamba Halmashauri nyingi hazitengi fedha. Nimefanya utafiti nimegundua kwamba hawatengi fedha kwa sababu, hakuna sheria. Wanatekeleza Waraka wa Waziri Mkuu tena wakati ule alikuwa Mheshimiwa Sumaye, ni muda mrefu sana. Naishauri Serikali, hebu ilete sheria hapa Bungeni tutunge sheria itakayoweka masharti ya kutenga fedha hizi kwa ajili ya halmashauri ziende kuwakomboa wanawake na vijana kwa sababu wameanzisha vikundi vingi sana, hawana uwezo wa kufikia vyombo vya fedha na huu mfuko peke yake ndiyo ukombozi kwa wanawake. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nizungumzie masharti ya vyombo vya fedha. Kuna taasisi za FINCA, PRIDE na mabenki mengine wanatoa mikopo, tunawashukuru sana kwa kazi nzuri wanayofanya. Naiomba Serikali iweke riba elekezi kwa sababu baadhi ya taasisi zinatoza riba kuanzia 1% - 35%. Hawa wanawake na vijana wanashindwa kurudisha huo mkopo matokeo yake wananyang’anywa magodoro na vitu vyao vya ndani. Badala ya mkopo kumsaidia yeye unamsaidia yule aliyemkopesha fedha. Hebu Serikali chukueni ushauri wangu, wekeni riba elekezi ili wanawake na vijana waweze kunufaika. (Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa mzungumzaji)
MHE. AMINA N. MAKILAGI: Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja. Ahsante sana.