Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Fedha za Ofisi ya Waziri Mkuu na taasisi zilizo chini yake pamoja na Mfuko wa Bunge kwa mwaka 2017/2018.

Hon. Zuberi Mohamedi Kuchauka

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Liwale

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Fedha za Ofisi ya Waziri Mkuu na taasisi zilizo chini yake pamoja na Mfuko wa Bunge kwa mwaka 2017/2018.

MHE. ZUBERI M. KUCHAUKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kuanza mchango wangu kwa kuzungumza Sera ya wazee nchini. Sera ya Wazee nchini ilikuwepo tangu mwaka 2003, lakini hadi leo Sheria kwa ajili ya utekelezaji wa Sera hii bado haijaletwa hapa Bungeni ili kukidhi mahitaji ya Sera ya Kitaifa ya wazee kama ilivyopitishwa mwaka 2003. Kumekuwepo kwa ahadi ya muda mrefu ya ulipwaji wa pensheni kwa wazee wote hasa wakulima waliotumikia uchumi wa nchi hii kwa uaminifu mkubwa. Pia kukosekana kwa Sheria hiyo kumefanya ushiriki wa wazee hao kwenye vyombo vya maamuzi kuwa hakuna. Katika ngazi zote za vyombo vya maamuzi, ushiriki wa wazee ni kama hakuna hivyo kuathiri maslahi ya wazee hao. Mheshimiwa Mwenyekiti, kuendelea kwa mauaji ya vikongwe nchini ni matokeo ya madhara ya kutokuwa na
sheria inayowatambua wazee nchini na pia ukosefu wa uwakilishi kwenye vyombo vya maamuzi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nijielekeze kwa Wakala wa Uvunaji wa Mali za Misitu (TFS). Sheria na kanuni zinazotumiwa na Taasisi hii ni bora ikafanyiwa marekebisho kwani kwa kiasi kikubwa imekuwa si shirikishi kwa jamii inayoizunguka au jirani na misitu husika. Mfano ushuru au tozo zinazopatikana katika uvunaji huu. Halmashauri zetuupatiwe kiasi cha asilimia tano tu. Kiasi hiki ni kidogo sana ukilinganisha na uharibifu unaotokana na kazi hii. Vile vile ukizingatia ulinzi shirikishi inakuwa ni vigumu sana kwa jamii kuona faida ya misitu hiyo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ushiriki wa TFS katika shughuli za maendeleo kwenye vijiji vinavyopakana na misitu midogo sana kitendo kinachochea jamii kutokuona faida ya moja kwa moja ya uwepo wa misitu hiyo. Kamati za Vijiji za uvunaji wa mali za misitu hazina elimu ya kutosha juu ya uvunaji endelevu. Hivyo kufanya wajanja wachache kutumia mwanya huo kuharibu mali za misitu bila jamii husika kunufaika. Kama ilivyo kwa maliasili, vijiji au Halmashauri upatiwa 25% kwa wawindaji, basi na TFS ifikiriwe kutoa kiasi kama hicho cha 25% kwa Halmashauri. Ili Halmashauri iweze kunufaika na uvunaji huo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nijielekeze kwa wapiga kura wangu. Wilaya ya Liwale ni wilaya yenye kata 20 lakini wilaya hii hadi leo ina kituo cha Afya kimoja tu. Jambo linaloifanya Hospitali ya Wilaya kubeba mzingo mkubwa sana. Ukizingatia Hospitali yenyewe tangu ilipopandishwa hadhi toka kituo cha afya miundombinu yake haijaboreshwa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, janga kubwa linaloikumba wilaya hii ni mgao mdogo wa fedha za dawa na basket fund. Mfano Mkoa wa Lindi una wilaya tano, wilaya inayopata mgao mdogo ni Liwale ukilinganisha na wilaya zingine. Cha kusikitisha ni kwamba katika Mkoa wa Lindi hospitali za wilaya, Hospitali za Liwale ndio inayoongoza kwa kuhudumia wagonjwa wengi kwa mwezi, lakini ndio inayopata mgao mdogo wa fedha. Basketi fund, Liwale milioni 350, Ruangwa bilioni moja, Nachingwea milioni 800, Kilwa milioni 600, hii si haki. Mateso yanayowapata wana
Liwale ni matokeo ya sensa ya watu na makazi ya mwaka 2012, hivyo, nashauri Serikali ikafikiria vinginevyo badala ya kuacha watu wakiteseka kwa magonjwa na ukosefu wa madawa. Fedha ya dawa Liwale milioni nane, Ruangwa milioni 21, Kilwa milioni 17 na Nachingwea milioni 18.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Madeni ya Walimu; pamoja na juhudi kubwa inayofanywa na Serikali juu ya kumaliza tatizo hili, lakini kasi yake ni ndogo ukilinganisha na ukubwa wa tatizo. Walimu ni wengi sasa wanaodai nyongeza ya mishahara inayotokana na kupandishwa madaraja na
wengine wanaocheleweshwa kupandishwa madaraja ingawa wanakidhi vigezo. Jambo hili linawakatisha tamaa Walimu wengi na kufanya shule nyingi kuwa na matokeo mabaya. Hali za walimu wetu ni mbaya kwa ujumla wanaishi katika mazingira magumu sana. Uhaba wa ajira
tu ndio unaowabakisha huko na si kufurahia ajira yao, kwani walio wengi hawajui hatima yao.
Mheshimiwa Mwenyekiti, mwisho, naomba kuishauri Serikali kuchelewa au kutopeleka Ruzuku ya OC kwenye Halmashauri zetu ni kurudisha nyuma maendeleo ya nchi yetu kwani Halmashauri inashindwa kutekeleza miradi yake ya maendeleo ikiwa ni pamoja na kutenga fungu la vijana na akinamama. Pengine Halmashauri hutakiwa kutekeleza maagizo ya Kitaifa bila kupewa fungu la fedha za kazi husika ikiwa ni pamoja na michango mbalimbali. Jambo hili hurudisha nyuma mipango ya Halmashauri kwani hulazimika kutekeleza miradi ambayo haikuwa kwenye mpango kazi wa Halmashauri husika.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kuwakilisha.