Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Fedha za Ofisi ya Waziri Mkuu na taasisi zilizo chini yake pamoja na Mfuko wa Bunge kwa mwaka 2017/2018.

Hon. Willy Qulwi Qambalo

Sex

Male

Party

CHADEMA

Constituent

Karatu

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Fedha za Ofisi ya Waziri Mkuu na taasisi zilizo chini yake pamoja na Mfuko wa Bunge kwa mwaka 2017/2018.

MHE. QAMBALO W. QULWI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze kwa kumshukuru Waziri Mkuu kwa kufanya ziara ya kihistoria mwishoni mwa mwaka jana Wilayani Karatu. Ziara hiyo ilileta matumaini mapya ya maisha kwa wakulima wadogo wadogo wa Bonde la Ziwa Eyasi wanaotumia kilimo cha umwagiliaji kwa kutumia chemchem zilizoko Qangded.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Waziri Mkuu kwa kusikiliza malalamiko ya wananchi wa bonde hilo kupitia mabango waliyomwandikia na kwa kuzingatia misingi bora ya uhifadhi wa vyanzo vya maji, Waziri Mkuu aliagiza mashine zote zilizoko mtoni ziondolewe na mipaka ya chanzo ihifadhiwe kwa mita 500 kila upande.
Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na kauli hiyo ya kiongozi mkubwa ambayo pia imezingatia sheria; viongozi wa chini yake waliopaswa kusimamia maagizo hayo wameshindwa kuchukua hatua.
Mheshimiwa Mwenyekiti, hivi tunavyoongea baadhi ya mashine bado ziko mtoni kabisa. Upimaji wa mipaka ya chanzo ulifanyika hivi karibuni lakini bado mipaka hiyo haizingatiwi na watu wanalima ndani ya eneo lililopimwa. Uhifadhi wa vyanzo vya maji ndiyo njia pekee ya kuinusuru
nchi hii kugeuka kuwa jangwa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nimwombe Waziri Mkuu akamilishe kazi hii njema aliyoianza kule Karatu kwa kutoa tena tamko kwa uongozi wa chini yake wasimamie kauli yake ambayo ni kauli ya Serikali.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Watanzania walio wengi wanajishughulisha na kilimo ili kupata chakula na pia mazao ya biashara. Kilimo chetu kimekuwa tegemezi kwa mvua jambo ambalo limepunguza mapato na mavuno pindi tunapokuwa na mvua chache. Niishauri Serikali kuanzisha kilimo cha umwagiliaji kwa kujenga mabwawa makubwa ambayo yatakinga maji nyakati za mvua. Nchi kadhaa duniani na hata hapa Afrika wamefanikiwa kwa kuwekeza katika miradi ya aina hiyo.