Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Fedha za Ofisi ya Waziri Mkuu na taasisi zilizo chini yake pamoja na Mfuko wa Bunge kwa mwaka 2017/2018.

Hon. Elias John Kwandikwa

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Ushetu

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Fedha za Ofisi ya Waziri Mkuu na taasisi zilizo chini yake pamoja na Mfuko wa Bunge kwa mwaka 2017/2018.

MHE. ELIAS J. KWANDIKWA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze kwa kutoa shukrani kwa Hotuba nzuri ya Mheshimiwa Waziri Mkuu na naunga mkono hoja.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru sana Waziri Mkuu kwa umakini wake na upendo mkubwa alionao anapotekeleza majukumu yake na unapompelekea jambo lolote yuko tayari kulishughulikia mara moja.
Mheshimiwa Mwenyekiti, namwomba tena Waziri Mkuu atusaidie kutatua mgogoro unaofukuta juu ya umiliki halali wa majengo ya Halmashauri ya Ushetu yaliyoko Kahama Mjini ambayo bila kuzingatia Sheria, Kanuni na Taratibu, Serikali ya Mkoa imeagiza yamilikiwe na Halmashauri
ya Mji wa Kahama na kunyima fursa Halmashauri ya Wilaya ya Ushetu kupanua wigo wa mapato yake na kuongeza huduma bora kwa wananchi. Vilevile inaiweka katika hatari ngumu kisiasa eneo letu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu suala la maji ya mradi wa Ziwa Viktoria; naishauri Serikali kuangalia impact ya upelekaji wa maji yaani kufanya mapitio kiasi gani au idadi gani ya watu wanasambaziwa maji kuliko kuridhika na dhana pekee ya kuwa maji yamefika Makao Makuu ya Wilaya
hali maji hayajawafikia wananchi walio wengi. Mfano; maji ya Ziwa Viktoria yamefika katika Makao Makuu ya Wilaya na wananchi wengi hawajasambaziwa maji hayo ikiwemo eneo lote la Jimbo la Ushetu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba Serikali iangalie suala la kutusambazia maji eneo la Jimbo la Ushetu sehemu ambayo ina shida kubwa ya maji.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa upande wa kilimo naiomba Serikali iweke mkazo na kusimamia na kuleta tija katika uzalishaji:-
(i) Suala la pembejeo ipatikane ya kutosha, ipatikane mapema (ii) Benki ya Kilimo iwezeshwe mtaji wa kutosha na isimamiwe vizuri ili iweze kutekeleza majukumu yake hususani:-
(a) Kutoa mikopo kwa wakulima.
(b) Kufanya utafiti wa kifedha na kiuchumi.
(c) Kutoa elimu kwa wakulima.
(d) Kuwajengea uwezo vijana na kuwawezesha kwenye miradi ya kilimo.
(e) Kuratibu utoaji mikopo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye eneo la madini naomba Serikali iwasaidie wachimbaji wadogo wadogo wapate maeneo yao ya uchimbaji.
Mheshimiwa Mwenyekiti, mfano katika eneo la Mwabomba Jimbo la Ushetu kuna hali ya sintofahamu wachimbaji wadogowadogo waliopo watakwenda wapi kufuatia eneo hilo kupewa mwekezaji ambaye anasuasua kuanza shughuli zake wakati huo huo Mheshimiwa Rais wetu
Dkt. Magufuli aliwaahidi wananchi kuwa hawatahamishwa eneo hilo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nipate ahadi ya Serikali juu ya hatma ya wachimbaji wadogo wadogo katika eneo hilo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja.