Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Fedha za Ofisi ya Waziri Mkuu na taasisi zilizo chini yake pamoja na Mfuko wa Bunge kwa mwaka 2017/2018.

Hon. Dr. Mwigulu Lameck Nchemba Madelu

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Iramba Magharibi

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Fedha za Ofisi ya Waziri Mkuu na taasisi zilizo chini yake pamoja na Mfuko wa Bunge kwa mwaka 2017/2018.

WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipa fursa na mimi niongelee vitu vilivyojitokeza kwenye eneo linaloangukia Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kiwango kikubwa Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi inahusisha Ofisi ya Vitambulisho vya Taifa, Zima Moto, Uhamiaji, Polisi na Magereza. Hata hivyo, kwa kiwango kikubwa masuala yaliyojitokeza zaidi yanahusisha, Polisi, Magereza, Zimamoto na Uhamiaji.
Mheshimiwa Mwenyekiti, la kwanza, sitasema kwa kirefu kwa sababu tutakuwa na fursa katika Wizara yangu tutakapoongelea suala la bajeti yetu na utekelezaji wa bajeti katika kipindi kilichopita lakini kwa utangulizi tu kati ya yale yaliyojitokeza toka kwa Wabunge wengi, moja ya hoja ilikuwa ni malipo yanayotakiwa kwenda kwa Askari wa Magereza, Zima Moto pamoja na Uhamiaji ambao bado hawajapata package yao kama wanavyoita wenyewe wakijilinganisha na wenzao ambao tayari walishapata.
Mheshimiwa Mwenyekiti, niwahakikishie tu Waheshimiwa Wabunge pamoja na vijana wetu kwamba jambo hilo linafanyiwa kazi na watapata kama ambavyo wamepata wenzao na kama ambavyo ilikuwa ahadi ya Serikali. Ni kwamba tu kwa utaratibu wa Wizara yetu ya Fedha na kwa utaratibu wa hali halisi, wanapofanya malipo kuna vitu walivyoviweka kama first charge. Wanatoa kwanza mshahara wa watumishi, deni la Taifa na baada ya hapo kinachobaki wanaangalia namna wanavyoweza kugawa katika matumizi mengine haya ambayo tumeyasema. Kwa
maana hiyo, ndicho kilichosababisha wagawe kwa mafungu fedha hizo ambazo zilikuwa zinaenda kwenye vyombo vyetu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, niwahakikishie vijana wetu walioko kazini wala wasivunjike moyo na wala wasiwe na hofu. Wale ambao walishapata na wenyewe watapata na mwisho wa siku wote watakuwa wamepata.
Ni ahadi ya Serikali na ni jambo ambalo litatekelezwa na ni jambo ambalo ni endelevu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nimelisikia sana kwa Waheshimiwa Wabunge, Mheshimiwa Mchengerwa alilisema, ndugu yangu Mheshimiwa Ridhiwani alilisema, Mheshimiwa Matiko amelisema na wengine waliochangia. Ni jambo ambalo kama Serikali tunalifanyia kazi kwa ukaribu na
tunashirikiana na wenzetu na niwaombe vijana wetu in particular askari wetu watambue ni kautaratibu tu wala hatuna maana ya kuweka madaraja, lakini ni utaratibu tu wa utoaji wa fedha kufuatana na upatikanaji wa dirisha la kulipia fedha hizo zinazokwenda kwenye matumizi haya tuliyoyataja.
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini jambo lingine ambalo liliongelewa sana na Waheshimiwa Wabunge na lilijitokeza kwa kiwango kikubwa ni suala la treatment ya Wabunge wanapokuwa hapa Dodoma na wanapokuwa kwenye maeneo yao ya kazi. Waheshimiwa Wabunge, nimelielezea
na kama nilivyosema kwenye briefing, tuna mambo mawili lazima tukubaliane nayo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, la kwanza ni kwamba nchi yetu inaendeshwa kwa mujibu wa sheria. Kwa hiyo, yale yaliyo ya sheria ni lazima sheria iongoze na ndivyo tulivyokubaliana na sisi ndiyo tuliotunga sheria. Hata hivyo, kuna mistreatment inayotokana na mtu mmoja mmoja, tumeyatolea maelekezo ili haki ya Wabunge na ya wananchi wengine iendelee kuzingatiwa. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, Mwalimu Nyerere aliwahi kusema kwamba kwa umaskini wetu tulionao tungetamani tuwape watu vitu vingi sana lakini hatuwezi tukawapa kila kitu wananchi wetu. Hata hivyo, kitu kimoja pekee ambacho tunaweza tukawapa wananchi wetu ni haki yao ya msingi, haki ambayo wanastahili na hicho ndicho ambacho na sisi tunakisemea.
Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa ukirejea kwa Waheshimiwa Wabunge, nimetolea maelekezo na linapotokea suala la aina hiyo Mheshimiwa Mbunge uko maeneo fulani, uko kazini au hata kwenye mikutano, kwa wale walio wapya ni vizuri tukatambulika na tukajitambulisha
na ni vizuri tukatoa hizo taarifa kwamba kutakuwepo na shughuli A, B, C, D kama ni ya mikutano na tukaendelea.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna watu wengine wameendelea kuelezea kuhusu mikutano. Tulishasema, Waheshimiwa Wabunge wanaruhusiwa kufanya mikutano yao kwenye majimbo yao. Nilirejee moja ambalo limeelezewa sana kuhusu Wabunge wa Viti Maalum. Wabunge wa Viti
Maalum majimbo yao ni kwenye mikoa yao na wenyewe watoe taarifa ili kuondoa usumbufu huo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini jambo lingine lililojitokeza ambalo na lenyewe nimeona nilitolee taarifa hapa leo, Waheshimiwa Wabunge na hasa katika kipindi hiki ambacho tuko Bungeni, Mheshimiwa Spika alishalisemea alipokuwa akitoa mwongozo kuhusu namna ya ukamatwaji
au kufanyiwa mahojiano kwa Waheshimiwa Wabunge, mimi nasisitiza kile kile alichosema Mheshimiwa Spika. Ni mamlaka yake, ameelekeza kama Mheshimiwa Mbunge atatakiwa kwa mahojiano, taarifa itatolewa kwa Mheshimiwa Spika. Hilo lilishasemwa na hivyo ndivyo itakavyokuwa. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini kwa upande wangu kwenye ile inayoangukia kwenye mamlaka yangu, naelekeza, kama suala ni mahojiano angalau kwa kipindi hiki ambacho Wabunge wako Bungeni hapa na wanafanya kazi ya kitaifa, waliyotumwa na wananchi waliowachagua, basi wale watakaokuwa wanataka mahojiano waje wawahojie Wabunge hawa hapa hapa Dodoma. Wachukue hayo maelezo hapa hapa Dodoma na wao warejee katika ofisi zao na yale maelezo waliyowahojia hapa. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna sababu kubwa tatu. Moja, kazi wanayofanya Waheshimiwa Wabunge hapa Dodoma ni ya kitaifa lakini pili unapunguza risk ya kumsafirisha Mbunge umbali mrefu huku unaenda tu kule kuchukua maelezo na tayari ulishafika pale pale na yeye
alikuwepo pale pale ungeweza kumhoji kile unachotaka kumhoji na ukaondoka na hayo maelezo. Kama ni vitu vingine ambavyo viko nje ya mhimili wangu kama ni vya kimahakama kwa maana kwamba viko nje ya Wizara yangu, basi hilo litaelekezwa na mamlaka husika kama ni la eneo ambapo anatakiwa akafanyie sio hapa Dodoma.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa mahojiano, yule anayetaka kumhoji Mbunge aje na kumbukumbu zote, aje yule yule ambaye anataka kumhoji. Bahati nzuri Idara yetu imekamilika kila mkoa, kwa hiyo, hata kwa kutuma tu kwamba mhoji kwenye hili na hili inawezekana. Pia yule ambaye ana maelezo aliyetaka kuhoji na yeye anaweza akaja akamhoji Mbunge hapa hapa na hilo likaisha.
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini usalama wa raia kwa ujumla wake, naendelea kurudia kusema kwamba, hatutaruhusu na hatutakubali uhalifu uendelee katika nchi yetu. Tunaendelea kupambana kama Serikali, kipaumbele kikubwa ni usalama wa raia wetu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, tunapooongelea usalama wa raia wetu tunaongelea maisha ya watu wetu. Waheshimiwa Wabunge wengine mlikuwa mnauliza Waziri wa Mambo ya Ndani mbona husemi? Niwaambie kitu kimoja, hii sio Wizara ambayo kila kitu ni habari. Siyo kila habari kwenye Wizara hii ni habari. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la msingi kwa Waziri wa Mambo ya Ndani siwezi kusema kabla vyombo vyangu havijanipa cha kusema na ni utaratibu wa utendaji kazi katika vyombo hivi. Waziri ukiwa mstari wa mbele kutenda kazi kwenye Wizara ambazo ni za vyombo lazima utoe fursa; moja, ya vyombo kufanya kazi; lakini mbili watu kutendewa haki ili vyombo vifanye kazi kwa mujibu wa sheria, siyo kwa mujibu wa macho ya Waziri yanavyoona kwa sababu taasisi hii inatakiwa ifanye kazi kwa mujibu wa sheria na kwa maslahi ya Taifa na siyo kwa maslahi ya Waziri au vitu binafsi vya Waziri. Ndiyo maana tunatoa fursa ya vyombo vyetu kufanya kazi na Wizara, ndiyo maana tunatoa fursa hii ya kuweka ushirikiano.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kama nilivyosema mengine tutaendelea kuyapata kwenye Wizara yetu na kwa kuwa hotuba hii ni kubwa basi tutapokea maelekezo kutoka kwa viongozi wetu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja kwa asilimia mia moja.