Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Fedha za Ofisi ya Waziri Mkuu na taasisi zilizo chini yake pamoja na Mfuko wa Bunge kwa mwaka 2017/2018.

Hon. Anthony Peter Mavunde

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Dodoma mjini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Fedha za Ofisi ya Waziri Mkuu na taasisi zilizo chini yake pamoja na Mfuko wa Bunge kwa mwaka 2017/2018.

NAIBU WAZIRI, OFISI YA WAZIRI MKUU, KAZI, VIJANA NA AJIRA: Mheshimiwa Spika, awali ya yote naomba nianze kwa kumshukuru Mwenyezi Mungu wa rehema kwa kutujalia Waheshimiwa Wabunge wote uzima na afya njema. Pia nichukue fursa hii kusimama mbele ya Bunge lako Tukufu ili kuchangia hoja ya bajeti ya Ofisi ya Waziri Mkuu, iliyowasilishwa na Mheshimiwa Waziri Mkuu.
Mheshimiwa Spika, nikiwa Naibu Waziri Ofisi ya Waziri Mkuu, ninayeshughulikia masuala ya Kazi, Vijana Ajira na Watu Wenye Ulemavu, naomba nitumie fursa hii kumshukuru sana Mheshimiwa Waziri Mkuu, Mheshimiwa Kassim Majaliwa Majaliwa, Mbunge na Mheshimiwa Jenista Joakim Mhagama kwa ushirikiano mkubwa na miongozo wanayonipa inayoniwezesha kutekeleza majukumu yangu kwa ufasaha.
Mheshimiwa Spika, kwa dhati kabisa naomba kutumia fursa hii kuwashukuru sana wananchi wa Jimbo la Dodoma Mjini kwa kuendelea kuniunga mkono na kushirikiana na mimi katika utekelezaji wa majukumu haya ya kila siku.
Mheshimiwa Spika, kwa heshima na taadhima naomba sasa uniruhusu nichangie hoja hii kwa kutoa ufafanuzi wa hoja mbalimbali ambazo Waheshimiwa Wabunge walichangia na kutaka ufafanuzi. Nitatoa ufafanuzi wa baadhi ya hoja na hoja nyingine zitajibiwa na Mheshimiwa Waziri wa Nchi na Mheshimiwa Waziri Mkuu.
Mheshimiwa Spika, hoja ambayo ilijotekeza ya kwanza kabisa ilikuwa ni masuala ya Usalama na Afya Pahala Pa Kazi (OSHA). Waheshimiwa Wabunge walitamani kusikia kwamba tunaendelea kusimamia afya na usalama wa wafanyakazi pahala pa kazi na hasa wafanyakazi ambao
wanafanya kazi katika maeneo ya migodini na viwandani, na hatua za kisheria zichukuliwe kwa wale wote ambao hawazingatii masuala ya afya na usalama wa wafanyakazi wao.
Mheshimiwa Spika, Serikali inapokea ushauri wa Kamati wa kuendelea kusimamia afya na usalama pahala pa kazi hususan migodini na Serikali itaendelea kutoa elimu na kuchukua hatua kwa waajiri wote ambao hawatazingatia masuala ya afya na usalama kwa wafanyakazi wao kwa mujibu wa sheria.
Mheshimiwa Spika, kila mtu anafahamu na ni dhahiri kwamba falsafa ya Serikali ya Awamu ya Tano ni ya uchumi wa viwanda ambayo itakwenda kuwaajiri Watanzania wengi sana wengi wao wakiwa ni vijana, kwa hiyo, sheria hii sasa itakuwa ni sehemu ya kuweza kui-protect nguvukazi ya nchi kutokana na haya ambayo yanaweza kutokea katika migodi na viwandani.
Mheshimiwa Spika, aidha katika kipindi cha mwaka 2016/2017 Wakala wa Afya na Usalama Pahala Pa Kazi (OSHA) umewachukulia hatua waajiri 701 waliokiuka matakwa ya Sheria ya Afya, Usalama Pahala Pa Kazi ikiwemo wamiliki wa migodi mikubwa iliyopo nchini.
Mheshimiwa Spika, hoja nyingine ambayo ilizungumzwa ni Serikali itoe elimu bora kwa watu wenye ulemavu ili wajiondoe katika hali ya utegemezi. Suala la kushughulikia changamoto za watu wenye ulemavu, ikiwemo kuwawezesha kujiondoa katika utegemezi ni moja kati ya vipaumbele ambavyo vimeainishwa kwenye Ilani ya uchaguzi wa Chama cha Mapinduzi ya mwaka 2015, Ibara ya 166; hivyo, Serikali itaendelea kutoa elimu bora kwa watoto wote nchini, wakiwemo watoto wenye ulemavu kwa kutoa vifaa saidizi kwa wanafunzi wenye ulemavu na vifaa vya kufundishia na kujifunzia. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, hivi sasa Serikali inasambaza vifaa hivyo kwa awamu tatu. Awamu ya kwanza ni kwa wanafunzi wasioona na viziwi, awamu ya pili vifaa vitasambazwa kwa watoto wenye ulemavu wa akili na wenye usonji na hatimaye kwa wenye ulemavu wa viungo. Hadi sasa vifaa vilivyosambazwa katika awamu ya kwanza katika shule za msingi na sekondari ni kama ifuatavyo; mashine za nukta nundu (brail machine) 932, shime sikio (hearing aids) 1,110, karatasi za kuandikia maandishi ya nukta nundu - rimu 2,548, karatasi za kudurufu maandishi ya nukta nundu - rimu 1,000, universal brail kits yenye vifaa mchanganyiko 1,495.
Mheshimiwa Spika, katika hoja zilizojitokeza pia hapa, Wabunge walizungumza kuhusu Mfuko wa Watu wenye Ulemavu kwamba haukutengewa fedha katika bajeti ya mwaka 2016/2017 hivyo Serikali ijitahidi kutenga fedha kwa ajili ya mfuko huu ambao utawezesha Baraza la Watu wenye Ulemavu kutekeleza majukumu yake ya kisheria.
Mheshimiwa Spika, katika mwaka 2017/2018 Serikali imetenga kiasi cha shilingi milioni 50 ambazo zitatumika kuandaa mfumo na uratibu wa uendeshaji wa mfuko wa watu wenye ulemavu. Aidha, watu wenye ulemavu wanaendelea kupata huduma mbalimbali, hususan
kuwawezesha kiuchumi kupitia mifuko, ikiwa ni pamoja na Mfuko wa Maendeleo ya Vijana na Mfuko wa Maendeleo ya Wanawake ngazi ya Halmashauri pamoja na programu ya kukuza stadi za kazi.
Mheshimiwa Spika, katika eneo hili pamoja na kuwa na programu nyingi sana za uwezeshaji katika kundi hili, lakini pia kila programu ya Wizara hasa katika ukuzaji ujuzi tumekuwa tukitenga asilimia kadhaa kwa ajili ya watu wenye ulemavu. Mfano wa programu mojawapo ni Programu ya
Youth Economic Empowerment ambayo iliwahusisha takribani vijana 9,100 katika mikoa mitano ya Mtwara, Lindi, Morogoro, Dar es Salaam na Pwani ambapo walijitokeza watu wengi wenye ulemavu na walipata fursa kushiriki katika mafunzo haya na walikuwa ni kati ya watu ambao walifanya vizuri sana. Kwa hiyo, kama Serikali imekuwa ni sehemu ya msisitizo pia, kuona namna ya kutoa fursa katika kundi hili.
Mheshimiwa Spika, pia nichukue fursa hii kumshukuru sana Mwenyekiti wa SHIVYAWATA, Dada Ummy Nderiananga, ambaye amekuwa akifanya kazi kubwa sana pamoja na Serikali katika kuhakikisha kwamba tunaongeza uelewa katika kundi hili la watu wenye ulemavu ili wengi zaidi wajitokeze kushiriki katika programu mbalimbali ambazo ziko chini ya Wizara.
Mheshimiwa Spika, ilijitokeza pia, hoja ya kwamba watoto wenye ulemavu wa macho kutokuwa na uwezo wa kurejea nyumbani nyakati za likizo kutokana na kutokuwa na wasindikizaji. Niliarifu tu Bunge lako kwamba Serikali tumeliona hili na tunalichukua na tutalifanyia kazi.
Mheshimiwa Spika, hoja nyingine iliyojitokeza ni kuitaka Serikali iwasilishe takwimu za hukumu zilizotolewa kwenye kesi zinazowahusu waliohukumiwa kwa makosa ya jinai, kuhusiana na mauaji ya watu wenye ulemavu wa ngozi.
Napenda kuliarifu Bunge lako Tukufu kwamba, takribani kesi 28 za ukatili wa jinai kwa watu wenye ulemavu zimetolewa hukumu na kesi 37 ziko Mahakamani. Nichukue fursa hii kuwashukuru sana mhimili wa Mahakama kwa kuendelea kutoa msisitizo mkubwa wa usikilizaji na umalizaji kesi hizi kwa wakati.
Mheshimiwa Spika, ilikuja pia hoja nyingine ya Wabunge walichangia uanzishwaji wa kambi za kilimo kwa ajili ya vijana ili iwasaidie vijana kuweza kujiajiri. Serikali kupitia Programu za Kukuza Ujuzi na Stadi za Kazi inalenga kuwawezesha vijana kujiajiri katika sekta za uzalishaji mali,
ikiwemo kilimo. Aidha, wadau mbalimbali wakiwemo FAO, Techno Serve, World Vision Tanzania, Heifer International, Swiss Contact, Planning International na ILO, wameendelea kutekeleza programu mbalimbali kuwawezesha vijana kujiajiri katika sekta ya kilimo pamoja na mnyororo wake wa thamani. Serikali pia kupitia Vituo vya Vijana vya Ilonga na Sasanda inaendesha programu za kilimo katika mfumo wa mashamba darasa ambapo vijana wanaojishughulisha na kilimo kutoka maeneo mbalimbali wanafika na kupata mafunzo hayo.
Mheshimiwa Spika, mafunzo yanayotolewa ni pamoja na kitalu nyumba kwa mazao ya mbogamboga, mazao ya biashara kama vile kahawa, mazao ya chakula, ufugaji wa ng’ombe, samaki na nyuki. Aidha, Serikali imezindua mkakati wa kuwawezesha vijana kujiajiri kwenye sekta ya kilimo pamoja na mnyororo wa thamani.
Mheshimiwa Spika, mkakati huu tunaufanya pamoja na Wizara ya Kilimo ambapo tuna mkakati wa Kitaifa wa kuwaingiza vijana kwenye kilimo, moja kati ya maeneo ambayo tunaanza nayo ni katika eneo la Morogoro - Mkulazi, ambapo kitajengwa kiwanda cha sukari chini ya mifuko ya
PPF na NSSf. Katika eneo lile zimetengwa takribani ekari elfu 63. moja kati ya eneo ambalo tulilichukua kubwa tutapatengeneza blocks za mashamba kwa ajili ya vikundi vya vijana na tunategemea kutoa ajira kupitia mashamba haya, ajira takribani 100,000.
Mheshimiwa Spika, vilevile siyo kwa wananchi wa Morogoro tu mashamba haya yanaweza pia yakatawanywa pembezoni mwa Morogoro, hasa katika Mkoa ambao miwa ile ikilimwa inaweza kufika kiwandani ndani ya saa 24. Kwa hiyo, vijana wote waliopo nje ya Morogoro lakini wenye uwezo wa kufanya shughuli ya kilimo, wana uwezo wa kulima mua huu na soko lake liko assured kwamba viwanda hivi vitachukua miwa hii. Kwa hiyo, naendelea kutoa wito kwa vijana wote nchi nzima kuona fursa hii na kujitokeza.
Mheshimiwa Spika, ilijitokeza pia hoja ya pongezi, Wabunge walipongeza kwa programu mbalimbali ikiwemo ya ukuzaji ujuzi, hasa kupitia viwanda vya Tooku Garments cha Dar es Salaam na Mazava Fabrics Morogoro. Vilevile walishauri kwamba programu hizi zipanuliwe na ziweze
kuwafikia vijana wengi zaidi. Pongezi zimepokelewa na Serikali itaendelea kupanua wigo wa utekelezaji wa programu ya kukuza ujuzi na stadi za kazi ili kuwafikia vijana wengi zaidi nchini. Katika mwaka wa fedha 2017/2018 vijana zaidi ya 17,350 watanufaika na mafunzo ya ujuzi na stadi za kazi yatakayotolewa sehemu mbalimbali nchini, ukilinganisha na vijana zaidi ya 9,120 ambao watanufaika mwaka 2016/2017.
Aidha, mafunzo ya utengenezaji wa bidhaa za ngozi yatakayotolewa na Taasisi ya Ufundi Dar es Salaam (DIT) Mjini Mwanza mwishoni mwa mwaka huu wa fedha yatawanufaisha pia vijana kutoka Shinyanga walioomba kujiunga na mafunzo hayo.
Mheshimiwa Spika, hoja nyingine ambayo ilijitokeza ni ya mkakati wa uwezeshaji wa vijana na akinamama kiuchumi uendane sambamba na kuwapatia elimu ya kitaalamu katika nyanja za ujasiriamali. Serikali kwa kushirikiana na wadau inaendesha programu mbalimbali za mafunzo ya ujasiriamali kwa vijana. Programu hizo zinaendelea kuongeza ujuzi kwenye maeneo mbalimbali. Mfano wa programu hizo ni pamoja na ufundi wa stadi za kazi kwa vijana wa Vyuo Vikuu, JKT, wafanyabiashara na waendesha bodaboda. Serikali imeanzisha utaratibu maalum wa majukwaa ya wanawake kwenye Mikoa na Halmashauri zote nchini. Katika majukwaa hayo wanawake wanapata fursa ya kupata elimu ya ujasiriamali, taarifa za mitaji na masuala mengine ya kuboresha shughuli zao za kiuchumi. Serikali pia inaendelea kuzisimamia kwa karibu Halmashauri zote nchini kulenga na kutoa fursa za mikopo kwa wanawake na vijana kwa asilimia tano kama ilivyoelekezwa.
Mheshimiwa Spika, ilizungumzwa pia hoja ya mikataba kwa wafanyakazi. Wabunge waliishauri Serikali kuendelea kusimamia sheria ili wafanyakazi wengi zaidi waweze kupata mikataba.
Mheshimiwa Spika, katika eneo hili ninataka nikiri kwamba, Ofisi ya Waziri Mkuu imeendelea kufanya kaguzi mbalimbali kuhakikisha kwamba Sheria ya Ajira na Mahusiano Kazini Namba 6 ya mwaka 2004, inafuatwa kwa waajiri wote kutoa mikataba, kama ambavyo kifungu Namba 14
kinavyosema. Kwa hiyo, tutaendelea kufanya kaguzi mbalimbali ili basi kuweza kuwabaini wale waajiri wote ambao wanakiuka Sheria hii na tunaendelea kuchukua hatua kuhakikisha kwamba wafanyakazi wa nchi hii wanapata mikataba yao na wafanye kazi wakiwa na mikataba.
Mheshimiwa Spika, kwa kumalizia katika hoja ambazo zimesemwa, baadhi ya wachangiaji walikuwa wanahoji mipango ya Serikali kama kweli ina nia thabiti ya kuwasaidia vijana wa nchi hii. Nataka niwaondoe hofu Waheshimiwa Wabunge ya kwamba hata ukiangalia trend, katika kipindi hiki cha muda wa mwaka mmoja kazi nyingi sana za vijana zimefanyika, mafunzo mengi sana yamefanyika na kwa kweli, ukiangalia kazi ambazo zimefanyika zimewagusa vijana moja kwa moja na imewasaidia sana kuwafanya vijana hawa waondokane na utegemezi. Sasa tunawatengenezea utaratibu ili vijana wengi zaidi waweze kujiajiri kupitia katika programu zetu mbalimbali.
Mheshimiwa Spika, chini ya Ofisi ya Waziri Mkuu katika kushughulikia masuala ya vijana jambo la kwanza kabisa ambalo tunalifanya ni kuwatambua kwanza vijana, tunafanya identification ya vijana kwa makundi yao. Tuna vijana wa aina tofauti, tuna graduates, lakini tuna vijana
ambao hawakupata fursa ya kupata elimu ya juu. Vilevile hatua ya pili tunayoifanya ni ya kuwarasimisha (formalization), hapa tunawaweka vijana katika vikundi kupitia SACCOS na kampuni vilevile.
Mheshimiwa Spika, ninao huu mfano wa vijana ambao wanafanya vizuri sana, ambao ni vijana kutoka Chuo Kikuu cha Sokoine ambao wao walihitimu pale chuoni na baadaye wakatengenezewa utaratibu na wakapewa mikopo. Vijana hawa wanaitwa SUGECO ambao wanafanya
shughuli za kilimo na hivi sasa ni kati ya vijana ambao wanafanya vizuri sana na wameanza kuwasaidia vijana wenzao nchini kwa kuwasaidia mitaji, vilevile na kuwapa mafunzo mbalimbali hasa katika maeneo ya kilimo. (Makofi)
Waheshimiwa Wabunge walikuwa wanahoji namna ya uwezeshaji wa vijana. Katika Ofisi ya Waziri Mkuu tunayo mifuko mingi sana, lakini mifuko hii pia tunaratibu pamoja na Wizara zingine. Lakini huu mfuko mkubwa ambao tunautumia ni Mfuko wa Maendeleo ya Vijana ambao mpaka ninavyozungumza hivi sasa tayari umeshakopesha takribani vikundi 297 kiasi cha shilingi bilioni 1.5 na vijana wamenufaika na tumeanza kuona matokeo na mabadiliko miongoni mwa vijana. Siyo hivyo tu, tuna Mfuko wa Uwezeshaji Wananchi Kiuchumi, Mfuko wa Rais wa Kujitegemea, vilevile tunao Mfuko wa Nishati ya Umeme Vijijini. Katika hili pia tunao mfuko wa kutoka BOT (SME) unaitwa Small and Medium Enterprises Credit Guarantee Scheme, hii yote inafanya kazi za kusaidia kuwawezesha vijana.
Mheshimiwa Spika, ilikuja hoja hapa ya kwamba kama Serikali tumejiandaaje? Inavyoonekana katika takwimu vijana wanaokwenda katika soko la ajira kila mwaka ni takribani vijana 800,000 mpaka 1,600,000, lakini nafasi za ajira zinazotengenezwa ni chache sana. Serikali tuliona jambo la kwanza la kufanya ili kumfanya kijana wa Kitanzania ajitegemee cha kwanza kabisa ilikuwa ni kuanza kuwabadilisha mtizamo, kuwabadilisha mtizamo vijana ilianza katika kuwapa elimu na kufafanua kwamba ajira maana yake ni nini. Kwa sababu mtazamo uliopo hivi sasa ni kwamba ili mtu aonekane ana ajira ni lazima awe tu ana ofisi yake, anavaa shati jeupe, ana tai, ana kiti cha kuzunguka, hiyo ndiyo ajira. Kwa mujibu wa Sera ya Ajira ya Taifa, inasema ajira ni shughuli yoyote halali ambayo inampatia mtu kipato. Kwa hiyo, tumeanza kuwaondoa vijana kimtazamo kuamini kwamba siyo wote lazima waajiriwe, kuna shughuli za kilimo, kuna shughuli za ufugaji, shughuli za ujasiriamali.
Ninavyozungumza hivi sasa tumetenga takribani ekari 85,000 nchi nzima kwa ajili ya shughuli hizi za vijana.
Mheshimiwa Spika, baada ya kuyasema hayo nashukuru sana. Naunga mkono hoja.