Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Fedha za Ofisi ya Waziri Mkuu na taasisi zilizo chini yake pamoja na Mfuko wa Bunge kwa mwaka 2017/2018.

Hon. Jenista Joackim Mhagama

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Peramiho

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Fedha za Ofisi ya Waziri Mkuu na taasisi zilizo chini yake pamoja na Mfuko wa Bunge kwa mwaka 2017/2018.

WAZIRI WA NCHI, OFISI YA WAZIRI MKUU, SERA, BUNGE, KAZI, VIJANA, AJIRA NA WENYE ULEMAVU: Mheshimiwa Spika, awali ya yote na mimi naomba nianze kwa kumshukuru sana Mwenyezi Mungu, mwingi wa rehema kwa kuweza kutufikisha tena siku hii ya leo tukiwa wazima na salama. Ninakushukuru sana wewe kwa kunipa nafasi ya kusimama mbele ya Bunge lako Tukufu ili niweze kujibu hoja za Waheshimiwa Wabunge kuhusu utendaji kazi wa Ofisi ya Mheshimiwa Waziri Mkuu.
Mheshimiwa Spika, nianze kwa kumpongeza sana Mheshimiwa Dkt. John Pombe Magufuli, Rais wetu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, amekuwa ni kiongozi mahiri, imara na shujaa katika kusimamia maendeleo ya nchi yetu. Naomba nichukue nafasi hii pia nimpongeze Makamu
wa Rais kwa kazi nzuri anayoifanya na vilevile kwa nafasi ya pekee kabisa, nimpongeze sana Mheshimiwa Kassim Majaliwa Majaliwa, Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, kwangu binafsi naomba nimshukuru sana Mheshimiwa Waziri Mkuu kwa jinsi anavyoniongoza, kwa jinsi anavyonisaidia kumsaidia kazi katika Ofisi yake. Mheshimiwa Waziri Mkuu naomba nikushukuru sana. Naomba niwahakikishie Waheshimiwa Wabunge, Mheshimiwa Waziri Mkuu ni mchapakazi, Mheshimiwa Waziri Mkuu ni jembe hasa linalotosha. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, pamoja na kuwapongeza Viongozi Wakuu hao niliowataja, nichukue nafasi ya pekee nimpongeze sana Mheshimiwa Antony Peter Mavunde, Naibu Waziri katika Ofisi ya Waziri Mkuu. Mheshimiwa Antony Mavunde amekuwa ni msaada mkubwa sana katika kazi zangu, naomba nimshukuru sana. Kwa nafasi ya pekee nichukue nafasi hii kumpongeza Mheshimiwa Antony Mavunde kwa sababu leo amepata baby girl, first born wake, Mungu ampe maisha marefu. (Makofi/Kicheko)
Mheshimiwa Spika, naomba nichukue nafasi hii kumkumbuka pia Balozi Dkt. Abdallah Possi ambaye alifanya kazi nzuri ya kunisaidia. Nichukue nafasi hii nimshukuru sana Mwanasheria Mkuu wa Serikali, amekuwa ni mshirika wangu mkubwa katika kuhakikisha shughuli za Bunge na shughuli za Serikali zinakwenda vizuri. Siwezi kuendelea na majibu ya hoja za Waheshimiwa Wabunge bila kutambua mchango
mkubwa wa Shirikisho la Vyama vya Wafanyakazi Tanzania linaloongozwa na Rais wao Ndugu Tumaini Nyamhokya na Katibu Mkuu, Dkt. Yahaya Msigwa, pamoja na Shirikisho la Waajiri Tanzania linaloongozwa na Mbunge mwenzetu Mheshimiwa Almasi Maige na Mtendaji Mkuu Ndugu Aggrey Mlimuka, wamekuwa wakitupa ushirikiano mkubwa. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, mwisho lakini sio kwa umuhimu nawashukuru sana wapiga kura wa Jimbo la Peramiho, Hapa Kazi Tu, tutaendelea na mwaka 2020 ni mambo vilevile, Hapa Kazi Tu, ushindi kwa Chama cha Mapinduzi. (Makofi/Kicheko)
Mheshimiwa Spika, kabla ya kujibu hoja hizi za Kamati nichukue nafasi hii kuwashukuru sana Mwenyekiti wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Katiba na Sheria, Ndugu yangu Mheshimiwa Mohamed Mchengerwa na Makamu wake, ndugu yetu Mheshimiwa Najma Giga, lakini na Wajumbe wa Kamati hiyo kwa ushurikiano mkubwa. Niwashukuru pia, Wajumbe wa Kamati ya UKIMWI inayoongozwa na Mheshimiwa Dkt. Faustine Ndugulile na Makamu wake Mheshimiwa Dkt. Tiisekwa na Wajumbe wote. Nichukue nafasi ya pekee kumshukuru sana dada yangu Mheshimiwa Hawa Ghasia, Mwenyekiti wa Kamati ya Bajeti na Ndugu yangu Mheshimiwa Josephat Kandege na Wajumbe wote kwa
ushirikiano mkubwa waliotupa.
Mheshimiwa Spika, kwa namna ya pekee niwashukuru sana Shirikisho la Vyama vya Wenye Ulemavu Tanzania, vikingozwa na dada Ummy. Naomba nitambue mchango wa pekee wa Wabunge wawili ndani ya Bunge hili wenye ulemavu, dada yangu Mheshimiwa Stella Ikupa Alex na dada yangu Mheshimiwa Amina Mollel, wanafanya kazi nzuri sana na tunashirikiana nao vizuri sana. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, nikushukuru wewe binafsi, Naibu Spika, Wenyeviti wa Bunge, Katibu wa Bunge na wafanyakazi wote wa Bunge kwa jinsi wanavyotusaidia ndani ya Serikali kutekeleza majukumu yetu hapa Bungeni sawasawa. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, kwa mujibu wa Kanuni ya 99(2) naomba sasa kwa heshima kubwa nitoe majumuisho ya hoja mbalimbali zilizotolewa na Waheshimiwa Wabunge. Ninaomba kwanza hotuba yangu hii iingie yote kwenye Hansard, vilevile tutaleta kitabu cha majibu ya maswali ya
Waheshimiwa Wabunge wote kwa sababu muda ni mfupi hatutaweza kuyajibu yote. Kabla ya kujibu hoja naomba niwahakikishie Waheshimiwa Wabunge, Mheshimiwa Nsanzugwanko alisema sana hapa, tuendelee kama waratibu wa Serikali kuangalia kuleta maendeleo kwa kuzingatia uwiano wa mikoa yetu na jinsi maendeleo yalivyo ndani ya mikoa yetu. Kwa hiyo, ndani ya Serikali tutaangalia kwa sababu, lengo letu ni kuhakikisha Watanzania nchi nzima wanaendelea bila kujali ukabila wala ukanda wala nini, lakini ni lazima wote wapate maendeleo.
Mheshimiwa Spika, nitaanza na hoja ya Makao Makuu Dodoma. Kulikuwa na hoja nyingi zinazohusu Serikali kuhamia hapa Dodoma. Hii ilikuwa ni ndoto ya Marehemu Baba wa Taifa, lazima niwakumbushe Waheshimiwa Wabunge. Tarehe 30 Agosti, 1973 mpaka tarehe 9 Septemba, 1973 Halmashauri Kuu ya chama cha TANU ambacho ni baba ni Chama cha Mapinduzi, iliketi Dar es Salaam na kuridhia kwamba Makao Makuu ya nchi yatakuwa Dodoma na mwaka1973 Chama cha TANU kiliamua na kupitisha maazimio hayo.
Mheshimiwa Spika, kwa uhamiaji tunaohamia nao kwenye Serikali ya Awamu ya Tano, wote tunakumbuka kwamba, tarehe 23 Julai, 2016 Mheshimiwa Rais wetu Dkt. John Pombe Magufuli alipokuwa anahutubia kwa mara ya kwanza kwenye Mkutano wa CCM kama Mwenyekiti wa Chama cha Mapinduzi, aliwatangazia Watanzania kupitia Mkutano Mkuu wa Chama cha Mapinduzi, Serikali ya Awamu ya Tano itahamia Dodoma. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, hivyo basi, Serikali hii imeshakwishakuhamia hapa Dodoma na tumehamia hapa watendaji wakuu wote, Mheshimiwa Waziri Mkuu akituongoza, Mawaziri, Naibu Mawaziri wote, Makatibu Wakuu wote, Naibu Makatibu Wakuu wote na baadhi ya Watumishi ambao tumehamia nao hapa Dodoma. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, wengi walifikiri hili ni suala la kisiasa na kuna watu wamechangia wanasema Serikali haina dhamira ya dhati. Naomba niwakumbushe huu ni utekelezaji wa Ibara ya 151 ya Ilani ya Uchaguzi ya Chama cha Mapinduzi ya mwaka 2015.
Mheshimiwa Spika, faida za kuhamia Dodoma, Wabunge wamechangia kuuliza ni zipi? Pamoja na kutusaidia kwamba Makao Makuu kuwa katikati ya nchi yetu, lakini tunaona kabisa kwamba Serikali itapunguza gharama kubwa sana za matumizi ya uendeshaji wa Serikali na hasa
inapokuwa vipindi vya Bunge, kuhamisha Serikali kutoka Dar es Salaam kuja kushughulika na shughuli za Bunge. Vilevile tutaenda kuchachua uchumi wa nchi kwa kuhakikisha kwamba tunatoa nafasi ya maeneo mengine kuendelea.
Mheshimiwa Spika, kulikuwa na hoja ya kuleta Bungeni Sheria ya Makao Makuu, naomba niwathibitishie Waheshimiwa Wabunge kwamba mchakato wa maandalizi ya sheria hiyo uko tayari na mara tu tutakapokuwa tumefikia hatua ya mwisho tutaomba ridhaa yako na wewe
umetuagiza sana na umetuambia hapa hakieleweki mpaka sheria mwaka huu iingie Bungeni. Tupo tayari tutawasiliana na Ofisi yako na tutaleta sheria hii humu ndani. Mpaka sasa tunaendelea kuhamia Dodoma kwa kutumia GN Na. 230 ya mwaka 1973 na hiyo nayo ni tamko la kisheria la Serikali.
Mheshimiwa Spika, tulipokea hoja nyingine ya kuhakikisha kwamba Mifuko ya Hifadhi ya Jamii kuwekeza katika ujenzi wa viwanda kama ni tija na inaweza ikawa na faida gani. Kwanza niseme kabisa kwamba uwekezaji katika sera hii ya viwanda unatokana pia na mpango wetu wa
maendeleo wa miaka mitano. Hivyo basi, Mifuko yetu ya Hifadhi ya Jamii imeamua kuwekeza kwenye miradi ya viwanda 25 yenye thamani ya dola za kimarekani milioni 153 mpaka sasa. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, tulichokifanya kama Serikali ni kuhakikisha kwamba uwekezaji huo unakuwa na tija na tija ya kwanza utakwenda kuzalisha ajira za watoto wa Kitanzania 310,000 kwenye viwanda hivyo 25. Kwa hiyo, ni jambo la kupongeza sana. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, vipo baadhi ya viwanda vimeshaanza kufanyakazi tutatoa orodha kwa Wabunge muda ni mfupi tungeweza kuvisoma hapa, Mheshimiwa Naibu Waziri ameweza kutaja baadhi ya viwanda hivyo. Tumesema pia viwanda hivyo vitasaidia pia kutengeneza soko la mazao yetu na kuongeza thamani ya mazao ya wakulima katika nchi yetu ya Tanzania. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, kulikuwa pia na hoja kuhusu mradi wa MIVARF, huu ni mradi wa miundombinu ya masoko na uongezaji wa thamani na huduma za fedha vijijini. Mradi huu Waheshimiwa Wabunge pamoja na Kamati walitaka kujua maendeleo ya ujenzi wa ukarabati wa barabara na ukarabati wa masoko Pemba na Unguja. Mradi huu ulianza kufanyiwa kazi mwaka 2014 na ulikamilika katika maeneo kadhaa na hasa kwenye eneo la barabara mwaka 2015 kule Pemba na Unguja. Kwa sasa tunaendelea na mradi wa kukamilisha maeneo ya masoko. Jumla ya kilometa za barabara 148.5 zimejengwa na masoko manne makubwa yameweza kujengwa kule Unguja na Pemba.
Mheshimiwa Spika, ninachotaka kusema mradi huu unazo faida nyingi na umekuwa ni mradi shirikishi, mradi huu umekuwa ni kichocheo kikubwa cha muonekano wa mashirikiano yetu ya Muungano kati ya Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Serikali ya Mapinduzi Zanzibar. Ninaomba tu niseme kwamba pamoja na mafunzo yanayotolewa kwa wananchi, jamii kushirikishwa kuweza kubadilisha mfumo mzima wa uzalishaji mazao na masoko yao, nawapongeza Wajumbe wa Kamati ya Katiba na Sheria na hasa Mheshimiwa Ally Saleh. Mheshimiwa Ally Saleh alikiri kabisa kwamba mradi huu ni kiashirio kizuri cha Muungano kati ya Tanzania Bara na Visiwani.
Mheshimiwa Spika, ninaomba niwaambie Waheshimiwa Wabunge tuunge mkono na mawazo ya Mheshimiwa Ally Saleh, lakini tujue kabisa kwamba Muungano wetu una faida kubwa na ni lazima tuendelee kuuunga mkono. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, kulikuwa na hoja iliyohusu Mfuko wa Fidia kwa Wafanyakazi. Mfuko huu umeanzishwa kwa Sheria Namba 20 ya mwaka 2008. Mfuko huu umeweka mfumo mzuri ambao ni wa kidijitali wa kuhakikisha kwamba taarifa zote zinazotokana na watu ama wafanyakazi
wanaopata ajali kazini zinapatikana kwa haraka na malipo kwa watu hao wanaopata ajali kazini yanafanyika kwa haraka. Sheria hii iliyoanzisha huu mfuko imeweza kuwakomboa wafanyakazi wengi sana katika nchi yetu ya Tanzania na tunategemea itafanya kazi nzuri ya kutoa fidia
kwa magonjwa, vifo na ajali zinazotokea maeneo ya kazi.
Mheshimiwa Spika, Wabunge walitaka kujua kazi zilizofanywa mpaka sasa. Mpaka sasa tumeshafundisha madaktari kama 359 nchini ambao wamepewa uwezo wa kubaini magonjwa na namna ya kutathmini athari na ulemavu unaotokana na ajali kazini. Kwa hiyo, naomba
niwahakikishie Waheshimiwa Wabunge kuwa kazi za mfuko huu kwa kuwa sasa zimeshaanza basi malalamiko ya wafanyakazi katika sekta ambazo zimeainishwa kwenye mfuko na Sheria ya Mfuko hatutakuwa tena matatizo ya kutoa fidia kwa wafanyakazi wote nchini. Niwaombe sana Waheshimiwa Wabunge mtusaidie kuwaeleza taasisi mbalimbali ambazo zinawaajiri katika maeneo yenu ili watambue sasa tuna mfuko huu wa fidia kwa wafanyakazi ambao umeshaanza kutoa fidia kwa wafanyakazi na wajisajili waajiri wote.
Mheshimiwa Spika, kulikuwa na hoja pia mfuko wa fidia kwa wafanyazi uzingatie sera na miongozo ya uwekezaji. Naomba nilihakikishie Bunge lako kwamba agizo hilo linasimamiwa vizuri na Serikali, vilevile linasimamiwa vizuri na SSRA ambaye ni mdhibiti wa sekta ya hifadhi ya jamii pamoja na Benki Kuu ambao ndio wamepewa kazi ya kusimamia uendeshaji na uwekezaji unaofanywa na mifuko ya hifadhi ya jamii katika nchi yetu ya Tanzania.
Mheshimiwa Spika, kulikuwa na hoja pia mfuko huu wa fidia kwa wafanyakazi uchukue jitihada za kutosha katika kupambana na kudhibiti mianya yote ya rushwa. Naomba kulihakikishia Bunge lako Tukufu kwamba mfuko unazingatia maagizo ya Serikali na umeweza kuweka miongozo ambayo inaongozwa na sheria iliyoanzishwa ya mapambano dhidi ya rushwa katika nchi yetu ya Tanzania hivyo, mfuko
unaendelea kutekeleza agizo hilo vizuri.
Mheshimiwa Spika, hoja nyingine ilikuwa ni kuboresha kiwanda cha Mpigachapa Mkuu wa Serikali na Waheshimiwa Wabunge na Kamati walituagiza tuhakikishe kwamba tunaboresha mazingira ya Mpigachapa Mkuu wa Serikali. Naomba niliarifu Bunge lako Tukufu kwamba kazi hiyo tuliianza kwenye bajeti ya mwaka 2016/2017 na tulitenga fedha za Kitanzania milioni 150 za kuanza mchakato wa zoezi hilo. Fedha hizo zimetumika mpaka sasa kumuweka Mshauri Elekezi ambayo ni Taasisi ya Viwanda na Ujenzi ya Chuo Kikuu cha Dar es Salaam na wao wameshaanza utafiti wa awali wa kuweza kuboresha Ofisi ya Mpigachapa Mkuu wa Serikali na Kiwanda chetu cha Uchapaji cha Serikali. Tayari taarifa ya awali tumeshaipokea na mwishoni mwa mwezi Aprili tutapokea taarifa kamili ya jinsi tunavyoweza kufanya kazi hiyo vizuri.
Mheshimiwa Spika, Serikali imeshafanya mazungumzo na Benki ya Rasilimali (TIB) kuona ni namna gani wanaweza kutusaidia fedha sasa za kuweza kujenga kiwanda kipya kizuri, kikubwa hapa Dodoma ili kuweza kusaidia shughuli hizo za Mpigachapa Mkuu wa Serikali. Tayari tumeshapata kiwanja na tumeshakilipia na umiliki wa kiwanja hicho umeshahamia kwenye Serikali tayari kwa kuanza kazi hiyo mapema iwezekanavyo.
Mheshimiwa Spika, kulikuwa na suala Sheria ya Maafa, tuliagizwa Serikali kupitia Sheria ya Maafa nchini, naomba niwaambie na niliarifu Bunge lako tukufu kwamba tayari Bunge lilishatunga Sheria ya Usimamizi wa Maafa Namba 7 ya mwaka 2015. Aidha, Kanuni za utekelezaji wa sheria hii zimeshakamilishwa na zinangoja tu muda ufike ili ziweze kutangazwa kwenye Gazeti la Serikali na ziweze kutumika inavyotikiwa.
Mheshimiwa Spika, kulikuwa na hoja ya kutoka Kambi ya Upinzani kwamba kumekuwa na ukimya kuhusu matumizi ya fedha zilizokusanywa wakati wa tetemeko la ardhi na pendekezo la kumwagiza CAG kufanya ukaguzi maalum wa matumizi ya fedha hizo. Ofisi ya Waziri Mkuu ilishaunda kikosi kazi maalum ili kufanya ukaguzi kufuatia maelekezo ya Mheshimiwa Rais Dkt. John Pombe Magufuli aliyoyatoa alipofanya ziara Mkoani Kagera tarehe 2 Januari, 2017. Jambo hili lilishaagizwa na Rais na tulishaanza kulitekeleza, kwa hiyo nadhani tutaendelea na maagizo yale Mheshimiwa Rais aliyokwishakuyatoa na tutaendelea kuyatekeleza. Hata hivyo, zipo kazi nzuri ambazo zimeshafanywa katika kurudisha miundombinu na hasa ya taasisi za Serikali kule Kagera.
Mfano mzuri ni ujenzi wa shule ya Ihungo, pia tumeboresha kwa kiasi kikubwa zahanati ya Ishozi na imeboreshwa vizuri sana. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, tumeboresha sana makazi ya wazee ya Kilima na vilevile tumeshatoa fedha za Kitanzania zisizopungua bilioni mbili kwa ajili ya kuanza ujenzi wa shule ya sekondari ya Nyakato. Kwa hiyo, nimuombe sana na kumshawishi tu Kiongozi wa Kambi Rasmi ya Upinzani Bungeni aliyetoa hoja hii atembelee shule hizo na maeneo hayo ataona kazi nzuri iliyokwisha kufanyika mpaka sasa.
Mheshimiwa Spika, kulikuwa na hoja ya Serikali kudhibiti Wabunge wa Upinzani wawapo Bungeni. Naomba niseme kwamba Serikali haina uwezo wa kufanya udhibiti wowote wa Wabunge wa Upinzani wawapo Bungeni ama hata Wabunge wa Kambi ya Chama Tawala. Majukumu ya Bunge yametajwa katika Ibara ya 84 ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ya mwaka 1977. Uendeshwaji wa shughuli za Bunge unaongozwa na Kanuni za Bunge na pale maamuzi yanapokuwa hayamridhishi Mbunge yeyote, Kanuni za Bunge zinamruhusu Mbunge huyo kuchukua hatua zaidi kwa mujibu wa Kanuni. Kwa hiyo, ninaomba nilithibitishie Bunge lako kuwa Serikali haina mkono wowote wa kumkandamiza Mbunge yeyote.
Mheshimiwa Spika, kulikuwa na hoja Serikali kutimiza ahadi ya milioni 50 nadhani Mheshimiwa Waziri wa Fedha ameijibu vizuri sana leo hapa ndani asubuhi. Ofisi ya Waziri Mkuu tunaendelea na maandalizi ya pensheni kwa wazee, tumeshakamilisha documents zote na taratibu sasa za kuwasilisha maandiko yetu katika vikao vya maamuzi Serikalini yanaendelea ili hatimaye tuweze kutekeleza Ilani ya Uchaguzi Ibara ya 165(e) kuhusu pensheni kwa wazee.
Mheshimiwa Spika, kulikuwa na hoja ya kutuuliza tumefikia wapi kuunganisha mifuko ya pensheni. Tumeshafika hatua nzuri, tathmini imefanyika, andiko la mapendekezo ya kuunganisha mifuko limeshaboreshwa na tunasubiri maamuzi ya Serikali. Tutaendelea kutoa fedha kwenye Mfuko wa UKIMWI lakini vilevile tutaendelea kutoa fedha za kutosha ili Mamlaka ya Kupambana Dawa za Kulevya nchini iweze
kufanya kazi zake vizuri. Niwaombe Waheshimiwa Wabunge mapambano dhidi ya UKIMWI na dawa za kulevya ni ya kwetu wote pamoja na ninaomba tushirikiane kwa pamoja kama Watanzania ili kupiga vita dawa za kulevya na UKIMWI.
Mheshimiwa Spika, pia tulipewa ushauri kuhusu kuboresha mfumo wa ufuatiliaji wa utekelezaji wa ahadi za Serikali za viongozi na Ilani ya Uchaguzi. Tumepokea ushauri huo na mfumo huu siku moja tutakuja kuwaonesha watatuunga mkono na watatusaidia ili kazi hii ifanyike sawa
sawa.
Mheshimiwa Spika, kulikuwa pia na hoja ya kuhakikisha kwamba Serikali inashughulikia tatizo la fao la kujitoa. Naomba tu niwambie Waheshimiwa Wabunge katika mafao ambayo yanaorodheshwa kama ni mafao yatolewayo kwenye sekta ya hifadhi ya jamii fao la kujitoa
halipo. Ibara ya 11 ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania inatueleza na inatupa mwongozo wa jinsi ya kuwakinga Watanzania na hasa siku za uzee na majanga yoyote yanayoweza kuwapata. Hata hivyo, kulingana na mabadiliko ya uchumi na Sera ya Hifadhi ya Jamii ibara ya 3(8) inatupa mwongozo wa kushughulikia namna nzuri ya kuona ni namna gani tunaweza kuwakinga Watanzania wanaokosa kazi ili waweze kumudu maisha yao. Naomba niwahakikishie Waheshimiwa Wabunge tumeanza mazungumzo na Shirikisho la Vyama vya
Wafanyakazi nchini na hivyo basi tunataka tumalize mzizi wa fitna wa fao la kujitoa ili wafanyakazi waweze kufanya kazi zao wakiwa na amani na suala la fao la kujitoa isijekuwa ni ajenda tena ya kuwasumbua katika shughuli na mifumo yao mbalimbali ya ajira. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, nimalize kwa kusema kwamba kwa sababu muda wangu umepita, ninaiunga mkono sana hoja hii na ninaomba Waheshimiwa Wabunge tuiunge mkono hoja hii ya Mheshimiwa Waziri Mkuu, kwa sababu mafanikio haya yote ambayo yamekuwa yakionekana dhahiri ni mafanikio ambayo yamekuwa yakiratibiwa na Mheshimiwa Waziri Mkuu wetu na ndugu yetu Kassim Majaliwa.
Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, ninaomba niwahakikishie Wabunge tutaendelea kuheshimu michango na ushauri wao na Serikali tupo tayari kufanya kazi kwa weledi mkubwa na uaminifu mkubwa kuhakikisha nchi yetu inasonga mbele kwa maendeleo, Hapa Kazi Tu, hatutalala na hivyo basi tunaamini baada ya miaka mitano tutakuwa tumepiga hatua ya kutosha. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, naona kengele karibu inagonga, naomba niunge mkono hoja hii, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi.