Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Fedha za Ofisi ya Waziri Mkuu na taasisi zilizo chini yake pamoja na Mfuko wa Bunge kwa mwaka 2017/2018.

Hon. Kassim Majaliwa Majaliwa

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Ruangwa

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Fedha za Ofisi ya Waziri Mkuu na taasisi zilizo chini yake pamoja na Mfuko wa Bunge kwa mwaka 2017/2018.

WAZIRI MKUU: Mheshimiwa Spika, naomba nianze kwa kumshukuru Mwenyezi Mungu mwenye rehema ambaye leo ameweza kutupa afya na kupata nafasi ya kuja kuhitimisha majadiliano ya bajeti yetu ya Ofisi ya Waziri Mkuu, taasisi zake na Mfuko wa Bunge kwa mwaka wa fedha 2017/2018.
Mheshimiwa Spika, naomba niwakumbushe Watanzania kwamba leo ni siku ya kumbukumbu ya hayati Edward Moringe Sokoine aliyekuwa Waziri Mkuu wa Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Awamu ya Kwanza alizaliwa tarehe 1 Agosti, 1938 na kufariki tarehe 12 April, 1984 takribani miaka 23. Naamini Watanzania wote tutaendelea kuungana pamoja kumuombea Kiongozi wetu aliyetutangulia mbele za haki ili Mungu aweze kuiweka roho yake mahali pema, amina.
Mheshimiwa Spika, niendelee kutoa shukrani zangu za dhati kwa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Katiba ya Sheria, Kamati ya Kudumu ya Bunge UKIMWI na Kamati ya Kudumu ya Bajeti kwa michango yao mizuri kwenye hoja ambayo niliwasilisha mbele yako.
Mheshimiwa Spika, kipekee nakushukuru sana wewe mwenyewe, Naibu Spika na Wenyeviti wote wa Bunge kwa kusimamia kwa umahiri mkubwa majadiliano ya hotuba ya Ofisi ya Waziri Mkuu, taasisi zake na Mfuko wa Bunge kwa pamoja. Pia ninawashukuru Waheshimiwa Wabunge wenzangu kwa pongezi zenu kwa Serikali na kwa michango yenye dhamira yenye kuboresha mipango na kazi zilizokusudiwa kutekelezwa na Serikali kwa mwaka wa fedha 2017/2018.
Mheshimiwa Spika, mjadala huu umedhihirisha namna ambavyo Bunge linaendelea kuimarika na kutekeleza wajibu wake wa kikatiba kuishauri na kuisimamia Serikali kikamilifu.
Nawashukuru tena Makatibu Wakuu wangu, Wakurugenzi, Makamishna, watumishi na watendaji wote ndani ya Ofisi ya Waziri Mkuu kwa kazi kubwa waliyoifanya kipindi chote cha bajeti hii katika kuratibu mambo yote muhimu.
Mheshimiwa Spika, mjadala huu leo ulichangiwa na Waheshimiwa Wabunge 148, ambapo Waheshimiwa Wabunge 99 walichangia kwa kuzungumza moja kwa moja hapa Bungeni na Waheshimiwa Wabunge 49 wamechangia kwa njia ya maandishi. Nawashukuru sana Waheshimiwa Wabunge wote waliochangia hoja yangu, hata hivyo kutokana na muda naomba mridhie nisiwataje kwa majina lakini majina ninayo na ninaomba yote yaingie kwenye Hansard ili iweze kuwa kumbukumbu muhimu siku za baadae.
Mheshimiwa Spika na Waheshimiwa Wabunge wenzangu, leo hii niko mbele yenu hapa sasa kuja kuomba ridhaa yenu mtupitishie bajeti yetu tufanye kazi za pamoja kwenye maeneo yenu ya kuboresha maendeleo na kusimamia maendeleo na watendaji wetu walioko kule ili tuweze
kupata matarajio ambayo tumeyakusudia. Serikali imejibu hoja hizo kupitia Mawaziri pia Mwanasheria Mkuu namshukuru sana, Naibu Mawaziri na hoja zilizosalia zitajibiwa kwa maandishi.
Aidha, kama ambavyo mnajua kwamba Ofisi ya Waziri Mkuu ndiyo ofisi ambayo inafanya shughuli zote za Serikali kwa hiyo, mambo mengi ambayo mmekuwa mkichangia Waheshimiwa Wabunge yalikuwa yanagusa sana kwenye Wizara za kisekta na kwa hiyo, zipo hoja ambazo sitazijibu hapa lakini zitakuja kuzungumzwa kwa kina na Wizara husika ili muweze pia kupata mwelekeo wa utekelezaji wa jambo ambalo mmeshauri.
Mheshimiwa Spika, niendelee kusema tu kwamba utendaji wa jumla wa Serikali ni mzuri, kabla ya kuanza hoja za Waheshimiwa Wabunge, naomba uniruhusu nibainishe baadhi ya mafanikio ya Serikali ya Awamu ya Tano chini ya uongozi thabiti wa Mheshimiwa Dkt. John Pombe Magufuli, Rais wetu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Nianze kwa kumpongeza sana yeye Mheshimiwa Rais, Makamu wa
Rais Mama Samia Suluhu Hassan na Mheshimiwa Rais wa Zanzibar Dkt. Ali Mohamed Shein kwa namna wanavyoendelea kuiongoza nchi yetu kwa uzalendo uliotukuka na kwa dhamira njema isiyotiliwa shaka.
Mheshimiwa Spika, nina hakika Watanzania wote ni mashuhuda wa kazi nzuri inayofanywa na Mheshimiwa Rais pamoja na timu yake katika kuongoza nchi yetu kwa weledi mkubwa na kwa mipango iliyo imara ili kuboresha maisha ya Watanzania. Katika kipindi cha mwaka mmoja ambacho nimeingia madarakani tumeushuhudia uongozi wake kuanza kwa miradi mikubwa na yenye tija kwa nchi yetu. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, nianze kueleza moja kati ya hiyo kati ya mambo ambayo yalikuwa yamechangiwa ni elimu bure isiyokuwa na malipo. Chini ya Serikali ya Awamu ya Tano ambapo watoto wote wa Tanzania wanapata elimu ya msingi na sekondari bila malipo, kila mwezi Serikali inapeleka shilingi bilioni 18.77 kwenye shule zote za Serikali nchini. Aidha, chini ya Serikali hii kiasi cha shilingi bilioni 3.3 zinatolewa kila
mwezi kwa walimu wakuu, wakuu wa shule kama motisha ya Viongozi hao na kufanya jumla ya shilingi bilioni 22.7 kila mwezi ambazo tunazipeleka ikiwa ni utekelezaji wa eneo hili. Tunajua zipo changamoto ambazo zimejitokeza pamoja na idadi kubwa ya vijana walioandikishwa na kusababisha upungufu wa madawati.
Nataka nitumie nafasi hii kuwashukuru sana Wabunge wenzangu, mlijitokeza sana baada ya Serikali kutoa wito wa kuchangia madawati kwenye shule zetu, mmetumia fedha zenu, mmetumia muda wenu, mmeshauri Halmashauri zenu kuweza kuchangia na leo hii tunaweza kusema tatizo la madawati limepungua sana kwenye shule zetu za sekondari na msingi. Nawashukuru sana Waheshimiwa Wabunge, tuende pamoja kwa ajili ya maendeleo yetu.
Mheshimiwa Spika, pia sekta ya afya imeboreshwa sana sasa hivi baada ya mwaka mmoja huu. Bajeti yetu pia ime-reflect hilo, kwamba bajeti ya mwaka 2015/2016 zilitengwa shilingi bilioni 31 lakini leo hii tuna shilingi bilioni 251 ambazo zinapelekwa kwenye Halmashauri zetu na kufikia
leo hii kila Halmashauri imeshapokea zaidi ya asilimia 75 ya fedha hii ya bajeti kwa ajili ya kutoa huduma za afya kwenye maeneo yetu, lakini tumeona pia ujenzi wa maduka ya madawa, mpaka sasa tumejenga maduka nane tunajenga maduka mengine katika kila mkoa ili kuweza kutoa huduma kwa karibu. Tumenunua magari ya ambulance 67 ambayo tunayapeleka kwenye vituo vya afya na tumeanza na Kanda
ya Ziwa ili kuanza kutoa huduma na kadri tunavyokuwa tunanunua tutajihakikishia kwamba tunapeleka kila Halmashauri kwenye vituo vya afya ili huduma iendelee.
Mheshimiwa Spika, tumeendelea kutoa huduma za mama na mtoto, tunajenga katika kila Halmashauri, tunaanza na Halmashauri 140 kwa kujenga wodi ya watoto, maabara ya damu, nyumba moja ya mganga na chumba cha upasuaji. Hiyo ndiyo kazi ambayo inaendelea kwa sasa
kwenye maeneo yetu. Pia jana Mheshimiwa Rais kama ambavyo mmepata kwenye vyombo vya habari ameshagawa vifaa vifuatavyo katika kila Halmashauri nchini.
Ametoa vitanda 25 kwenye kila Halmashauri, vitanda vitano kati ya hivyo ni vile ambavyo vinatumika katika kujifungulia, magodoro 25, mashuka 50 na vifaa tiba seti tano kila Halmashauri, huu ni mkakati wa kuboresha sekta ya afya.
Tutaendelea vizuri, nataka tuwahakikishie sekta ya afya pamoja na changamoto zake tutafikia hatua nzuri. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, sekta ya uzalishaji, ujenzi wa reli ya kati, Serikali imeendelea na jitihada za kuimarisha reli ya kati kwa lengo la kurahisisha usafiri wa usafirishaji wa mizigo na abiria ndani ya nchi na sasa kupitia fedha tuliyotenga, trilioni moja, tumeanza utekelezaji.
Mheshimiwa Spika, leo hii, tarehe 12 Aprili Mheshimiwa Rais ameweka jiwe la msingi saa tatu zilizopita tayari kwa ujenzi wa reli kwa kiwango cha standard gauge. Hii ni sehemu ya mkakati wa kuchochea maendeleo kwenye nchi yetu.
Mheshimiwa Spika, pia kwenye ujenzi wa viwanda; leo hii tumeshasajili viwanda 2,169 nchini, viwanda hivi katika sekta mbalimbali na tunaamini kupitia michango yenu kwamba tuimarishe kilimo ili viwanda vifanye kazi ni wazo ambalo tumelichukua, tutalifanyia kazi ili viwanda vyetu viweze kufanya kazi. Bado tumefungua milango viwanda vije na tunaendelea kufanya hivyo. Mkoa wa Pwani kwa sasa unaongoza kuwa na viwanda vingi sana, tuna viwanda vikubwa 83 na vidogo zaidi ya 200. Tunatoa wito Halmashauri na mikoa zitenge maeneo kwa ajili ya viwanda, mikakati ambayo mmetushauri Waheshimiwa Wabunge tutaizingatia ili viwanda vyetu hivi tuweze kuvifanyia kazi.
Mheshimiwa Spika, tumeboresha sana sekta ya usafiri wa anga kama ambavyo tulieleza kwenye taarifa yangu ya awali nilipokuwa nawasilisha taarifa yangu kwamba tumenunua ndege mbili na nne zinakuja, lengo letu ni kuhakikisha kwamba tunaboresha usafiri wa njia ya ndege,
pia tunakamilisha Terminal III uwanja wa ndege ikiwa ni mpango wa uimarishaji wa viwanja vya ndege. Tunaendelea kukamilisha Uwanja wa Mwanza, ukarabati wa Uwanja wa Ndege wa Kimataifa Kilimanjaro (KIA), Uwanja wa Songwe - Mbeya, vilevile Serikali inaendelea na ujenzi wa viwanja vya ndege pale Geita, Tabora, Kigoma, Sumbawanga, tutajenga pia Lindi na Shinyanga.
Serikali imeanza maandalizi kwa ajili ya ukarabati wa ujenzi wa viwanja vya ndege vya Musoma, Mtwara, Lindi na Songea. Kazi hii itaendelea kwenye viwanja ili ndege zile tulizonunua ziweze kusafiri kwenye maeneo yote ambayo tumeyataja ndani ya nchi lakini lengo letu hasa ni kuimarisha utalii wa wageni wa kutoka nje na watalii wa ndani ambao ni sisi wenyewe.
Mheshimiwa Spika, tumeimarisha pia barabara na Serikali inaendelea na kukarabati na kuboresha barabara ili kuunganisha nchi nzima. Kwa sasa tunakamilisha barabara za ngazi ya mikoa na maeneo yote sasa tunajenga barabara za ngazi ya mikoa na ninyi wote ni mashahidi, kule upande wa Magharibi, Kigoma, Kasulu mpaka Nyakanazi kazi zinaendelea, lakini pia Tabora – Kaliua kwenda kutokea Malagarasi – Uvinza kazi inaendelea, Rukwa kupitia Mpanda kwenda kutokea Uvinza kazi inaendelea, lakini pia hapa katikati Iringa – Dodoma mpaka Babati tumebakiza kilometa 20, 30 kazi inakamilika na huko Kusini tumejenga barabara kutoka Tunduru – Songea na tunakwenda mpaka Mbinga
tunashuka mpaka Mbamba bay ili kudhihirisha kwamba kazi hizi zinafanywa maeneo yote nchini, naomba mtuunge mkono ili tuendelee na tufanye kazi. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, baadhi ya Waheshimiwa Wabunge wamejadili sana kuhusu suala la madeni ya wakandarasi, wazabuni, watumishi na watoa huduma.
Nataka niwahakikishie Waheshimiwa Wabunge, hawa wakandarasi na watoa huduma wote ndugu zetu, makampuni ya nje, tunaendelea kulipa na wakandarasi wengine ambao wametoa huduma tunaendelea kuhakiki madeni yao, tunataka tuhakikishe kwamba tunalipa huduma
zote. Kwa hiyo, Waheshimiwa Wabunge muendelee kutuunga mkono ili tuhakikishe kwamba jambo hili hatupati tena lawama kutoka kwa wenzetu ambao wanatoa huduma Serikalini.
Mheshimiwa Spika, suala lingine Bunge lako tumetoa fedha, najua Waheshimiwa Wabunge walikuwa na mashaka juu ya huduma za Bunge. Bunge hili tumeliongezea fedha, shilingi bilioni 21 ili liweze kufikia tarehe 30 Juni, kwa hiyo, Bunge hili halina mashaka litafika. Lakini maombi ya bajeti mpya tumepandisha mpaka bilioni 121 ambazo pia zitafanya Bunge lijalo liweze kuendelea kwa mwaka ujao wa fedha.
Kwa hiyo, nataka niwahakikishie kwamba Serikali yetu ni sikivu, tumewasikia vilio vyenu, ushauri wenu na sasa tunatekeleza. Tunaomba ridhaa yenu leo ili fedha hii tuweze kuitoa na Bunge letu liweze kufanya kazi yetu. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, naomba nianze kujibu hoja mbalimbali ambazo Waheshimiwa Wabunge wameweza kuzitoa na nianze na ya kiongozi mwenzangu, Mheshimiwa Freeman Mbowe, Mbunge lakini pia Kiongozi wa Kambi ya Upinzani. Najua swali lake la kwanza limejibiwa na
Mheshimiwa Naibu Waziri, lakini nataka niongeze pale aliposhauri kwamba sasa Serikali itoe maelekezo kwa Halmashauri ili kuongeza ajira angalau 20,000 kila mwaka katika miradi mbalimbali ndani ya Halmashauri.
Mheshimiwa Mbowe, Kiongozi wa Kambi ya Upinzani, nataka kukuambia kwamba tayari natoa maelekezo na kwa maelekezo haya sasa nataka Halmashauri zote zizingatie mwongozo wa bajeti ya Serikali unaotolewa na Hazina kila mwaka unaozitaka Mamlaka za Serikali za Mitaa, Wizara na taasisi zote kubainisha fursa za ajira zinazotarajiwa kupatikana kila mwaka kutokana na utekelezaji wa miradi ya maendeleo. Vilevie mwongozo huo unazitaka sana taasisi hizo kutoa taarifa za ajira zinazozalishwa kutokana na utekelezaji wa miradi hiyo ili pia na sisi tuweze kutoa taarifa kwa Waheshimiwa Wabunge wajue kinachoendelea kupitia Halmashauri zao.
Mheshimiwa Spika, tulikuwa na hoja ya pili ya hali ya upatikanaji wa chakula nchini. Kama ambavyo nilisema kwenye Hotuba yangu ya Bajeti ya mwaka 2017/2018 ipo ukurasa wa 21. Katika msimu wa kilimo uliopita wa mwaka 2016/2017 hali ya upatikanaji wa mvua haikuwa nzuri kwenye mikoa, hasa ile ambayo inapata mvua wakati wa vuli na hali ya mavuno katika baadhi ya maeneo hayo iliyumba kwa sababu hakukuwa na mvua za vuli, leo hii tunaendelea kupata mvua, tulichokifanya ni kusisitiza wafanyabiashara wetu wa ndani waendelee kusafirisha vyakula kutoka vinapopatikana mpaka eneo ambalo lina upungufu mkubwa na tulibaini zile Wilaya zetu 55, taratibu zinaendelea na Mheshimiwa Waziri wa Kilimo anasimamia upatikanaji wa chakula kwenye maeneo hayo kupitia wafanyabiashara wetu wa ndani.
Mheshimiwa Spika, nitoe wito kwa mvua zinazoendelea sasa, maeneo mengi mvua zinanyesha tujitahidi basi kupanda mazao ya muda mfupi ili yaweze kuiva katika kipindi kifupi ili msimu ujao wa mavuno tuweze kufanya tathmini, je, tumepata chakula cha kutosha, tuna upungufu wapi, ile akiba tuliyonayo tutaona namna ambavyo tunaweza tukaisambaza kwenye maeneo yetu.
Kwa hiyo Mheshimiwa Mbunge ambaye alitoa hoja hii, Serikali imejipanga kwa utaratibu huo na tutaisimamia kikamilifu.
Mheshimiwa Spika, hoja ya tatu ilikuwa ni kuwa na mipaka mingi yenye vipenyo vingi pamoja na ukanda mrefu wa bahari ambao umefanya udhibiti wa uingizaji wa dawa za kulevya kuwa mgumu sana. Serikali imeshauriwa kupitia Kamati za Ulinzi na Usalama za Mikoa kutoa elimu kwa jamii zinazoishi mipakani ili zishirikiane na vyombo vya dola kwenye maeneo hayo ili kudhibiti hali hiyo. Mamlaka ya Kudhibiti na
Kupambana na Dawa za Kulevya imeshaanza kutoa elimu kwa Kamati za Ulinzi na Usalama katika maeneo ya mipaka ya Tunduma, Kasumulo, Namanga, Horohoro na Mtukura ili kuweza kutoa elimu ya juu ya athari za dawa za kulevya kwa jamii inayoishi mipakani.
Aidha, elimu hii itatolewa kwa wananchi kadri hali inavyoruhusu ili wananchi wote kwa pamoja washiriki katika mapambano dhidi ya dawa za kulevya badala ya kuviachia vyombo vya dola peke yake. Kwa hiyo, kazi hiyo inaendelea ili tuweze kuimarisha maeneo haya.
Mheshimiwa Spika, kulikuwa na hoja ya mapambano dhidi ya dawa za kulevya ili kulinda watoa taarifa na pendekezo la kutaifisha mashamba ya bangi. Tatizo la dawa za kulevya ni janga kubwa, tumelizungumza mara nyingi na linaathiri sana ustawi wa nchi yetu. Serikali imedhamiria kwa dhati kabisa kupambana na mtandao wa dawa za kulevya nchini. Mafanikio katika mapambano ya dawa za kulevya yanahitaji sana ushirikiano wa kutosha kutoka kwa wananchi, hivyo napenda sana kulihakikishia Bunge lako Tukufu kwamba watoa taarifa za wahusika wa dawa za kulevya watalindwa na wanaendelea kulindwa kwa mujibu wa sheria za kulinda watoa taarifa na mashahidi ambao wanatoa ushahidi wa kesi hizi na kwa mujibu wa sheria ile ya mwaka 2015 (Whistleblowers and Witness Protection Act, 2015).
Mheshimiwa Spika, Serikali inalipokea pendekezo hili kutaifisha mashamba ya bangi na litaendelea kutafakari utekelezaji wake vilevile. Pale ambapo tutajiridhisha kuwa adhabu hii itatosha inaweza kutoa fundisho kwa wananchi wanaojihusisha na kilimo cha bangi, Serikali haitasita kuleta Bungeni Muswada wa Mabadiliko ya Sheria ili pia tuweze kupata mwongozo mwingine zaidi kutoka kwako.
Mheshimiwa Spika, kulikuwa na hoja ya tano ya kuongeza kituo cha tiba za methadone na sober houses za Serikali angalau moja kila mkoa. Uanzishwaji wa vituo vya tiba kwa kutumia methadone unategemea ukubwa wa tatizo la matumizi ya dawa za kulevya na uwepo wa
miundombinu ya msingi katika mkoa husika. Hadi sasa kuna vituo vya methadone katika Hospitali za Muhimbili, Mwananyamala na Temeke Mkoani Dar es Salaam, vilevile Serikali inakusudia kufungua vituo kama hivyo katika mikoa ya Arusha, Dodoma, Kilimanjaro, Mbeya, Morogoro, Mwanza, Pwani na Tanga. Kwa kuwa matibabu ya methadone yanasaidia sana watumiaji wa dawa za kulevya aina ya heroin tu pekee, Serikali inatarajia kuanzisha nyumba ya upataji nafuu (sober house) kila mkoa, huduma hii itakuwa ni kwa ajili ya kuwasaidia warahibu wengine wa aina zote za dawa za kulevya badala ya kuwaachia watu binafsi ambao mpaka sasa wanaendesha nyumba 17 za upataji nafuu nchini.
Hata hivyo, niwasihi sasa wale wote waendelee na kazi hiyo na kama wapo wadau wengine wataendelea kutuandalia nyumba za aina hiyo, tutazipokea na tutazisajili lakini Serikali inaendelea kuandaa mwongozo wenye lengo la kusimamia na kuratibu hizo nyumba zote za watu binafsi.
Mheshimiwa Spika, tulikuwa na hoja nyingine ambayo Serikali ilishauriwa iongeze vituo vya afya, vifaa tiba, wahudumu wa afya wenye weledi wa kupunguza umbali wa kupata huduma za wanaoishi na virusi vya UKIMWI; Ilani ya Uchaguzi ya CCM ya Sera ya Maendeleo ya Afya ya Msingi inaelekeza Serikali kuboresha huduma za afya ya msingi kwa kjenga zahanati kila kijiji, kituo cha afya kila kata na Hospitali
ya Wilaya kila Wilaya.
Aidha, Serikali ina mkakati wa kuongeza idadi ya wataalam wa afya nchini kote. Jambo hili limezungumzwa na Wabunge wengi wakiuliza maendeleo ya ujenzi wa Hospitali za Wilaya, zahanati na vituo vya afya. Nataka niwahakikishie Waheshimiwa Wabunge kwamba kadri
tunavyopata fedha na kuzitenga katika bajeti tutaendelea pia kuhamasisha wananchi kuanzisha miradi ya ujenzi wa zahanati, vituo vya afya na Serikali itaendelea kuunga mkono kwa lengo la kila kijiji kuwa na zahanati yake, kila kata iwe na kituo cha afya na Wilaya ziweze kuwa na Hospitali za Wilaya na yale majukumu yote ya Wizara ya Elimu pamoja na TAMISEMI yataendelea kuimarishwa ili maeneo yote yawe
yanapata huduma ikiwemo na uwepo wa watumishi wa afya. (Makofi)
Kwa hiyo, Waheshimiwa Wabunge ushauri wenu kwenye eneo hili tumeupokea, nataka niwahakikishie kwamba tutaufanyia kazi.
Mheshimiwa Spika, kulikuwa na hoja nyingine ambayo inataka Serikali itoe elimu ya kujikinga na VVU kwa kutumia mbinu mbalimbali ikiwemo elimu kwa njia ya sinema na kuanzisha vilabu vya mapambano dhidi ya VVU katika shule zote kuanzia msingi hadi sekondari na kuandaa mitaala ya elimu ya UKIMWI katika ngazi zote za elimu ya msingi hadi Vyuo Vikuu. Nia ya Serikali katika hili ni kuona elimu ya UKIMWI
inawafikia wote wanaostahili nchini. Serikali ina magari ya sinema katika mikoa yote 20 ya Tanzania Bara ambayo pia hutoa elimu ya UKIMWI kwa njia ya sinema. Mkakati tulionao sasa pia na mikoa mitano ya Tanzania Visiwani nayo itapata magari ya sinema ili kuendelea kutoa huduma nchini kote.
Wizara ya Elimu kwa pamoja na Wizara ya Elimu ya Zanzibar imetoa mitaala kufundisha wanafunzi kuhusiana na elimu ya UKIMWI kwenye shule zetu. Serikali inatoa wito pia kwa Makatibu Tawala wa Mikoa na Wakurugenzi wa Halmashauri kuyatumia ipasavyo magari hayo na kuhakikisha kwamba walimu wapya wanapitishwa vema katika mitaala hiyo pamoja na kuanzisha clubs za kuhamasisha mapambano
dhidi ya UKIMWI katika shule, vyuo vyote nchini na mahali pote ambapo kuna mikusanyiko ya watu.
Mheshimiwa Spika, kulikuwa na ushauri unaosema Serikali ibuni chanzo mahsusi cha kutunisha Mfuko wa UKIMWI (Aids Trust Fund) kama ilivyo kwa mifuko mingine mfano REA na maji ili kufanikisha mapambano dhidi ya UKIMWI. Kupitia Bunge lako napenda kuwahakikishia kwamba ushauri huu uliotolewa na Waheshimiwa Wabunge umepokelewa na Serikali itaufanyia kazi. Malengo yetu ni kuhakikisha kwamba
mfuko huu tukiuanzisha, tukiutunisha huduma zote zinaweza kuwafikia mpaka walioko vijijini, kwa hiyo, jambo hili Waheshimiwa Wabunge tumelipokea. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, tulikuwa na hoja pia ya kuweka utaratibu wa kufuatilia fedha zinazotolewa na wafadhili kwenye Mashirika yasiyokuwa ya Kiserikali zinazojihusisha na masuala ya UKIMWI. Utaratibu wa kufuatilia fedha zinazotolewa kwenye NGO’s upo na tumekuwa tukisisitiza
ufuatwe vizuri. Mathalani nilipofanya ziara mkoani Arusha hivi karibuni nilirudia wito wa kuzifanyia kaguzi za mara kwa mara NGO’s zinazofanya kazi nchini. Hivyo, ushauri wangu wa Kamati kuhusu hitaji la kufanya ukaguzi kwenye NGOs zinazoshughulikia UKIMWI utaendelea kuzingatiwa kama ambavyo tumetoa maelekezo. Natoa wito kwa wakurugenzi wote wa Halmashauri zetu za Wilaya nchini waendelee
kuhakikisha wadau wa UKIMWI wanaofanya kazi kwenye maeneo yao wanakaguliwa kulingana na Sheria ya UKIMWI ya mwaka 2008 na Sheria ya Mashirika Yasiyo ya Kiserikali ya mwaka 2002, ili tuweze kujiridhisha wanapata nini kwa ajili ya huduma gani, kiasi gani kinatumika ili wanufaika waweze kuridhika kwenye huduma hii.
Mheshimiwa Spika, hoja nyingine ambayo ilikuwa imetolewa na Waheshimiwa Wabunge ni juu ya Serikali kujiridhisha kuhusu masuala ya kitaalam ya kufanya mapitio na maboresho ya sheria stahiki katika kutekeleza mpango wa kuunganisha mifuko ya pensheni; hili limezungumzwa vizuri sana na Waziri wa Nchi, Mheshimiwa Jenista Mhagama.
Lakini zoezi la kuunganisha mifuko ya pensheni linafanyika kwa kuzingatia ushauri wa kitaalam. Katika kutekeleza jukumu hilo mifuko yote ya pensheni imefanyiwa tathmini ambayo pamoja na mambo mengine imebainisha kuwa kuunganisha mifuko ya pensheni ndiyo njia bora ya kuimarisha sekta ya hifadhi ya jamii nchini.
Aidha, Serikali imeandaa andiko la mapendekezo ya kuuunganisha mifuko, kazi hii imefanyika kwa kushirikisha wadau muhimu katika sekta husika. Serikali itaendelea kutoa taarifa za mara kwa mara juu ya hatua iliyofikiwa kwenye mpango huo wa kuunganisha mifuko.
Mheshimiwa Spika, kulikuwa na ushauri mwingine kwamba mifuko ya hifadhi ya jamii inayojishughulisha kuwekeza kwenye uchumi iweze kuendelea na uwekezaji huo hasa kwenye maeneo ya viwanda. Uwekezaji ni kazi mojawapo ya Mifuko ya Hifadhi ya Jamii na lengo la
uwezeshaji ni kulinda thamani ya michango ya mwanachama pamoja na kukuza uwezo wa mifuko, kupitia na kulipa mafao kwa wanachama wake pamoja na wanapopatwa na majanga mbalimbali yanayowasababishia kukosa kipato. Majanga hayo ni kama vile maradhi, uzee na kifo, kwa msingi huo uwekezaji kwenye viwanda unavyofanywa na Mifuko ya Hifadhi ya Jamii sasa una manufaa makubwa sana kwani pamoja na kulinda thamani ya fedha za michango ya wanachama, uwekezaji huu unakuza mapato ya Serikali, unatoa fursa za ajira na hivyo kusaidia kuongeza idadi ya wanachama watakaoweza kuongeza michango yao kwenye mfuko husika.
Mheshimiwa Spika, Mifuko ya Hifadhi ya Jamii na Serikali kwa pamoja vitaendelea kuhakikisha kwamba uwekezaji unaofanywa na mifuko ya hifadhi ya jamii unazingatia miongozo ya uwekezaji ili mifuko hiyo isiweze kupata hasara kubwa, tunashukuru jambo hili linaendelea
na tutakuja kuwapa mrejesho.
Mheshimiwa Spika, tulikuwa na hoja ya uboreshaji wa daftari la kudumu la wapiga kura na utoaji wa elimu ya kupiga kura. Kwa mujibu wa Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Tume ya Taifa ya Uchaguzi inayo jukumu la kuboresha daftari la kudumu la kupiga kura. Katika mwaka wa fedha 2017/2018 Tume ya Taifa ya Uchaguzi itaweka kipaumbele katika uboreshaji wa daftari la wapiga kura na Tume ya Taifa ya Uchaguzi imepewa jukumu la kutoa elimu ya mpiga kura nchini kote na kusimamia na kuratibu asasi, taasisi na watu wanaotoa elimu kwa mpiga kura. Tume pia imeendelea kutoa elimu ya mpiga kura kwa njia mbalimbali ikiwemo kutumia redio, television, kukutana na wadau,
kupitia maonyesho mbalimbali pamoja na kushiriki mikutano katika ngazi ya Mikoa na Halmashauri.
Mheshimiwa Spika, iko hoja ambayo ilizungumzia suala la mgogoro wa uongozi ndani ya Chama cha CUF.
Jambo hili limezungumzwa kwa hisia kali na sisi tumelipokea lakini nataka niseme tu kwamba hoja hii kwa namna ambavyo imejadiliwa na Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Katiba na Sheria, Kambi Rasmi ya Upinzani Bungeni na Waheshimiwa Wabunge mbalimbali wameweza kuijadili sana. Serikali haifurahishwi na migogoro ndani ya vyama vya siasa kwani inadumaza demokrasia nchini na kusababisha mifarakano isiyokuwa na tija. Ofisi ya Msajili wa Vyama vya Siasa kama mlezi wa vyama vya siasa imekuwa ikishiriki sana kikamilifu katika kuhakikisha kwamba migogoro ndani ya vyama vya sisa inatatuliwa kwa majadiliano.
Mheshimiwa Spika, katika hili mgogoro uliopo ndani ya Chama cha CUF, Ofisi ya Msajili wa Vyama vya Siasa ilitoa ushauri kulingana na taratibu zilizopo, hata hivyo wakati usuluhishi ukiendelea, baadhi ya wanachama wa CUF ambao hawakuridhika na usuluhishi uliofanywa na Msajili walipeleka shauri Mahakamani ili kudai haki yao kwenye mhimili ya Mahakama ikiwa ni pamoja na suala la ruzuku ambalo Mahakama imetoa zuio la muda mpaka shauri la msingi lililoko Mahakamani litakapotolewa uamuzi. Kwa kuwa masuala haya yapo Mahakamani na kwa kuwa Waheshimiwa Wabunge mnataka jambo hili lingepata nafasi ya kuzungumzwa basi ni vizuri tukaiacha Mahakama ifanye kazi yake halafu tuje tulizungumze. Hiyo ni rai yangu na namna nzuri ya kuweza kutatua mgogoro (Makofi)
Mheshimiwa Spika, namshukuru sana Mheshimiwa Mwanasheria Mkuu kwa jambo ambalo limezungumzwa sana hapa ndani, suala la
usalama na kutokuwa na uhakika wetu Waheshimiwa Wabunge. Jambo hili kama ambavyo Mwanasheria amelieleza, Serikali inalifanyia kazi na hapo baadae tutakuja kutoa taarifa ya Serikali kwenu kwa sasa tunawasihi Waheshimiwa Wabunge tuache vyombo vyetu vifanye kazi, vifuatilie ni nini hiki kinaendela, nani anaendelea nacho, malengo ni nini ili tuje tujiridhishe kama je, matendo haya yanayozagaa huko ni matendo ambayo yanakubalika?
Kimsingi hayakubaliki, lakini taarifa rasmi tutakuja kuileta Bungeni Waheshimiwa Wabunge wenzangu.
Mheshimiwa Spika, kwa kuwa leo ulinipunguzia muda na niliona nitumie muda huu kuzungumza haya machache, nashukuru nimefika mwisho wa maelezo yangu ili nirudi tena kwa Waheshimiwa Wabunge kuomba ridhaa yao ya fedha tuweze kutekeleza na yale ambayo mliyasema ambayo sijayajibu lakini nina uhakika kwa maelekezo ninayoyatoa kwa Wizara ni lazima waje wafafanue vizuri ya hoja zote ambazo mlizitoa Waheshimiwa Wabunge ili tupate mwelekeo. Nataka niwahakikishie kwamba ushauri wenu tumeuchukua ili tuufanyie kazi katika kipindi cha mwaka mmoja wa fedha kinachokuja baada ya ninyi kuridhia maombi yetu ambayo tunayo hapa.
Mheshimiwa Spika, kama nilivyosema hapo awali,muda usingeweza kutosha kujibu hoja zote zilizotolewa, Waheshimiwa Wabunge wote waliochangia hoja, tumejifunza mengi sana kutoka kwenu, kwenye kupitia michango yenu na tuko tayari kuendelea kujifunza zaidi kutoka kwenu Waheshimiwa Wabunge na ni jukumu letu kuwasikiliza na kupokea ushauri wenu.
Mheshimiwa Spika, nchi hii ni yetu sote na kila mmoja wetu anaowajibu wa kulisukuma mbele gurudumu la maendeleo ya nchi yetu, kila mchango wa Mheshimiwa Mbunge una thamani kubwa sana kwetu na ninawashukuru sana kwa ushauri, maangalizo na mafunzo mliyotupa.
Nataka niwahakikishie ushauri huu wakati mwingine tunautekeleza tunapokuja kwenye Majimbo yenu, nitaendelea na ziara zangu kwenye maeneo yenu ili kutekeleza na haya ambayo mmetushauri. Bado tuko pamoja, nataka niwahakikishie ushirikiano ambao tutawapa wakati
wote katika kipindi cha mwaka wa fedha ujao. Endeleeni kutoa ushauri kwa Serikali hata kwa maandishi tu wakati wowote siyo lazima Bungeni, popote ili tuweze kufikia hatua nzuri ya maendeleo, na sisi tutapokea ushauri huo na kuona namna bora ya kuufanyia kazi. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, kila Mtanzania mkiwemo Waheshimiwa Wabunge mnawajibika kuiacha Tanzania ikiwa ni nchi bora zaidi ya tulivyoikuta. Ili kuifikisha azma hiyo inabidi tuanze kuwa tayari kujinyima mambo mazuri tuliyoyazoea angalau kwa muda ili kuimarisha misingi ya ujenzi wa
Tanzania yetu. Ninawasihi sana Waheshimiwa Wabunge wenzangu muielewe dhamira ya Serikali na mtuamini katika kusimamia rasilimali ya nchi yetu kwa manufaa yetu na vizazi vijavyo. Serikali imejipanga vizuri katika kulinda maslahi ya nchi hii na wananchi wake. Hivyo nawaomba muendelee kutuunga mkono kwa kupitisha bajeti yetu ya Ofisi ya Waziri Mkuu ambayo leo hii iko mbele yenu na tunaomba ridhaa
yenu ili tufanye kazi kwa pamoja. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, ninapohitimisha hoja yangu tena katika siku ambayo Taifa letu kama ambavyo nimeeleza ninalazimika kuwakumbusha Watanzania wote tuendelee kumuenzi mpambanaji huyo wa haki za wanyonge kwa kuunga mkono jitihada za Serikali ya Awamu ya Tano za
kupambana na rushwa na ubadhirifu wa mali za umma.
Tumuombe tena Mwenyezi Mungu aendelee kumpumzisha Hayati Edward Moringe Sokoine aliyekuwa Waziri Mkuu Awamu ya Tatu. Mungu ailaze roho yake mahali pema peponi, amin.
Mheshimiwa Spika, nirudie tena kwa Waheshimiwa Wabunge wenzangu, niko chini yenu kuomba ridhaa yenu kwenye mpango ambao tutauleta.
Mheshimiwa Spika, baada ya maelezo hayo naomba kutoa hoja, ahsante sana.