Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 - Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa na Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora

Hon. Leah Jeremiah Komanya

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Meatu

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 - Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa na Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora

MHE. LEAH J. KOMANYA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kunipatia nafasi hii ili niweze kuchangia hoja ya Wizara ya TAMISEMI pamoja na Utumishi; Utawala Bora.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza napenda kumpongeza Mheshimiwa Rais kwa kazi nzuri anazozifanya. Wananchi wa Mkoa wa Simiyu wanamuunga mkono Mheshimiwa Rais kwa kazi zote anazozifanya za kupambana na wote wasio na nia nzuri na nchi. Hii yote imejidhihirisha
katika ziara yake aliyoifanya mapema mwezi wa Kwanza katika Mkoa wa Simiyu.
Mheshimiwa Naibu Spika, naendelea kumpongeza na kumshukuru Mheshimiwa Rais kwa kutuzindulia Kiwanda cha Chaki kilichopo Maswa Mkoani Simiyu. Katika uzinduzi wake, alitujengea mazingira ya kuona namna ya kuweza kupanua kiwanda hicho na tayari sasa hivi kiwanda hicho kitapanuliwa kwa kushirikiana na Halmashauri pamoja na TIB. Naomba niwajulishe tu kwamba chaki za Maswa ni nzuri; na vijana wako hapa Dodoma kwe ye maonesho wanazo hizo chaki. Kwa hiyo, nawaombeni Waheshimiwa Wabunge mfike mzione ili muweze kununua katika Halmashauri zenu na kukuza uchumi wa vijana wa Maswa. Mheshimiwa Naibu Spika, naendelea kumshukuru Mheshimiwa Rais kwa kutuzindulia barabara ya lami ya kutoka Lamadi mpaka Bariadi yenye kilometa 71, kuweka jiwe la msingi katika ujenzi wa barabara ya lami kutoka Mwigumbi mpaka Maswa yenye kilometa 52. Mheshimiwa Rais alipokuwa Mkoani Simiyu aliahidi sasa utekelezaji wa ujenzi wa lami wa barabara ya Maswa mpaka Bariadi yenye kilometa 50 uanze. Hivi sasa ninavyoongea, mchakato wa kumpata Mkandarasi unaendelea. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nitoe ushauri upande wa Serikali. Nimeshuhudia miradi mingi mikub wa wakati ikitekelezwa, wakandarasi wamekuwa wakija na vijana kufanya kazi ambazo zingeweza kufanywa na vijana ambao wanatoka pale pale. Wakandarasi wengine
wameweza kuthubutu kuja hata mpaka na unga kwenye eneo analoweza kufanyia kazi. Naomba Serikali isaidiane na wakandarasi, kuwatumia vijana wa eneo hilo.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kuwa mradi ule utatekelezwa katika Wilaya ya Bariadi, Itilima na Maswa, wachukue vijana wa kutoka pale kwa sababu nina imani wanazo nguvu na ni waadilifu. Pia wanunue bidhaa zinazotokea katika maeneo yale. Kuna samaki wazuri wanapatikana katika soko la Bariadi ambao wanavuliwa katika Ziwa Victoria Wilaya ya Busega; kuna nafaka nzuri inatoka Wilaya ya Itilima; na mchele mzuri unaotokea katika Wilaya ya Maswa. Nawakaribisheni sana. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, niendelee kwa kusema, Mheshimiwa Rais wakati anafanya kampeni zake mwaka 2015, alipokuwa Wilayani Meatu aliawaahidi wananchi kwamba atawawezesha kujenga nyumba bora kwa kupunguza bei ya vifaa vya ujenzi. Hapa ninapoongea, mfuko
mmoja wa saruji Wilayani Meatu ulikuwa unauzwa shilingi 20,000/=, lakini kwa sasa hivi unauzwa shilingi 16,000/=; lakini bei hiyo bado iko juu ukilinganisha na wilaya za jirani. Hii inatokana na kwamba simenti inapokuja, ni mpaka ifike Shinyanga halafu ianze kurudi tena kuja Wilaya ya Meatu. Changamoto ya kutatua mzunguko wa usafiri huu ni ukamilishaji wa ujenzi wa Daraja la Mto Sibiti. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, nafahamu daraja hilo linatekelezwa na TANROAD, Singida, lakini vikao vya Mfuko wa Barabara vya Mkoa wa Simiyu toka mwezi wa Tisa tumekuwa tukiahidiwa kwamba, vifaa viko China vinatengenezwa, leo yapata miezi saba, vifaa vile havijaletwa. Tunaomba basi ujenzi huu uharakishwe, vifaa hivyo viletwe ili daraja hilo liweze kufungua milango ya biashara kwa Mkoa wa Simiyu, hususan Wilaya ya Meatu.
Mheshimiwa Naibu Spika, barabara hiyo itakapoanza kazi, itasaidia wananchi. Mwananchi anapoondoka Meatu kwa kupitia Shinyanga, anatumia sh. 95,000/= kwa sababu inabidi aende Shinyanga, alale Shinyanga kesho yake asafiri. Kwa kutumia daraja la Mto Sibiti pale, atatumia sh. 45,000/= kufika Dar es Salaam. Kwa hiyo, ataokoa sh. 50,000/= pamoja na siku moja ambayo angeweza kutumia katika shughuli nyingine. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nichangie upande wa maji. Katika hotuba ya Waziri wa TAMISEMI amesema kwamba Serikali imeunda vyombo vya utumiaji maji COWSO, vipatavyo 1,800 kwa ajili ya usimamizi na uendelezaji wa vituo vya maji, ili kuhakikisha miradi hiyo inakuwa endelevu. Mimi nikiwa Mjumbe wa Kamati ya LAAC, tumekuwa tukitembelea miradi hiyo, tumeona changamoto mbalimbali katika uendeshaji wa hiyo miradi iliyokabidhiwa kwa wananchi.
Mheshimiwa Naibu Spika, Kamati zile hazijajengewa uwezo namna ya uendeshaji wa miradi hiyo. Kamati hizo hazijui hata namna ya utunzaji wa fedha, namna ya kupokea mapato, hazina hata 'O' and 'M' Accounts (Operation and Maintenance Account), kiasi kwamba tatizo likitokea
wanapaswa wachukue fedha ili mradi uendelee. Matokeo wamekuwa wakichangishana fedha kienyeji na kusababisha hata ile gharama kwa ndoo kuwa kubwa. Tunaomba vyombo vile viwezeshwe ili viweze kuendesha miradi hiyo ya maji. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, nimalizie mchango wangu kwa 5% ya wanawake na vijana. Ni kweli Halmashauri zimekuwa zikitenga fedha kwa ajili ya kuwawezesha akinamama na vijana, lakini Halmashauri zimekuwa zikiishia kutenga tu bila kutoa michango ile kwa akinamama. Kwa
kuwa michango hiyo haiko kisheria, ni waraka tu unaotumika, wakati tukiwa mbioni kuandaa sheria, nashauri ili utekelezaji ufanyike vizuri, basi ajenda hii ya mchango iwe ya kudumu kwenye vikao vya RCC ili Mkuu wa Mkoa na Kikao chake aanze yeye kwanza kufuatilia badala ya kusubiri Kamati ya LAAC ndiyo ije kwanza ionekane kwamba ule mchango ndiyo kwanza wameuona. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hayo machache, naunga mkono hoja.