Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 - Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa na Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora

Hon. Ester Alexander Mahawe

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 - Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa na Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora

MHE. ESTHER A. MAHAWE: Mheshimiwa Naibu Spika ahsante sana. Kwanza kabisa napenda kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa ajili ya kutupa afya sisi wote tulioko ndani ya Jengo hili Tukufu la Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kwanza kabisa nielekeze pongezi zangu za dhati kwa Mheshimiwa Rais Dkt. John Pombe Magufuli kwa kazi yake nzuri sana anayoifanya kupitia kwa Mawaziri hawa wawili wa TAMISEMI, Mheshimiwa Simbachawene na Mheshimiwa Jafo, kwa kweli kazi inafanyika. Niseme tu kwa upande wa Mkoa wa Manyara tunashukuru sana Serikali, tayari tumeanza kuona kwamba kwa kweli kazi inapigwa. Tunategemea kuboreshewa zahanati zetu katika Wilaya nne za Mkoa wa Manyara; Wilaya ya Mbulu Mjini na Jimbo la Mbulu Vijijini, Babati Mjini, Babati Vijijini na Wilaya ya Simanjiro, zahanati ile ya Urban Orkesumet inakwenda kuboreshwa sasa kwenda kwenye hadhi ya kituo cha afya; shughuli hii siyo ndogo.
Mheshimiwa Naibu Spika, pia naomba nipongeze juhudi za Serikali. Tumekuwa na kilio cha maji muda mrefu katika Wilaya ya Simanjiro sasa mradi mkubwa wa maji kutoka Mto Ruvu unaelekea katika eneo la Orkesumet Makao Makuu ya Wilaya ya Simanjiro, ni mradi ambao utaondoa tatizo la maji kwa kiwango kikubwa sana, kwa kweli naipongeza Serikali. Wale wanaosema hakuna kinachofanyika na bajeti iliyoletwa hapa mwaka jana ni hewa siyo kweli.
Mheshimiwa Naibu Spika, pia niseme kwamba tayari tender ya Daraja la Magara ambalo tumekuwa tukilipigia kelele sana watu wa Babati na watu wa Mbulu, imetangazwa. Niiombe Serikali iwahishe kupeleka fedha daraja lile lianze kutengenezwa ili wananchi wetu waanze kupona.
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nijielekeze kwenye TASAF. Mfuko huu wa TASAF kwa kweli binafsi katika kutembea kwetu tulipokuwa kwenye Kamati katika Mikoa ya Mbeya, Iringa na Njombe ulionesha mafanikio makubwa sana katika kuondoa umaskini wa wananchi wetu. Wananchi hawa wenyewe wametoa ushuhuda jinsi gani Mfuko huu umekuwa wa msaada sana kwao. Watoto wanakwenda shule, watoto
wanapelekwa clinic kwa idadi kubwa, watu wanapata bima ya afya; huu siyo Mfuko wa kubezwa hata kidogo.
Mheshimiwa Naibu Spika, niiombe Serikali na yenyewe iweze kuchangia sehemu inayotakiwa kuchangia ili Mfuko huu uendelee kudumu na kuendelea kusaidia kwa sababu wananchi wengi wameshatoka katika hali ya umaskini. Wale walio-graduate unaona kabisa tayari wana nyumba bora, maisha yao yamebadilika. Ni Mfuko ambao kwa kweli unahitaji kuongezewa nguvu.
Mheshimiwa Naibu Spika, lakini hapo hapo pia niseme kwamba kuna changamoto ndogo ndogo zilizojitokeza kwenye zile kaya ambazo zilionekana ziliingizwa kinyume na utaratibu. Ninachoshauri tu ni kwamba, haki itendeke kwa watu wale ikiwa huenda wengine waliondolewa bila kuona kwamba wanastahili ama la maana pia walipaswa kurejesha fedha zile walizokwishapewa.
Mheshimiwa Naibu Spika, nashauri kwamba wale waratibu waliohusika kuingiza watu ambao hawakuhusika wao wawajibike zaidi kuliko mwananchi ambaye hali yake ni duni na alishapewa fedha zile za kujisaidia na bado anapaswa kurudisha. Kama alipewa kwa sababu ni maskini anazitoa wapi leo? Kwa hiyo, nashauri hili lifanyike kwa umakini mkubwa sana.
Mheshimiwa Naibu Spika, kuna huu MKURABITA. MKURABITA katika maeneo ya Njombe tumeona watu wametoa ushuhuda. Wale ambao ardhi zao zimerasimishwa na tayari wanatumia zile hati zao kuchukua mikopo mikubwa katika Mabenki tofauti. Tulishangaa kuona kwamba mtu ana uwezo wa kukopeshwa kuanzia milioni 100 mpaka 400 kwa kutumia hati hizi za Kimila, kwa kweli ni hatua kubwa mno Serikali imepiga katika hili. Niendelee kuitia moyo Serikali yangu ya kwamba sasa iendelee kupanua wigo wa kusaidia hati hizi za kimila zipatikane katika maeneo mengine ambayo hayajafanyiwa kazi namna hiyo. MKURABITA ushirikiane na Halmashauri zetu mbalimbali nchini ili wananchi
wetu waweze kufaidika. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, pia wakati mwingine kuna changamoto katika upelekwaji wa fedha. Tunafahamu mambo yaliyofanyika ndani ya kipindi cha mwaka mmoja kwenye Serikali yetu kupitia Mheshimiwa Rais ni mambo makubwa na mambo mengi ambayo kiukweli hayapaswi
kudhihakiwa, bali tumtie Rais wetu moyo kazi inapigwa sana. Hata hivyo, niombe, bajeti hii tunayoijadili sasa iweze kupelekwa kwa wakati katika Halmashauri zetu. Kuwe na ushirikiano mkubwa na wa kutosha kati ya Serikali Kuu na Halmashauri zetu ili kwamba kazi ziweze kufanyika kwa wakati.
Mheshimiwa Naibu Spika, ilijitokeza pia changamoto kuhusu zile asilimia tano za wanawake na tano za vijana. Kwa sababu ya kucheleweshwa kwa fedha hizi za OC kufika kwa wakati katika Halmashauri, imeonekana ile asilimia 10 kuelekezwa katika mambo mengine katika Halmashauri kwa, mfano; suala la madawati, maabara na vitu vya namna hiyo, hatulaumu zote ni kazi, lakini kwa sababu fungu hili lipo kisheria basi Serikali iangalie namna bora zaidi ya kufikisha zile fedha kwa wakati ili akinamama na vijana waweze kujikwamua katika lindi hili la umaskini kupitia kukopeshwa fedha zile za asilimia tano za vijana na tano za wanawake.
Mheshimiwa Naibu Spika, najua tayari tulimaliza changamoto za madawati, sasa hivi maeneo mengi tuna changamoto kubwa ya upungufu wa madarasa, mashimo ya vyoo pamoja na nyumba za Walimu. Ni kweli kwamba elimu bora inahitaji uwekezaji, hakuna muujiza; Walimu hawa watakapokuwa pia wamepata maeneo mazuri kwa maana ya madarasa toshelevu watafundisha watoto wetu vizuri na wanafunzi hawa wataelewa. Pia matundu ya vyoo yaendane sawa sawa na idadi ya wanafunzi walioko kwenye shule husika. Nafahamu Serikali yetu sikivu imejipanga kwa hili kwa mwaka huu wa 2017/2018 ili kuhakikisha tunaondokana na changamoto hii.
Mheshimiwa Naibu Spika, suala hili la upungufu nalo linaendelea kwenye maeneo mengine kama zahanati ambapo tuna upungufu mkubwa wa vyumba ama nyumba za wafanyakazi wa kada ya afya. Waganga wetu hawana mahali pa kuishi, wanaishi mbali na maeneo ambayo
yanapaswa kutolewa huduma za afya. Tunaomba pia Serikali itazame hilo katika kipindi hiki cha bajeti.
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kwa dakika chache zilizobaki niweze kusema machache kuhusu habari ya utumishi na utawala bora. Nasikitika sana kwa bahati mbaya sana niliyoiona kwenye hotuba ya dada yangu Mheshimiwa Ruth; sikuona, hotuba yao haikugusa suala zima la rushwa ambalo Serikali yetu imepambana nalo na sasa inaanza kuwa hadithi. Si hivyo tu, utawala bora ni pamoja na uhakiki mkubwa na mrefu uliofanywa na Serikali ili kuondoa mianya yote iliyokuwa inatumika kupoteza fedha za nchi hii. Kazi hiyo imefanyika kwa umakini mkubwa na fedha nyingi zimeokolewa, lakini hili hatukuliona pia likizungumzwa. Kwa hiyo, niseme tu, najua kwamba kazi yao siyo kuisifu Serikali yetu, lakini sisi kama Waheshimiwa Wabunge wa Chama Tawala, kwa kweli tunapongeza sana juhudi hizi ambazo zimefanywa katika awamu hii.
Mheshimiwa Naibu Spika, lakini niombe tu kwamba juhudi hizi ziendelee kufanywa na Serikali. Nampongeza sana Mheshimiwa Angella Kairukiā€¦.
T A A R I F A....
MHE. ESTHER A. MAHAWE: Mheshimiwa Naibu Spika siipokei kwa sababu unapojua kusema mabaya tu ujifunze kusema na mema pia.
Mheshimiwa Naibu Spika, suala zima la uwajibikaji (accountability) lilikuwa halipo mahali pale, leo kuna accountability ukifika hata kwenye ofisi zetu za Serikali unasikilizwa hakuna tena njoo kesho, njoo kesho kutwa, ni sehemu ya utawala bora. Unafika hospitali unatibiwa hakuna
rushwa ni sehemu ya utawala bora. Hii kazi inafanywa na Serikali hii ya Awamu ya Tano ya Dkt. John Pombe Magufuli.
Mheshimiwa Naibu Spika, lakini pia ubadhirifu haupo tena, tayari Serikali ipo kazini inapambana na suala zima la ubadhirifu wa mali ya umma; hayo yote tumeyaona, mbona hatukuyaona kwenye hii hotuba? Wamesema hii ni Serikali ya kuhakiki, yes, we are after accountability, lazima kuwe na uhakiki ili kila mmoja awajibike kwa zamu yake. Wakati Serikali haihakiki wanasema Serikali gani hii, leo inahakiki wanasema Serikali ya kuhakiki; wanadamu hawana jema, Mawaziri wetu chapeni kazi tuko nyuma yenu.
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba pia nizungumzie suala la performance based payments. Kuna zile on call allowances, labda kwa Madaktari na Manesi au kwa Walimu wetu. Wakati mwingine baadhi ya Walimu wametuhumiwa labda wanafanya biashara ya bodaboda wakati wa vipindi, kwa hiyo labda madarasa hayafundishwi inavyotakiwa. Ifike mahali ile performance based payment ifanye sehemu yake ili kuboresha huduma katika taasisi mbalimbali.
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kuunga mkono hoja. Ahsante sana.