Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 - Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa na Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora

Hon. Grace Sindato Kiwelu

Sex

Female

Party

CHADEMA

Constituent

Special Seats

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 - Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa na Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora

MHE. GRACE S. KIWELU: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi na mimi nichangie machache katika Bajeti hii ya Ofisi ya Rais. Nianze kwa kuziunga mkono hotuba zote mbili za Kambi ya Upinzani na niishauri Serikali isijisikie vibaya wala kuona aibu kuchukua yale mazuri yaliyomo katika hotuba zetu. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze na suala la utawala bora. Utawala bora ni pamoja na kuviruhusu vyama vya siasa kutimiza wajibu wake kwa kufanya mikutano ya hadhara, lakini toka imeanza Serikali hii ya Awamu ya Tano, imekuwa na uoga na sijui ni kwa sababu gani wakati mnatamba kwamba mnafanya kazi zenu vizuri na hapa ni kazi tu, lakini mmekuwa mkivipiga marufuku vyama vya upinzani kufanya mikutano na kutoa ruhusa kwa Madiwani na Wabunge. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mkumbuke kuwa katika vyama vyetu tuna viongozi wa vyama wa Kitaifa, tunao Wajumbe wa Kamati Kuu ambao sio Wabunge na siyo Madiwani, je, hawa watafanyia wapi kazi zao. Kwa hiyo, nataka kuiambia Serikali ya Chama cha Mapinduzi waache kunyima haki kwa vyama vingine vya upinzani wakati wao wanapokuwa kwenye maeneo ambayo sio ya kwao wanahutubia wananchi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mgombea wetu wa Urais alipata kura zaidi ya milioni sita na wa Chama cha Mapinduzi alipata kura milioni nane, tofauti ya kura milioni mbili. Yeye anapita kuwashukuru Watanzania, lakini huyu wa kwetu aliyepata kura milioni sita mnakataa asiende kuwashukuru wananchi ambao walimuunga mkono, hii siyo haki kabisa! Tunaomba Katiba iheshimiwe kwa sababu ninyi ndio mmekuwa mkivunja Katiba wakati vyama vya siasa vipo kihalali, vya upinzani na hata hicho cha CCM, kwa hiyo, tupewe haki sawa kuhakikisha tunazungumza na Watanzania. Kutuambia tusubiri mpaka 2020 hamtutendei haki. Chama chochote cha siasa mtaji wake ni watu. Kwa hiyo, tunapokwenda kufanya mikutano, tunakwenda kuzieneza sera zetu na kupata wanachama wa kujiunga na chama chetu, lakini nashindwa kuelewa sijui uoga wenu ni nini. Niwaambie tu, huko nje Watanzania wameshakata tamaa na Chama cha Mapinduzi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nije kwenye suala la afya. Kumekuwa na tatizo ndani ya nchi yetu la vifo vya akina mama na watoto. Naliomba Bunge na Serikali, ifike wakati tuhakikishe kwamba tunakwenda kupunguza vifo hivi kwa kuhakikisha tunatenga bajeti ya kutosha kwa akina mama ili waweze kupata huduma bora wanapofika kwenye vituo vya afya ikiwemo huduma ya upasuaji, kwa sababu akina mama wengi wamepoteza maisha kutokana na vituo vyetu kutokuwa na vifaa na hasa madaktari na wahudumu wa afya pamoja na dawa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, naiomba sana Serikali na sisi kama Bunge tulisemee hili ili kuhakikisha vifo vya akina mama na watoto katika nchi yetu vinapungua. Nawaomba Wabunge wenzangu tukatoe elimu kwenye maeneo yetu tunayotoka na kuwaomba akina mama pindi wanapokuwa wajawazito waweze kuhudhuria kiliniki, hii itasaidia sana kupunguza vifo vya akina mama na watoto.

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala lingine ni Bima ya Afya. Suala hili limekuwa ni tatizo kubwa sana, hata Waheshimiwa Wabunge wenyewe humu ndani ni mashahidi. Zipo hospitali ambazo zinakataa kupokea Bima ya Afya hata kwa Waheshimiwa Wabunge, sembuse huko kwa wananchi wetu ambao ni wengi. Yapo maduka ya dawa yanakataa kupokea kadi hizi.

Kwa hiyo, naiomba Serikali kwanza itoe elimu kwa wadau wote wahusika umuhimu wa hii Bima ya Afya ili wananchi wengi waweze kujiunga katika bima hii waweze kupata huduma nzuri ya afya. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, niongelee suala la elimu. Hapa kwanza naomba nimpongeze na kumshukuru Mheshimiwa Simbachawene. Katika bajeti iliyopita nilizungumzia shule ya watoto walemavu Njiapanda. Kulikuwa kuna baadhi ya watumishi walikuwa hawajalipwa, nakushukuru kwamba watumishi wale wamelipwa, lakini pia namshukuru Waziri wa Elimu Mheshimiwa Mama Ndalichako, alikwenda kutembelea shule ile na niliongea na Mwalimu Mkuu akaniambia kwamba yale niliyoyasema yakiwemo shule ya sekondari ya watoto wenye ulemavu, mchakato umeanza.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru, lakini naomba mchakato uende haraka kwa sababu watoto wale mwaka huu wanakwenda kufanya mtihani wa darasa la saba. Tunaomba sana ili mwakani nao waweze kujiunga kidato cha kwanza, tusiwaache watoto hawa nyuma kwa sababu wanao uwezo na hawa ndio viongozi wetu wa baadaye. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lingine nizungumzie shule za Kata. Mkoa wetu wa Kilimanjaro hasa kule Uchagani waliitikia vizuri sana ujenzi wa shule za Kata na kuna baadhi ya vijiji vina shule mbili mpaka tatu za sekondari na hii sasa imeleta upungufu wa wanafunzi; kwa mfano, katika kijiji cha Kitandu katika Kata ya Uru Mashariki tunazo shule mbili na katika shule moja ya Mawela tuna madarasa zaidi ya manne hayana wanafunzi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naishauri Serikali, pamoja na kuwa shule hizi zilijengwa na nguvu za wananchi, mngewashauri waweze kutumia shule moja aidha, kwa kufanya hostel, kuhamisha shule moja kwenda kwenye shule nyingine ili ile shule nyingine iweze kutumika hostel au tukaweza kuifanya o-level ili wale watakaomaliza pale waweze kuingia kwenye hii shule nyingine kuliko kuacha madarasa wazi, inakuwa haina faida. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lingine elimu yetu tumeona inaendelea kushuka na hii ni kwa sababu Wakaguzi hatujawatengea fedha za kutosha za kuweza kukagua shule zetu. Naiomba sana Serikali iweze kutenga fedha za kutosha ili Wakaguzi hawa waweze kufanya kazi zao ipasavyo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, niongelee suala la posho za Madiwani. Wabunge wenzangu wamesemea sana posho za Madiwani. Tunajua Waheshimiwa Wabunge wanapokuwa hawapo, Madiwani wamekuwa wanafanya kazi kubwa sana. Naiomba Serikali, kwenye hotuba yetu ya Upinzani kwa upande wa TAMISEMI tumeomba kuongeza posho zao. Najua Madiwani wako kwenye ile Sheria ya Mafao, lakini mafao yao mwishoni yanakuwa ni madogo kwa sababau ya posho wanazozipata. Kwa hiyo, naomba posho zao ziongezwe na hii ni pamoja na Wenyeviti wa Vijiji, Vitongoji na Mitaa. Halmashauri nyingi zimekuwa haziwapi fedha. Naiomba TAMISEMI, aidha, itoe mwongozo au itunge sheria ya kuzielekeza Halmashauri zetu kuhakikisha Wenyeviti hawa wanalipwa fedha zao. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, la mwisho nizungumzie ujenzi wa stand ya Ngangamfumuni. Mheshimiwa Simbachawene tunakuomba sana, mchakato huu ulishakamilika na TIB tayari walishakubali kutoa fedha, kujenga na kusimamia ndani ya miaka 15 wakisharejesha fedha zao watukabidhi stand. Kwa hiyo, nakuomba sana Mheshimiwa Waziri utukubalie kusaini ili tuweze kupata fedha hizo kwa maendeleo ya wananchi wetu wa Manispaa ya Moshi na kwa Taifa zima. Sioni ni kwa sababu gani unapata kigugumizi. Sitaki kuamini zile sababu zilizosemwa juzi kwa sababu yapo niliyokuomba na ukayafanya, kwa hiyo, nikuomba tena kwa mara hii stand ya Ngangamfumuni muweze kutupatia kibali na ujenzi huo uweze kuanza mara moja.

Mheshimiwa Mwenyekiti, la mwisho ni suala la Ben Saanane. Mimi ninatoka Mkoa wa Kilimanjaro na ni Mbunge wa Viti Maalum, akina mama wa mkoa ule wanaulizia Ben Saanane yupo wapi na leo Kiongozi wa Upinzani ameuliza swali hapa, tungependa kujua Ben Saanane alipo, na kwa taarifa walizosema ambazo sina hakika nazo tunataka taarifa sahihi, kama kweli Ben yupo basi tumpate na kama hayupo ni vizuri mkatuambia ili familia yake ijue kama wameshampoteza Ben kama alivyosema Mbunge wa Rombo walie.