Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 – Ofisi ya Makamu wa Rais, Muungano na Mazingira

Hon. January Yusuf Makamba

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Bumbuli

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 – Ofisi ya Makamu wa Rais, Muungano na Mazingira

WAZIRI WA NCHI, OFISI YA MAKAMU WA RAIS (MUUNGANO NA MAZINGIRA): Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nakushukuru sana kwa kunipa nafasi hii na nakupongeza kwa namna ambavyo umetuongoza tangu asubuhi. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nianze kwa kutoa shukrani kwa wote waliochangia katika hoja yetu, kwanza kwa Kamati zote mbili, lakini pia kwa wasemaji wote wawili wa Kambi ya Upinzani kwenye masuala ya Muungano na Mazingira. Tumepokea maoni ya Waheshimiwa Wabunge wote, kwa heshima na taadhima na moyo mkunjufu na ushauri mlioutoa tutaushughulikia. Wamechangia Wabunge 57 na kwa kweli kwa hoja ya siku moja kwa Wabunge 57 ni wengi, inaonyesha ni jinsi gani ambavyo kuna hamasa kubwa katika mambo haya.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna baadhi ya mambo ambayo tutayatolea majibu sasa na kuna mengine tutayatolea majibu kwa maandishi na kuwapelekea Waheshimiwa Wabunge kwa sababu muda tulionao hapa hautatutosha.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nimefurahi na kufarijika kwamba yanapokuja masuala ya mazingira Waheshimiwa Wabunge wote wa upande huu na upande ule tunaungana. Kwa hiyo, napata faraja kwamba katika vitu vinavyoliungasha Bunge ni hifadhi ya mazingira. Hiyo inafanya kazi yangu iwe rahisi. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, ninao marafiki wengi kwa upande ule kwa sababu ya masuala ya mazingira. Wapo watu ambao wanaonekana ni wakorofi kwa upande mmoja, lakini ukiingia ndani ya nyoyo zao ni wanamazingira wazuri sana hata Mheshimiwa Halima Mdee ni mwanamazingira mzuri sana, kwa hiyo, nawashukuru sana. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, imani yangu ni kwamba kwa kadri siku zinavyoenda kila Mbunge atakuwa mwanamazingira na hili linatupa faraja kubwa sana. Hii inatokana na hali halisi ambayo Waheshimiwa Wabunge wanaiona katika majimbo yao na huko wanakoishi kuhusu uharibifu wa mazingira. Imani yangu ni kwamba hamasa hii itapelekea uwekezaji mkubwa katika hifadhi ya mazingira nchini.
Mheshimiwa Mwenyekiti, niende haraka haraka kwenye hoja zilizotolewa. Kwanza, ni Mfuko wa Mazingira. Watu wengi wamezungumza kuhusu hili na nimesikitika kidogo dada yangu Mheshimiwa Dkt. Immaculate Sware ametulaumu kwamba miaka yote mfuko upo haujaanza, nilidhani kwamba angesema hongereni angalau kwa kuanza mwaka huu na ningependa utupe moyo na utuunge mkono kwa sababu ndio tumeanza na tunahitaji support yako. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, Waheshimiwa Wabunge wengi wameongelea namna ya kuupatia mfuko fedha. Sheria iliyoanzisha mfuko huu iko wazi kabisa vyanzo vimeainishwa humu. Katika nchi yetu zipo shughuli za kiuchumi na kiuzalishaji mali ambazo zinapelekea uharibifu wa mazingira. Kwa mfano, biashara ya mkaa ambapo Serikali inapata mapato, lakini biashara ile inaharibu mazingira; biashara ya magogo, Serikali inapata mapato lakini biashara ile inaharibu mazingira; uingizaji wa magari chakavu, Serikali ina-charge zaidi kwa shughuli hiyo lakini fedha hii haiji kwenye mazingira na uchimbaji wa madini vilevile kwenye leseni kuna fees zinatolewa. Kwa hiyo, sisi tunaongea na wenzetu wa Wizara ya Fedha kuona ni namna gani katika hizi shughuli ambazo zinaharibu mazingira lakini Serikali inapata tozo basi sehemu ya tozo ije kwenye Mfuko wa Mazingira. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, ukiangalia Sheria ya Mazingira katika kifungu cha 213 kinaelezea sources of funds kwa mazingira na kinasema; “(a) such sums of money as may be appropriated by Parliament.”
Mheshimiwa Mwenyekiti, kifungu hizi kinawapa nguvu Waheshimiwa Wabunge kuujaza mfuko huu pesa. Kwa hiyo, hatuna sababu ya kulalamika kuhusu fedha kidogo kwenye hifadhi ya mazingira wakati sisi wenyewe Wabunge tuna uwezo wa kuwa-appropriate pesa kwa ajili hiyo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, imezungumzwa hapa kuhusu suala la Baraza la Rufani. Na mimi nakubaliana na Mheshimiwa Mbunge aliyesema kwamba Waziri siyo kazi yako kupiga faini, ile ni kazi ya Mkaguzi wa Mazingira na imeandikwa kwenye sheria. Nakubaliana kabisa na yaliyoelezwa kwamba wewe ni mamlaka ya rufaa kwa anayepigwa faini na hata mimi nikifanya kitendo kile naweza kukatiwa rufaa kwenye Baraza la Rufaa. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini moja ya changamoto ya kutokuwepo kwa Baraza ni mfuko huu kutokuwa na pesa kwa sababu ukienda kwenye sheria kifungu cha 205 vyanzo vya fedha za Baraza la Rufani kinasema ni Mfuko wa Mazingira. Kwa hiyo, kama Mfuko wa Mazingira hauna fedha Baraza la Rufani halipo. Kwa hiyo, utaona kuna muunganiko wa ujenzi wa kitaasisi wa hifadhi na usimamizi wa mazingira. Kwa hiyo, tukilimaliza suala la Mfuko wa Mazingira tutakuwa tumemaliza suala la Baraza la Rufani vilevile. Nadhani Mheshimiwa Gekul ndiye aliyezungumzia jambo hilo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa ujumla kuhusu fedha kidogo kwenye hifadhi ya mazingira ukweli upo wazi, wote mnaona. Jawabu ni moja kupanga fedha zaidi na pili kuujaza mfuko. Hata hivyo, kuna jambo lingine tumelifanya na nimesema kwenye hotuba kwamba mwaka huu sasa tumefanikiwa kila Mamlaka ya Serikali za Mitaa, Sekretarieti ya Mkoa na Wizara itakuwa na kifungu kwenye bajeti kinaitwa kifungu cha hifadhi ya mazingira kwa sasa hakuna. Wenzetu watakapokuwa na vifungu hivyo wataamka na kupanga shughuli za hifadhi za mazingira.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini tunahangaika kutafuta ufadhili kwenye hifadhi ya mazingira kutoka kwa wenzetu sehemu mbalimbali. Tumeeleza asubuhi kwamba kwa jitihada za ofisi yetu tumeweza kufanikisha upatikanaji wa shilingi bilioni 230 kwa ajili na mradi wa maji. Tunaendelea na nataka niwahakikishie kama Mungu akipenda na kama tutaendelea kuwepo kwenye nafasi hizi nikisimama tena hapa mwakani, nitakuja na habari nzuri zaidi kuhusu upatikanaji wa fedha nyingi zaidi kutokana na ufadhili. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu viroba Mwanasheria Mkuu ameliongelea sina haja ya kurudia sana lakini napenda kukumbusha tu kwamba Serikali ilitoa taarifa ya kwanza kabisa ya dhamira yake ya kupiga marufuku viroba na mifuko ya plastiki Bungeni hapa kwenye bajeti ya mwaka jana mwezi Mei na mpaka shughuli ile imesimamishwa ilikuwa Machi 1 ni miezi kumi. (Makofi)
Kwa hiyo, sikubaliani kabisa na hoja kwamba hakukuwa na taarifa ya kutosha. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kilichokuwepo ni kwamba wenzetu kwa kuzoea ile habari kwamba Serikali ikisema haitendi kuna watu kabisa waliingiza mitambo wakatengeneza stock mpya. Ukienda kwenye Hansard hapa Bungeni utaona hilo, lakini tarehe 16 Agosti, pia tukatoa taarifa kwa umma kwamba tutapiga marufuku viroba tarehe 01 Januari 2017, lakini unakutana na mtu anakuambia mimi nimeingiza mzigo juzi. Sasa kama unaagiza mzigo wakati ukiwa na taarifa kwamba Serikali ina dhamira gani kuhusu biashara hiyo yanayokukuta ni kwamba umeamua wewe mweyewe yakukute. Licha ya hivyo, Serikali itaendelea kufanya mazungumzo na wafanyabiashara hawa ili kuangalia utaratibu nzuri wa namna ya kumaliza kabisa shughuli hii. Wote tunakubaliana kuna manufaa makubwa zaidi kwenye kupiga marufuku shughuli hii kuliko kuacha iendelee, hilo halina ubishi. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu upandaji miti, Waheshimiwa Wabunge wengi wamezungumza kuhusu utaratibu wa upandaji miti hapa nchini. Tunafahamu kwamba tangu uhuru nchi yetu imefanya jitihada mbalimbali za kupanda miti, lakini hatukupa mafanikio ya kuridhisha. Mkakati mpya tulioutengeneza umezingatia sababu za kufeli kwa mipango ya siku za nyuma, umeshirikisha sekta binafsi na mamlaka zote, tumeandika kila kata hapa nchini inastawi mti gani na unapaswa kupandwa wakati gani. Mkakati huo tutautoa kwa ajili ya kuelimisha Wabunge na wananchi jinsi ya kuutekeleza.
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini hapa nchini idadi ya miti yote iliyopo asilimia kumi tu ndiyo ya kupanda asilimia 90 ndio miti ya asili inayoota yenyewe. Kwa hiyo, namna nzuri ya kuwa na miti hapa nchini ni kuhifadhi ile ambayo tunayo tayari, ile miti ya asili. Kwa sehemu kubwa nchi yetu ina miti ya miyombo ambayo inaamka kwa haraka zaidi pale inapoachwa ikue. Kwa hiyo, kikubwa zaidi ni kuacha kupanda miti na kupanda miti vilevile lakini matumaini makubwa yapo kwenye kuhifadhi miti na misitu tuliyo nayo. Ipo miradi mingi zaidi na taratibu nyingi tutazitumia.
Mheshimiwa Mwenyekiti, dada yangu Mheshimiwa Pauline amesema asubuhi kwamba kuna harufu ya kifisadi kwenye baadhi ya miradi, lakini hakutusaidia kwamba ni katika eneo gani hasa kwa sababu ufisadi upo wa namna nyingi. Je, ni kwenye procurement au malipo? Namwomba hata kwa kuninong’oneza anieleze ili nilishughulikie jambo hili kwa sababu ni jambo hatutaki liwepo kwenye ofisi yetu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka niwakikishie kwamba miradi hii kwa masharti ya ufadhili wake kila mwaka inakaguliwa na Mkaguzi na Mdhibiti Mkuu wa Serikali. Kumefanyika ukaguzi 2013/2014, 2014/2015 na ripoti ya 2016 inakuja na wamejiridhisha kabisa kwamba miradi ile iko safi kabisa na inatekelezwa kwa kiwango kilichotarajiwa. Kwa hiyo, sisi tunaamini kabisa kwamba hakuna tatizo lolote lakini kama dada yangu Mheshimiwa Pauline una taarifa naomba unijulishe ili nianze kufuatilia hapo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Waheshimiwa Wabunge wengi wamezungumzia kuhusu matumizi ya mkaa. Matumizi ya mkaa ni changamoto kubwa na ni sababu kubwa inayopelekea uharibifu wa mazingira nchini mwetu. Sisi kama Ofisi ya Makamu wa Rais tumeamua kuchukua leadership kwenye jambo hili kwa sababu ndugu yangu na mzee wangu Mheshimiwa Profesa Maghembe mkaa kwake ni chanzo cha mapato, wakati mimi kwangu mkaa ni uharibifu wa mazingira. Mimi nina interest kubwa zaidi nchi yetu ika- transition kutoka kwenye matumizi ya mkaa kwa sababu kwa kadri siku zinavyoenda nishati za kupikia mbadala zinaendelea kuwa nafuu na zinaweza kushindana kwenye soko la mkaa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, sisi tulifanya kongamano kubwa ambalo tuliliongoza na wadau wote wa utengezaji wa mkaa. Tumeamua kuanzisha shindano kubwa kabisa la kitaifa na wale majasiriamali wote wanaoweza kutengeneza nishati mbadala waje watuonyeshe tutawapa zawadi. Zawadi ya kwanza kabisa itakuwa zaidi ya shilingi milioni 400 na tutawawezesha kupanua biashara yao hiyo, viwanda vya mkaa vitaanzishwa ili taratibu tuondoe mkaa kwenye soko siyo kwa kuupiga marufuku bali kwa kuufanya ushindwe kwa bei na nishati nyingine. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nafahamu kwamba kuna Wakuu wa Wilaya na baadhi ya maeneo wamepiga marufuku usafirishaji wa mkaa kutoka kwenye maeneo yao ni hatua njema. Hata hivyo, lazima twende nayo taratibu kwa sababu mji kama Dar es Salaam ambapo asilimia 60 ya mkaa unatumika Dar es Salaam na pale hakuna sehemu unaweza kuzalisha mkaa, kwa hiyo, lazima tuwezeshe watu kupata nishati inayolingana na bei ya mkaa ndipo tuweze kupinga marufuku kabisa matumizi ya mkaa. Huko ndiko tunakoelekea, hii road map ambayo tunakuja nayo itaeleza miaka mingapi na kwa utaratibu gani tutaondoa matumizi ya mkaa hapa nchini. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini niseme tu pia katika mkaa unaozalishwa nchini kwa sehemu kubwa mkaa huo unakwenda kuchoma nyama Uarabuni. Ukienda kwenye bandari zile za Bagamoyo, Mbweni majahazi na majahazi yamejaa mkaa unaenda Unguja. Unguja haiwezi kutumia mkaa wote ule unaoenda kule, ukifika Unguja unapanda tena unaenda Mombasa - Shimoni. Ukifika kule unawekwa kwenye magunia mazuri made in Kenya unaenda kuchoma nyama Uarabuni. Nataka niombe ruhusa ya Mheshimiwa Rais niende Kenya nikazungumze na wenzetu ili tuweze kuona namna gani tunaweza kushirikiana pamoja na Wizara Maliasili kupiga kabisa marufuku suala hili. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, Waheshimiwa Wabunge wengi wameongelea kuhusu namna tunavyoweza kuzibalisha taka ngumu ziwe rasilimali. Sisi kwenye ofisi yetu hazipiti wiki mbili tunapokea mwekezaji, mapendekezo, proposal ya mtu anayetaka kuzalisha umeme kwa kutumia taka. Bahati mbaya sana hawa watu wanaoleta hii miradi wanazunguka sana hawajui pa kuanzia. Wengine wanaanzia TANESCO, wengine Wizara ya Nishati, wengine TAMISEMI, wengine wanakuja kwetu na wengine wanakwenda EWURA. Kwa hiyo, matokeo yake ni kwamba hapa nchini mpaka sasa hakuna mradi uliofanikiwa kwa sababu hakuna mwongozo
na utaratibu wa kushughulikia miradi hii wakati taka zipo nyingi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo Mheshimiwa Makamu wa Rais mwezi Mei ataitisha kikao ambacho kitakuwa ni kati ya sisi Wizara ya Nishati, TAMISEMI Halmashauri za Majjiji zote EWURA na TANESCO na kikao hicho ndicho kitaamua kuhusu mwongozo wa kukaribisha uwekezaji wa sekta binafsi kwenye shughuli ya kuchakata kata. Kwa wale Waheshimiwa Wabunge ambao wamekuwa na hoja hizi, naomba wawe na subira Serikali itatoa mwongozo kutoka kwenye Ofisi ya Makamu wa Rais kuhusu namna gani tunaweza kurahisisha na kuharakisha uwekezaji wa sekta binafsi katika kuchakata taka.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu mazingira ya bahari na pwani, Waheshimiwa Wabunge wengi wamezungumza kuhusu mambo mawili. Kwanza, uvuvi haramu lakini pili watu wanaokaa pwani wanajua jinsi fukwe zinazovyoliwa kutokana na mabadiliko ya tabianchi. Sisi ofisi yetu inao mkakati, Mheshimiwa Ghasia na Waheshimiwa wengine wameongea, mtakumbuka miezi mitatu iliyopita ofisi yetu sisi na mimi niliongoza nilikuwa Mwenyekiti wa kikao cha Mawaziri kama sita hivi tena wazito, Mheshimiwa Mwinyi, Mheshimiwa Mwingulu, Wizara ya TAMISEMI na Maliasili ambapo tulikaa na kutengeneza mkakati wa pamoja wa kukabiliana na uvuvi haramu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika wiki chache zijazo mtaona operesheni kubwa ya Kiserikali, tusingependa kuizungumza kwa sababu tunakabiliana na watu wanaofanya kazi shughuli haramu ambayo itamaliza kabisa tatizo hili la uvuvi haramu. Vilevile tutaendelea kutafuta fedha kwa ajili ya kugharamia miradi ya mabadiliko ya tabia nchi katika maeneo ya kanda za Pwani kwa kujenga kuta kama tunavyojenga pale Ocean Road, Pangani, Kigamboni na Zanzibar lakini kupanda mikoko kama tunavyofanya kule Rufiji. Kwa hiyo, tunaendelea kutafuta fedha nyingi kwa ajili hiyo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu mchango wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Serikali ya Mapinduzi Zanzibar kwa Zanzibar, Mheshimiwa Shamsi Vuai Nahodha na Mheshimiwa Ali Hassan Omar King wameongelea, hii ndiyo dhamira yetu. Ule mradi aliouongelea Mheshimiwa Shamsi nimechukua mawazo yale na tutaupanua na kuukuza. Shida kubwa ya wavuvi wadogo ni kuweza kufika mbali. Kwa hiyo, ili uwasaidie, usiwasadie kwa namna ambayo wataendelea kufika pale pale karibu. Kwa hilo, tumelichukua na tutalifanyia kazi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini pia tunaamini kwamba mchango wa Tanzania Bara kwa maendeleo ya Zanzibar siyo wa Serikali peke yake bali hata mfumo wa uchumi unaowezesha biashara kubwa zaidi na rahisi zaidi kwa pande zote mbili ili Zanzibar uchumi wake uhamasike zaidi kutokana na kuwa karibu na sehemu yenye uchumi mkubwa zaidi. Kwa hiyo, tutaendelea kushirikisha wenzetu wataalam wa biashara na uwekezaji ili tuweze kukamilisha hilo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Muungano is a fact of life yaani lazima tukubaliane wote hapa na hata kama hukubali na kama viongozi lazima tuwe honest kwamba hatuna namna nyingine zaidi ya Muungano. Mwingiliano ni mkubwa, ni wa muda mrefu na gharama ya kuuondoa ni kubwa zaidi kuliko juhudi tunazoweza kuzitumia kuzirekebisha. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, nadhani uwekezaji kwenye kuimarisha Muungano ni muhimu zaidi kuliko tafakuri ya namna tunavyoweza kuachana. Kwa hiyo, napenda juhudi za wanasiasa wa pande zote mbili ziwe katika kuuimarisha Muungano huu. Mnanifahamu mimi ni mtu ambaye sina tatizo na mawazo ya aina yoyote na hakuna hoja inaweza kutufarakanisha au kututenganisha kwenye Muungano. Kwa hiyo, siasa nzuri zaidi ndugu zangu siyo siasa ya kuubeza Muungano ni ya kujenga, siasa nzuri zaidi siyo ya kuupa jina baya ili uhalalishe kuumong’onyoa. Siasa nzuri ni kuupa hadhi yake unaostahili ili tuweze kuwekeza katika juhudi za kuuimarisha.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Ally Saleh amesema kwamba utaratibu wa kutatua kero haufai, lakini nitaka nimwambie tu kwamba utaratibu huu wa tangu mwaka 2006 ndiyo umetupunguzia kero kutoka 15 mpaka tatu sasa hivi. Kwa hiyo, ndugu yangu kama kuna mawazo ya utaratibu bora zaidi sisi tuko wazi kabisa na mimi nipo tayari kupokea mawazo kuhusu utaratibu bora wa kushughulikia kero za Muungano kwa sababu nchi hii ni yetu sote na mawazo bora zaidi ya kuimarisha Muungano ofisi yetu inayapokea. Kwa hiyo, tupendekeze tu kama yapo mawazo mengine.
Mheshimiwa Mwenyekiti, baadhi ya Waheshimiwa Wabunge wamezungumza kuhusu kukauka kwa mito, vyanzo vya maji na maziwa, ni kweli. Katika ziara zangu nchini nafanya makusudi kutembelea vyanzo vya maji, maziwa na mito. Nimetembelea Ziwa Tanganyika, Ziwa Jipe, Chala, Natron, Manyara, Eyasi na nimejionea mwenyewe jinsi gani tunavyoelekea kwenye kuangamia.
Waheshimiwa Wabunge, ninaposema kuelekea kuangamia ninamaanisha hivi, ukienda kule Jipe utaona zile jamii za pale hata aina ya samaki wanazovua ni visamaki vidogo, mtu akitaka kwenda kuvua ni lazima apite kwenye magugu yaliyojaa kwenye ziwa. Lile ziwa nusu liko upande wa Tanzania na nusu liko upande wa Kenya. Ukipiga picha ziwa lile utaona upande wa Tanzania ndiyo kumejaa magugu, upande wa Kenya kuna hoteli pembeni ya ziwa watu wanaogelea, hii ni aibu kubwa kwa nchi yetu na hii tunafanya wenyewe. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, sisi kama Ofisi ya Makamu wa Rais tumeamua kwamba tutaanzisha mradi mkubwa kabisa wa kitaifa wa kutunza maziwa madogo madogo katika nchi yetu. Nimewaambia kabisa wataalam wa Wizara nitawapa likizo ya wiki tatu wakakae mahali waandike mradi wa maziwa madogo nane hapa nchini na namna tunavyoweza kuyahifadhi. Kwa hiyo, tutawaletea taarifa hiyo tutakapokuwa tumekamilisha. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka niwaambie hali ya uharibifu wa vyanzo vya maji ni kubwa sana tutapoteza mito katika nchi hii. Waheshimiwa Wabunge, naomba niseme, watoto na wajukuu zetu watakuja kutushangaa sisi tulikuwa ni watu wa namna gani ambao tulikuwepo na kushuhudia na kuwezesha upoteaji wa kitu kama mto, unawezeshaje mpaka mto upotee? Kwa hiyo, ngoja niishie hapo nisije nikasema maneno mabaya. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu NEMC, Waheshimiwa Wabunge wamesema kwamba kuna haja kubwa ya kujenga uwezo wa NEMC na hilo tunalifanya. Ni taasisi ambayo imepewa mamlaka makubwa lakini uwezo wake wa kitaasisi na fedha hauendani na majukumu iliyopewa na sheria. Kwa moja ya kazi yetu sisi ni kujenga uwezo wa taasisi hii ili iendane na hadhi na heshima ya taasisi yenyewe.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye nchi nyingine Mkurugenzi Mkuu wa NEMC analindwa kutokana na kazi kubwa anayoifanya. Nchi hii Mkurugenzi Mkuu wa NEMC anaweza akapita kantini hata hujui ni nani wakati ni taasisi kubwa yenye mamlaka makubwa kabisa inayoweza kuzuia hata ndege zisiruke kwa sheria hii. Mkurugenzi Mkuu wa NEMC anaweza akasema Emirates isiondoke mpaka nijihakikishie kwamba haivujishi mafuta, ndiyo nguvu ya kisheria ya taasisi zetu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo sisi moja ya majukumu yetu tangu tulipoingia Wizarani ni kujenga uwezo wa kitaasisi, ndiyo maana tumefufua Mfuko na Baraza la Rufaa. Watu wa NEMC mkiongea nao watawambia, NEMC tuliyoikuta na NEMC ya sasa kama alivyosema Naibu Waziri ambayo ilikuwa inakusanya shilingi bilioni 5 sasa hivi 12 ni tofauti. Kazi hiyo itaendelea na katika siku chache zijazo mtasikia kazi tutakayoifanya NEMC ya kubadilisha mambo pale.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Mzee wangu Mheshimiwa Nsanzugwanko ananiangalia sana nataka niseme jambo lake, mwaka jana wakati tunawasilisha bajeti hapa, Mheshimiwa Nsanzugwanko na Mheshimiwa Bilago walisimama na kushika mshahara kwa kusema kwamba hatujazungumza lolote kuhusu uharibifu wa mazingira unaofanywa na wakimbizi. Nataka niwaambie kwamba baada ya lile jambo mimi nikafanya safari kwenda kwenye kambi za wakimbizi, bahati mbaya sikusema kwenye hotuba na nikatembelea Nyarugusu, Makere, Mtabila na vijiji vyote vinavyozunguka kambi za wakimbizi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nikawaita wakuu wote wa UNHCR kule Kigoma na nikawapa maelekezo yafuatayo siyo kwa mdogo ni kwa barua. Kwanza, makambi yote ya wakimbizi Tanzania yafanyiwe EIA. Sheria yetu inasema, maeneo ya makazi makubwa lazima yawe na environmental impact assessment lakini nilistajabishwa kwamba makambi yale yalikuwa hayana environmental impact assessment. Kwa hiyo, kwanza tukawapiga faini kwamba hawakuwa na EIA lakini pia tukawalazimisha wafanya EIA ambayo itatoa masharti ya matumizi ya eneo lile ikiwemo hifadhi ya mazingira, hilo ni agizo la kwanza nililowapa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, agizo la pili nililowapa, ni kwamba walikuwa na pilot project ya kuwapa majiko ya gasi wakimbizi. Tukasema kwanza isiwe pilot iwe ni mradi, lakini usiishie kwa wakimbizi bali uishie pia kwa jamii inayozunguka kambi hizo ili wasikate kuni. Agizo la tatu nililowapa ni kwamba wachangie kwenye miradi ya maendeleo katika vijiji vinavyozunguka makambi ya wakimbizi. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, najua alininong’oneza kwamba atashika tena mshahara lakini naamini taarifa hii itamridhisha na ataachia mshahara wangu kwa sababu kazi tumefanya na tunafuatilia. Ulinituma na nimeenda.
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini pia ulisema kwamba Kasulu kuna tatizo la vyanzo vya maji na tumepeleka timu na tutaandika mradi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, Waheshimiwa Wabunge, naomba nimalize kwa kusema kwamba kazi tuliyopewa na Taifa ya kusimamia uimara wa Muungano tunaifanya vizuri, naamini kabisa kwamba katika kipindi cha mwaka mzima uliopita, hamjasikia kelele, malalamiko kuhusu Muungano kama mlivyokuwa mmezoea kusikia siku za nyuma. Hili jambo halijatokea kwa ajali kwamba watu wamelala ni kwamba kuna kazi imefanyika ya kuhakikisha kwamba tunapunguza kero na malalamiko. Muungano na jina baya la Muungano halipo tena kwenye vichwa vya habari. Hii siyo kwa sababu akina Mheshimiwa Ally Saleh wanachapana bakora kule hapana, hii ni kwa sababu tumefanya kazi. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini pia wote mnafahamu kwamba hifadhi ya mazingira kama alivyosema Naibu Waziri na Mwenyekiti imeongezeka na tutaendelea kufanya kazi kubwa, naomba muendelee kutuamini na kutuwezesha. Kama mnavyojua sisi ni rafiki wa watu wote na kwa maneno hayo, nategemea hatutapata shida sana kwenye kupitisha bajeti. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nawashukuru wote waliochangia na naomba kutoa hoja.