Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 – Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano

Hon. Mariamu Nassoro Kisangi

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 – Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano

MHE. MARIAM N. KISANGI: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi na mimi niwe mchangiaji katika Wizara hii muhimu. Kwanza naomba niipongeze Serikali ya Chama cha Mapinduzi, Mheshimiwa Rais, Waziri Mkuu, Makamu wa Rais, Mawaziri wote wa Serikali pamoja na Makatibu Wakuu wote kwa utendaji wao mzuri uliotukuka. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, napenda niwaambie wenzangu wanaosema kwamba Serikali ya Chama cha Mapinduzi haikutimiza ilani zake; nawaambia Serikali ya Chama cha Mapinduzi imetimiza ilani yake kwa kiasi kikubwa ndiyo sababu wakachaguliwa Wabunge wengi wa Chama cha Mapinduzi kutoka katika majimbo mbalimbali, lakini pia wakachaguliwa Madiwani wengi wa Chama cha Mapinduzi kutoka katika kata mbalimbali, lakini pia Halmashauri nyingi zimeongozwa na Madiwani, Wenyeviti wa Chama cha Mapinduzi. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, ukweli ni kwamba Serikali ya Chama cha Mapinduzi inafanya mambo mazuri sana. Napenda nimpe pongezi za kipekee Rais wetu, Mheshimiwa Dkt. John Pombe Magufuli, kwa kazi kubwa anayoifanya katika Mkoa wetu wa Dar es Salaam toka kuchaguliwa kwake. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Rais wetu alipochaguliwa tu, alifanya upanuzi wa haraka wa barabara ile ya Morocco kwenda Mwenge. Pia alifanya ufunguzi wa Daraja la Kigamboni, daraja muhimu sana; alizindua ujenzi wa flyover ya TAZARA, mradi ambao unagharimu shilingi bilioni 99; alifungua mradi wa mabasi yaendayo kasi ambayo yamekuwa msaada mkubwa sana kwa wananchi wa Dar es Salaam ambao walikuwa na tatizo kubwa la msongamano wa magari.
Mheshimiwa Naibu Spika, pia Mheshimiwa Rais alifanya mapokezi ya ndege mbili za Bombadier katika Uwanja wa Ndege wa Dar es Salaam; alizindua mradi wa interchange ya Ubungo, mradi ambao unagharamia pesa kiasi cha shilingi bilioni 177; alizindua ufunguzi wa mradi wa ujenzi wa Mabweni ya Chuo Kikuu cha Dar es Salaam; amefungua ujenzi wa reli ya standard gauge kule Pugu, Dar es Salaam, mradi ambao utatumia pesa takribani USD bilioni 1.2; hilo siyo suala dogo. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Rais pia alizindua ujenzi wa nyumba za wakazi wa Magomeni; ametoa pesa katika mradi wa Uwanja wa Ndege wa Dar es Salaam ili ukamilike kwa haraka, hiyo siyo kazi ndogo. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, leo nawaomba wananchi wangu wa Mkoa wa Dar es Salaam, nami ndio Mbunge wenu kutoka Chama cha Mapinduzi, mlionileta Bungeni nije niwawakilishe, nawaambieni Serikali hii imeamua kwa dhati kabisa kuhakikisha Mkoa wa Dar es Salaam sasa unakuwa mkoa wa utalii, miundombinu yote inaboreka, ndege tumepata; lakini kubwa mimi nilipoingia katika Bunge hili kipindi kilichopita, nilizungumzia juu ya Uwanja wa Ndege wa Dar es Salaam…
TAARIFA...
Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana kwa kunitolea ufafanuzi, maana anaelewa Mwalimu mwenzangu, anajifanya haelewi.
Mheshimiwa Naibu Spika, nasema hivi, Serikali ya Tanzania inaongozwa na Mheshimiwa Rais wa Chama cha Mapunduzi na itaendelea kuwa Serikali ambayo inatekeleza Ilani ya Chama cha Mapinduzi na yeye Mheshimiwa Waitara anatakiwa atekeleze Ilani ya Chama cha Mapinduzi, atake asitake afanye hivyo. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba sasa niendelee. Tunataka kujengewa nyumba za wakazi wa Magomeni na tumesikia kilio cha wananchi wale, jinsi walivyokuwa wanalia kwa kunyanyaswa kuondolewa katika maeneo yao. Wananchi wale leo Mheshimiwa Rais ameona kilio chao; ameamua kwa dhati ya moyo wake kuhakikisha anawapatia makazi bora wananchi wale wa Magomeni. Siyo jambo dogo, ni jambo ambalo sisi kama Wabunge wa Dar es Salaam, tena nampongeza sana Mbunge wangu wa
Kinondoni kwamba yeye alishiriki pamoja na kwamba yuko Upinzani, alishirikiana na Mheshimiwa Rais akaenda pale kwenye uzinduzi wa nyumba zile, hiyo ndiyo siasa. Wanasiasa tufike sehemu, pale yanapofanyika mazuri tuunge mkono, siyo kila kitu tunapinga tu. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, nampongeza na kumshukuru Mheshimiwa Rais kwa hilo tena nasema zile nyumba azijenge kwa haraka, wananchi wale wakae. Sambamba na hao, wananchi wa Ilala Mchikichini nao wanazisubiri kwa hamu nyumba hizo wajengewe na wananchi wa Temeke mwisho nao wanazisubiri. Nimwambie Mheshimiwa Rais na Wizara na Mawaziri, kazeni buti, fanyeni kazi, tekelezeni Ilani ya Chama cha Mapinduzi. (Makofi/ Kicheko)
Mheshimiwa Naibu Spika, katika Wizara hii sasa, nitajikita katika maeneo yafuatayo; kwanza nitachangia katika barabara, bandari, uwanja wa ndege, reli na mawasiliano.
Mheshimiwa Naibu Spika, katika upande wa barabara, naomba kabisa Serikali pamoja na kumsikia Mheshimiwa Waziri kwamba kuna mpango wa ujenzi wa flyover ya Charambe, naiomba Serikali mpango huo utekelezeke kwa sababu idadi ya watu Mbagala imekuwa kubwa. Kuna msongamano mkubwa kutoka kwenye round about ya Mbagala Rangitatu kuelekea Charambe, Chamazi na Mbande. Mpango huo ukitekelezwa, basi Mbagala yetu sasa nayo itaendelea kuwa vizuri. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba barabara inayotoka kwenye Daraja la Kigamboni kuelekea Kibada na Kigamboni, hiyo sasa ifanyiwe kazi kwa haraka kwa sababu wakati huu wa mvua barabara hiyo ilikuwa tatizo. Pamoja na daraja zuri tulilojengewa na Serikali, lakini pale upande mwingine kumalizia kile kipande, naiomba Serikali kwa kupitia NSSF wawaamrishe wafanye kwa haraka sana ujenzi ule ukamilike. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba Serikali iangalie ujenzi wa barabara ya Nzasa – Kilungule kuvuka kwenda Buza. Barabara hiyo itaungana na ile barabara ya Jet – Davis Corner inayotoka Jet inakwenda Davis Corner. Barabara hiyo ni msaada mkubwa kwa wananchi. Barabara hiyo inawasaidia watu ambapo kunapokuwa na msongamano mkubwa Mbagala Rangitatu, wanaotoka kwenda Airport wanapita Nzasa wanashuka Bondeni wanaunganisha Buza wanaenda wanakutana na ile barabara mpaka Jet, mtu anakwenda uwanja wa ndege kwa haraka sana. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, naiomba Serikali, mara nyingi barabara hii imekuwa ikiingizwa kwenye mipango, inatoka; mara inaenda kwenye mpango mwingine. Naiomba sasa Serikali, kupitia Mheshimiwa Waziri wangu akaisimamie, barabara hii ni msaada mkubwa kwa wakazi wa Mbagala. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba sasa Serikali iangalie uwezekano wa kujenga barabara kutoka Mbande kwenda Mipeku - Mkuranga. Wananchi wanapata shida sana hususan akina mama wajawazito, magari hayapiti hata yenye four wheel, lakini wanabebwa kwenye pikipiki kuja Mbande kupata huduma ya afya ya mama na mtoto. Naomba barabara hiyo ijengwe. Ikijengwa barabara hiyo, itakuwa mkombozi mkubwa kwa wananchi wanaotoka Mipeku kuja kupata huduma za afya, hasa akina mama kwenye hospitali au dispensary ya Mbande, Temeke. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba sasa nizungumzie upande wa bandari. Pamoja na kazi kubwa inayofanywa na bandari na hasa ile ambayo inaendelea kufanywa ya kuongeza kina cha bandari kutoka geti namba moja mpaka namba saba, lakini naomba sasa bandari itueleze ajira ndogo ndogo zinazotolewa na bandari kwa vijana, nataka mpango wa ajira ndogo ndogo…
(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)
Mheshimiwa Naibu Spika, naunga mkono hoja. Naipongeza sana Serikali, Mheshimiwa Waziri, Manaibu Waziri wote wa Wizara ya Uchukuzi. Fanyeni kazi kwa bidii.