Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Mpango wa Pili wa Maendeleo wa Taifa kwa kipindi cha Miaka Mitano kuanzia mwaka 2016/2017 – 2020/2021

Hon. January Yusuf Makamba

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Bumbuli

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Mpango wa Pili wa Maendeleo wa Taifa kwa kipindi cha Miaka Mitano kuanzia mwaka 2016/2017 – 2020/2021

WAZIRI WA NCHI, OFISI YA MAKAMU WA RAIS, MUUNGANO NA MAZINGIRA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa kunipa fursa na nianze kwa kutoa pongezi kubwa kwa Wizara ya Fedha na Mipango kwa kuandaa Mpango madhubuti waliouwasilisha hapa Bungeni. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, mwaka jana tulienda kwenye uchaguzi na kila chama kilitoa ahadi kwa Watanzania. Watanzania wakakiamini Chama cha Mapinduzi na wakaamini kwamba ahadi za CCM ndizo zinazotekelezeka, jukumu la kwanza kabisa la chama kinachoshinda uchaguzi ni kuunda Serikali. Kwa hiyo, Serikali imeundwa, Serikali imara na Serikali madhubuti. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, jukumu la kwanza la Serikali iliyoundwa baada ya uchaguzi ni kutengeneza mpango unaotafsiri Ilani na ahadi za chama kilichoshinda. Hilo ndilo tunalolifanya sasa. Jukumu la pili la Serikali iliyoshinda ni kutengeneza bajeti za kila mwaka za kutekeleza mpango ambao tumesema unatafsiri ilani na ahadi za chama, hilo ndilo linalokuja katika kikao hiki. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo mantiki ya kawaida inasema kwamba kama wenzenu wameshinda, wameunda Serikali, wametengeneza mpango ambao unatafsiri yale yaliyowafanya washinde, wenzenu mnapaswa kuwapa nafasi watekeleze mipango yao na bajeti yao. Wanaposhindwa baada ya miaka mitano au katikati tunapofanya tathmini ndipo tunapokuja na kusema ninyi mmeshindwa. Hatuwezi wakati tunatengeneza mpango wetu ambao unatafsiri yale tuliyowaahidi Watanzania tunasimama tunasema ninyi kile, ninyi kile, ninyi hiki. Tupeni nafasi, ni Serikali mpya, tutekeleze ya kwetu katika mwaka wa kwanza kabisa wa Serikali hii ndipo tuje tuzungumze yale ambayo...
Mheshimiwa Naibu Spika na Waheshimiwa Wabunge, kwa staili na kasi ya Serikali hii ya Awamu ya Tano hakuna hata chembe ya shaka kabisa kwamba yale tuliyoyaahidi, tuliyoyaandika katika Mpango wetu huu na katika bajeti tutakayoileta yatatekelezwa kwa ukamilifu. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, tukitazama sura, kauli, umakini wa Rais wetu na Wajumbe wa Baraza lake la Mawaziri na Wabunge wa upande wa CCM kwa ujumla, hakuna shaka yoyote kwamba tumedhamiria kutengeneza nchi mpya. Tumedhamiria kutengeneza Taifa jipya, Taifa lenye haki, Taifa lenye usawa na Taifa lenye heshima. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, huko nyuma katika miaka mingi tulijaribu kutengeneza Taifa la namna hiyo…
MHE. MCH. PETER S. MSIGWA: Mheshimiwa Naibu Spika Taarifa!..
WAZIRI WA NCHI, OFISI YA MAKAMU WA RAIS, MUUNGANO NA MAZINGIRA: Mheshimiwa Naibu Spika, kwa heshimia na taadhima napenda kuikataa taarifa hiyo na napenda kuikataa bila kueleza sababu, sababu za kuikataa ni dhahiri kabisa. Isingependeza kupoteza muda kueleza sababu za kuikataa kwa sababu zinaeleweka. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika naomba niendelee …
NAIBU SPIKA: Waheshimiwa Wabunge, naomba basi tusikilizane!
WAZIRI WA NCHI, OFISI YA MAKAMU WA RAIS, MUUNGANO NA MAZINGIRA: Mheshimiwa Naibu Spika, kwa aina ya taarifa iliyotolewa haistahili hata kuielezea kwa nini naikataa. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba niendelee kwa kueleza kuhusu mazingira. Nashukuru sana kwamba katika Bunge hili kuna Wabunge wengi wanamazingira na naomba sana tutakapoleta bajeti yetu ya Ofisi ya Makamu wa Rais tutatoa dira mpya na mwelekeo mpya wa namna ya kulinda na kuhifadhi mazingira ya nchi yetu, tunaomba mtuunge mkono. Tutaeleza namna tunavyotaka kujenga uwezo wa kitaasisi wa Serikali na uwezo wa kifedha wa Serikali katika kugharamia shughuli za ulinzi wa mazingira. (Makofi)
Mwisho ni kuhusu Muungano, kuhusu Uchaguzi wa Zanzibar. Vitabu vinavyotuongoza kuhusu suala la Zanzibar kwa maana ya Katiba ya Zanzibar na Sheria ya Uchaguzi ya Zanzibar vinatuelekeza kwamba jambo hili limekwisha. Suala hili limekwisha, treni imeshaondoka kwenye kituo, wenzetu hawakushiriki, wamefanya uamuzi wa kimkakati ambao umewaondoa katika ushiriki wa siasa na maendeleo ya Zanzibar. Ni uamuzi wao, ni uamuzi ambao wataendelea kuujutia.
Mheshimiwa Naibu Spika, sisi kama CCM tunaamini kwamba ujenzi wa Taifa letu kwa ujumla ni jukumu letu sote na tunawakaribisha wenzetu hata kama wako nje ya Serikali kuendelea kushirikiana na sisi kuijenga Zanzibar na kuijenga Tanzania. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana.