Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 – Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano

Hon. Vedasto Edgar Ngombale Mwiru

Sex

Male

Party

CUF

Constituent

Kilwa Kaskazini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 – Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano

MHE. VEDASTO E. NGOMBALE: Mheshimiwa Naibu Spika, nikushukuru kwa kunipa nafasi ili basi na mimi niweze kuchangia katika hotuba hii ya Wizara ya Miundombinu.
Mheshimwia Naibu Spika, kabla sijaanza nichukue nafasi hii kutoa pole kwa majirani zangu wa Rufiji kwa mafuriko maana kuanzia jana Mto Rufiji umefurika, kwa hiyo, nitoe pole sana, hata yale maghorofa yetu yote yameanguka chini.
Mheshimiwa Naibu Spika, nianze na mawasiliano. Katika Jimbo langu la Kilwa Kaskazini kuna kata ambazo bado hazijapata mawasiliano ya simu; kuna Kata za Kibata, Kandawale na Kijumbi hazijapata mawasiliano ya simu, lakini pia kuna vijiji vya Namakolo na Chapita katika kata ya Namayuni havijapata mawasiliano ya simu. Katika kata ya Kipatimu kuna kijiji cha Nkarango na kijiji cha Nandete havijapata mawasiliano ya simu. Niishauri Serikali ijitahidi maeneo hayo niliyoyataja yaweze kupata mawasiliano ya simu.
Mheshimiwa Naibu Spika, barabara; nianze na barabara ya kutoka Nangurukuru kwenda Liwale ambayo ina kilometa 230. Barabara hii ina umuhimu katika mambo makuu matatu; kwanza ni barabara ambayo imepitia katika majimbo matatu, Jimbo la Kilwa Kusini, Jimbo la Kilwa Kaskazini na Jimbo la Liwale, lakini la pili ni barabara ambayo imepita katika Hifadhi yetu ile ya Selous. Kwa hiyo, barabara hii kama ingekuwa imetengenezwa ingetusaidia sana katika utalii. Pia la tatu Waheshimiwa Wabunge tusijisahau, nyakati zile za uchaguzi Wabunge wengi huelekea maeneo ya Liwale, maeneo ya Ngende kwa sababu ya mambo yetu yale, mimi nafikiri ninyi mnayafahamu, lakini cha kushangaza ni kwamba barabara hii inasahaulika. Kwa hiyo, niiombe Serikali, barabara hii ni muhimu sana. (Kicheko)
Mheshimiwa Naibu Spika, wakati mwingine nashangaa ni vigezo gani vinatumika kuamua sasa ni barabara ipi ijengwe kwa kiwango cha lami? Kutoka Nangurukuru mpaka Liwale ni mbali sana, Wilaya ya Liwale iko pembezoni kabisa na katika Ilani ya Chama cha Mapinduzi ilieleza kwamba ingefanya upembuzi yakinifu lakini nimeangalia katika hotuba hakuna chochote kilichopangwa. Kwa hiyo, Mheshimiwa Waziri, nikuombe basi uwafikirie wale watani wangu Wangindo na sisi Wamatumbi ili basi na sisi tufaidi matunda haya ya uhuru. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, barabara ya Kwankocho – Kivinje. Barabara hii ni ya urefu wa kilometa tano na ni ahadi ya Rais wa Awamu ya Nne, Mheshimiwa Jakaya Mrisho Kikwete. Barabara hii inaunganisha barabara inayokwenda Kilwa Masoko na Hospitali ya Wilaya ya Kinyonga pamoja na Mji wa kitalii wa Kilwa Kivinje. Barabara hii imeahidiwa lakini mpaka sasa hakuna chochote kilichofanyika. Niiombe Serikali iijenge barabara hii kwa kiwango cha lami ili basi tupate urahisi wa kwenda katika hospitali ile ya Wilaya ya Kilwa Kivinje. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, Barabara ya Njianne – Kipatimu. Barabara hii inahudumiwa na wenzetu wa TANROADS lakini inapita katika miinuko ya milima na kuna milima ambayo kama itatengenezwa katika kiwango cha changarawe basi tutaendelea kupata matatizo tu. Niishauri Serikali milima ile kwa mfano Milima ya Ndundu pale Namayuni, Ngoge, Kinywanyu pamoja na na Mlima wa Karapinda pale darajani basi ingewekwa katika kiwango cha lami ili kuhakikisha kwamba barabara ile inapitika kwa wakati wote. (Makofi)
Lakini isitoshe, nikumbushe pia, Rais wa Awamu ya Nne, Mheshimiwa Jakaya Mrisho Kikwete katika sherehe za kumbukumbu ya Vita ya Majimaji mwaka 2010 kule Nandete aliahidi kujenga barabara kutoka Nandete mpaka Nyamwage, ahadi ile imeota mbawa sijui kama utekelezaji wake unakwenda vipi. Niikumbushe Wizara, Mheshimiwa Rais aliahidi na ningependa kuona utekelezaji wake unafanyika.
Mheshimiwa Naibu Spika, maelekezo yanayotoka kwamba Mkoa na Mkoa utaunganishwa kwa barabara ya lami, lakini sisi Mkoa wa Lindi na Mkoa wa Morogoro hatujaunganishwa kwa barabara. Niishauri Serikali ione uwezekano sasa wa kujenga barabara kutoka Mkoa wa Lindi kwenda Mkoa wa Morogoro, na hii pengine inatengeneza uwezekano mwingine wa kwenda katika Mikoa ya Kusini, isiwe lazima ukitokea Dodoma uende Dar es Salaam, ufike Rufiji, uende Kilwa kwenda Kusini basi ukifika Morogoro uingie Liwale - Nachingwea uende Kusini. Naomba ombi hili lishughulikiwe kwa sababu na sisi watu wa Lindi tuna haki ya kuunganishwa na wenzetu wa Morogoro ili basi kuleta ustawi wa watu hao.
Mheshimiwa Naibu Spika, nizungumzie sasa suala zima la ukarabati wa uwanja wa ndege wa Kilwa Masoko. Kwenye bajeti ya mwaka jana tulichangia bajeti lakini hakuna chochote kilichofanyika. Niishauri Serikali iufanyie ukarabati uwanja wa ndege wa Kilwa Masoko kwa sababu ni muhimu sana kwa shughuli za utalii, kama ambavyo mnafahamu Mji wa Kilwa ni mji wa kitalii, ni mji wa kale, watalii wengi wanakuja lakini hatuna uwanja wa uhakika wa ndege, kwa hiyo Serikali ishughulikie suala hilo.
Mheshimiwa Naibu Spika, kuna suala zima la upanuzi wa Bandari ya Kilwa Masoko. Kilwa Masoko tuna bandari ya asili, lakini mpaka sasa ile bandari haijafanyiwa chochote. Niishauri Serikali ione uwezekano wa kupanua bandari ya Kilwa Masoko ili basi meli kubwa ziweze kutia nanga pale na sisi watu wa mikoa ya Kusini au watu wa Kilwa mazao yetu basi yauziwe pale pale Kilwa, maana Meli kubwa zikija hatutakuwa na sababu ya kupeleka mazao Dar es Salaam. Tunalima korosho, tunalima ufuta, bandari ya Kilwa ikifanya kazi basi mazao yale tunaweza tukayauzia Kilwa na hivyo kupandisha bei ya mazao ya wakulima.
Mheshimiwa Naibu Spika, mwisho kwa masikitiko makubwa nizungumzie suala zima la stand ya mabasi kwa Mikoa ya Kusini. Mikoa ya Kusini kwa jiografia yake, barabara inayosafirisha abiria kutoka Dar es Salaam kwenda Mikoa ya Kusini inatokea maeneo ya Mbagala Rangi tatu, lakini mpaka sasa hatuna stand inayoeleweka ya mabasi kutoka Mikoa ya Kusini. Tunapata shida kubwa maana stand zinazotumika
pale Mbagala Rangi tatu ni stendi za watu binafsi, na kwa sasa kuna ubaguzi mkubwa unafanyika kwa magari yanayotokea Kilwa.
Mheshimiwa Naibu Spika, tumelazimishwa kwa magari yanayotokea Kilwa tuka-park uchochoroni huko ambako zina-park daladala hali ya kwamba Kilwa ni mkoa wa Lindi na kuna mabasi mengine ya Mkoa wa Lindi yana- park katika stand ambayo iko barabarani sasa tunashindwa kuelewa ni kwa nini watu wa Kilwa tutengwe?
Mheshimiwa Naibu Spika, lakini nichukue nafasi hii pia kuishauri Serikali ijenge stand kwa ajili ya mabasi ya mikoa ya Kusini; kwa sababu kwa jiografia ya Jini la Dar es Salaam haiwezekani mtu anayetoka Mtwara, Kilwa au Lindi kwenda Ubungo, haiwezekani. Kwa hiyo Serikali ifikirie kujenga hiyo stendi ili kuondoa adha hii kwa wananchi wa mikoa ya Kusini.
Mheshimiwa Naibu Spika, nikushukuru, ahsante.