Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 – Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano

Hon. Omary Tebweta Mgumba

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Morogoro Kusini Mashariki

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 – Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano

MHE. OMARY T. MGUMBA: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru sana kwa kunipa nafasi hii nami nitoe mchango wangu katika Wizara hii ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano. Wenzangu wengi wametoa pongezi kwa Serikali yetu ya Chama cha Mapinduzi Awamu ya Tano. Na mimi nitakuwa ni mnyimi wa fadhila kama sitashukuru kidogo walichonifanyia katika Jimbo letu la Morogoro Kusini Mashariki. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nichukue nafasi hii kumshukuru Mheshimiwa Rais, Dkt. John Pombe Magufuli, kwa nia ya dhati kwa mara ya kwanza ukiondoa ile Barabara ya lami ya Taifa, Dar es Salaam - Morogoro ya kwanza tangu miaka 50 ya Uhuru ndiyo Dkt. John Pombe Magufuli alipokuja kuzindua Uwanja wa Ndege wa Kijeshi wa pale Kizuka, ametuzawadia kilometa zaidi ya 15 kutuwekea lami. Tunamshukuru sana nasi tunaanza kuona matunda ya Serikali ya Chama cha Mapinduzi kwa mara ya kwanza kuwa na barabara la lami. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pia nimshukuru Mheshimiwa Waziri wa Ujenzi, Naibu Waziri, Katibu Mkuu na Uongozi wa TANROADS Mkoa wa Morogoro ukiongozwa na Engineer Dorothy Mtenga na timu yake nzima, kwa usikivu mkubwa ambapo tulipopeleka maombi yetu ya kupandishwa barabara kutoka Wilaya kwenda Mkoa, barabara ya Ubena Zomozi - Ngerengere - Tununguo mpaka Mvuha, mwaka huu imepandishwa na nimeiona na imetengewa fedha. Nawashukuru sana huu ndiyo utekelezaji Ilani ya Chama cha Mapinduzi jinsi tulivyoahidi inaonekana namna inavyotekelezwa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, mwisho ni ombi kuhusu barabara hii ya Ubena Zomozi kwenda pale Kizuka ingawa cha kupewa hakina nyongeza na hii ilikuwa ni zawadi mahsusi kwa Mheshimiwa Rais kwa Jeshi letu, kwa walinzi wetu wale wa Kizuka, walinzi wa mipaka yetu, kama mnavyofahamu Mheshimiwa Waziri pale Kizuka tuna kambi nne, pamoja na ile ya Sangasanga ya wale wazee wa kazi mliowaona pale wakitoa burudani juzi pale uwanjani. Sasa wale barabara yao inaanzia Mdaula mpaka Sangasanga, ombi langu kwako na ninafikiri Serikali iko hapa, umfikishie Mheshimiwa Rais, tunaomba hawa nao ni wapiga kura wangu wasione kama wametengwa, basi hizi kilometa zao saba zingewekewa lami kama walivyowekewa wenzao wa Kizuka, litakuwa ni jambo jema sana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya hapo niende kwenye barabara. Kama tulivyosema barabara ya kwanza ya lami ndiyo hiyo itakuja kilometa 15 kutoka ahadi ya Rais, lakini kuna barabara muhimu kuliko yote ya Bigwa - Kisaki. Ni barabara ambayo kila wakati tunaiongelea hapa lakini bahati mbaya sijaiona humu. Barabara hii ni muhimu sana kwa sababu inapita katika tarafa nne za jimbo hili, inapita tarafa ya Mkuyuni, tarafa ya Matombo, tarafa ya Mvuha, tarafa ya Bwakila, lakini cha muhimu barabara hii inakidhi sera. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, barabara hii inaunganisha Mkoa wa Morogoro na Mkoa wa Pwani kwa upande wa Rufiji. Kutoka Kisaki kwenda Rufiji ni kilometa 60 tu na kutoka Morogoro Mjini kwenda Kisaki kilometa 170. Kwa hiyo, utakuwa umefika Rufiji kwa kilometa 230, itakuwa ina mchango mkubwa sana kitaifa badala ya mtu anayetoka Kanda ya Ziwa, Kanda ya Kati, Kanda ya Nyanda za Juu, Morogoro yenyewe akienda Mtwara analazimika mpaka atembee kilometa 200 kwenda Dar es Salaam, baadae atoke 170 kwenda Kibiti mpaka Rufiji, ndiyo hapo tutakuwa tumeokoa gharama kubwa sana kwa kutengeneza barabara hii. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, tutaokoa msongamano Dar es Salaam, tutaokoa gharama za usafirishaji pia barabara hii ikitengenezwa tutarahisisha kufika katika Mbuga yetu ya Selous kupitia Kisaki kwa ukaribu zaidi kwa hiyo, tutaongeza mapato ya kiuchumi kupitia utalii. Kwa hiyo, naomba sana barabara hii ijengwe kwa kiwango cha lami kama ilivyoahidiwa tangu 2005 na Mheshimiwa Dkt. Jakaya Kikwete, akarudia 2010 pia 2015 na nishukuru ipo kwenye ilani, basi utekelezaji ufanyike haraka iwezekanavyo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo la pili, kwenye barabara hii ya Bigwa - Kisaki, ningeomba hawa waliopisha barabara waliokuwa kwenye hifadhi, wamefanyiwa tathmini muda mrefu sana Mheshimiwa Waziri. Sasa ni wakati muafaka wakalipwa fidia mapema ili ikifikia wakati wa kutengeneza hiyo barabara basi iende kwa haraka sana. Naomba ukija kufunga mjadala wako ni vizuri tupate commitment ya Serikali tujue ni lini watu waliopisha barabara watalipwa fidia zao kwa sababu mpaka sasa hivi, zaidi ya miaka mitano wamekaa hawafanyi uendelezaji wowote, hawafanyi kitu chochote. Kama unavyojua nyumba yoyote ikiwa karibu na barabara inakuwa ni nyumba ya biashara siyo ya makazi, watu wana-frame zao, watu wana viwanda vyao vya matofali, vyote vimesimama kwa kusubiri kupisha hii barabara. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo la tatu niende kwenye upande wa reli. Ninamshukuru sana Mheshimiwa Dkt. John Pombe Magufuli na Serikali nzima ya Awamu ya Tano kwa ujenzi wa reli ya kati. Hii reli ya kati ina manufaa makubwa sana katika Mkoa wa Morogoro, hususan katika Jimbo langu. Inapita Kidunda, Ngerengere, Mikese pamoja na Mkulazi. Kwa hiyo, itakuwa na manufaa makubwa sana kiuchumi, itaturahisishia gharama za uzalishaji, gharama za usafirishaji kwenda chini, matokeo yake itakuwa faida kubwa kwa wananchi wa Morogoro. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ombi langu katika hili, kuna watu ambao wameathirika na maendeleo haya ya reli ya kati. Kuna watu wamekaa zaidi ya miaka 20 leo wamepewa notice wanatakiwa wahame ndani ya mwezi mmoja. Mheshimiwa Waziri, hata kama huyo mtu ahame ndani ya mwezi mmoja atapata wapi nafasi hiyo ya kwenda kujenga, muda ndani ya mwezi mmoja apate makazi. Ombi langu la kwanza wangeongezewa muda hata kama miezi sita, ili wapate nafasi ya kujenga kule ambako wanaenda, la pili kwa wale waliokaa zaidi ya miaka 12, Shirika la Reli lilikuwepo walikuwa wanaangalia, watu walishajua pale mahali pao, leo kuja kumhamisha mtu huyu bila chochote kama sheria inavyosema kwamba mtu akikaa zaidi ya miaka 12 mahali hapo anahesabika ni pake. Ni vizuri mngewapa kifutia jasho angalau waende kurudisha pale walipokuwa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, linguine ni kuhusu mawasiliano. Kuna kata zangu zaidi ya tano kwenye tarafa ya Ngerengere, kata ya Maturi, kata ya Mkulazi, kata ya Seregete, kata ya Tununguo na kata ya Kibuko, tarafa ya Mkuyuni, zote hazina mawasiliano, zaidi ya vijiji 30. Nakuomba sana hivi vijiji tuvipatie mawasiliano hasa huku Mkulazi kwenye mradi mkubwa unakotekelezwa sasa hivi na wawekezaji NSSF kwa ajili ya kiwanda cha sukari. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pia katika mawasiliano niongelee kuhusu TTCL. TTCL ni shirika la kwetu, nilikuwa nasikia kuna baadhi ya wenzetu hapa walikuwa wanalifananisha na shirika la huko nje. Jamani hata hayo mashirika yanayosifika huko Ethiopia kwanza yaliwezeshwa mtaji na Serikali yao, pili, yalilindwa na ushindani kwa mashirika mengine kwa muda mrefu mpaka yalipokaa sawasawa ndiyo wakaruhusu mataifa mengine au mashirika mengine kwenda kufanya bisahara pale. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa ni vizuri kwa sababu shirika hili ni letu, kupitia Serikali, Serikali ni vizuri ikaongeza mtaji kama inavyofanya kwenye ATC ili shirika hili li-take off baada ya hapo na ikiwezekana hata huu mtaji tuwape kama loan ili kuwapa uwajibikaji hawa wafanyakazi wa TTCL wajue kwamba tumekopeshwa na Serikali, ni hela za Watanzania zinapaswa zirudishwe kwa wakati na hata kama siyo kwa faida, lakini zirudi Serikalini zije zifanye kazi nyingine. Lakini kuwaacha kwenye ushindani huu mkubwa, tumeona hapa mashirika mengine yamekuja kuomba huku mtaji, tukiwaacha hawa TTCL washindane na ma-giant hao sasa hivi hatuwezi kuwatendea haki na halitaweza kwenda mbele sana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pili pia kwenye TTCL, wanatoa huduma zinatumika na Serikali na taasisi nyingine na sisi wengine, ni vizuri tukawalipa zile ankara zao. Mara nyingi mashirika mengi ya Serikali yanakufa ni kwa sababu hatuyaendeshi kibiashara, tunayaendesha kiserikali kama vile yanatoa huduma. Tunatumia huduma zao, wakati wa kulipa hatulipi, baadae madeni yanakuwa makubwa, shirika linashindwa kujiendesha kibiashara.

Naomba Serikali yangu ni vizuri kama tunadaiwa na TTCL ili tuipe nguvu i-take off hapo ilipo tuilipe madeni yao ili waweze kusimama na kwenda kwenye ushindani. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, mwisho kuhusu TTCL ni kwamba sasa…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba niunge mkono hoja. Nakushukuru sana.