Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 - Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano

Hon. Joseph Michael Mkundi

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Ukerewe

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

2

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 - Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano

MHE. JOSEPH M. MKUNDI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa kunipa fursa hii ya kuchangia hotuba ya Waziri wa Uchukuzi, Ujenzi na Mawasiliano ambayo ni muhimu sana. Kwanza naunga mkono hotuba ya Msemaji wa Kambi Rasmi ya Upinzani.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Pili, nikitambua kwamba kuna maeneo nimekwishatoa mchango kwa maandishi niombe sasa nichangie hasa kwa kusisitiza kwenye maeneo kama matatu ambayo kwangu naona ni muhimu sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze na Jimbo langu la Ukerewe. Sisi ni watu tunaotoka Visiwani, nimekuwa namsikia ndugu yangu Mheshimiwa Mbaraka Kitwana Dau analalamika juu ya mazingira ya Mafia, mazingira ya Ukerewe kama nilivyosema ni visiwa na usafiri wetu mkuu ni lazima tu-cross maji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunategemea kutumia vyombo vya usafiri kama meli, cha kusikitisha tuna shirika muhimu sana la Kampuni ya Huduma za Meli (MSCL) ni kampuni muhimu sana. Ukerewe tumekuwa na Meli za MV. Butiama, MV Clarias, bahati mbaya sana zimekuwa na matatizo kwa muda mrefu mfano MV Clarias, kila mara inaharibika. MV Butiama ina zaidi ya miaka minne haifanyi kazi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika hotuba ya Waziri nimeona wanaongelea utengenezaji wa Meli ya MV Butiama, haiko specific kwamba utengenezaji huu unatarajia kukamilika lini ili kuwasaidia wananchi wa Ukerewe wanaotaabika na usafiri usio wa uhakika wa meli.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninashukuru kwamba kuna kampuni binafsi ya MV. Nyehunge ambayo ina-operate pale sasa hivi, lakini hii Kampuni ya Huduma za Meli ni kampuni muhimu sana, nimekuwa naongea na watumishi wa kampuni hii wanachoomba wao wanataka tu uwezeshwaji ili Kampuni hii ianze kufanya kazi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, wiki iliyopita kuna mchangiaji mmoja ametoa mfano akasema kwamba ni vigumu sana kwa kampuni za meli kupata harasa. Ni kweli nakubaliana naye, Kampuni kwa mfano hii ya Huduma ya Meli kama itawezeshwa ni moja kati ya makampuni ambayo yanaweza kutoa pesa kwa Serikali kutokana na utendaji wao, imani yangu ni kwamba watafanya kazi vizuri na kwa faida na sehemu ya faida ile wataipa Serikali.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa ni mwaka mzima hata pesa za ruzuku OC Serikali imeshindwa kuwapa kampuni hii, wameshindwa kulipwa mishahara, hata Bima ya Afya wamekatiwa kwa sababu wameshindwa kulipa pesa, matokeo yake naambiwa kuna wakati mpaka watumishi wanaenda kupanga foleni ili viongozi wa kampuni hii waweze kuwasaidia watumishi angalau familia zao zipate matibabu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba sana Serikali wasaidieni Kampuni hii iweze kuwa imara, iweze kusimama na kufanya kazi zake, kwa sababu wanachoomba wao kampuni hii ya meli wanataka tu uwezeshwaji ili waanze kazi. Kama wataanza kufanya kazi wana uhakika wa kuendelea kulipana mishahara na kufanya shughuli zao bila matatizo. Kwa nini Serikali mnaicha Kampuni hii inataabika kiasi hiki. Hebu niombe Serikali tafadhali MSCL waweze kusimama wa- take off kuliko kuwaacha katika mazingira wanaishi kama yatima, hawalipani mishahara, watumishi wanaugua hawawezi kwenda hospitali kwa sababu hawana bima tena, wasaidieni tafadhali. Iwezesheni MSCL iweze kufanya kazi, hii ni Kampuni muhimu sana kuweza kuisaidia hata Serikali kama chanzo chake cha mapato. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sambamba na hilo kama nilivyosema, kule tunaishi visiwani, kuna vivuko kwa mfano cha MV Nyerere nimekuwa nawasiliana na Mheshimiwa Naibu Waziri mara kwa mara, ambacho kina operate kati ya Ukala na Bugolola. Kivuko hiki kina muda mrefu na sasa injini zake zimechakaa zimeanza kuleta matatizo. Kwa mfano, wiki mbili zilizopita kivuko hiki kimezima katikati ya maji zaidi ya mara mbili na kuzua taharuki kwa abiria waliokuwa katika meli ile. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba Mheshimiwa Waziri wakati anafunga mjadala aweze kutuambia na hasa wananchi wa Jimbo la Ukerewe wanaotumia kivuko hiki nini suluhisho la kudumu la Kivuko cha MV Nyerere? Kinahitaji kitengenezwe ili watu wanaosafiri katika kivuko kile wawe na uhakika wa maisha yao. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kivuko kinasafiri, kwanza mahali kinapofanya kazi ni umbali ambao hauwezi kuzidi hata dakika arobaini na tano, lakini kivuko kile kwa sababu ya kuchoka kwa injini zake kinasafari zaidi ya masaa mawili, sasa fikiria kina safiri masaa mawili bado kinazima katikati ya maji! Hii inazua taharuki na kukatisha watu tamaa. Wakati Mheshimiwa Waziri anapokuja ku-wind up ningeshukuru sana kama atanipa suluhisho la kivuko hiki na kuweka mazingira ya kudumu na ya uhakika ya usafiri kwa wakazi wa Kisiwa cha Ukala. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Kisiwa cha Irugwa vilevile pale Ukerewe, kina wakazi zaidi ya elfu 20, lakini wanasafiri kutoka kule kwa mfano watumishi wanasafiri kwa siku tatu. Ili atoke Irugwa aje atape huduma kwenye Makao Makuu ya Wilaya inabidi apite Musoma Vijijini kwenye Jimbo la Profesa Muhongo, aende Musoma Mjini kwenye Jimbo la Mheshimiwa Mathayo, aende Bunda kwenye Jimbo la Mheshimiwa Ester Bulaya apite Kisolya ndiyo aje Nansio. Naomba Mheshimiwa Waziri mtuangalie kwenye eneo hili Kisiwa cha Irugwa lini Serikali itafikiria kuweka usafiri wa kudumu katika eneo hili. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nije kwenye eneo la barabara, nimesoma kwenye hotuba hapa sijaona chochote juu ya ujenzi wa daraja linalounganisha Kisolya na Rugezi. Serikali ina mpango gani juu ya ujenzi wa daraja hili ambalo litakuwa suluhisho la matatizo ya usafiri kwa wakazi wa Ukerewe. Ningeshukuru sana kama Mheshimiwa Waziri wakati wa kufunga atanipa maelezo ni nini mkakati wa Serikali juu ya ujenzi wa daraja hili, kwa sababu tayari hatua za awali zilishaanza, nini kinaendelea, nitashukuru sana kama Mheshimiwa Waziri ataniambia nini kinachoendelea. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika mradi wa ujenzi wa mradi wa ujenzi wa barabara ya Bunda – Nansio, nimeona kwenye hotuba kuna awamu ya pili ambayo inaongelea ujenzi wa kilometa 51 kati ya Kibala na Kisolya. Niombe sana Mheshimiwa Waziri. Kutoka Kisolya ambapo awamu hii ya pili inakomea mpaka Nansio Mjini ni kama kilomita kumi na zinabaki, naomba badala ya kujenga kilometa 51 kilometa 10 zikabaki ni bora Serikali ikaunganisha kilometa hizi katika kilometa 51 ili ufanyike mradi wa pamoja, badala ya kutengeneza kwa awamu miradi miwili tofauti ambayo naamini itakuwa ni gharama zaidi kuliko kama itaunganishwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niongelee suala la mawasiliano; nimeona jitihada za Mfuko wa Mawasiliano kusambaza huduma hii ya mawasiliano, lakini bado kuna matatizo makubwa sana ya mawasiliano kwenye kisiwa cha Ukerewe hasa katika Kisiwa cha Ukara. Katika karne hii si jambo jema sana kwamba unaenda mahali unakuta wanakijiji wanakusanya eneo moja ili wapate mawasiliano ya kupiga simu. Kwa hiyo, naomba Mheshimiwa Waziri tuweze kupata mawasiliano kwenye kisiwa cha Ukerewe, maeneo yote yaweze kupata mawasiliano, ambayo yatasaidia hasa kuharakisha shughuli za kiuchumi za wananchi kwa eneo la Ukerewe.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo, nashukuru sana.