Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 - Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano

Hon. Dunstan Luka Kitandula

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mkinga

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 - Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano

MHE. DUNSTAN L. KITANDULA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze kwa kuunga mkono hoja kuhusiana na Bajeti ya Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano. Aidha, nampongeza Mheshimiwa Waziri, Naibu Waziri na Watendaji katika Wizara hii kwa kazi kubwa wanayoifanya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, uwepo wa miundombinu ya uhakika ya barabara katika maeneo ya vijijini una umuhimu mkubwa katika kufungua fursa za kiuchumi na hivyo kuharakisha maendeleo kwa wananchi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunapojiwekea lengo la ujenzi wa barabara za lami kuunganisha Mkoa kwa Mkoa, tuna wajibu vile vile wa kutoa msukumo kwa barabara za aina hiyo zenye umuhimu wa kimkakati katika usalama na kukuza fursa ya kuongeza/kuunganisha vivutio vya utalii.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mabokweni – Gombero – Maramba – Bombo Mtoni – Kitivo – Mlalo hadi Same ni barabara mbadala ya kuunganisha Mkoa wa Tanga na Mkoa wa Kilimanjaro. Barabara hii inapita kwenye maeneo makuu ya uzalishaji mazao ya chakula na biashara. Ni barabara inayounganisha maeneo haya ya Bandari ya Tanga na nchi jirani ya Kenya. Aidha, kwa upande wa usalama wa nchi, barabara hii ni barabara ambayo ina umuhimu wa kiusalama kwa nchi yetu kutokana na ukweli kuwa inaambaa katika mpaka wetu na nchi ya Kenya. Hivyo, kufanya zoezi la kukagua na kulinda mpaka wetu kuwa na uhakika zaidi kinyume na ilivyo sasa ambavyo tunalazimika maeneo mengi kupitia Kenya ili kuweza kukagua mpaka wetu na Kenya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, barabara ya Mabokweni – Maramba – Bomba Mtoni – Mlalo hadi Same ni barabara muhimu kwa kukuza utalii, kwa kuunganisha Mbuga ya Saadani na Mkomazi ambayo inagusa Wilaya ya Mkinga eneo la Mwakijembe ambako yapo maeneo ya asili ya mazalia ya faru. Kwenye Umba Game Reserve, Wilaya ya Lushoto eneo la Mlalo hadi Wilaya ya Same kwenye Mkoa wa Kilimanjaro.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ujenzi wa barabara hii kwa kiwango cha lami kutaimarisha na kuunganisha Sekta ya Utalii siyo tu kwa Mbuga ya Sadaani na Mkomazi, bali kutaunganisha utalii kwa watalii kutoka Zanzibar kuweza kutembelea vivutio kutoka Saadani, Amani, Nature Reserves, Mapango ya Amboni hadi maeneo ya utalii ya Ngorongoro, Mlima Kilimanjaro na kadhalika. Aidha, barabara hii itavutia watalii toka Mombasa, Kenya; kuvutika kwa urahisi zaidi kuja Tanzania kupitia Horohoro, Mbuga ya Mkomanzi kuanzia Mkinga hadi Kilimanjaro. Naiomba Serikali kuipa kipaumbele barabara hii kwa kuanza kufanya upembuzi yakinifu ili iweze kujengwa kwa kiwango cha lami.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naipongeza Serikali kwa kuanza ujenzi wa reli kwa standard gauge. Naishauri Serikali kwamba, umefika wakati sasa tuanze kuweka mfumo wa infrastructure bond katika ujenzi wa reli na barabara zetu. Nashauri tujifunze kwa wenzetu wa Nigeria, India na Israel katika kutumia infrastructure bonds katika kujenga miundombinu muhimu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naipongeza Serikali kwa kutenga shilingi milioni 865 kwa ajili ya fidia kwa wananchi katika barabara ya Tanga - Horohoro. Hata hivyo, naisihi Serikali ihakikishe fedha hizi zinapatikana kwa sababu hii imekuwa kero ya muda mrefu kwa wananchi. Aidha, ni vyema kukawa na ushirikishaji wa karibu kwa uongozi wa eneo husika pindi malipo yatakapokuwa yanafanyika ili kuhakikisha kila anayestahili kuliwa anapata haki yake.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naishukuru Serikali kwa kutenga fedha, shilingi milioni 120 ku-upgrade Mkinga Township Road kilometa nne.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja, nikikumbusha kuwa bado barabara ya TANROADs kuunganisha Maramba na Makao Makuu ya Wilaya katika Mji wa Kasero haijakamilika. Aidha, eneo la Magoli bado ambalo barabara itapita pembeni ya Kijiji halijakamilika.