Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 - Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano

Hon. Zuberi Mohamedi Kuchauka

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Liwale

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 - Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano

MHE. ZUBERI M. KUCHAUKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nichukue fursa hii kuchangia hotuba hii kwa kuanza na hali za barabara zetu hapa nchini. Hali ya barabara zetu nyingi ni mbaya hasa majira ya masika ambapo barabara nyingi zinajifunga hasa kwa zile za changarawe na udongo. Hali hii huchangiwa zaidi na wakandarasi kuzijenga chini ya kiwango. Kwa barabara za lami hali ni mbaya pia, barabara nyingi hujengwa chini ya kiwango. Jambo linalo igharimu nchi yetu kutumia fedha nyingi za matengenezo ya mara kwa mara.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ubovu wa barabara za lami nchini huchangiwa kwa kiasi kikubwa na kukosa umakini au utaalam wakati wa upembuzi yakinifu na usanifu wa kina ambapo ndio humwongoza Mkandarasi. Kwa ajili hiyo wakandarasi wengi inashindikana kuwatia hatiani kwa sababu mara zote kosa sio lao.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa nijikite kwenye Sera ya Kitaifa juu ya kuunganisha mikoa yetu kwa barabara za lami. Hadi leo kuna baadhi ya mikoa haijaunganishwa japo mikoa mingine sasa inaunganishwa kati ya wilaya hadi wilaya wakati mikoa mingine haijaunganishwa. Kwa mfano Mkoa wa Lindi na Mkoa wa Morogoro au Mkoa wa Lindi na Mkoa wa Ruvuma. Barabara ya Lindi – Morogoro kupitia Wilaya za Liwale na Ulanga ni muhimu sana hasa kwa sasa ambapo Serikali imehamia Dodoma, kwa sababu Mikoa ya Lindi na Mtwara kuja Dodoma kupitia njia hiyo ni fupi sana; hivyo kuipunguzia Serikali Matumizi ya Mafuta kwa watumishi wa mikoa hiyo, kuja Dodoma.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa naomba nijielekeza Jimboni kwangu Liwale. Liwale ni Wilaya yenye umri wa miaka 42, lakini hadi leo Wilaya hiyo inakabiliwa na tatizo kubwa la mawasilino ya simu na barabaram jambo linaloifanya Wilaya hii kuwa nyuma kimaendeleo. Katika Mkoa wa Lindi Liwale ndiyo Wilaya iliyo mbali zaidi kutoka Mkoani, kama kilomita zaidi ya 300. Barabara ya Liwale – Nachingwea, japo imetajwa katika Ilani ya CCM Lakini sioni juhudi za Serikali katika utekelezaji wake.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Barabara ya Nanguruku – Liwale ni kama mshipa wa damu kwa Wilaya ya Liwale. Pamoja na kwamba Liwale inaongoza kwa zao la korosho na ufuta katika Mkoa wa Lindi lakini bado wakulima hao wanapata bei ndogo ya mazao yao, jambo linalopunguza pato la Halmashauri na Serikali kwa ujumla kwani wafanyabiashara hutoa bei ndogo kwa sababu ya ubovu wa barabara.

Mheshimiwa Mwenyekiti, wakazi wa Wilaya za Masasi, Tunduru na Nachingwea wangeweza kutumia barabara hii ya Nangurukuru – Liwale kwani ndiyo barabara fupi kwao kwa kwenda na kutoka Dar es Salaam kupitia Liwale, hivyo kuongeza umuhimu wa barabara hii. Pamoja na Liwale kupakana na hifadhi ya Selou, watalii wanashindwa kuja Liwale kwa sababu ya ukosefu wa miundombinu ya barabara na simu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hapa naomba kupata maelezo ni kipi kianze kati ya miundobinu na simu maendeleo ya watu. Naomba barabara hii ijengwe ili ufuta, viazi na korosho za Wanaliwale ili zipate bei nzuri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mawasiliano ya simu ni muhimu sana lakini hadi sasa ni chini ya asilimia 40 tu ya vijiji 76 vya Wilaya ya Liwale, vina mawasiliano ya simu. Ukiondoa mawasiliano ya simu na barabara hakuna namna nyingine ya mawasiliano kwa wakazi wa Liwale kwani hakuna redio inayosikika Liwale.