Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 - Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano

Hon. Oran Manase Njeza

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mbeya Vijijini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 - Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano

MHE. ORAN M. NJEZA: Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kumpongeza Waziri wa Ujenzi Uchukuzi na Mawasiliano, Naibu Waziri na Timu nzima ya Wizara kwa ripoti nzuri na pia bajeti nzuri ya mwaka 2017/2018.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia napenda kumpongeza Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mheshimiwa Dkt. John Pombe Joseph Magufuli na Mheshimiwa Samia Hassan Suluhu Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Mheshimiwa Kassim Majaliwa Majaliwa Mbunge, Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa kuiongoza vema nchi yetu katika utekelezaji wa Ilani ya CCM 2015/2020.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Wizara ya Ujenzi Uchukuzi na Mawasiliano ni muhimu sana katika uchumi wa nchi yetu na katika kipindi cha bajeti ya 2016/2017. Serikali imefanya vizuri sana kama ifuatavyo:-

(1) Ujenzi wa reli ya standard gauge umeanza;
(2) Serikali imeendelea kulipa madeni ya wafanyakazi wa TAZARA ambapo shilingi billioni 16.8 zimelipwa kati ya shilingi billioni 22.9 zilizokuwa zinadaiwa;
(3) Serikali iliingia mkataba wa ununuzi wa ndege sita, ndege mbili aina ya Bombardier dash 8-Q400 ziliwasili nchini Septemba, 2016;
(4) Ujenzi wa Mkongo wa Taifa wa mawasiliano;
(5) Ujenzi wa barabara za juu kwenye makutano ya TAZARA unaendelea vizuri; na
(6) Ujenzi wa barabara na madaraja mbalimbali unaoendelea nchi nzima.

Mheshimiwa Mwenyekiti, dunia ya leo ya ushindani mkubwa wa kibiashara umepelekea biashara ya Kimataifa kuwa ya masaa 24 na siku saba za wiki na ili kuwe na tija na ufanisi katika uchumi wetu tunahitaji uboreshaji wa miundombinu ya barabara, reli, bandari pia mawasiliano.

Mheshimiwa Mwenyekiti, changamoto za usafirishaji na miundombinu ya bandari yamepelekea kwa kiasi kikubwa gharama kubwa za ndani (domestic supply chain costs) kwa bidhaa zetu na hata pembejeo za kilimo ukilinganisha na nchi zingine.

Mheshimiwa Mwenyekiti, gharama kubwa ya mbolea kwa mkulima wa Tanzania imebebwa na gharama za bandari, usafiri wa barabara na hata ucheleweshwaji wa kutoa mzigo bandarini. Mnyororo wa gharama za mbolea kwa mkulima wa Tanzania, hivi sasa asilimia 47 ni gharama za ndani port charges, transportation, taxes and mark up, wakati asilimia 53 ni gharama ya kununulia nje ya nchi CIF kwa kulinganisha na nchi ya Ufilipino gharama ya ndani ni asilimia 16 tu na CIF ni asilimia 84. Pia nchi ya Myanmar gharama za ndani za mbolea ni 23% tu wakati gharama za kununulia CIF ni asilimia 77, hivyo mzigo mkubwa wa bidhaa za Tanzania unatokana na uchukuzi, tozo mbalimbali za bandari na matumizi ya barabara.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nashauri Serikali iboresha TAZARA pia ili mbolea isafirishwe kwa reli badala ya barabara ambayo ni gharama kubwa sana. Pia napendekeza Serikali iendelee kuboresha bandari ili meli kubwa ziweze kuingia kwa urahisi, vilevile shehena za mizigo ya mbolea zipewe kipaumbele cha kupakuliwa bandarini. Pia kuwepo na kituo kimoja cha huduma kwa wateja one stop centre.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na kuboresha bandari ya Dar es Salaam na TAZARA napendekeza kujenga bandari kavu katika eneo la kimkakati la Inyala, Mbeya ili wateja wa Zambia, Malawi, DRC Congo na hata wafanyabiashara Watanzania kutoka Nyanda za Juu Kusini wasilazimike kuchukua mizigo yao.

Mheshimiwa Mwenyekiti, miundombinu ndiyo chachu na tija bora hasa katika sekta ya kilimo ambayo ndiyo mhimili wa uchumi wetu wa Tanzania. Barabara za vijijini ni muhimu sana kwa kusafirisha mazao ya kilimo na pia kupunguza gharama za usafiri wa pembejeo na urahisi wa kupeleka mazao sokoni.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ili kuboresha usafirishaji wa mazao ya kilimo na pia kuunganisha mikoa kwa barabara za lami (trunk roads) napendekeza Serikali kuboresha barabara zinazounganisha Mkoa wa Mbeya na mikoa mingine kama vile babaraba ya Isyonje-Kikondo Makete - Njombe, barabara ya Mbalizi-Shigamba-Ileje inaunganisha Mbeya na Ileje - Songwe, barabara ya Mbalizi-Makongorosi inaunganisha Mbeya na Songwe.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ili kuboresha usafirishaji wa mazao na pembejeo, napendekeza kupandishwa hadhi barabara za kimkakati zikiwemo Kawetere-Mwabowo- Ikukwa, Mbalizi-Iwindi-Jojo, Inyala-Simambwe na Imezu – Garijimbe (mchepuo/bypass)

Mheshimiwa Mwenyekiti, wakati Serikali inajenga barabara ni muhimu pia kuzingatia vigezo vya kiuchumi pamoja na ahadi za Marais waliostaafu na Rais aliye madarakani, pamoja na barabara zilizotajwa hapo juu. Mheshimiwa Rais wa Awamu ya Nne na Rais wa sasa waliahidi ujenzi wa barabara ya mchepuo by pass ya kilomita 40, kuanzia Mlima Nyoka Inyala-Ijombe-Swaya-Igale-Iwindi- Songwe. Pamoja na kupunguza msongamano pia ni barabara inayounganisha machimbo mapya ya umeme wa jotoardhi na mgodi mpya wa Pandahill.

Mheshimiwa Mwenyekiti, changamoto za kiwanja cha ndege cha Songwe ni pamoja na kukosekana kwa uzio wa uwanja na kutokuwa na navigational aids, ikiwemo taa katika njia za kutua na kurukia ndege. Eneo la uwanja wa Songwe lina ukungu hususani wakati wa asubuhi na hivyo kuwa vigumu kwa marubani wa ndege kuona kiwanja vizuri. Kukosekana kwa taa kumepelekea na kusababisha usumbufu mkubwa kwa abiria na hata mashirika ya ndege.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kutokana na ukanda wa Mikoa ya Nyanda za Juu Kusini kuwepo kwa mazao mengi ya kilimo, hasa matunda, mbogamboga na hata maua, kuna fursa za ndege za mizigo kuchukua hayo mazao na kupeleka moja kwa moja soko la nje. Kutokana na ukosefu wa taa navigation aids na uzio mashirika ya ndege za mizigo yameshindwa kuanza usafirishaji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nashauri Serikali kuhakikisha kabla ya mwaka wa fedha 2016/2017 kwisha, fedha zilizokuwa zimetengwa kwa ajili ya taa, navigation aids na uzio wa kiwanja cha Songwe, zinatolewa ili kukamilisha kazi hizo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kama ilivyokuwa uchukuzi, na ujenzi, mawasiliano ni muhimu sana kwa wakulima vijijini. Serikali inapoangalia kuanzisha soko la mazao Tanzania, commodities exchange market ni muhimu sana kwa sasa kuhakikisha maeneo ya vijijini yanakuwa na minara ya mawasiliano. Napendekeza Serikali iharakishe ujenzi wa minara ya mawasiliano hasa kwa vijiji ndani ya Halmashauri ya Wilaya ya Mbeya, vikiwemo Vijiji vya Itala, Mkuyuni, Ulenje, Wambishe, Ihango, Mashese, Nyalwela, Mwela, Shango, Ngole, Ikukwa, Ipusizi, Izyira, Shizuvi, Shisyete, Isonso na Igalukwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja.