Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 - Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano

Hon. Prof. Makame Mnyaa Mbarawa

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mkoani

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 - Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano

AZIRI WA UJENZI, UCHUKUZI NA MAWASILIANO: Mheshimiwa Mwenyekiti, awali ya yote, napenda kuchukua fursa hii kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa kutuwezesha kuwepo hapa kukamilisha kazi ambayo niliianza wiki iliyopita.

Aidha, napenda kutoa shukrani zangu za dhati kwako wewe binafsi Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Naibu Spika, Wenyeviti wengine wote na Katibu wa Bunge kwa kusimamia kwa ufanisi mkubwa majadiliano yote kwenye Mkutano huu wa Saba wa Bunge letu Tukufu. Kwa namna ya kipekee, napenda pia kumpongeza Kiongozi wa Shughuli za Bunge, Mheshimiwa Kassim Majaliwa Majaliwa, Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa umahiri wa hali ya juu anaoendelea kuuonyesha na kutuongoza sisi wasaidizi wake. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nachukua fursa hii pia kuwashukuru Wenyeviti na Wajumbe wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Miundombinu na Kamati ya Bajeti kwa kufanya kazi kwa karibu na Wizara yangu. Naahidi kwamba Wizara ninayoingoza itayafanyia kazi yote yaliyoshauriwa na Kamati hizi ya kusimamia, kuendedesha, kuboresha na kuendeleza miundombinu na huduma za sekta ya ujenzi, uchukuzi na mawasiliano kwa weledi wa hali ya juu.

Napenda kumshukuru Msemaji wa Kambi ya Upinzani wa Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano kwa maoni na mapendekezo yake kuhusu bajeti hii. Mwisho lakini si kwa umuhimu, napenda kuwashukuru Waheshimiwa Wabunge wote waliochangia hoja hii kwa kuzungumza na kwa maandishi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Taifa letu limejipanga kuwa nchi ya kipato cha uchumi wa kati ifikapo mwaka 2020/2025. Katika kufikia lengo hili, Taifa limelipa kipaumbele sekta ya viwanda na uendelezaji rasilimali watu ili kuwezesha kufikia lengo tunalokusudia. Wizara yangu itafanya jitihada kubwa kuweka mazingira wezeshi kwa kujenga miundombinu bora ili kurahisisha uendelezaji wa viwanda hapa nchini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nalihakikishia Bunge lako hili Tukufu kwamba mimi na Mheshimiwa Naibu Waziri wangu pamoja na watendaji wote wa Wizara tutasimamia ujenzi wa miundombinu muhimu ya usafirishaji na ya uunganishaji maeneo ya uzalishaji wa viwanda hivyo na maeneo ya mahitaji yaani masoko ya ndani na ya nje ya nchi. Ninawaomba Waheshimiwa Wabunge wote tuunganishe nguvu zetu ili pamoja na Serikali yetu inayoongozwa na Mheshimiwa Dkt. John Pombe Joseph Magufuli, Rais wa jamhuri ya Muungano wa Tanzania tuwezeshe Taifa letu kufikia ndoto hii.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya masuala hayo ya jumla, sasa noamba nijikite kujibu hoja za Waheshimiwa Wabunge kwa kuzingatia sekta tatu yaani sekta za ujenzi, uchukuzi na mawasiliano. Mheshimiwa Naibu Waziri tayari amejibu baadhi ya hoja za Waheshimiwa Wabunge kwa kuzingatia makundi ya Wabunge na maeneo ya kisekta. Kazi yangu kubwa itakuwa ni kujibu hoja kuu zilizojitokeza ambazo zitakuwa msingi wa utekelezaji wa majukumu ya Wizara kwa mwaka wa fedha 2017/2018.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kitakwimu Waheshimiwa 29 walichangia wakati wa majadiliano ya hoja ya Waziri Mkuu na wakati wa majadiliano ya Wizara yangu tumepokea michango ya Waheshimiwa Wabunge 68 waliotoa maoni yao kwa kuzungumza na michango kwa maandishi 98. Nawashukuru sana Waheshimiwa Wabunge kwa michango yenu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nilihakikishie Bunge lako Tukufu kwamba Wizara itajibu hoja zote za Waheshimiwa Wabunge kwa maandishi na kuwapatia majibu ya maandishi kwa njia ya kitabu kitakachoandaliwa kabla ya kuanza Mkutano wa Nane wa Bunge letu Tukufu. Hivyo kwa yale ambayo hatutaweza kuyajibu hapa leo kwa sababu ya muda kutotosha, majibu yatapatikana kupitia kitabu kitakachoandaliwa na Wizara yangu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba sasa nijikite kujibu hoja za Waheshimiwa Wabunge nikianzia na sekta ya mawasiliano, uchukuzi na mwisho sekta ya ujenzi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimeamua kuanzia sekta ya mawasiliano kwa sababu wewe leo ni Mwenyekiti na ulikuwa mchangiaji wa kwanza kwenye sekta hii na hasa ulijikita kwenye suala la TTMS. Ulisema kwamba iko haja ya Serikali kuangalia upya mfumo wa TTMS.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nilieleze Bunge lako Tukufu pamoja na Watanzania wote kwamba mfumo wa TTMS umejengwa kwa utaratibu wa jenga, endesha na kabidhi (Build, Operate and Transfer - BOT) na hivyo hakuna malipo yoyote ya awali yaliyolipwa na Serikali kwa mkandarasi wakati wa utekelezaji wa mradi huo. Mkataba wa uendeshaji ni miaka mitano na mkandarasi atakabidhi mfumo huo wa TTMS kwa Serikali kupitia TCRA mwezi Oktoba, 2018 na kuwezesha Serikali kumiliki mtambo huo kwa asilimia mia moja.

Mheshimiwa Mwenyekiti, gharama za ujenzi wa mtambo huo kwa mkandarasi yanatokana na malipo yanayotokana na termination fee ya senti 25 kwa simu zinazoingia ndani ya nchi (international incoming calls), mgawanyo ni kama ifuatavyo:-

Mkandarasi analipwa senti nne za dola kwa ajili ya mtambo ule, senti 12 zinakwenda kwa mtoa huduma yaani makampuni ya simu, senti 8 zinakwenda Serikalini na senti moja ya dola inakwenda kwa Mamlaka ya Mawasiliano Tanzania kwa ajili ya kusimamia mtambo huo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, huduma zinazotolewa kwa sasa ni kama ifuatavyo; kusimamia simu za kimataifa (international incoming calls); kusimamia simu za ndani (local off network monitoring); Kusimamia ubora wa huduma (quality of service platform) na kusimamia au kutambua simu za ulaghai (anti-fraud management system).

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba niliarifu Bunge lako Tukufu toka mtambo huo kufungwa mpaka sasa hivi tuna kesi 22 mahakamani na Serikali imepoteza pesa nyingi kupitia wizi huo wa njia za panya. Kwa mfano, mpaka sasa hivi Serikali imepoteza takribani shilingi bilioni 15.2 kupitia wizi wa mawasiliano kwa njia za panya. Kama ingekuwa hakuna mfumo wa TTMS tunaamini wizi ungekuwa mkubwa sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia mtambo huo sasa hivi unaweza kuona miamala ya fedha zote zinazopita hapa nchini kupitia kwenye mitandao ya mawasiliano. Taarifa na takwimu za miamala ya fedha hutumiwa na Mamlaka ya Mapato Tanzania na huwasilishwa BoT. BoT na Mamlaka ya Mapato Tanzania zote zimepewa uwezo wa kuweza kuona takwimu mbalimbali zinazopita kwenye mtambo huu hasa za fedha.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia mtambo huu una uwezo wa kutambua rajisi ya namba za utambulisho wa simu za kiganjani (Central Equipment Identification Register). Kwa sasa mtambo huu hauna uwezo wa kutambua revenue assurance kwa maana ya kutambua mapato ingawa kumefungwa kifaa kwa kila NOC ya mtoa huduma. Network Operative Centre ya Vodacom, Airtel, Tigo kumefungwa sensor kwa ajili ya kupata information hizo lakini bahati mbaya mtambo huu mpaka sasa haujaweza kutambua.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa nini mtambo huu haujaweza kutambua code hiyo ni kwa sababu kulikuwa na mvutano mkubwa baina ya sisi Serikali kwa upande wa TCRA na mkandarasi yule kwa sababu alikuwa anasema hiyo huduma ya revenue assurance ilikuwa haipo kwenye mkataba. Tumevutana nao kwa zaidi ya miezi tisa na mwisho tumekubaliana kwamba aweke platform hiyo ya revenue assurance bure bila ya malipo yoyote na kazi hiyo imeanza.

Tunaamini kwamba itakapofika mwezi Agosti, mkandarasi yule ataweza kuweka mfumo huo na hapo tutaweza kupata malipo sahihi ya simu zetu kupitia kwenye mtambo ule. Naomba nieleze kwamba maoni yako tumeyachukua na tutazidi kuyafanyia kazi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hoja nyingine uliyozungumza ni ya TTCL kwamba Serikali ifanye kila inavyoweza ili kuiwezesha TTCL kwa sababu TTCL ni kampuni ambayo kama itawezeshwa vizuri itakuwa na uwezo wa kuchangia sana pato la Serikali. Serikali tunakubaliana na wewe na tuko kwenye mpango madhubuti wa kuhakikisha kwamba sasa TTCL tunaiwezesha na kuhakikisha kwamba inachangia inavyowezekana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna mambo ya msingi ambayo Serikali tumeyafanya kuiwezesha TTCL. La kwanza kabisa tumeiruhusu TTCL kutumia rasilimali zake zenyewe. TTCL ina rasilimali nyingi ili kuweza kukopa shilingi bilioni 96. Jambo la pili ambalo tumelifanya kwa TTCL kwa sababu kwenye sekta ya mawasiliano issue siyo pesa ni masafa, TTCL tumewapa masafa ya Mhz 1800 kwa ajili ya teknolojia ya 4G LTG. Mpaka sasa hivi TTCL wameweza kufika mikoa kumi na mingine itaendelea mwaka huu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia TTCL tuna mpango wa kuwapa tena masafa mengine mapya ya 800Mhz itakapofika mwezi wa Juni, 2017. Kwa kuiwezesha TTCL tumeipa Data Center kwa ajili ya uendeshaji na inapata malipo kwa uendeshaji huo. Pia TTCL tumeipa kuendesha Mkongo wa Taifa na inapata malipo kupitia mkongo huo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile ulizungumzia kuhusu technology ya internet of things, tumejipanga. TTCL ni kampuni ambayo itaweza kujiingiza kwenye biashara hii ya Internet of things ambayo naamini ikienda kwenye biashara hii na kwa vile ina Mkongo wa Taifa itafanya vizuri sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kuzungumza machache kuhusu sekta ya mawasiliano, naomba sasa nijikite kwenye sekta ya Uchukuzi. Wakati wa majadiliano ya hoja ya Waziri Mkuu pamoja na hoja niliyotoa tokea wiki iliyopita, michango mingi ya Waheshimiwa Wabunge imegusa miundombinu ya reli, huduma za uchukuzi kwa njia ya anga, miundombinu ya bandari na miundombinu ya viwanja vya ndege.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kwanza nianzie na miundombinu ya reli. Reli tunayotumia sasa ya meter gauge imejengwa mwaka 1905 kwa ajili ya mizigo isiyozidi tani milioni tano kwa mwaka. Kwa reli hiyo treni ilikuwa inaenda mwendo kasi mdogo na ilikuwa na uwezo wa kutumia uzani wa tani 11 kwa excel. Mtawala wa Uingereza alipokuja yeye aliibadilisha kidogo treni hiyo badala ya kwenda kwa kutumia
mvuke akaifanya iweze kwenda kwa kutumia kwa diesel na ikawa na uwezo wa tani 14 kwa excel.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hata hivyo, miundombinu ya treni hii kwa sasa imechakaa sana na mwendo wake mkubwa sasa inakuwa kilometa 30 kwa saa. Kwa uchumi tunaotaka kwa viwanda kwa treni hii haiwezekani. Serikali ya Awamu ya Tano imeamua sasa kujenga reli mpya ya standard gauge yenye uwezo wa kubeba mizigo ya tani milioni 17 kwa mwaka. Treni hii itatumia umeme, ni treni ambayo itakwenda mwendo kasi wa kilometa 160 kwa saa kwa treni ya abiria. Reli hii itahimili mzigo mkubwa wa tani 35 kwa excel. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kama mnavyofahamu Mheshimiwa Rais aliweka jiwe la msingi kwa ajili ya ujenzi wa reli hii kutoka Dar es Salaam - Morogoro. Gharama ya ujenzi wa reli hii ilikuwa ni dola bilioni 1.212 za Kimarekani sawa na shilingi trilioni 2.2. Urefu wa njia ambao tumeweka jiwe la msingi ni kilometa 300 ambapo kutoka Dar es Salaam - Morogoro ni kilometa 205 na kilomita 95 ni za mapishano ya reli hiyo. Kwa ujumla itakuwa ni kilometa 300. Katika kujenga reli hii kwa kila kilomita moja tutatumiwa dola za kimarekani milioni nne.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nifanye kidogo comparison na wenzetu wa Kenya. Gharama ya ujenzi wa reli ya Kenya ya standard gauge kutoka Mombasa - Nairobi ni dola za kimarekani bilioni 3.8. Urefu wa njia ya reli ya kutoka Mombasa - Nairobi pamoja na maeneo ya kupishana ni kilometa 609. Kwa hiyo, kwa upande wa Kenya kilometa moja imegharimu dola za kimarekani milioni 6.23 wakati ya Tanzania kila kilometa moja imegharimu dola za kimarekani milioni nne. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hivi tunavyozungumza tumeanza kufanya evaluation kwa ajili ya kumpata mkandarasi wa ujenzi wa kipande cha Morogoro - Makutupora chenye urefu wa kilometa 336. Tunaamini mapema Juni, tutaweza kuweka jiwe la msingi kwa ajili ya ujenzi wa reli kutoka Morogoro - Makutupora.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa upande wa Makutupora - Tabora, Tabora - Isaka na Isaka - Mwanza zabuni zitafunguliwa mwisho wa mwezi huu. Aidha, kwa upande wa matawi ya Kaliua – Mpanda - Karema, Tabora – Kigoma, Uvinza – Msongati zabuni kwa matawi hayo zitatangazwa mara baada ya kukamilika usanifu wa kina ambao utamalizika hivi karibuni.

Mheshimiwa Mwenyekiti, safari ya treni ya abiria kutoka Dar es Salaam mpaka Morogoro kwa kutumia reli ya standard gauge itachukua saa 1.30. Kutoka Dar es Salaam - Dodoma itatumia saa 2.45. Kutoka Dar es Salaam - Mwanza itachukua saa 7.40. Kutoka Dar es Salaam - Kigoma itachukua saa 7.45. Bado tunaangalia uwezo wa kupunguza muda huo kwa kuongeza speed. Tunaamini baada ya Singida tunaweza kuongeza speed kutoka 160 tukaenda mpaka 200 kwa sababu eneo lile lipo tambarale na tunaamini tunaweza kufanya hivyo ili Watanzania hawa sasa waweze kufika maeneo yao kwa muda mfupi zaidi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa upande wa treni ya mizigo kwa kutumia reli hii tunayojenga itakuwa na uwezo kwa kusafirisha mizigo ya tani 10,000 kwa mara moja sawa na makontena 400 ya futi ishirini, ishirini. Hii ni sawa na semi- trailer 500 zenye uwezo wa kubeba tani 20 kwa kila semi- trailer moja. Treni hii itakuwa na mwendo kasi wa kilometa 120 kwa saa. Treni ya mizigo inakuwa tofauti na treni ya abiria, treni ya abiria inakwenda kwa kasi kuliko treni ya mizigo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Waheshimiwa Wabunge vilevile walizungumzia kidogo kuhusu Northern Corridor huko Kenya. Nikilinganisha na wenzetu wa Northern Corridor, treni ya mizigo ya wenzetu itakuwa inachukua makontena 216 kwa wakati mmoja wakati ya Tanzania itakuwa inachukua makontena 400 kwa wakati mmoja. Treni ya mizigo ya wenzetu itakuwa inakwenda mwendo wa kilometa 80 kwa saa wakati ya Tanzania itakuwa inakwenda kilometa 120 kwa saa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa mfano kutoka Dar es Salaam - Kigali ambapo urefu ni kilometa 1,461, mzigo kutoka bandari ya Dar es Salaam mpaka Kigali itachukua saa 13 kwa kutumia treni yetu. Kutoka Mombasa - Kigali (Rwanda) ni kilometa 1,659.3. Kwa hiyo, treni ya mizigo kutoka bandari ya Mombasa - Kigali itachukua saa 21, mara mbili ya muda ambao itachukua treni yetu. Naamini kabisa ndani ya moyo wangu kwa kasi tunayokwenda nayo treni hii itamalizika haraka na naamini kabisa mizigo ya Rwanda, Burundi, DRC na hata ya Uganda hapo baadaye itapita kwenye bandari yetu ya Dar es Salaam. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kulikuwa na hoja juu ya fedha za ujenzi wa reli. Lengo la Serikali ni kujenga mtandao wa reli kwa kutumia fedha za ndani na za mkopo wenye masharti nafuu. Kipande cha Dar es Salaam - Morogoro katika mwaka wa fedha 2016/2017 tulitenga shilingi trilioni moja na bajeti hii ambayo tutaipitisha leo tumetenga shilingi bilioni 900. Kutokana na mahitaji makubwa ya fedha za ujenzi wa reli, Serikali imeendelea kufanya mazungumzo na wafadhili mbalimbali ikiwemo Serikali ya Uturuki, China na wengine ili kupata mikopo yenye masharti nafuu. Kwa mfano, wiki iliyopita Serikali kupitia RAHCO ilikuwa na mazungumzo na mabenki matano kutoka nje kuhusu kupata mkopo wa bei nafuu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kulikuwa na hoja kuhusu ujenzi wa reli ya Mtwara – Mbamba Bay na matawi yake ya kwenda Liganga na Mchuchuma yenye urefu wa kilometa 1,000. Mwaka wa fedha 2017/2018 tunategemea kutangaza zabuni kwa ajili ya kumpata mkandarasi, lakini reli hii tutaijenga kwa mfumo wa PPP.

Kuhusu ujenzi wa reli ya Tanga – Arusha - Musoma, katika mwaka wa fedha 2017/2018, Serikali imetenga shilingi bilioni moja kwa ajili ya kazi ya upembuzi na usanifu wa kina wa ujenzi wa reli hii. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia kulikuwa na hoja kuhusu TAZARA kwamba Serikali ina mikakati gani ya kuifanya TAZARA iweze kujiendesha kwa faida. Reli ya TAZARA iliyosanifiwa kubeba tani milioni 5 za mzigo kwa mwaka ili kusafirisha tani hizo unahitaji injini au locomotives 174. Kwa hivi sasa TAZARA inasafirisha tani 128,105 kwa mwaka. Sasa hivi TAZARA ina wastani wa vichwa 13 tu ambavyo vinatumika kwa mwaka. Ili TAZARA kuweza kusafirisha mzigo tani 1,273,000 zilizoweza kusafirishwa mwaka 1977/1978 inahitaji vichwa vya treni 48. Injini hizi 13 zilizopo sasa ni asilimia 27 ya vichwa vyote vinavyohitajika ambavyo vilitumika mwaka 1977/1978.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ili kuisaidia TAZARA, Serikali tumejipanga kama ifuatavyo; kwanza, Serikali ya Tanzania kupitia bajeti hii tumepanga kuweka shilingi bilioni 26 kwa ajili ya kusaidia TAZARA. Tunaamini na wenzetu wa Zambia watatenga kiasi kama hicho ili kuweza kuisaidia TAZARA. Pili, tayari Serikali zetu mbili zimefanya mabadiliko makubwa ya viongozi wa ngazi za juu ikiwa ni pamoja na kuajiri Mtendaji Mkuu mpya, Naibu Mkurugenzi Mtendaji Mkuu mpya na Meneja wa Mkoa wa Tanzania mpya na kinachoendelea sasa ni uajiri wa Meneja wa Mkoa wa Zambia ambao uko katika hatua za mwisho za kiutawala.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ili kuisaidia TAZARA iweze kufanya biashara sasa hivi tupo kwenye mpango wa kufanya marekebisho ya Sheria Na.4 ya mwaka 1995. Wataalam wa nchi zote mbili wapo kwenye hatua ya mwisho kukamilisha marekebisho hayo. Baada ya hapo marekebisho hayo yatapelekwa kwenye Baraza la Mawaziri na mwisho yatakuja kwenye Bunge lako Tukufu ambalo tunaamini litaweza kupitisha marekebisho hayo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba sasa nijikite kwenye huduma za uchukuzi kwa njia ya anga. Mwaka jana niliahidi kuanza kuchukua hatua za kulibadilisha Shirika la Ndege la Tanzania (ATCL) ili hatimaye liweze kujiendesha kibiashara. Tayari tumeunda Bodi mpya na Menejimenti yenye weledi na uzalendo wa hali ya juu kuiendesha kampuni hii ambapo mpaka sasa hivi tunajua itakapofika mwaka 2018 itakuwa na ndege mpya sita. Bodi na Menejimenti ya ATCL zinaendelea na taratibu za kuirudisha kampuni hii kwenye Chama cha Watoa Huduma za Usafiri wa Anga Duniani Ili mtu akiwa eneo lolote lile duniani aweze kununua tikiti bila usumbufu wowote. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika mwaka wa fedha 2016/2017 zilitengwa shilingi bilioni 500 fedha za ndani kwa ajili ya ununuzi wa ndege. Tayari Serikali imenunua ndege tatu za Bombadier Q400 zenye uwezo wa kubeba abiria 76 kila mmoja na kulipa malipo ya awali ya ndege mbili ya aina ya CS Series 300 zenye uwezo wa kubeba abiria 127 kila moja. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia Serikali imelipa pesa za awali za ndege ya masafa marefu ya aina ya Boeing 787-8 dreamliner yenye uwezo wa kubeba abiria 262. Katika kipindi cha bajeti 2017/2018 zimetengwa shilingi bilioni 500 kwa ajili ya kukamilisha malipo ya ndege zilizotajwa hapo juu pamoja na malipo ya ndege nyingine mpya ya masafa marefu ya aina ya Boeing 787-8 Dreamliner. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nizungumzie ndege 12 za terrible teens. Siku tatu zilizopita tumesikia maneno mengi hapa Bungeni na kwenye mitandao kuhusu ndege 12 za terrible teens ambazo zimeundwa na Boeing. Terrible teens ni ndege za mwanzo aina ya Dreamliner 787 zilizotengenezwa na Boeing miaka sita, saba iliyopita huko nyuma. Ndege hizo ni nzito kidogo ikilinganishwa na ndege za kisasa za Dreamliner 787-8, zina uzito wa zaidi ya tani nne mpaka sita ukilinganisha na ndege za kisasa za dreamliner. Ndege hizi zina upungufu, kwa sababu ndege hizi ni nzito kwa hiyo zinakula mafuta zaidi ukilinganisha na ndege za kisasa. Pia ndege hizi hazina uwezo wa kwenda masafa ya mbali kwa mfano kutoka Dar es Salaam mpaka New York inabidi ziende mpaka sehemu zijaze mafuta ili ziweze kuendelea. Ndege za kisasa za Dreamliner zinaweza kutoka Dar es Salaam mpaka New York bila kunywa mafuta na ikafika New York na ikaanza safari kwa kunywa mafuta huko New York.

Mheshimiwa Mwenyekiti, terrible teens zinazozungumzwa hapa, kawaida ndege tunaitaja kwa line number kwa hiyo mimi nitataja line number. Terrible teens zinazozungumzwa hapa ni line number 4 na ya pili ni line number 5. Ndege hizi mbili sasa hivi zinatumiwa na Boeing as a test aircraft. Ndege nyingine inayozungumzwa hapa ni line number 10 ambayo Ethiopian Airways wameshaonesha nia ya kuinunua. Ndege nyingine inayozungumzwa ni line number 11 ambayo inatumiwa na Boeing Bussiness Jet. Ndege nyingine inayozungumzwa ambazo zina uzito mkubwa Line number 12 ambayo Ethiopian Airways imeonyesha interest ya kuichukua. Ndege nyingine ni Line 13 na 14 ambazo vilevile Ethiopian Airways imeonyesha interest ya kuichukua. Ndege nyingine ni line 15 ambayo kuna kampuni moja ya Air Australia imeichukua; Line 16 Ethiopian Airways imeonyesha nia ya kuichukua; Line 17 Ethiopian Airways imeonyesha nia ya kuichukua; Line 18 Ethiopian Airways imeonyesha nia ya kuichukua na Line 19 kulikuwa na maneno kwamba Rwanda Air inaweza kuichukua lakini mpaka sasa hivi haijawekwa vizuri na Line 22 kuna kampuni ya Air Australia imeonyesha kuichukua.

Mheshimiwa Mwenyekiti, si kweli kwamba ndege iliyonunuliwa na Serikali kwa Shirika la Ndege la Air Tanzania Boeing 787-8 Dreamliner ni miongoni mwa ndege 12 za terrible teens dreamliners ambazo zilikosa soko. Tuna ushahidi wa kutosha kuhusu jambo hili. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali imeingia mkataba na Boeing wa kutengeneza ndege mpya yenye line number 719. Ndege inayozungumzwa hapa kwamba tumeichukua ilikuwa iende Rwanda ina line number 19, yetu sisi ni line number 719, ni tofauti. Pia Serikali imeweka ratiba ambayo tutaifuatilia ndege hiyo hatua kwa hatua. Kinachoendelea sasa hivi tunachagua injini ya ndege. Dreamliner inatumia injini za aina mbili, inatumia Rolls-Royce na General Electric (GE). Kabla ya ndege kumalizika mnapewa uhuru wa kuchagua, tunalolifanya sasa hivi ATCL ni kuchagua injini gani tuweke kwenye ndege ile kwa vile ndege hii ni mpya sio kama maneno yaliyoletwa kwenye mitandao. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nawaomba sana Waheshimiwa Wabunge wakiwa na jambo kama hili ambalo linahitaji maelezo ya kitaalam wawasiliane na sisi Serikalini. Tupo saa 24, siku saba kwa wiki, siku 365 kwa mwaka, Serikali ipo. Waheshimiwa Wabunge, elimu haina mwisho naomba tujifunze. Pia naomba sana Waheshimiwa Wabunge tushirikiane kujenga Shirika letu la Ndege la ATCL, tushirikiane kujenga nchi yetu, hatuna nchi nyingine Waheshimiwa Wabunge, maendeleo hayana chama sisi sote tunahitaji maendeleo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, maelezo yaliyoelezwa katika tovuti ya Boeing ni sahihi katika mantiki ya kisoko maana bei iliyowekwa katika tovuti hiyo ambayo walisema Tanzania wamenunua ndege kwa pesa hizo ni sahihi. Ile bei iliyowekwa pale ni list price, ni bei ya ndege, lakini wakati wa kununua ndege kunakuwa na mazungumzo marefu. Pamoja na kuwekwa bei hiyo kwenye tovuti, mazungumzo marefu yalifanyika na tulipewa punguzo kubwa sana, Serikali ilipata bei nzuri. Naomba niwahakikishie Waheshimiwa Wabunge na Watanzania wenzangu Serikali imenunua ndege mpya aina ya Boeing 787-8 Dreamliner, ndege ya kisasa na kwa bei nafuu sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimemaliza hilo la ndege, naomba sasa nijikite kwenye hoja ya Mheshimiwa ambaye alitaka kujua Air Tanzania kama tumeuza route zetu kwa South Afrika. Route za ndege haziuzwi ni mali ya nchi. Route za ndege zinapatikana kwa kuweka makubaliano ya nchi na nchi. Kwa hiyo, route zote za Air Tanzania bado ni mali ya Tanzania na wakati wowote tutaweza kuipa Air Tanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hivi navyozungumza na ninyi Air Tanzania inafanya tathmini ya njia zitakazoweza kuhudumiwa na ndege za masafa ya kati na masafa marefu. Njia hizo zitajumuisha zile zilizokuwa zikihudumiwa hapo zamani yaani njia ya kuendea Oman, Dubai, London, Entebe, Nairobi, Johannesburg, Lusaka na Bujumbura.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia Mheshimiwa Mbunge alisema wenzetu wa Kenya Airways wameuza route yao kutoka Nairobi kwenda London sijui kwa dola milioni 20. Narudia tena route haiuzwi ni makubaliano ya nchi na nchi. Ninavyofikiria Kenya Airways walichowauzia Oman Air ni slot ya kuingia pale Heathrow Airport kwa sababu kuingia Heathrow Airport ni very expensive. Kwa kila sekunde tano Heathrow Airport kunaruka ndege. Walilolifanya wao ni kuzungumza na Kenya Airways wapate ile slot, lakini si kuwauzi route, si sahihi. Sisi tukitaka kwenda London, London kuna Airport tatu; Heathrow Airport, City Airport na Luton Airport. Hizi mbili kwa maana ya City Airport na Luton ni rahisi, bei yake sio kama Heathrow. Naomba kuwaambia Waheshimiwa Wabunge na Watanzania kwamba ATCL hawajauza routes na imejipanga kwenda route zote. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, najua muda unanikimbia lakini nizungumze tu lingine, Mheshimiwa Mbunge aliuliza kwa miaka kumi Mamlaka ya Usafiri wa Anga imekusanya kiasi gani na Zanzibar imepeleka kiasi gani? Mamlaka ya Usafiri wa Anga haikusanyi mapato, kazi yake kubwa ni kuangalia usalama wa nchi ya Tanzania. Mapato yanayokusanywa na Mamlaka ya Anga yanatumiwa kwa ajili ya kununua vifaa mbalimbali vya kuangalia usalama wa anga letu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwaka 2008 Serikali ya Zanzibar kwa bahati mbaya sana iliamua kuchukua mapato yanayotokana na tozo za abiria kwa upande wa Airport ya Zanzibar, lakini Mamlaka ya Usafiri wa Anga haitakiwi kuipa Serikali ya Muungano wala Serikali ya Zanzibar. Jambo hili lipo kwenye sheria ya kuunda mamlaka hii kwa hiyo hakuna pesa yoyote kwa kipindi cha miaka kumi ambayo tumeipeleka Zanzibar sababu sheria hairuhusu hilo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kwa haraka haraka nijikite na hoja ya bandari. Kulikuwa na hoja kwamba taasisi zilizopo pale bandarini ziweze kufanya kazi saa 24. Tunavyozungumza taasisi mbalimbali zilizopo pale bandarini zinafanya kazi saa 24. Nachukua fursa hii kuwaomba wateja wetu na mawakala wetu wa forodha kupata huduma bandarini wakati wowote ndani ya saa 24.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna suala la gharama kuongezeka kutokana na VAT kwa huduma zinazotolewa kwa wakala wa mizigo inayosafirishwa kwenda nchi za jirani. Ushauri huu tumeuchukua, tunaufanyia kazi na tutaupeleka Wizara ya Fedha ili uweze kufanyiwa kazi zaidi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kulikuwa na hoja ya kupunguza tozo ya dola 23 ya Kimarekani kwa tani kwa mzigo wa shaba ambapo bandari nyingine shindani kwa mfano Durban zinatoza dola za Kimarekani 17.86. Ni kweli mzigo wa shaba hutozwa dola 23 kwa tani, hata hivyo tozo za Bandari za Dar es Salaam hufanyika kwa dola za Kimarekani wakati bandari ya Durban mzigo hutozwa kwa rand yaani currency ya South Africa. Hali hii husababisha gharama za bandari za Durban kuwa ndogo wakati sarafu hiyo inapokuwa dhaifu ikilinganishwa na dola hasa sasa hivi ambapo exchange rate dola moja ni rand 13.41.

Aidha, tozo kwa upande wa Bandari ya Dar es Salaam hupungua hadi kufikia dola 17 kutegemeana na kiasi cha mzigo na hali ya ushindani. Kwa vile hatuko fixed tunajaribu kuwa flexible na tunabadilika sana.

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MWENYEKITI: Nakuongezea dakika mbili lakini vilevile tujibu kuhusu share za Serikali ambazo ziko Airtel.

WAZIRI WA UJENZI, UCHUKUZI NA MAWASILIANO: Mheshimiwa Mwenyekiti, kama tunavoyojua Bandari ya Dar es Salaam ina changamoto kubwa kuhusu miundombinu, lakini tuna mradi ambao sasa tumejipanga kuhakikisha kwamba tunaboresha kina cha maji cha Bandari ya Dar es Salaam na pia kujenga gati mpya kwa ajili ya kuteremshia magari.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sitakuwa na muda wa kwenda kwenye barabara lakini Mheshimiwa Naibu Waziri amezitaja nyingi. Waheshimiwa Wabunge hatutaweza kujibu kila kitu hapa muda hauwezi kuturuhusu lakini mjue tu kwamba maelezo na ushauri wenu hasa kwenye kuangalia sera ya barabara ya kuunganisha mikoa mbalimbali tumeichukua na tutaifanyia kazi kuhakikisha kwamba mikoa yote ya Tanzania inaunganishwa kwa barabara. Hatuwezi kuingia kwenye uchumi wa kati bila kuunganisha mikoa yetu yote na barabara. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nimalizie kwa kusema kuwa bajeti ya Wizara yangu mwaka 2017/2018 ni bajeti ya kuanza kuweka mazingira ya uwekezaji kwenye sekta ya viwanda na kuinua uchumi wa nchi yetu kijumla ili uchumi wa kipato cha kati ifikapo mwaka 2020/2025 uweze kufikiwa. Kama nilivyoliomba Bunge lako Tukufu mwanzo wa hotuba yangu ndivyo ninavyomalizia kwa kuwaomba tuunganishe nguvu zetu kwa kushirikiana na Waheshimiwa Wabunge katika kutekeleza malengo ya Wizara yangu. Kwa kufanya hivyo, nchi yetu itafikia uchumi wa kati ifikapo mwaka 2020/2025.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya maelezo hayo sasa...

MWENYEKITI: Mheshimiwa Waziri subiri kwanza, share za Serikali ziko Airtel zinafanya nini? Airtel mpaka leo haijatoa faida kwa nini msizichukue mkazipeleka TTCL? (Makofi)

WAZIRI WA UJENZI, UCHUKUZI NA MAWASILIANO: Mheshimiwa Mwenyekiti, wewe ni Mwenyekiti ukiuliza swali lazima nilijibu. Kwa heshima yako, tumelichukua wazo lako kuhusu share za Serikali ndani ya Airtel na tunalifanyia kazi. Ni jambo ambalo tunatakiwa tufanye utafiti wa kina, tufanye mambo mengi ya kitaalam, siyo jambo ambalo naweza kutoa jawabu hapa kwa sababu jambo la shares watu ile ni business yao. Hata hivyo, tumelichukua na tutalifanyia kazi tu haina shida. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya maelezo hayo, sasa naomba kutoa hoja.