Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Hotuba ya Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018.

Hon. Lolesia Jeremia Maselle Bukwimba

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Busanda

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Hotuba ya Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018.

MHE. LOLESIA J. BUKWIMBA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipa nafasi ili na mimi niweze kuchangia Wizara muhimu kabisa Wizara ya Afya.

Kwanza nianze kwa kutoa pongezi kwa Mheshimiwa Rais John Pombe Magufuli kwa kazi kubwa anayoifanya ndani ya Taifa letu hasa katika suala la maendeleo kwa ujumla. Wote tunaona kazi inayofanyika ndani ya nchi yetu kwa kipindi kifupi cha mwaka mmoja na tunaona mambo makubwa yanafanyika kwa namna ya kipekee. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia nichukue nafasi hii kumshukuru sana Mheshimiwa Waziri Ummy Mwalimu kwa kutupatia gari la wagonjwa katika Kituo cha Afya Katoro. Napenda kutoa salamu hizi kutoka kwa wananchi wa Jimbo la Busanda hasa Katoro, salamu hizi kwa kweli wamekushukuru na wamekupongeza wamefurahia sana na wanasema hakika vifo vya akinamama vitakwisha sasa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile nichukue nafasi hii kumshukuru Mheshimiwa Naibu Waziri Kigwangalla, kupitia wataalam wa taasisi ya AMREF walikuja kuzindua mradi mkubwa sana wa kuweza kuboresha huduma za afya katika Kituo cha Afya Chikobe, Zahanati ya Nyamalimbe, Zahanati ya Rwamgwasa pamoja na Kituo cha Afya cha Kashishi. Kwa hiyo, kipekee nitumie fursa hii kushukuru sana AMREF kwa kazi kubwa kuweza kuungana pamoja na Serikali katika kuboresha huduma hizi kwa wananchi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile nichukue nafasi hii kuwashukuru GGM kwa kuweza kujenga mochwari pale katika Kituo cha Afya Katoro. Hakika ushirikiano huu pamoja na Serikali yetu inaonesha jinsi ambayo tutaweza kutatua changamoto mbalimbali za afya katika sehemu mbalimbali katika Taifa letu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya shukrani hizo, napenda kuzungumzia suala la watumishi. Katika sekta ya afya kweli kuna upungufu mkubwa sana wa watumishi, nikiangalia katika Halmashauri yangu ya Wilaya ya Geita kuna upungufu mkubwa sana, mahitaji ni watumishi 824, waliopo ni watumishi 345, kwa hiyo upungufu ni mkubwa sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nitumie fursa hii kwa kuwa Serikali inakusudia kutoa ajira iangalie upungufu huu katika Halmashauri ya Wilaya yangu ya Geita, ndiyo maana kunatokea hata hivi vifo, vilevile kunatokea changamoto mbalimbali kwa sababu kuna upungufu mkubwa sana wa wataalam wa afya hasa katika sehemu za vijijini ambapo kunakuwa na upungufu mkubwa zaidi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile nimesoma hii bajeti ambayo Mheshimiwa Waziri ameiwasilisha, kipekee sijaweza kuona ujenzi wa hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Geita. Ninaomba katika majumuisho Mheshimiwa Waziri uweze kutueleza wananchi wa Geita kwamba kuna mpango gani sasa wa kuanzisha ujenzi wa Hospitali ya Rufaa katika Mkoa wa Geita.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninasema hivyo kwa sababu hospitali ambayo sasa hivi imepewa hadhi kuwa ya rufaa ni Hospitali ya Wilaya ya Geita na sababu hiyo hatuna kabisa hospitali ya Wilaya kwa sasa. Tunaomba Serikali ione umuhimu sasa wa kuanzisha hospitali ya Mkoa ili kurahisisha huduma kwa wananchi wa Mkoa wa Geita. Kumbuka Mkoa wa Geita tuna watu wengi sana zaidi ya milioni moja, kwa sababu hiyo tunahitaji huduma. Nichukue fursa hii kumuomba Mheshimiwa Waziri muangalie uwezekano wa kipaumbele katika kuhakikisha kwamba tunapata Hospitali ya Mkoa wa Geita. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile katika suala la mama na mtoto, nilikuwa nikiangalia bajeti, ninapenda kuunga mkono hoja ya Kamati ya Bunge ambayo imezungumzia katika ukurasa wa 33, kutokana na kwamba bajeti imepunguzwa hasa katika kupunguza vifo vinavyotokana na uzazi kwa asilimia 33.8. Mimi naungana na Kamati, kuona kwamba Serikali iangalie umuhimu wa kuweza kuongeza bajeti hii kwani akina mama wengi wanakufa kutokana na suala la kujifungua. Kwa vile tunapunguza bajeti maana yake ni kwamba tatizo hili litashindwa kutatulika kwa sababu bajeti imepunguzwa.

Kwa hiyo, niiombe Serikali iangalie uwezekano mkubwa wa kuendelea kuongeza bajeti hasa katika suala hili, ili kuwezesha kupunguza vifo vya kina mama hasa wakati wa kujifungua na katika uzazi baada ya kujifungua. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la afya ni suala muhimu sana. Serikali kupitia Sera ya Taifa inasema kwamba kila kijiji tuwe na zahanati, kila kata tuwe na kituo cha afya. Suala hili ukiangalia kiuhalisia hasa katika sehemu mbalimbali Tanzania na hasa nikiangalia kwenye Jimbo langu tuna upungufu mkubwa kabisa. Mimi ninazo kata 22, lakini katika kata hizo ninavyo vituo vya afya vinne tu, hivyo bado tatizo ni kubwa. Naiomba Serikali iwekeze zaidi katika kuhakikisha kwamba iweze kutekeleza sera yake ambayo ni kuwa na kituo cha afya kwenye kila kata na kila kijiji tuwe na zahanati ili kuweza kuboresha huduma hasa kwa akina mama wajawazito pamoja na watoto. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda pia kuzungumzia suala la watoto wetu wa kike waliopo hasa katika sekondari. Wakati wa hedhi, tunaomba Serikali iwaangalie watoto hawa tuweze kutoa hivi vifaa vya kujihifadhi, kutokana na kwamba wengine wanashindwa hata kuendelea na masomo kwa sababu hiyo.

Kwa hiyo, niombe katika bajeti hii iangalie uwezekano kwenye shule zetu za sekondari watoto wapewe huduma hii, wapewe vifaa vya kujihifadhi, wengine wanashindwa kuendelea na masomo hasa kipindi hicho wanashindwa ku- concentrate katika masomo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nichukue nafasi hii kuiomba Serikali kama bajeti haijapangwa basi waangalie namna ya kuipanga ili kuweza kunusuru watoto wetu ili waweze kuendelea mbele zaidi hasa watoto wa kike ambao wapo shuleni. Sambamba na hilo nilikuwa naomba pia Serikali ipunguze kodi, iondoe kodi kabisa zile pad ziwe zinaingia free zisiwe na kodi zozote. Hii itawezesha pia akina mama pamoja na wasichana kuweza kupata vifaa hivi kwa bei nafuu ili waweze kujihifadhi. Kwa sababu hali ya hedhi ni hali ya kawaida tu ambayo Mwenyezi Mungu ameiweka kwa wanawake, ni nature, kwa hiyo Serikali inatakiwa ituangalie wanawake, iangalie namna yakutusaidia na kutu-support. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika suala la maendeleo ya jamii, ninapenda kuungana na wenzangu, kusema kwamba Halmashauri nyingi kwa kweli hazitilii mkazo suala la maendeleo ya jamii. Haiwezekani kama tutaweza kushindwa kusimamia sekta ya maendeleo ya jamii, hatutaweza kufikia maendeleo ambayo tumekusudia katika nchi yetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunasema nchi yetu tunaelekea kwenye viwanda, tutafikaje kwenye viwanda bila kuimarisha sekta ya maendeleo ya jamii? Hivyo nitumie fursa hii kuiomba Wizara iweke mkazo…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja.