Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Hotuba ya Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018.

Hon. Felister Aloyce Bura

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Hotuba ya Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018.

MHE. FELISTER A. BURA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi ya kuchangia na pia nampongeza Mheshimiwa Ummy, Waziri wa Afya pamoja na Watendaji wote wa Wizara kwa kazi ambazo tunaziona kwa macho pamoja na ukata wa fedha ambazo wanazipata kwa mwaka.

Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kuongelea kituo chetu cha afya kile kilichopo pale Chamwino - Ikulu, ni kituo ambacho kingeweza kuwa mfano kwa vituo vingi vya afya, lakini kile kituo hakina watendaji, hakina madaktari, hakina wauguzi, hakina vifaa tiba kituo ambacho kiko kwenye geti la Ikulu.

Mheshimiwa Waziri, ninaiomba Serikali sasa kwamba kituo kile kitazamwe kwa macho ya huruma ili wananchi wa Wilaya ya Chamwino waweze kupata huduma nzuri karibu na geti la Ikulu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninaiomba Serikali kukamilisha majengo ya kituo cha afya Mima na Mbori. Vituo hivi vya afya vina zaidi ya miaka kumi havijakamilika. Kati ya wale wanawake 556 wanaokufa kwa mwaka, wanawake walio jirani na kituo cha afya Mima na Mbori ni kati ya hao wanawake 556.

Mheshimiwa Ummy nitafurahi sana ukiacha alama katika Wizara hii maana wewe ni mwanamke mwenzetu, wewe ni mwanamke kama wanawake wanaopata mimba na kupata matatizo makubwa. Nikusihi, ninajua bajeti yako siyo kubwa, una bajeti kidogo sana na niwasihi Waheshimiwa Wabunge tutakapokuja kujadili bajeti kubwa tuhakikishe kwamba Wizara hii inapata fedha za kutosha kwa sababu ndiyo Wizara inayoangalia afya za Watanzania. (Makofi)

Mheshimiwa mwenyekiti, hata wanawake ambao wanatamani kupata huduma ya ugonjwa wa cancer, kujua afya zao hawapati kwa sababu vituo vyetu havina wataalam. Sasa ukitaka kupunguza wagonjwa katika hospitali zetu za rufaa lazima uimarishe vituo vya afya, lazima uimarishe zahanati zetu na unaziimarisha kwa huduma, kwa kuwa na watendaji wa kutosha.

Nikusihi na niisihi Serikali yangu sikivu, sasa kwamba sasa ifike wakati kwamba zahanati zetu zinaimarishwa, vituo vya afya vinakuwa na watendaji wa kutosha, vifaa tiba na wahudumu wa kutosha kwa ajili ya Watanzania.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimeona Taasisi ya Jakaya Kikwete imefanya kazi kubwa ya kukoa shilingi bilioni 3.75, lakini fedha walizopewa pamoja na kuomba shilingi bilioni nne wamepata shilingi milioni 500 tu. Hivi wanaweza wakafanya nini? Wamefanya kazi kubwa kwa Watanzania, wameokoa Watanzania walio wengi. Naomba Serikali yetu iiangalie taasisi hizi ambazo zinafanya kazi za kuwasaidia Watanzania katika kuimarisha afya zao. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia tusiwavunje moyo Madaktari Bingwa wetu, wasomi hawa tusiwavunje moyo, kama ni fedha wapelekewe ili ziwasaidie katika kutoa huduma.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia nizungumzie dirisha la wazee. Hospitali zetu zina dirisha la wazee, lakini je, dirisha la wazee kuna dawa? Wazee ni asilimia sita tu ya Watanzania lakini je, wanapata dawa katika dirisha lao?

Mheshimiwa Mwenyekiti, tuliandika andiko maalum kwa ajili ya kituo cha afya Bahi, mpaka leo wanawake wanakufa kule Bahi kwa sababu ya kukosa huduma muhimu katika kituo cha afya Bahi tena kiko barabarani, kingesaidia na ajali zinazopatikana maeneo yale. Hawana x-ray, hawana huduma yoyote yaani ni kituo cha afya duni sana, lakini ni kituo cha afya cha Wilaya. Sasa hivi Wilaya ya Bahi ina zaidi ya mika kumi tangu ianzishwe.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nizungumzie pia wodi ya wazazi Hospitali ya Mkoa. Tulikuomba shilingi bilioni moja tu mwaka jana ulipotembelea ile hospitali, tukakuamini Dada Ummy kwamba utatufikiria na utatuombea hizo hela...

(Hapa kengele ililia kuashiria kuisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MHE. FELISTER A. BURA: Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja.