Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Hotuba ya Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018.

Hon. Hamida Mohamedi Abdallah

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Lindi Mjini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Hotuba ya Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018.

MHE. HAMIDA M. ABDALLAH: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipa nafasi. Nianze kwa kumpongeza Mheshimiwa Waziri Ummy kwa uwasilishaji wa taarifa yake, iliyosheheni afya za Watanzania.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niipongeze sana Serikali kwa jitihada kubwa inayofanya katika kuimarisha na kuboresha afya zetu Watanzania. Lakini niendelee kuipongeza Serikali kwa kutuunganisha Watanzania katika mfumo rasmi wa bima ya afya. Nimpongeze kwa dhati kabisa Mkeshimiwa Waziri Ummy na Naibu wake kwa jitihada kubwa sana waliyoifanya katika kampeni ya kuhamasisha mfuko huu wa bima ya afya. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pale kwetu Lindi tunashukuru kwa dhati kabisa, Mheshimiwa Waziri Ummy aliandaa utaratibu wa kampeni rasmi, japokuwa yeye hakufika lakini wawakilishi wake walifanya kazi na jitihada kubwa ilionekana na tuliweza kuongeza idadi ya watu wanaotumia bima ya afya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na jitihada hizi kubwa zinazoonekana za kuimarisha na kuboresha afya za Watanzania, bado tuna changamoto kubwa sana. Katika upande huu wa bima ya afya inaonekana watumiaji wa bima ya afya ni wengi lakini upatikanaji wa dawa umekuwa ni duni kabisa. Kwa hiyo, naiomba Wizara kuimarisha katika eneo hili la upatikanaji wa dawa ili wananchi waweze kupata tiba vizuri kabisa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika hospitali yetu ya Mkoa wa Lindi tuna changamoto mbalimbali. Tuna changamoto kubwa sana ya Madaktari Bingwa, kwa sababu Hospitali ya Sokoine Mkoa wa Lindi ni Hospitali ya Rufaa ya Mkoa, wateja wake wakubwa ni wananchi kutoka Wilaya zote za Mkoa wa Lindi, hivyo tunahitaji Madaktari Bingwa katika Hospitali yetu ya Sokoine.

Mheshimiwa Waziri Ummy alituahidi kutupatia madaktari wanne, ningependa kujua madaktari hawa watakuja lini katika hospitali ya Mkoa wa Lindi?

Mheshimiwa Mwenyekiti, Hospitali ya Lindi ni hospitali kongwe iliyojengwa mwaka 1954, naishukuru sana Serikali kwa kuifanyia ukarabati wa kutosha na majengo yanaonekana ni mazuri, majengo nadhifu, yanapendeza lakini bado tuna changamoto kubwa ya miundombinu ya maji taka. Ninaiomba sana Serikali kusimamia katika eneo hili ili hospitali hii iweze kuwa na miundombinu ya maji machafu katika mfumo mzuri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia upatikanaji wa maji safi pale Sokoine ni mdogo kabisa, tunajua hali ya mji wa Lindi hakuna kabisa maji, wananchi wa Lindi bado tunaendelea kupata shida, lakini bado tunaendelea kuiamini Serikali yetu na jitihada kubwa inayofanya ya kuimarisha upatikanaji wa maji katika Mji wa Lindi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia bado katika hospitali ya Sokoine kuna changamoto kubwa sana ya x-ray. X-ray iliyopo imeshapita muda wake wa matumizi, inashindwa kufanya kazi na wagonjwa wanashindwa kupata huduma hii ya x-ray. Ninamuomba kwa dhati kabisa Mheshimiwa Waziri Ummy kuitazama Lindi Sokoine ili tuweze kupata x-ray mpya iweze kuwahudumia wananchi wa Mkoa wa Lindi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninamuomba Mheshimiwa Waziri Ummy, hospitali ya Wilaya ya Kilwa katika eneo la mortuary hakuna majokofu ya kutunza maiti pale, ninaomba kwa dhati kabisa Mheshimiwa Waziri Ummy tuitazame Wilaya ya Kilwa ili wahakikishe katika eneo lile la mortuary tunapatiwa majokofu ili tuweze kufanya kazi zetu vizuri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tuna hospitali ya Wilaya ya Liwale, tunayo x-ray pale katika hospitali ya Wilaya lakini mtaalam wa ku-operate mashine hizi za x-ray hakuna, Mheshimiwa Waziri Ummy tunaomba utuangalie...

(Hapa kengele ililia kuashiria kuishakwa muda wa Mzungumzaji)

MHE. HAMIDA H. ABDALLAH: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kuunga mkono hoja, ahsante sana.