Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Hotuba ya Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018.

Hon. Hawa Abdulrahiman Ghasia

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Mtwara Vijijini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Hotuba ya Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018.

MHE. HAWA A. GHASIA: Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda nikushukuru kwa kunipa nafasi nami kuweza kuchangia. Napenda nianze kwa kumpongeza Mheshimiwa Waziri, Naibu wake pamoja na watendaji wote wa sekta ya afya ambayo kwa kweli wanafanya kazi nzuri, ngumu na yenye changamoto kubwa lakini bado wanaonesha kuimudu, kwa hiyo napenda nimpongeze sana. Mheshimiwa Waziri amesoma hotuba yake vizuri ambayo inaonesha anajiamini lakini pia sekta hii anaijua vizuri. Ameonesha malengo bayana ambayo anakusudia katika bajeti hii kutatua kero ambazo ziko ndani ya sekta ya afya. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimshukuru Mheshimiwa Waziri kwa kunisaidia kunipatia gari la wagonjwa kwa ajili ya Kituo cha Afya cha Kitele, kwa kweli namshukuru sana. Pia nimshukuru Mheshimiwa Naibu Waziri TAMISEMI kwa kutoa ufafanuzi kuhusu suala la upanuzi wa Kituo cha Afya Nanguruwe na Nanyumbu kuwa hospitali ya Wilaya, kwa sababu ilileta mkanganyiko mkubwa sana, kwa hiyo nawashukuru sana kwa hilo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kutoa maombi yafuatayo kwa Serikali. Ombi la kwanza ni kwamba bajeti hii iliyotengwa kwa kweli inatosha. Tunachoomba ni Wizara ya Fedha kuhakikisha kwamba pesa hizo zinakwenda kwa wakati ili yale tuliyoyapanga yaweze kutekelezwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ombi la pili, namwomba Mheshimiwa Waziri wa UTUMISHI, kwa dhati kabisa, kama ambavyo wanatoa vibali vya kuajiri Walimu basi awamu hii wajitahidi na Sekta hii ya Afya itolewe vibali vya kuajiri. Kwa kweli hali ni mbaya sana kwenye vituo vya afya hasa kutokana na huu uhakiki wa vyeti uliofanyika, vijijini kwetu huko kumeathirika zaidi kuliko hata mijini. Kwa hiyo tunaomba watoe vibali vya kuajiri Madaktari, Wauguzi pamoja na Matabibu. Kama wangesema sekta moja tu ipewe kibali, basi mimi ningesema ni sekta ya afya. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nirudi katika maombi ya mkoa wangu, Mkoa wa Lindi na Kanda ya Kusini kwa ujumla. Kila Kanda ina Hospitali ya Kanda ya Rufaa. Kanda ya Kusini ujenzi ulianza karibu miaka 10 iliyopita, lakini kwa miaka hii miwili mfululizo naona kama ujenzi umesimama inatengwa bilioni mbili na hiyo haitoki. Kwa hiyo, nimwombe Mheshimiwa Ummy mdogo wangu afanye huruma kwa ndugu zake wa Kusini, atakapokuja basi atuambie ametuandalia nini cha matumaini ili kuhakikisha hospitali ile inakamilika kabla ya mwaka 2020 ili huduma ziweze kutolewa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika bajeti iliyopita Kamati ya Bajeti iliweka maombi na mapendekezo ya kuongeza tozo kwa ajili ya kupata pesa za kujenga vituo vya afya na zahanati katika kila Halmashauri. Lengo ikiwa ni kuboresha huduma za afya na pia kupunguza vifo vya akinamama na watoto. Serikali iliomba ipewe muda ifanye tathmini ili katika bajeti hii, waje na mpango mahususi wa kujenga kituo cha afya angalau kimoja kwa kila Halmashauri na zahanati angalau nne kila Halmashauri. Sasa upande wa TAMISEMI bahati mbaya wakati wa bajeti yao sikuwepo, lakini pia nimesoma kwenye makabrasha yao sikuona na upande wa sekta ya afya sioni. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ile tathmini Mheshimiwa Ummy nina uhakika wamemaliza. Kwa hiyo, tutaomba atakapokuja kutoa ufafanuzi au kutoa majibu atuambie, wametenga kiasi gani na baada ya kufanya tathmini wameona gharama ni kiasi gani na mwaka huu wanahisi ni kiasi gani kitatosha ili kuweza kujenga hivyo vituo vya afya na zahanati.

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala lingine ambalo pia nataka nilizungumzie ni suala la udahili wa kada zote za afya, iwe Madaktari, Wauguzi, Wafamasia kwa kweli uongezwe na sio udahili tu, lakini waajiriwe na Serikali. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja