Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Hotuba ya Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018.

Hon. Joseph Michael Mkundi

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Ukerewe

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

2

Ministries

nil

Hotuba ya Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018.

MHE. JOSEPH M. MKUNDI: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza ni kuhusu maradhi yasiyo ya kuambukiza. Kumekuwa na ongezeko kubwa la watu wanaosumbuliwa na maradhi kama shinikizo la damu, kisukari na kadhalika ambayo hayakuwa ya kawaida siku za nyuma, lakini kuna matatizo makubwa ya upatikanaji wa huduma ama matibabu kwa maradhi haya hasa kwenye maeneo ya vijijini. Tofauti na waathirika wa UKIMWI ambapo huduma zimesogezwa hadi katika zahanati na vituo vya afya, wagonjwa wa kisukari, shinikizo la damu na mengineyo yanayofanana na haya wanapata wakati mgumu kupata huduma. Naishauri Serikali isogeze huduma za maradhi haya kama ilivyofanya kwa huduma za waathirika wa UKIMWI.

Pili, ugumu wa huduma Visiwani Ukerewe. Kwa sababu za kijiografia wagonjwa wengi kisiwani Ukerewe wamekuwa wanapoteza maisha kwa kukosa huduma hasa panapohitajika kuwapeleka Hospitali ya Rufaa ya Bugando. Kwa mujibu wa ratiba ya meli, usafiri wa mwisho toka Ukerewe kwenda Mwanza unapatikana saa nane mchana, na njia ya kivuko (ferry) usafiri wa mwisho ni saa 11 jioni, baada ya hapo usafiri mwingine hadi siku inayofuata. Kwa hiyo, inapotokea dharura inapopelekea kutoa rufaa ili mgonjwa apelekwe Hospitali ya Mkoa au ya rufaa baada ya muda huo litakuwa ni kudra ya Mwenyezi Mungu ili awe hai hadi kesho yake.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ombi langu la ushauri wangu kwaSerikali ni kwamba itoe ambulance boatkwa Halmashauri ya Wilaya Ukerewe ili kusaidia kwenye matukio ya dharura kuwahisha wagonjwa kwa ajili ya matibabu zaidi.

Tatu, ni kuhusu Mfuko wa Afya ya Jamii (CHF). Kuna tatizo la upatikanaji wa huduma kwa wanachama wa CHF hasa upungufu wa dawa na huduma kutotolewa kwenye maeneo mengine tofauti na pale ambapo mfaidika amejiunga. Jambo hili linakatisha tamaa. Nashauri Serikali iangalie upya na kuweka mfumo mzuri wa upatikanaji huduma kwa wanachama wa CHF ili kumwezesha mwanachama kupata huduma eneo lolote ama kituo chochote nchini ili mradi yeye ni mwanachama na ana kitambulisho.

Nne, ni kuhusu huduma kwa wazee. Halmashauri nyingi bado hazijatoa vitambulisho kwa wazee wala kutenga dirisha maalum la wazee, jambo hili linasababisha usumbufu mkubwa kwa wazee pale wanapohitaji kupata huduma za afya. Nashauri Serikali itilie mkazo na ikiwezekana kuweka muda maalum ili kuzibana Halmashauri zote nchini kutekeleza jambo hili.

Tano, kuongeza vituo vya afya na zahanati. Kwa kuwa ni sera ya Serikali kuhakikisha kila kata inakuwa na kituo cha afya na kila kijiji kinakuwa na zahanati, Serikali ihakikishe mahali ambapo vituo na zahanati vimejengwa basi maeneo hayo yasaidiwe na kupewa vifaa na watumishi ili kuwezesha zahanati hizo na vituo vya afya vifanyekazi ya kutoa huduma kwa wananchi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mfano, Halmashauri ya Wilaya Ukerewe imeweza kujenga kituo cha afya Nakatunguru, lakini sasa ni zaidi ya miaka mitatu toka kimekamilika kimeshindwa kuanza kwa kukosa vifaa na majengo yanaanza kuchakaa. Lengo la kituo hiki ilikuwa ni kupunguza msongamano wa wagonjwa kwenye hospitali ya Wilaya. Nashauri Wizara iwezeshe kituo hiki ili kuanza kutoa huduma kwa wananchi.

Sita ni uhaba wa watumishi. Kuna uhaba mkubwa wa watumishi wa afya kwenye maeneo ya pembezoni kama Ukerewe. Jambo hili linapelekea uhafifu wa utoaji wa huduma kwenye maeneo haya. Nashauri Serikali itoe motisha kama vile posho ya mazingira magumu kwa watumishi waliopo na kufanyakazi kwenye maeneo haya.