Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Hotuba ya Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018.

Hon. Mohamed Omary Mchengerwa

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Rufiji

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Hotuba ya Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018.

MHE. MOHAMED O. MCHENGERWA: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza kabisa, nampongeza sana dada yangu, Mheshimiwa Ummy Mwalimu, Mbunge na Waziri wa Afya pamoja na Naibu wake kwa kazi nzuri ya kuwatumikia wananchi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nina mambo machache sana. Jambo la kwanza, naipongeza sana Serikali ya Mheshimiwa Dkt. John Pombe Joseph Magufuli kwa kazi nzuri ya kuwatumikia wanyonge; pili, nyongeza ya Wizara, hii Bajeti itaweza kuwasaidia Watanzania wengi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nizungumzie Jimbo langu la Rufiji. Kwa bajeti mbili sasa za Wizara hii, Serikali imesahau Wilaya ya Rufiji. Mwaka 2016 haikutengwa fedha yoyote kwa ajili ya Hospitali yetu ya Wilaya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Rufiji ni moja ya maeneo ambayo Serikali inapaswa kutoa kipaumbele sana. Hii ni kutokana na kwamba, kwa muda mrefu Jimbo la Rufiji limesahaulika. Kwa sasa tuna changamoto kubwa sana za kiusalama; kumewepo na ujambazi mkubwa na mauaji yanayoendelea; na kunahitajika mahitaji makubwa ya huduma bora za afya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hospitali yetu ilijengwa mwaka 1960, lakini mpaka sasa haijawahi kukarabatiwa na majengo mengi ni mabovu yanayohitaji kubomolewa. Hakuna hata vitanda vya upasuaji; kilichopo kimoja ni cha miaka ya 1960; hali ya hospitali ni mbaya sana. Wakati wote yanapotokea matatizo makubwa kwa watu kudhuriwa kwa risasi, tunalazimika kusafirisha majeruhi kwenda Wilaya ya jirani.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Rufiji ilizaliwa kabla ya uhuru, lakini ndiyo Wilaya yenye matatizo makubwa. Umuhimu wa kuiboresha Hospitali ya Wilaya hauepukiki, kwa kuwa umbali uliopo kutoka Rufiji kwenda Hospitali ya Mkoa wa Pwani ni wa masaa zaidi ya sita kutoka Makao Makuu ya Wilaya ya Utete. Wagonjwa wengi hufia njiani.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwisho kabisa, naipongeza Serikali kwa kutuletea Mganga Mkuu Mchapakazi. Naomba huruma ya Mheshimiwa Waziri, akisaidie Kituo cha Afya Ikwiriri kuongeza vifaa na ununuzi wa jenereta; Kituo cha Afya Moholo, kutuongezea fedha za ununuzi wa vifaa; na ujenzi katika Kituo cha Afya Mwaseni Mloka.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba Mheshimiwa Waziri akifika hapa azungumze kauli ya Wizara yake ili kuweza kusaidia Watanzania wanyonge walioko Rufiji ambao hukosa msaada wa matibabu kutokana na hali ya Hospitali yetu ya Wilaya iliyojengwa mwaka 1960; akinamama wanakufa kutokana na uhaba wa Watumishi, kuwahudumia majeruhi wanaoshambuliwa na majambazi, matatizo yanayoendelea kila wiki sasa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kuwasilisha na naunga mkono hoja.