Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Hotuba ya Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018.

Hon. Zuberi Mohamedi Kuchauka

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Liwale

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Hotuba ya Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018.

MHE. ZUBERI M. KUCHAUKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza kabisa, napenda kutoa shukurani zangu za dhati kwa Mheshimiwa Waziri na Naibu Waziri kwa kusikiliza kilio cha Wanaliwale na hatimaye kutupatia Madaktari wawili hivi karibuni. Namwomba Mungu awaongezee umri mrefu. Hata hivyo, naendelea kusisitiza kuwa tatizo la ikama ya watumishi katika Wilaya ya Liwale bado ni tatizo kubwa. Wilaya ya Liwale yenye Kata 20 na Vijiji 79 ina Zahanati 31 tu na Kituo kimoja cha Afya. Jambo hili linaifanya Hospitali ya Wilaya kuwa na mzigo mkubwa kuliko uwezo wa hospitali hiyo. Zahanati zote zinaendeshwa na enrolled nurses (EN). Wilaya nzima ina Clinical Officer wanne tu. Vile vile kuna mashine ya X-Ray ambayo haina mtaalam wa kupiga picha.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kutokana na Halmashauri kuwa na mapato kidogo na hivyo kushindwa kujenga hospitali mpya ili kukidhi mahitaji ya sasa kwa hospitali iliyokuwepo, ni ile iliyokuwa Kituo cha Afya cha Liwale Mjini kwani miundombinu ya hospitali hiyo siyo rafiki kwa sasa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mgao wa madawa kwenye Halmashauri ya Liwale ni mdogo sana hasa ukilinganisha na Halmashauri za jirani. Ni bora sasa Serikali ikatumia takwimu za Hospitali hiyo badala ya kutumia takwimu za mwaka 2012 (sensa). Kwa maneno mengine, kuna wakazi zaidi ya 10,000 wa Wilaya ya Liwale ambao hawana dawa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kuwa Serikali inatambua kuwepo kwa wazee nchini, kwa nini Serikali haitaki kuleta Sheria ya Wazee nchini ili kuwatambua huko, kuwepo kisheria. Wazee wengi nchini wanaishi kama wakiwa, kienyeji, kwani hawajui hatima yao katika nchi hii. Hawazijui haki zao. Namwomba Mheshimiwa Waziri alete hiyo sheria hapa kwa kuzingatia kuwa wote ni wazee watarajiwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tumekuwa na ukiritimba mkubwa sana juu ya matengenezo na service za mashine za X-Ray nchini. Hadi sasa kampuni pekee iliyopewa kazi hiyo nchi nzima ni Kampuni ya Philips. Je, Serikali haioni imefika wakati sasa wa kutafuta kampuni nyingine, kwani kampuni hiyo imeshindwa kazi? Ubovu wa mashine za X-Ray ni wa nchi mzima.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Sera ya Mama na Mtoto pamoja na kupewa kipaumbele katika Wizara hii, bado utekelezaji wake siyo wa kuridhisha kwani huduma hii bado haijawafikia akinamama wa vijijini mahali ambapo zahanati au vituo vya afya vikiwa mbali na vijiji hivyo. Hata hivyo ni vyema basi Serikali ikawekeza zaidi kwenye miundombinu ya usafiri vijijini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, uhaba mkubwa wa fedha ni jambo linalofanya Halmashauri nyingi kukosa dawa licha ya kuwa wanalipa dawa hizo, MSD haina uwezo kuleta dawa kwenye Halmashauri zetu kwa mujibu wa mahitaji ya Halmashauri husika. Vile vile wakati mwingine huleta dawa nje ya wakati na pengine nje ya mahitaji halisi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Posho ya Mazingira Magumu (On Call Allowance) kuziacha chini ya Halmashauri ni kutokuwatendea haki watumishi wa kada ya Madaktari kwani vipaumbele vya Halmashauri hutofautiana toka Halmashauri moja hadi nyingine, hivyo kukosa uwiano wa vipato vya watumishi hawa. Hivyo ni bora posho hizi na allowance zake zikachukuliwa na Wizara husika ili zitolewe kwa mazingira yalivyo sasa kwa watumishi wa ngazi husika kutokana na mazingira ya kazi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, vile vile kuna ubaguzi mkubwa sana wa watumishi kupandishwa madaraja. Kuna watumishi wa muda mrefu hawajapandishwa wakati wapo wa muda mfupi wamepandishwa japo wana vigezo vinavyolingana, jambo linalopunguza morali ya kazi na ufanisi kazini. Vile vile viko vitendo kwa kuadhibu watumishi kwa kuwashusha vyeo na mishahara yao bila kuzingatia sheria za kazi. Jambo hili hupunguza ufanisi wa mhusika na matokeo yake hasira zote huishia kwa wagonjwa.