Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Hotuba ya Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018.

Hon. Janet Zebedayo Mbene

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Ileje

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Hotuba ya Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018.

MHE. JANET Z. MBENE: Mheshimiwa Mwenyekiti, namshukuru Mungu kwa wema wake kwa Taifa letu na kwa Bunge letu. Ahsante kwa kunipa nafasi ya kuchangia hoja iliyoko Mezani. Naunga mkono hoja.

Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kuchukua nafasi hii kumpongeza Waziri wa Wizara hii muhimu, Mheshimiwa Ummy Mwalimu; Naibu Waziri Mheshimiwa Dkt. Hamis Kigwangalla, Mbunge wa Nzega, Katibu Mkuu na Naibu Katibu Mkuu na watendaji wote wa Wizara hii kwa kazi nzuri na kubwa wanayoifanya kuhudumia wananchi kwa weledi mkuu na umahiri wa kiasi cha kuridhisha. Pongezi nyingi sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kujikita kwenye wasilisho la Mheshimiwa Waziri kwenye eneo la maendeleo ya jamii, jinsia, wazee na watoto. Ni kweli, kuwa, kwa ujumla wake bajeti ya Wizara imeongezeka mara dufu, lakini Fungu 53 bado halijatendewa haki.

Mheshimiwa Mwenyekiti, idara hii ndiyo inayofanya kazi ya kuhamasisha wananchi tangu ngazi ya kaya, shina, kijiji, kata, tarafa, wilaya, mkoa hadi Taifa. Hii idara ikiwezeshwa kikamilifu itasaidia sana kuweka mazingira mazuri kiasi kwamba, hata huduma za afya uhitaji wake utapungua. Idara hii inapaswa kuwa na Maafisa Maendeleo ya Jamii, Maafisa Ustawi wa Jamii kila kata, ili wawe wahamasishaji na waraghibishi wa mafunzo yanayohusu usafi wa mazingira (sanitation), masuala ya lishe bora kwa ujumla, lakini pia kwa watoto wanawake na wazee, masuala ya chanjo mbalimbali, masuala ya ujasiriamali, biashara, masoko na kadhalika. Hata Mawaziri wa Sekta nyingine huwatumia hawa Maafisa Maendeleo kuhamasisha masuala mbalimbali.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hali hii ni muhimu sana kuhakikisha kuwa Idara hii ina vitendea kazi vya muhimu kwa majukumu yake kwa maana ya magari, pikipiki, ofisi zinazokidhi, computer na watumishi wa kutosha na wenye weledi wa kutosha kwenye masuala haya. Hali iliyopo hairidhishi na maafisa hawa wengi wamekata tamaa. Idara hii ni muhimu sana kwa kuhakikisha kuwa mikakati ya kinga dhidi ya magonjwa, elimu kwa vijana juu ya mabadiliko ya maumbile na jinsi ya kupambana na mihemuko kwa njia sahihi na salama, idara iwezeshwe kutimiza haya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, udumavu; napenda kuishauri Serikali kuendeleza mkakati ulioanzishwa na Mheshimiwa Jakaya Kikwete wa Scalling Up Nutrition (SUN) kitaifa. Serikali ilete Bungeni mkakati wa uwekezaji katika lishe ili kupambana na tatizo kubwa la udumavu nchini. Katika hili, pamoja na juhudi zinazofanywa za kuhamasisha lishe bora kwa mama mjamzito na mtoto, Serikali ifanye yafuatayo:-

Kwanza, katika mikopo inayotolewa kwa Serikali basi Serikali i-negotiate fungu la kuwekeza kwenye siku 1,000 za kwanza za mtoto. Kwa sababu, bado hatujaona kuwa hili ni kipaumbele katika Taifa. Kwa sababu kuwekeza katika siku za kwanza 1,000 za mtoto kutahakikisha vizazi salama kwa mama na mtoto, lakini pia, itapunguza vifo vya mama na mtoto na kuleta ukuaji wa uchumi kwa kiasi kikubwa.

Pili, Serikali iweke mazingira mazuri kwa sekta binafsi kuingia katika uwekezaji kwenye masuala/huduma/mazao ya lishe. Serikali haiwezi kulifanya hili peke yake.

Tatu, Serikali ianzishe Jamii ya Vijana wa Kujitolea (Volunteer Community Workers) ambao watafundishwa masuala ya uraghibishi wa afya vijijini na watakuwa wa msaada mkubwa kwa karibu sana na kuongeza tija kwenye shughuli za Wizara katika ngazi ya kaya, tawi, hata na wilaya. Hawa kwa kuwa, watatokana na maeneo hayo watakuwa na gharama ndogo.

Nne, Serikali katika kujenga maadili mema kwa jamii zetu iangalie uwezekano wa kuanzisha utaratibu wa wanawake watu wazima kutoa ushauri nasaha kwa vijana wanawake wakati wa balehe, ujauzito na wanapokuwa katika ndoa zao.

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la wazee bado halijakaa vizuri kwa maana ya mkakati mahsusi wa kuwahudumia wazee kiafya, kiuchumi na kisaikolojia. Iko haja ya kuwa na njia inayotambulika ya kuwawezesha wazee kujisajili kwenye kata zao ili huduma kwao ziwe rahisi katika kila nyanja. Wazee mahitaji yao mengi ni ya kisaikolojia jinsi ya kuukabili uzee, lakini pia kiafya na mwisho lishe bora.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Watoto Njiti; idadi ya watoto hawa inaongezeka katika watoto 10 wanaozaliwa mmoja ni njiti na wanapona kwa 40% tu. Hii ina maana vifo vya watoto wachanga vinachangia kwa 40% ya vifo vya watoto chini ya miaka mitano. Kila siku watoto 100 wanakufa kwa sababu ya complications kama kushindwa kupumua na kuzaliwa kabla ya wakati. Kila mwaka watoto 213,000 wanazaliwa njiti, watoto zaidi ya 9,000 wanazaliwa kwa matatizo hayo. Vifo vya watoto njiti ni sababu ya pili kwa ukubwa wa vifo vya watoto wachanga Tanzania. Kumekuwa na ongezeko kubwa na hatua madhubuti zinahitajika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali ihakikishe suala la watoto njiti linafahamika na jamii kwa ujumla kuwa sio mkosi, wala kosa lolote la mzazi, ukoo wala jamii na kuwa watoto njiti wanaweza kukua vizuri na kuwa raia wema na wenye akili timamu na afya njema, ilimradi wapate matunzo yanayofaa kwa kuwarudisha katika afya njema.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali ihakikishe vituo vya afya na hospitali zinapata vifaa muhimu vya kuwatunzia watoto njiti kama oxygen concentrator ya kumsaidia mtoto kupata oxygen; neonatal jaundice and phototherapy ya kugundua jaundice(manjano) mapema; rescuscitation machine ya kumstua mtoto ili apumue mara tu akizaliwa maana mapafu yake yanaweza kuwa hayana nguvu ya kutosha; electric and manual suction machine ya kutoa uchafu kooni na puani kusafisha njia ya kupitisha hewa; digital thermometer ya kupima na kudhibiti joto la mwili wa motto; diaspect machine ya ku-check damu ya mtoto kama inatosha.

Mheshimiwa Mwenyekiti, wazazi wafundishwe jinsi ya kutunza watoto njiti kwa kuhakikisha wanawabeba kama kangaroo na hawawaachi wazi.