Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Hotuba ya Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018.

Hon. Amina Nassoro Makilagi

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Hotuba ya Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018.

MHE. AMINA N. MAKILAGI: Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kuchukua nafasi hii kukushukuru wewe na kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa kuniwezesha kusimama na kutoa mchango wangu katika hoja hii muhimu ya Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii Jinsia, Wazee na Watoto. Nianze kwa kuunga mkono hoja na sababu zangu za kuunga mkono hoja ni kama ifuatavyo:-

(i) Randama na hotuba ya Waziri imeandaliwa vizuri na kitaalam; na
(ii) Serikali ya CCM chini ya uongozi wa Rais Dkt. John Pombe Magufuli, Makamu wa Rais, Mheshimiwa Mama Samia Suluhu Hassan, Waziri Mkuu, Waziri mwenye dhamana, Naibu Waziri, Katibu Mkuu na watendaji wa Wizara hii wanafanya kazi nzuri ya kuhakikisha wanaboresha huduma za afya hapa nchini. Ni ukweli usiopingika kuwa katika kipindi hiki kifupi, wameendelea kuonesha dhamira ya dhati ya Serikali ya CCM ya kuboresha huduma za afya kwa wananchi, hongereni sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na pongezi, kwanza napenda kushauri Serikali:-

(a) Itoe fedha za kutosha za utekelezaji wa majukumu ya sekta hii muhimu;

(b) Iboreshe maslahi ya wafanyakazi wa sekta ya afya na maendeleo ya jamii na kuongeza idadi ya wafanyakazi;

(c) Iendelee kununua vifaa tiba katika zahanati, vituo vya afya, hospitali za wilaya na mkoa;

(d) Ipeleke wataalam kama vile Madaktari na Wauguzi katika hospitali, vituo vya afya na zahanati zote;

(e) Iandae mpango maalum utakaoleta matokeo ya haraka ya ujenzi wa vituo vya afya, zahanati na ukamilishaji wa mpango wa hospitali za rufaa za kila mkoa, lengo likiwa ni kupunguza msongamano wa wagonjwa katika hospitali za Muhimbili, KCMC na Bugando. Hapa naishauri Serikali kujenga vituo vya afya viwili viwili katika kila halmashauri, kwa halmashauri tulizonazo 183 x 2 x 3 = 1,098;

(f) Ikamilishe vituo vya afya vilivyojengwa kwa nguvu za wananchi ili visaidie kutoa huduma badala ya kubaki kuwa magofu;

(g) Iongeze fedha kwa ajili ya ujenzi wa Hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Mara (Mwalimu Nyerere Memory Center);

Mheshimiwa Mwenyekiti, pili, napenda kuongelea huduma ya afya ya uzazi na mtoto. Pamoja na kuipongeza Serikali kwa jitihada zake za kuboresha huduma inayotakiwa kwa wanawake kabla ya ujauzito, wakati wa ujauzito, wakati wa kujifungua na wiki sita baada ya kujifungua, naomba niungane na Serikali katika ukurasa wa 16 kuwa kweli bado ipo changamoto kubwa ya wanawake wanaofariki wakati wa uzazi. Kwa mujibu wa tafiti zilizopo hapa nchini ya mwaka 2015 zinaonesha kwamba vifo vinavyotokana na uzazi havijapungua, idadi ya vifo ni 556 kwa kila vizazi 100,000.

Mheshimiwa Mwenyekiti, napongeza mpango wa Wizara ulioandaliwa na unaotekelezwa kuanzia 2016 hadi 2020. Hapa napenda nipate muhtasari juu ya mpango huo, tangu mpango huo umeanza kutekelezwa tumeweza kuokoa vifo vingapi vya wanawake? Ni kwa nini vifo vimeongezeka badala ya kupungua? Takwimu za 2016/2017 zinaonesha hali ikoje juu ya vifo vya wanawake ikilinganishwa na ya mwaka 2015?

Mheshimiwa Mwenyekiti, tatu, watoto wanaozaliwa kabla ya wakati (njiti). Kwa mujibu wa utafiti uliofanywa na Mamaye 2017 kwa kushirikiana DFID, watoto 2,013 wanazaliwa kabla ya wakati na watoto 3,900 waliozaliwa bila kufikisha umri, wanafariki dunia. Watoto wanaozaliwa kabla ya wakati pia ni sababu ya watoto wanaofariki kabla ya kufikisha miaka mitano.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ili kunusuru maisha ya watoto wanaozaliwa kabla ya wakati naishauri Serikali kufanya yafuatayo:-

(i) Tuwe na wodi/chumba maalum kwa ajili ya watoto hawa kwa sababu hali ilivyo sasa hakuna vyumba maalum katika baadhi ya vituo vya afya na hospitali zetu;

(ii) Kuwe na vitanda vya kutosha kwa ajili ya kuwalaza watoto hao;

(iii) Kuwe na mashine ya kusaidia watoto kupata joto ili kuwafanya waishi;

(iv) Kuwe na mashine za kuondolea ugonjwa wa manjano; na

(v) Elimu kwa jamii itolewe.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nne, ugonjwa wa saratani – shingo ya kizazi, matiti na tezi dume. Pamoja na kuishukuru Serikali kwa jitihada zake za kupambana na ugonjwa wa saratani kwa kuboresha Taasisi ya Saratani ya Ocean Road na hospitali za kanda ili ziweze kutoa huduma kwa wagonjwa wa saratani, bado ugonjwa wa saratani umekuwa ndio ugonjwa tishio kwa wanawake na wananchi wengine kwa ujumla. Kwa kuwa ugonjwa huu ni hatari na dawa za saratani ni ghali sana, naiomba Serikali itenge na kutoa fedha kwa ajili ya kununua vifaa tiba vya ugonjwa wa saratani. Pia naomba Serikali itoe msamaha wa matibabu kwa wagonjwa wa saratani kama ilivyo kwa wagonjwa wa UKIMWI kwa sababu wanawake na wananchi wanaougua ugonjwa huu wa saratani hawana uwezo wa kumudu kununua dawa za ugonjwa huu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tano, dirisha la wazee, wanawake na wajawazito na watoto chini ya miaka mitano. Pamoja na kupongeza Serikali kwa kuweka na kuanzisha dirisha la wazee na wanawake wajawazito na watoto chini ya miaka mitano, bado ipo changamoto kubwa ya utoaji huduma hii kwa wazee, wanawake wajawazito na watoto. Changamoto kubwa sana ya kundi hili ni dawa/ fedha zinazopelekwa hazitoshelezi. Nashauri, Serikali iwapatie huduma za bima ya afya wazee, wanawake na watoto. Pia iongeze fedha kwa ajili ya kuhudumia kundi hili na kuondoa adha wanayoipata kwa kukosa huduma ya afya kama ilivyokusudiwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sita, uwezeshaji wa wanawake kiuchumi. Wanawake ndiyo nguvu kazi, wanawake ndiyo walezi wa familia, unapomkomboa mwanamke kiuchumi unakomboa familia kwa ujumla. Taarifa inaonesha jitihada zilizofanywa na Serikali katika kuwezesha wanawake kupitia mipango na program mbalimbali kwa kuwekeza nguvu zaidi kwa wanawake na watu wenye ulemavu. Pamoja na kupongeza Serikali, nina ushauri katika maeneo yafuatayo:-

(i) Mfuko wa Maendeleo ya Wanawake kutoka Serikali Kuu. Mfuko huu umekuwa ni mkombozi. Kwa vipindi vya miaka ya hivi karibuni na hata bajeti ya mwaka 2017/ 2018, mfuko huu haukutengewa fedha. Naomba Serikali itenge na kutoa fedha kwa aili ya Mfuko wa Maendeleo ya Wanawake kama ilivyofanyika kwa vijana. Kutotenga fedha kwa ajili ya wanawake ni kurudisha nyuma jitihada za wanawake katika kujikomboa kiuchumi kwa sababu mfuko huu unaotolewa na Wizara ulikuwa ni ukombozi kwa vikundi vya wanawake badala ya kutengewa 10% ya Mfuko wa Wanawake na Halmashauri tu ambao pia hakuna uhakika kwa sababu Halmashauri nyingi hazitengi na kutoa fedha hizo.

(ii) Tatizo la kutolipa 10% ya wanawake na vijana. Lipo tatizo katika Halmashauri kutotenga 10% kwa ajili ya mfuko wa vikundi vya maendeleo ya wanawake na vijana katika Halmashauri zetu. Naomba kutoa ushauri kwamba kwa kuwa utaratibu wa kutoa fedha hizo 10% ya vikundi vya wanawake na vijana ni maagizo yaliyotolewa na Waziri Mkuu miaka zaidi ya 20 iliyopita, Serikali ilete Muswada ili Bunge litunge sheria itakayoweka utaratibu wa kutenga, kutoa na kurudisha fedha hizo kwa vikundi vya maendeleo ya wanawake na vijana kuliko ilivyo sasa, kwani jambo la kutoa fedha hizo limebaki kama ni jambo la hisani na si jambo la lazima kwa sababu hakuna sheria inayotekelezwa.

Kwa mujibu wa Taarifa ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG) kila unapofanyika ukaguzi linatokea tatizo la kutotoa fedha kwa vikundi vya wanawake na vijana, Halmashauri zilizo nyingi zimeonesha yapo madeni makubwa. Hapa ningependa kusikia kauli ya Serikali juu ya ulipaji wa madeni haya ili fedha hizi zielekezwe katika kutoa mikopo kwa vikundi vya wanawake na vijana.

(iii) Riba katika taasisi zinazotoa mikopo kwa vikundi vya wanawake. Pamoja na kuzipongeza taasisi za fedha kwa kutoa mikopo midogo na mikubwa kwa vikundi vya wanawake na vijana, lipo tatizo kwa baadhi ya taasisi za fedha viwango vyao vya riba ni vikubwa sana mpaka kufikia 35%. Jambo hili husababisha wanawake na vijana kushindwa kujikomboa kiuchumi badala yake wameambulia kufanya kazi za uzalishaji na kuwanufaisha waliowapa mikopo na wao kuambulia kutaifishiwa mali zao kwa mfano vifaa vya nyumbani kama vitanda, magodoro, vyombo na kuuziwa mashamba. Nashauri Serikali itoe riba elekezi kwa taasisi zote zinazotoa mikopo kwa vikundi vya wanawake na vijana lengo likiwa ni wanawake na vijana wanufaike na mikopo hiyo kuliko ilivyo sasa.

(iv) Benki ya Wanawake ilianzishwa kuwakomboa wanawake waishio vijijini na mijini ambao hawana fursa za kufika taasisi nyingine za fedha. Nashauri Serikali itoe fedha kwa benki hii ili ipate mtaji wa kufungua matawi katika mikoa yote hapa nchini. Vilevile masharti ya kutoa mikopo kwa vikundi vya wanawake yaangaliwe upya kwa sababu hayatofautiani na masharti ya benki zingine, hivyo wanawake walio wengi hasa waliolengwa na kuanzishwa kwa benki ni wanawake wanyonge ambao hawana mali za kuweka kama dhamana wanashindwa kukopa katika benki hii. Hivyo, malengo ya kuanzishwa kwa benki hii bado hayajafikiwa. Pia Serikali irejee upya masharti ya kutoa na kurudisha mikopo ili Benki hii ya Wanawake iwe mkombozi kwa wanawake na Watanzania kiuchumi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja.