Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Hotuba ya Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018.

Hon. Angellah Jasmine Mbelwa Kairuki

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Nominated

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Hotuba ya Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018.

WAZIRI WA NCHI, OFISI YA RAIS, UTUMISHI NA UTAWALA BORA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi na nianze kwa kuunga mkono hoja hii ya Hotuba ya Bajeti ya Waziri wa Afya. Kipekee nipende kumpongeza sana pacha wangu Mheshimiwa Ummy Mwalimu pamoja na Naibu wake Dkt. Hamisi Kigwangalla kwa kazi kubwa na nzuri ambayo wanaifanya katika kuboresha utoaji wa huduma ya afya, masuala ya maendeleo ya jamii, ulinzi kwa mtoto pamoja na masuala mengine ambayo yako chini ya usimamizi wa Wizara yao. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ningependa tu kuongelea suala kubwa kuhusiana na ajira. Waheshimiwa Wabunge wengi wamezungumza kwa hisia kubwa, lakini lengo kubwa ikiwa ni kupaza sauti kwenye suala zima la umuhimu wa kuwa na watumishi katika sekta ya afya wanaotosheleza kwa ajili ya kutoa huduma ya afya iliyo bora. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kipindi cha miaka mitano kuanzia mwaka 2010 mpaka mwaka 2015, Ofisi yangu imetoa vibali vya ajira 52,947 kwa ajili ya kada mbalimbali katika sekta ya afya. Ukiangalia katika mwaka huo huo miaka hiyo mitano takribani watumishi 14,860 hawakuripoti katika vituo walivyopangiwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, changamoto kubwa, mahitaji ni makubwa lakini udahili katika vyuo vyetu pia haujajitosheleza na tumeshaanza kuchukua hatua ya kushirikiana na Wizara ya Afya pamoja na vyuo vikuu vinavyotoa taaluma hizo ili kuona ni kwa namna gani wanaweza kuongeza udahili ili kuhakikisha kwamba tunakuwa na wataalam wa kutosha watakaotosheleza soko letu la ajira.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tumeanza kuchukua hatua, kama ambavyo mmeshasikia tumeshaanza kuajiri watumishi wa sekta ya afya, Madaktari 258 na tayari wameshapangiwa katika Hospitali ya Rufaa ya Mbeya, Hospitali ya Benjamin Mkapa Dodoma, Kibong’oto pamoja na Mirembe. Vile vile kwa upande wa TAMISEMI wamewapangia pia katika Halmashauri mbalimbali za Wilaya pamoja na Halmashauri nyingine za miji. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nilieleza jana na leo pia nilieleza; kwa kutambua zoezi letu lililokuwa likiendelea, baada ya matokeo ya uhakiki wa vyeti; tunatambua ni kweli katika hospitali nyingi, katika vituo vingi vya afya na zahanati kumekuwa na upungufu mkubwa baada ya baadhi ya watumishi nao kuwa wamekumbwa na kadhia hiyo. Tumechukua hatua za haraka na za makusudi, tumeshatoa kibali cha ajira kwa ajili ya watumishi 15,000 na tutaweza kuwapangia. Tumeanza mashauriano na TAMISEMI ili kuweza kujua ikama ikae vipi, eneo gani lina upungufu mkubwa; na tunaamini kwa wiki ijayo zoezi hili litaweza kufika katika sehemu nzuri zaidi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sambamba na hili, hii ni kati ya sasa na mwezi Juni, lakini kwa kiasi kikubwa watumishi wengi pia watakuwa katika sekta ya afya. Kwa hiyo, niwatoe hofu sana Waheshimiwa Wabunge, tutajitahidi kucheza na namba hizo 15,000 na tunaamini zitaweza kwa kiasi kikubwa kupunguza upungufu mkubwa wa wataalam wetu uliopo katika sekta hii ya afya. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, vile vile katika mwaka ujao wa fedha kuanzia mwezi Julai tutatoa pia tena ajira nyingine 52,436 na kwa kiasi kikubwa ajira nyingi zitakwenda katika sekta ya afya, elimu pamoja na Sekta nyingine. Kwa hiyo niwatoe tu hofu Waheshimiwa Wabunge, nimewasikiliza vizuri na tutaangalia kwa kweli ikama imekaa vipi kuhakikisha kwamba yale maeneo ya pembezoni, maeneo yenye upungufu mkubwa na kada zile za kipaumbele basi zitaweza kutendewa haki kama ambavyo inahitajika. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sambamba na hilo napenda nizungumzie suala zima la telemedicine. Nilimsikia Mheshimiwa Mbunge mmoja wa Mbeya akielezea umuhimu wa kuweza kutoa matibabu au rufani kwa njia ya telemedicine. Bahati nzuri kwa kushirikiana na Wizara ya Afya na Ofisi yangu Wakala wa Serikali Mtandao tunahimiza masuala ya matumizi ya TEHAMA katika huduma mbalimbali.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tayari kupitia mradi wa RCAP ambao tunafadhiliwa na Benki ya Dunia na kwa kushirikiana na Wizara ya Afya tumeshaweza kujenga mfumo huu wa telemedicine na mfumo umekamilika, lakini vile vile tumeshafunga vifaa mbalimbali na tumesimika mfumo katika vituo vyote isipokuwa Mafia ambako kulikuwa kuna changamoto kidogo ya mawasiliano lakini tunaendelea kuifanyia kazi na naamini suluhisho litaweza kupatikana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tumeshatoa mafunzo kwa watumiaji wa mfumo huu wa telemedicine, lakini vile vile tutaanza majaribio kuanzia tarehe 15 Mei mwaka huu hadi tarehe 15 Juni na tunaamini majaribio haya tutayafanya katika Hospitali ya Mkoa wa Lindi, Hospitali ya Wilaya ya Nyangao Lindi Vijijini, Hospitali ya Wilaya ya Nachingwea, Hospitali ya Rufaa Morogoro, Hospitali ya Wilaya Turiani, Hospitali ya Wilaya Kilosa pamoja na Hospitali ya Taifa ya Muhimbili. Baada ya majaribio hayo tunaamini sasa tutakuwa katika nafasi nzuri zaidi kwa kushirikiana na Wizara ya Afya kwenda katika hospitali zote kama nilivyoeleza awali.

Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo lingine ambalo ningependa nilizungumzie ni suala zima la maslahi kwa watumishi wa sekta ya afya. Waheshimiwa Wabunge wameeleza kwa hisia kubwa na ni kweli tunatambua risk mbalimbali ambazo wataalam hawa wanakutana nazo wanapokuwa wanatenda kazi zao. Vile vile tumejitahidi kuweka aina mbalimbali za maslahi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ombi langu kubwa na rai kwa waajiri, wanapopanga bajeti zao wahakikishe wanazingatia stahiki mbalimbali za watumishi wakiwemo watumishi wa sekta ya afya. Waangalie masuala mazima ya on-call allowances. Wameeleza Waheshimiwa Wabunge masuala ya upungufu wa uniforms na wamefanya mpaka comparison kwa nini sekta nyingine wananunuliwa na sekta nyingine hazinunuliwi. Tuombe sana kwa masuala ya muhimu kama haya ni vema mwajiri katika first charge ya vipaumbele vyake akaweka masuala haya. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru na naunga mkono hoja.