Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Hotuba ya Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018.

Hon. Dr. Hamisi Andrea Kigwangalla

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Nzega Vijijini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Hotuba ya Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018.

NAIBU WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa fursa hii. Awali ya yote napenda nianze kwa kumshukuru sana Mwenyezi Mungu mwingi wa rehema na mwenye kurehemu kwa kunijalia afya njema na kuniwezesha kusimama mbele ya Bunge lako Tukufu ili nami niweze kujibu hoja mbalimbali za Waheshimiwa Wabunge wenzangu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba ufikishe kwa Mheshimiwa Spika salamu zangu za masikitiko makubwa lakini pia nikuunganishe na wewe kwenye salamu hizo za pole pamoja na Waheshimiwa Wabunge wenzetu wote kwa misiba mbalimbali iliyotukuta. Tukianza na msiba wa aliyekuwa Spika wa Bunge la Tisa la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Samuel John Sitta, lakini pia Wabunge wenzetu Mheshimiwa Hafidh Ali Tahir na Mheshimiwa Dkt. Elly Marco Macha. Kwa wote hawa naomba Mwenyezi Mungu azilaze roho zao mahali pema peponi. Amina.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nitumie nafasi hii kwa namna ya kipekee kumshukuru sana Mheshimiwa Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto kwa kunipa ushirikiano na kunishirikisha kwa ukaribu katika utekelezaji wa jukumu hili la kusimamia na kuiongoza Wizara hii. Pia naomba nimshukuru mke wangu mpenzi Dkt. Bayum Kigwangalla na watoto wetu Sheila, Hawa na H.K Junior kwa kunitia moyo na kunivumilia wakati wote ninapokuwa mbali na familia yangu nikitekeleza majukumu mbalimbali ya kila siku ya ujenzi wa Taifa letu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, vile vile nikushukuru wewe kwa kunipa nafasi hii, lakini pia kwa kipekee nimshukuru Mheshimiwa Spika, Naibu Spika na Wenyeviti wote wa Bunge kwa uongozi thabiti mnaotoa kila siku na ushirikiano mnaotupa katika kutekeleza majukumu yetu tuliyopewa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia niishukuru kwa dhati Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Huduma na Maendeleo ya Jamii na Waheshimiwa Wabunge wote kwa ushirikiano mkubwa wanaonipatia siku hata siku.

Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kuwapongeza watumishi wote wa Wizara yetu ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto wakiongozwa na Katibu Mkuu Idara Kuu ya Afya, kaka yangu Dkt. Mpoki Ulisubisya na Katibu Mkuu Idara Kuu ya Maendeleo ya Jamii ndugu yangu mama Sihaba Nkinga pamoja na wafanyakazi wote wa sekta za afya na maendeleo ya jamii nchini kwa kazi yao nzuri na iliyotukuka ambayo wamekuwa wakiifanya kila siku katika kuboresha maisha ya Watanzania wenzetu. Nawaomba sana tuendelee kufanya kazi kwa ushirikiano huu, lakini pia kwa uadilifu mkubwa ili kufikia malengo yetu tuliyopewa na kufikia malengo ya Taifa kadri tunavyotarajiwa na Watanzania wenzetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nawashukuru Waheshimiwa Wabunge wote waliochangia kwa maandishi na kwa kusema hapa Bungeni. Michango yenu kwa hakika inalenga kuboresha huduma za afya na maendeleo ya jamii zinazotolewa na kusimamiwa na Wizara yetu. Kama mlivyoona ndugu zangu, hoja zilizotolewa ni nyingi lakini muda tuliopewa hautoshi kujibu hoja zote, hivyo majibu ya kina ya hoja moja baada ya nyingine tutayawasilisha kwa maandishi na Waheshimiwa Wabunge wote mtapatiwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo naomba sasa nijibu hoja chache ambazo nimepewa nizizungumzie katika maeneo mbalimbali kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, la kwanza, naomba kuzungumzia kuhusu mfumo wa afya (health system). Kwa hakika mfumo wa afya tangu tumepewa majukumu haya na Watanzania mwaka 2015 umeendelea kuimarika kwa kasi ya ajabu. Mafanikio haya ya kuimarika kwa mfumo wa afya yaani (health system) hayawezi kuzungumziwa bila kuutambua na kuuthamini mchango mkubwa wa viongozi wetu wakuu wanaoongozwa na Rais wetu mpendwa Mheshimiwa Dkt. John Pombe Joseph Magufuli ambaye hata kabla hajatuteua sisi kwenye nafasi hizi alionesha nia yake ya dhati ya kutaka kuleta mabadiliko kwenye Sekta ya Afya kwa kuanza kusimamia sekta hii yeye mwenyewe kwa ziara zake maarufu za kushtukiza alizozifanya Hospitali ya Taifa Muhimbili na matokeo yake sote tunayafahamu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini pia kiongozi wetu Mkuu mwingine Mheshimiwa mama Samia Suluhu Hassan ambaye amekuwa champion wa mambo yote yanayohusu akinamama lakini pia afya ya uzazi salama ambapo pia amekuwa karibu sana na Wizara hii akitupa mwongozo, maelekezo na ulezi wa kila siku katika utekelezaji wa majukumu yetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini vile vile, Mheshimiwa Waziri Mkuu naye amekuwa mstari wa mbele kwenye utekelezaji wa majukumu ya sekta hii na tumemwona kila alipofika kwenye mkoa wowote ule kwenye nchi yetu amekuwa akitusaidia kufanya usimamizi wa moja kwa moja yeye mwenyewe.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimelisema hili kwa sababu linatokana na utafiti ambao umefanywa na Taasisi isiyo ya Kiserikali ya TWAWEZA, ambapo katika utafiti huo matokeo waliyatoa mwaka jana katikati, wameonesha kwamba mfumo wa afya umeimarika kutokana na takwimu za sauti za wananchi ambao waliwahoji. Kwa msingi huo mafanikio haya kazi yetu sasa ni kuendelea kuyalinda lakini pia kuendelea kusonga mbele siku hata siku.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hoja ya pili ninayopenda kuzungumzia inahusu rasilimali watu. Mfumo wa afya una vitu vikubwa vitatu; cha kwanza ni rasilimali watu; cha pili ni vifaa, vifaa tiba, dawa, vitendanishi; lakini cha tatu ni miundombinu ya kutolea huduma za afya. Eneo la muhimu kuliko yote katika muktadha wa kutoa huduma bora za afya ni eneo la rasilimali watu. Waheshimiwa Wabunge wengi wamezungumzia suala hili kwa uchungu kuanzia kwenye mambo ya udahili, ajira kwa watumishi kwenye sekta hii pamoja na motisha, yote haya yanahusu eneo la rasilimali watu. Kwa kuwa ni wengi waliochangia, nawatambua wachache tu, wengine naomba mjue kwamba katika majibu ya hoja kwa ujumla wake mtapata majibu ya kina na majina yenu yatakuwa yamewekwa humo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, michango ambayo napenda kuifafanua kwa ujumla wake kwa sababu muda hautoshi ni mchango wa Mheshimiwa Devotha Minja, Mheshimiwa Susan Lyimo, Mheshimiwa Mussa Sima, Mheshimiwa Juliana Shonza na Mheshimiwa mama Anna Makilagi. Kwa pamoja wamezungumzia mambo ya motisha na mambo mbalimbali, lakini pia kuna Waheshimiwa Wabunge wengine wamezungumzia mambo ya fukuza fukuza ambayo imekuwa ikifanyika na naomba nizungumzie hili la mwisho nililolisema.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza sisi kama Wizara ya Afya hatupendezwi sana na fukuza fukuza isiyofuata utaratibu kwa sababu sisi tuna jukumu la kusimamia sekta hii na katika kusimamia sekta hii tunafahamu hatuwezi kutimiza malengo yaliyopo kwenye Sera ya Afya ya Taifa bila kuwa na rasilimali watu ambayo ina motisha ya kutosha. Ni kwa msingi huo, mara kwa mara tumeshuhudia Waziri wa Afya akitolea msimamo thabiti suala hili. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, rasilimali watu kwenye sekta ya afya ni ina gharama kubwa sana, kuanzia kwenye training kuja kwenye ajira, gharama za kuwalipa mishahara, gharama za kuwapa motisha, gharama ya kumhudumia daktari mmoja ni kubwa sana ukilinganisha na wataalam kwenye sekta nyingine. Wataalam hawa wanatoa huduma kwa kiwango cha hali ya juu sana na mara nyingi, nje ya muda wao wa kawaida wa kufanya kazi. Kwa namna yoyote ile, watumishi wa Sekta ya Afya wanapaswa kutiwa moyo na sio kudhalilishwa kama ambavyo Waheshimiwa Wabunge mmekuwa mkisema hapa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, na sisi kwenye sekta hii tunasema tutaendelea kulinda maslahi ya watumishi wa Sekta ya Afya kama hawatofukuzwa au kusimamishwa kazi kwa taratibu za kimaadili ambazo sisi Wizara ya Afya tunazisimamia. Kuna taratibu za kiutawala hayo hatutayaingilia, lakini kwa mambo yote yanayohusu uadilifu wa watumishi kwenye sekta ya afya, mabaraza yote ya kitaaluma yako chini ya Wizara yetu na hivyo mtu yoyote yule awe kiongozi anayesimamia eneo lake la utawala ni lazima afuate utaratibu wa kisheria ambao unasimamiwa na Wizara yetu. Tunahitaji staha kwa wataalam hawa ili waendelee kupata moyo wa kuwahudumia Watanzania wenzetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye eneo hili la rasilimaliwatu tumepata mafanikio makubwa sana katika miaka ya hivi karibuni. Miaka iliyopita takriban 15, (miaka hiyo na mimi nilikuwa nasoma udaktari Chuo Kikuu) tulikuwa tunahitimu si zaidi ya 100 kwa nchi nzima; lakini leo hii kwa mwaka tuna uwezo wa kuzalisha Madaktari takriban 1,100 kila mwaka unaopita. Pia Wauguzi tu kwa mfano miaka hiyo ya 2000 mpaka 2005, tulikuwa tuna uwezo wa kuzalisha Wauguzi wasiozidi 3,500; leo hii ninavyozungumza hapa tuna uwezo wa kuzalisha Wauguzi wapatao 13,562, hii ni idadi kubwa sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, changamoto inayokuja, kwa bahati mbaya hatuisimamii sisi kwenye sekta yetu na tunaendelea na mazungumzo na wenzetu ili tuweze kuipatia ufumbuzi, ni changamoto ya kuwa-absorb kwenye mfumo wa afya wataalam wote ambao tunawazalisha. Hii changamoto si yetu peke yetu, ni changamoto sana sana unaweza ukasema ya kitaifa kwa sababu inahusiana na ukomo wa bajeti, jambo ambalo linahusiana na ukuaji wa uchumi wetu. Kwa hivyo hatuwezi kumnyooshea kidole mtu yeyote yule kati yetu kwa sababu ni jambo ambalo wakati mwingine liko nje na uwezo wetu wa kibinadamu, kwa sababu kama hakuna pesa za kuwalipa mishahara, unafanya nini hata kama unatamani kuwaajiri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hivyo, pamoja na mafanikio makubwa tuliyoyapata kwenye eneo la production ya heath care workers lakini tuna changamoto kubwa sana ya absorption ya health care workers kwenye health system ya nchi yetu. Changamoto hii tutaendelea kuitatua taratibu kama ambavyo Waziri anayehusika na Manejimenti ya Utumishi wa Umma amesema.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Waheshimiwa Wabunge wengi wanapotaka kupata watumishi kwenye maeneo yao wanazungumzia kupata watumishi kutoka Wizara ya Afya; lakini wanasahau kwamba bajeti ya watumishi hawa iko kwenye dhamana ya watumishi ambao ni Accounting Officers kwenye maeneo yao; Makatibu Wakuu, Makatibu Tawala, Wakurugenzi wa Halmashauri na Wakurugenzi wa Hospitali mbalimbali, wote hawa wanapaswa kupanga bajeti kwa ajili ya kuajiri rasilimali watu kwenye sekta ya afya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sisi kazi yetu ni kuzalisha, kuwasajili, kuangalia wanafanyaje kazi, kuangalia uadilifu wao na takwimu za rasilimali watu kwenye sekta ya afya nchini lakini si kuajiri. Kibali cha kuajiri kipo kwa wenzetu wa Menejimenti ya Utumishi wa umma lakini pia mishahara ipo
kwa wenzetu wa Hazina. Bajeti ya kuwaajiri ipo kwa Wakurugenzi wetu wa Halmashauri. Kwa hivyo, napenda kutumia jukwaa hili kuwaomba Waheshimiwa Wabunge waanze kwanza wao wenyewe kwenye Halmashauri zao kupanga bajeti ya kuajiri rasilimaliwatu ya kutosha kwenye maeneo yao kabla ya kuja kuomba sisi tuwasaidie. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, changamoto nyingine kwenye eneo hili la rasilimali watu ni changamoto ya retention ya health care workers. Changamoto ya kuhakikisha rasilimali watu kwenye sekta hii inabaki kwenye eneo husika, haiondoki kwa sababu tunaona sasa hivi Madaktari hao wachache tulionao kwa zaidi ya asilimia 70 wapo kwenye maeneo ya mijini tu, maeneo ya vijijini hakuna. Wakati wanapangwa na Wizara ya Afya pale mwanzoni ukifuatilia kuna tracer studies mbalimbali zinazofanyika ambazo zinafuatilia wafanyakazi walihitimu wapi, walihitimu lini na walipelekwa wapi na sasa wako wapi imeonekana kwamba wengi wanaopelekwa kwenye maeneo ya pembezoni wanahama kutoka huko, wanahamia kwenye maeneo ya centre; wanahamia kwenye Wilaya za Mjini ama kwenye miji mikubwa ama kwenye hospitali kubwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hii ni changamoto ambayo inasababishwa na kuwepo kwa imbalances za kijiografia ambazo zinajitokeza kwenye mfumo wa afya, ambapo kuna baadhi ya maeneo ni lucrative, ni ya kijani zaidi kuliko maeneo mengine. Sasa kwa msingi huo ni lazima waajiri, kwa maana ya Wakurugenzi ama Wakurugenzi wa Hospitali ama wa Halmashauri ama Makatibu Tawala, wanapowaajiri ni lazima watengeneze package ya kutoa motisha kwa rasilimali watu kwa maeneo yao.

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala ambalo nataka kulizungumzia limeshazungumziwa na Mheshimiwa George Simbachawene, linahusu ugatuaji wa madaraka (decentralization by devolution) na hili limezungumziwa na Waheshimiwa Wabunge wengi, Mheshimiwa Lwota, Mheshimiwa Restituta Mbogo, Mheshimiwa Jasmine Tiisekwa, Mheshimiwa Bashe, Mheshimiwa Makilagi na Mheshimiwa Shally Raymond, naomba niliache hilo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la maendeleo ya jamii. Kwenye suala la maendeleo ya jamii mambo makubwa yaliyozungumziwa hapa jambo la kwanza ni la training. Waheshimiwa Wabunge pamoja na Kamati wamechangia kwamba Vyuo vya Maendeleo ya Jamii tuvihamishe kutoka kwetu tuvipeleke Wizara ya Elimu. Jibu la hoja hii ni fupi tu, kwamba vyuo hivi sio vyuo vikuu ni vyuo vya kada za kati ambazo zinahitajika kwa ajili ya kuendeleza Sekta yetu ya Maendeleo ya Jamii na hivyo si lazima vikae kule kwenye Wizara ya Elimu, japokuwa mitihani yote ambayo inatolewa na vyuo hivi inatolewa na Taasisi ya NACTE lakini pia vinasimamiwa na NACTE ambayo ni Taasisi iko chini ya wenzetu wa Wizara ya Elimu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, changamoto kubwa tuliyonayo kwenye eneo hili ni namna ya kuwaajiri – absorption kama nilivyosema pale mwanzoni. Tunao watumishi wengi ambao tunawazlisha kila siku wataalam kwenye eneo hili lakini namna ya kuwaajiri ni changamoto. Nitoe rai kwa Waheshimiwa Wabunge na viongozi wote wanaosimamia maendeleo kwenye mikoa na wilaya kuweka bajeti ya kuajiri wataalam hawa, lakini pia kuweka bajeti kwa ajili ya kuwapa vitendea kazi na kuwapa maeneo ya kazi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tumeshaeleza kwamba Sera yetu ya Maendeleo ya Jamii inataka kwa uchache wawepo wawili kwenye kila Kata, wasikae kwenye ofisi kuu pale Wilayani, wakae kwenye kata, wapewe vyombo vya kufanyia kazi ili waweze kutekeleza majukumu yao.

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la nne linahusu huduma za tiba kwenye Hospitali za Muhimbili, MOI, Ocean Road, Kitengo cha Psychiatric kimezungumziwa pamoja na kitengo cha moyo JKCI pamoja na KCMC na Bugando.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hapa nitazungumzia moja tu la tiba ya saratani. Tiba ya saratani wakati tunaingia kwenye majukumu haya zilikuwa haziridhishi kwa kiasi kikubwa sana, lakini mikakati ambayo imewekwa imeanza kuboresha huduma kwenye eneo hili kwa kasi ya ajabu. Kwa sababu kwa mfano, tiba ya chemotherapy ilikuwa mtu anapaswa kusubiri kwa miezi zaidi ya mitatu, leo hii tumeweza kupunguza waiting time kutoka hiyo zaidi ya miezi mitatu mpaka kufikia wiki tano hadi sita tu na tunakusudia kufikia mwisho wa mwaka huu tuweze kushusha waiting time mpaka kufikia kati ya wiki mbili mpaka wiki nne mgonjwa awe ameshapata tiba anayostahili.

Mheshimiwa Mwenyekiti, la pili, hakukuwa na baadhi ya vifaa vya kutolea tiba ya mionzi. Vile vilivyokuwepo vimekuwa ni vya zamani sana na sasa tayari tumepewa bajeti na tuko katika mchakato wa kununua mashine mpya ya linear accelerator pamoja na CT simulator kwa ajili ya kutoa tiba ya mionzi, ambao tuna uhakika mwisho wa mwezi huu utakamilika. Tuna malengo ya mbali zaidi ya kununua mashine nyingine ya kisasa ambayo katika ukanda huu wa maziwa makuu hakuna hata nchi moja imefunga mtambo huo unaoitwa Pet CT ambao nao lengo lake ni kufanya uchunguzi na kubaini kwa uhakika zaidi yaani kufanya dermacation ya eneo ambalo limeathiriwa na cells ambazo ni malignant ambazo zina cancer.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini pia kwenye Hospitali ya Taifa ya Muhimbili kuna mambo makubwa mawili yanafanyika pale ambayo ni state of the art, ni ya kisasa sana, na hii ni upandikizaji wa kifaa cha usikivu kinachojulikana kama cochlea implant. Hizi ni operations mpya ambazo zitaanza kufanyika pale na zitatusaidia kupunguza idadi ya wagonjwa wanaokwenda kutibiwa nje ya nchi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia tunaanza kufanya operation za kupandikiza mafigo katika Hospitali ya Taifa ya Muhimbili na hii pia itatusaidia kupunguza wagonjwa kwenda nje ya nchi. Hili ni jambo ambalo Mheshimiwa Rais alilizungumza wakati anazindua Bunge hapa hapa Bungeni la kupunguza idadi ya wagonjwa wanaoenda kutibiwa nje ya nchi kwa kuboresha huduma za rufaa ndani ya nchi yetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, la mwisho ambalo napenda kuzungumzia ni hospitali za rufaa za mikoa. Hili lingeweza kwenda sambamba na lile la decentralization by devolution ambalo nimeliruka kwa sababu limeelezewa.

Waheshimiwa Wabunge wengi na hususan Wajumbe Kamati yetu ya Huduma na Maendeleo ya Jamii, wamekuwa wakitamani sana, huduma za afya zisimamiwe moja kwa moja na Wizara ya Afya Makao Makuu, yaani kama Sectorial Ministry. Sisi tunadhani na tunaamini kwa dhati kabisa kwamba mfumo uliopo sasa ndio mfumo mzuri zaidi wa kuhudumia wananchi kwenye sekta hii ya afya hapa nchini, kwa sababu wananchi kwa kupitia mfumo huu wanakuwa na sauti ya moja kwa moja kwenye huduma zinazotolewa kwenye vituo vya afya kule chini mpaka kufikia ngazi ya hospitali ya wilaya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunachoki-plan na kufikiria ndani ya Serikali kwa sasa ni angalau kama tutaweza tutenganishe mifumo miwili ya kutoa huduma za afya. Bado ipo katika fikra, kwamba mfumo wa afya ya msingi yaani kutoka zahanati, kituo cha afya mpaka ngazi ya hospitali ya wilaya usimamiwe na wenzetu wa TAMISEMI kupitia mamlaka zao za Serikali za Mitaa, lakini hospitali za mkoa kwa sababu ni hospitali za rufaa uje kwenye fungu 52, yaani Wizara ya Afya usimamiwe huku pamoja na huduma nyingine za rufaa. Ni wazo ambalo tunalifikiria ili ku-accommodate mapendekezo mbalimbali ambayo yamekuwa yakitolewa na Waheshimiwa Wabunge.

NAIBU WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa fursa hii na naomba kuunga mkono hoja ya Waziri wa Afya.