Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Ofisi ya Waziri Mkuu kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017

Hon. Issaay Zacharia Paulo

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mbulu Mjini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Ofisi ya Waziri Mkuu kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017

MHE. ZACHARIA P. ISSAAY: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nichukue nafasi hii kuipongeza Serikali yangu ya Chama cha Mapinduzi, nimpongeze sana Mheshimwa Rais na kumuombea kila lililo jema katika maisha yake. Nichukue nafasi hii pia kumpongeza Mheshimiwa Waziri Mkuu na juhudi zake na Baraza la Mawaziri kwa ujumla. (Makofi)Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza niwatake Wabunge wetu wote tuendeshe siasa za kistaarabu na siasa za utashi mwema. Tumekuja huku Bungeni tukiwa na nia njema ya kuzungumza matatizo wa wananchi wetu.
MHE. ZACHARIA P. ISSAAY: Mheshimwa Naibu Spika, nichukue nafasi hii kwanza kuipongeza Serikali kwa Mpango wake wa bajeti wa mwaka huu 2016/2017 ni mpango mzuri kwa kuwa unagusa maisha ya Watanzania na hasa hasa kupeleka fedha nyingi katika ngazi za chini.
Mheshimiwa Naibu Spika, nichukue nafasi hii kuzungumzia mambo machache. Kwanza, nizungumzie eneo la miundombinu. Kwa kweli tumekwama sisi Wilaya ya Mbulu katika ile barabara ya Magara, nimwombe sana Mheshimiwa Waziri na Wizara yake watuonee huruma waangalie ule mlima na jinsi ambavyo nguvu ya Serikali inahitajika sana. Kwa kweli katika mwaka huu wa bajeti nashukuru kwa nia njema ya Serikali kwa kutenga fedha za bajeti katika ule mpango wa kujenga bwawa la umwagiliaji kule kwetu na ile barabara pia kwa ajili ya mlimani kuna nia njema hadi sasa tuendelee kuona ni namna gani tunakusanya mapato ili tuweze kutatua tatizo hili la jumla.
Mheshimiwa Naibu Spika, la pili nizungumzie jinsi ambavyo tunaweka vipaumbele katika ule utatuzo wa kero za wananchi. Kwa kawaida mtu hawezi kutambua juhudi za aliyeko kwenye uendeshaji wa chombo, mara nyingi mtu mwingine huwa haoni kama anayeendesha chombo anaendesha vizuri. Mimi niseme tu kwamba jitihada hizi ni kubwa na juhudi za Rais ni kubwa na ndiyo maana anaamua kupeleka fedha kwenye yale maeneo nyeti inapobidi na ambayo ndiyo kero kwa wananchi wetu. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, niiombe Serikali iendelee na kasi yake iliyoanza nayo, iendelee kufanya kazi zake kwa juhudi zote, iendelee kuona mawazo yote tunayochangia katika hii bajeti ni kwa namna gani yanaingia katika mpango wetu na yaweze kutatuliwa pale inapobidi. Si kwamba tunashindwa kutekeleza miradi, ni uwezo wetu lakini pamoja na makwazo mbalimbali. Niitake Serikali iangalie kwa dhati kabisa eneo la majanga. Eneo la majanga na dharura kwa maana ya maafa ya mvua, njaa, magonjwa na maafa mengine yoyote yanakwamisha mipango ya bajeti kwa kila mwaka kwa sababu yanajitokeza baada ya sisi kupanga mipango. Kwa hiyo, niitake Serikali ione ni kwa namna gani inatazama maeneo yanayoweza kuzuilika katika majanga yanayotokea. Mara nyingi tumepata majanga makubwa lakini yanatokea baada ya Serikali kupanga bajeti.
Mheshimiwa Spika, katika mwaka huu wa bajeti ulioisha tulikuwa na dosari nyingi kwenye miradi mingi kwa kukosa fedha. Kwa hiyo, naiomba Serikali kwa kadiri inavyowezekana ione ni namna gani basi hata ile miradi iliyokwama inaingizwa kwenye mpango wa bajeti. Kwa sababu katika ngazi za chini huwa wao bado wanategemea mpaka Juni 30 ile miradi itapata fedha lakini nikitazama naona miradi mingi itakosa fedha na isipohamishiwa katika mwaka wa fedha unaokuja basi ile miradi itakuwa imesahaulika na ni miradi viporo na haitaweza kukamilika kwa namna yoyote ile kwa sababu itakwama.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza bajeti au mpango wa maendeleo wowote ni mpango endelevu unaotekelezwa kwa awamu na unapofika ukomo wa muda uliotarajiwa maeneo yote ambayo hayakufanikiwa hayana budi kuhamia kwenye ule mpango mpya unaoendelea. Kwa hiyo, kila mtu au kila mdau wetu atazame, tuunganishe nguvu katika kukusanya nguvu kwa wadau wa maendeleo, Serikali kama Serikali na wananchi wetu huwa wana mchango mkubwa katika eneo hilo kwa kutoa michango yao ya hali na mali katika kuchangia shughuli za maendeleo.
Mheshimiwa Naibu Spika, tulianza na mambo mengi sasa hivi tunakejeliwa na shule za kata lakini bado zimeendelea kufanya vizuri na tulikuwa na tatizo la madawati limeendelea kutatuliwa. Kwa kawaida isingekuwa rahisi kila mtu atambue mchango wa Rais kwa sababu hapa tunatofautiana kiitikadi na ndiyo jitihada zinakwamishwa. Kwa hiyo, wote kwa pamoja tuunge jitihada za Rais na Waheshimiwa Mawaziri wala msikwazike nendeni kwenye Majimbo, kama nilivyowaalika kwenda Jimbo la Mbulu Mjini nendeni bila kunitafuta mimi, hamna sababu ya kunitafuta mimi Mbunge niko wapi, jitihada kubwa inahitajika kutoka kwao wao waende kwa wakati na waweze kutusaidia katika ile hatua nzuri wanayotarajia. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, nizungumzie suala lingine la shilingi milioni 50 zinazolalamikiwa. Bado ni mapema sana, ndiyo tumeanza mwaka wa bajeti ya Serikali. Huu ni mwanzo wa kujadili bajeti ya Serikali na jinsi tunavyojadili hii, matokeo yake na changamoto zake baadaye ni sisi ndiyo tutakwenda kujadili kama Wabunge kwa niaba ya wananchi. Wananchi wana haiba na hamu kubwa ya kuona kwamba matatizo yao tunayajadili bila kupoteza muda na bila kuendeleza propaganda za kukwazana na porojo katika ukumbi huu wa mjadala wa matatizo ya wananchi kitaifa.
Mheshimiwa Naibu Spika, nichukue nafasi hii pia kuzungumzia maeneo machache katika bajeti hii ambayo yanahitaji kutazamwa sana. Moja ni yale yaliyoguswa na Ilani ya Chama cha Mapinduzi kwa sababu Ilani hiyo ndiyo imeweka ahadi kwa wananchi na wananchi wanategemea ahadi yao itatekelezwa kwa jinsi ambavyo viongozi walioomba kura walisema na jinsi ambavyo Ilani imetafsiriwa kwao. Eneo hili linahitaji kutazamwa ni namna gani Ilani na zile ahadi za Rais zinaingizwa kwenye mipango ya mwaka hadi mwaka.
Mheshimiwa Naibu Spika, Rais alipokuwa Jimboni Mbulu aliahidi lami kilometa tano, naomba basi Serikali kila mwaka iweke utaratibu wa kutatua ahadi yake hiyo. Aliweka ahadi ya kuweka zege mlima Magara na daraja la Magara na pia barabara ya Mbuyuni - Magara - Mbulu ipate lami. Kwa sababu eneo hilo kwa jiografia ni hatarishi na kila kiongozi aliyeenda Mbulu ilikuwa hatuna sababu ya kumpitisha huko lakini ndiyo barabara pekee inayotuunganisha sisi na Babati kama makao makuu ya Mkoa na ndiyo inayotuunganisha sisi pia na mji mkubwa wa kibiashara wa Arusha.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, kwa ujumla niseme bajeti ni nzuri, naunga mkono hoja na naomba Serikali isimamie utekelezaji wa bajeti kwa kuzingatia vipaumbele na kwa jinsi ambavyo bajeti hii itagusa maisha ya mwananchi wa chini ili mwisho wa siku matokeo mazuri ya hapa kazi tu yaonekane.
Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana, nashukuru kwa kunipa nafasi.