Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 – Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo

Hon. Amina Saleh Athuman Mollel

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 – Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo

MHE. AMINA S. MOLLEL: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi nami niweze kuchangia bajeti ya Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo na naomba tu kwanza kabisa ni-declare interest kabisa kwamba na mimi ni mwanahabari, kwa hiyo, Wizara hii ni ya kwangu na inanihusu sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, awali ya yote namshukuru Mwenyezi Mungu kwa kutujaalia kutupa afya na kuweza kujumuika hapa. Kwanza kabisa nampongeza sana Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, kwa kazi nzuri anayoifanya. Pili, nampongeze Mheshimiwa Waziri pamoja na Naibu Waziri, dada yangu pamoja na Mheshimiwa Mwakyembe kwa kazi nzuri wanayoifanya katika Wizara hiyo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kuzungumzia masuala mawili. Kwanza nianze na TBC kwa sababu ndiyo ambayo imenifanya mimi nikawa Amina hapa nilipo. Nimefanya kazi TBC kwa miaka nane. Shirika la Utangazaji TBC lina hali mbaya kiasi ambacho jitihada zinahitajika kwa kweli ili kuona ni kwa jinsi gani tunawasaidia. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, TBC ni chombo cha umma, ni shirika pekee la habari la umma katika nchi hii na ndiyo chombo cha Serikali na siku zote wanasema kwamba ni vyema ukaanza na nyumbani kwako. Huwezi kwenda kwingine pasipo kuanza na nyumbani kwako. Inatia uchungu unapoangalia vyombo vingine vya habari vina hali nzuri wakati sisi chombo chetu kina hali mbaya. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hali halisi naijua sana TBC, mitambo yake imechoka mno, inahitaji siyo kufanyiwa marekebisho, bali inahitajika mitambo mingine mipya ili kuweza kwenda na wakati huu uliopo. Hata kama hao wafanyakazi, kwa kweli wakati mwingine ile morally ya kazi inashuka. Siku moja mjitolee tu mwangalie hata wanapokuwa katika matukio mbalimbali ambayo wao wanahusika muone ni kwa jinsi gani wanavyojitoa katika kuhakikisha kwamba jahazi linakwenda, lakini ndani yake maumivu na mateso wanayopata kwa mitambo ilivyo chakavu, inatia uchungu sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, naomba na nina imani sana na Serikali na nina imani sana na Mheshimwa Dkt. Mwakyembe. Kwanza yeye ana taaluma hiyo ya habari lakini vilevile ni mwanasheria. Kwa maana hiyo, ni matarajio yangu makubwa sana kwa Serikali na wewe pamoja na dada yangu mpendwa Mheshimiwa Anastazia kwamba mtaliangalia kwa jicho la huruma na kwa jicho la pekee Shirika la Utangazaji Tanzania (TBC).

Mheshimiwa Mwenyekiti, vile vile naomba maslahi ya wafanyakazi wa TBC yaangaliwe. Wana miezi saba hawana posho na kama mnavyojua, watu wanategemea kwa kiasi kikubwa sana hizo posho. Mishahara mara nyingi tunakopa; na kama umekopa mshahara, unategemea ile posho ndiyo iweze kukusaidia. Sasa kama hata hiyo posho hupati miezi saba! Juzi juzi wamelipwa posho ya miezi minne na bado wanadai posho ya miezi saba. Jamani hebu tuwe na huruma tuwafikirie wafanyakazi hawa wa TBC ambao wanajitoa. Kwanza hawa ni wazalendo wa hali ya juu ambao wanahakikisha kwamba TBC inasimama na kwenda, pamoja na changamoto zote zilizopo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia naomba Mheshimiwa Waziri atakapokuja ku-wind up atuambie hivi tangu StarTimes wameingia ubia na TBC mpaka leo ni miaka mitano tayari imepita na nilijua ule mkataba ni wa miaka mitano, lakini kumbe unakwenda mpaka miaka kumi. Naomba Mheshimiwa Waziri aje atuambie kwamba TBC tangu imeingia ubia na StarTimes imefaidika nini? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa sababu wako pale, wanatumia eneo lile la TBC pamoja na kwamba tunawahitaji sana wawekezaji, lakini hatuhitaji wawekezaji ambao wanakuja kutunyonya. Tunataka wawekezaji ambao na sisi tutafaidika. StarTimes kama kweli katika yale makubaliano ya Mkataba wao wangetimiza vyema, leo hii Shirika hili la Utangazaji la TBC lisingekuwa na shida iliyopo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nafurahi sana kwamba Mkurugenzi wa TBC ataweza ku-perform vizuri endapo mtamwezesha. Tido alipoingia alikuta TBC ina shilingi bilioni sita ndiyo maana TBC ikapanda juu kwa haraka sana, lakini ameingia Mkurugenzi wa sasa, hakuna fedha, madeni chungu mzima, atawezaje ku-perform? Mimi nawaomba sana mhakikishe kwamba mnaisaidia TBC ili iweze ku-perform vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia namwomba kaka yangu Rioba, kwa upande mwingine ni shemeji yangu, dada yangu ameolewa huko Ukuryani huko Musoma, Mara. Namuamini sana na nina matarajio makubwa sana naye, lakini pia kaka yangu Rioba punguza ukali. Umekuwa mkali mno kiasi kwamba hata wafanyakazi wakikuona wanakukimbia kama panya. Punguza ukali tushirikiane. (Makofi)

Mfano, hata sisi huku tunafanya kazi vizuri sana na Spika. Ukiweka ukaribu vizuri na wafanyakazi, pamoja na kwamba ndiyo huo ukaribu uwe na mipaka ili muweze kushirikiana na kufanya kazi vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lingine naomba kujibu baadhi ya hoja kuhusu uhuru wa habari; na mimi hapa nitanukuu tu mambo machache. Kwa mfano, tofauti na mawazo ya wenzetu ambao wanasema kwamba nchi hii haina uhuru wa vyombo vya habari, naomba ninukuu kwa kusema kwamba nchi hii ina idadi ya vyombo vya habari na njia nyinginezo za mawasiliano.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa mfano, Tanzania ina magazeti na majarida 428, redio 148, televisheni 32 na watumiaji wa internet wapatao milioni 20, yaani nusu ya nchi; na kuna lines za simu zilizosajiliwa na zinazotumika zipatazo milioni 41; robo tatu ya idadi ya watu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, vile vile ripoti mbalimbali duniani, Tanzania iko juu duniani na Afrika. Ukiacha jinsi ambavyo wanazungumza hapa, Tanzania kwa mfano, taarifa ya mwaka huu ya Chama cha Wanahabari Wasio na Mipaka (Reporters Without Borders) ambayo inasema kwamba, kwa mujibu wa ripoti hiyo, Tanzania ni miongoni mwa nchi 20 bora katika uhuru wa habari Afrika. Ya kwanza katika Afrika Mashariki ikiwa ni ya 83 duniani ambapo Kenya ni ya 95, Uganda ni 112, Sudan Kusini 145, Congo-DRC ni ya 154, Rwanda ya 159 na Burundi iko katika nafasi ya 160. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa mujibu wa ripoti hii, Tanzania Kimataifa pia imezizidi baadhi ya nchi kubwa ya huko Ulaya. Katika nchi hizo mfano, Marekani na Asia katika uhuru wa kujieleza na habari; Tanzania imezidi nchi za Ugiriki, Israel, Brazil, Paraguay, Uganda, Falme za Kiarabu, Cameroon, Tunisia na Guinea. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sheria ambayo ilitungwa mwaka 2016 hapa ya Huduma ya Habari namba 12 ya 2016 ni sheria ambayo imeleta mageuzi makubwa sana katika kutetea uhuru wa habari kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa mfano, imebainika…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa mzungumzaji)

MHE. AMINA S. MOLLEL: Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja kwa asilimia mia moja.