Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 – Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo

Hon. Rashid Abdallah Shangazi

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mlalo

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 – Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo

MHE. RASHID A. SHANGAZI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi ya kuchangia hoja iliyoko mbele ya Bunge lako Tukufu. Nami nianze kushukuru na kumpongeza Mheshimiwa Dkt. Harrison Mwakyembe pamoja na Naibu wake kwa kazi nzuri ambayo ameleta. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka niseme kwamba Wizara hii pamoja na ufinyu wa bajeti, lakini ni Wizara ambayo inaweza ikajitengenezea fedha katika maeneo mbalimbali. Kwa hiyo, Mheshimiwa Mwakyembe anao wajibu wa kuhakikisha kwamba anakuwa celebrity katika hii Wizara.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nianze na Shirika la Utangazaji la Taifa TBC. Bajeti iliyopita TBC kupitia Wizara walituahidi kwamba Halmashauri 81 ambazo TBC ilikuwa haisikiki kwamba wanatafuta fedha na watahakisha kwamba katika bajeti ya mwaka huu maeneo hayo yatakuwa yamefikiwa; nasikitika kwamba mpaka sasa TBC haisikiki katika maeneo ya mbali hasa ya pembezoni.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimejipa kazi ya kufanya utafiti, ukiondoa kule Mlalo ambako tunapakana na nchi jirani ya Kenya, lakini kule Rombo kwa Mheshimiwa Selasini pia haipatikani. Juzi nilikuwa Peramiho kwa Mheshimiwa Mhagama, nako huko wanapata redio za Msumbiji. Huko Nkasi kwa Mheshimiwa Keissy anapata redio za Kongo; ukienda Kakonko Kigoma, wanapata redio za Burundi. Sasa hii ni hatari sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunaposema dhima na dira ya Wizara hii ni pamoja na kuwa na Taifa linalohabarishwa vizuri linaloshamirika na kiutamaduni lenye kazi bora za sanaa na lenye umahiri mkubwa katika michezo ifikapo 2025. Bila kuwa na chombo cha habari cha Taifa ambacho kinafikia hayo maeneo, hii itakuwa ni ndoto. Kwa hiyo, naomba sana Wizara ihakikishe kwamba TBC inafanya kazi kwa ufanisi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Mlata hapa alikuwa anaelezea namna ambavyo Clouds FM wameanza ambayo sasa hivi ni Clouds Media. Walianza kwenye chumba kimoja, lakini sasa hivi Clouds ipo nchi nzima, inasikika kwa mawimbi haya ya FM. Tatizo la TBC ni nini? Kama tatizo ni hii teknolojia mpya kwa nini tusirudi kwenye teknolojia ya zamani? Maana wakati ule wakati wa short wave, medium wave na AM ilikuwa inapatikana nchi nzima. Hawa wasanii akina Mzee Jangala, Majuto na wengineo wote tulikuwa tunawasikiliza kwenye vipindi, hatuwaoni lakini tuna-enjoy. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tulikuwa tunaona kabisa huu ndiyo utamaduni wa Kitanzania; walikuwa na vipindi vizuri vya kuelimisha wakati wa Kampeni za Malaria, Kampeni za Chaguzi na kampeni mbalimbali za nchi hii. TBC sasa hivi nao wanaigiza kwenye redio hizi za kizazi kipya. Nataka nitoe tahadhari kwamba tusipokuwa makini, hata Millad Ayo ambaye ameanza juzi juzi hapa, anaweza akaja akaizidi TBC. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala lingine ni suala zima la michezo. Mheshimiwa Waziri ameeleza michezo kwa mapana, lakini nasikitika kwamba bado michezo inaonekana kwamba ni mpaka wadau washiriki. Hakuna jitihada Mahususi za Wizara yenyewe kutenga fedha kwa ajili ya kwenda kuhuisha michezo kwenye mashule, vyuo na hata huko mitaani. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nasikitika sana kuona kwamba wakati wa Mwalimu Nyerere vyanzo vyetu vya bajeti vilikuwa ni vichache sana, tena tulikuwa tunategemea zaidi mazao ya kilimo, yeye aliwezaje? Wale Marijendali wote uliowataja ni wa wakati wa Mwalimu. Inashindikana vipi sasa hivi wakati michezo hii imekuwa ni kama biashara? Kwa hiyo, namwomba Mheshimiwa Waziri, aanze kuwatambua wadau lakini pia lazima Serikali na yenyewe iweke bajeti mahususi kwa ajili ya kuhuisha michezo mashuleni, vyuoni na katika maeneo mbalimbali. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika eneo hili, naomba nichukue fursa hii kumpongeza sana Mheshimiwa Naibu Spika Tulia Ackson, yeye ameanzisha mashindano kule Mkoani Mbeya pamoja, Wilayani Kyela. Kwanza alianza na utamaduni na hili ndiyo eneo ambalo lipo katika Wizara ya Mheshimiwa Waziri. Pia kuna mashindano, anashindanisha ngoma za asili za makabila mbalimbali yaliyopo ukanda ule wa Mbeya. Mwaka huu kuna mpango wa kufanya mashindano haya yawe ya Kitaifa, tuone ngoma kutoka Pemba, kutoka Tanga na pengine popote. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, wadau kama hawa ni vizuri sana tukawaunga mkono ili angalau Watanzania hawa wa kizazi kipya ambao wanaanza kusahau mila na desturi zao waweze kujua kwamba nchi hii ina utamaduni na ina desturi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sambamba na hilo, mwaka huu pia kulikuwepo na mashindano ya Tulia Marathon,

yamefanyika katika Jiji la Mbeya. Haya ni mashindano ambayo nayo yanapaswa kuungwa mkono. Kwa sababu sasa hivi Marathon pekee tunayoitumia hapa Tanzania inayotambulika duniani ni hii ya Kilimanjaro Marathon. Kilimanjaro Marathon tayari imeshaanza kuzidiwa, sasa hivi washiriki wamekuwa ni wengi sana kiasi kwamba sasa wakati mwingine wanakosa nafasi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, tuitumie fursa hii. Pamoja na jitihada nzuri pia za kutangaza Utalii wa Kusini, tunayo Mbuga yetu ile ya Kitulo, tunayo Ruaha, lakini hizi Mbuga hazijatangazwa vizuri. Kwa kutumia michezo hasa kutumia hii Tulia Trust tunaweza tukazitangaza vizuri kupitia Marathon, kwa hiyo, namwomba Mheshimiwa Waziri, Wizara yake iweze kukaa na Mdau huyu kuona hii Marathon inaweza ikatambulika Kimataifa ili tupate washiriki mbalimbali. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine ni suala zima la michezo hasa mpira wa miguu. Mpira wa miguu sisi bado tumekuwa ni washindani wa kubahatisha. Hawa vijana wa Serengeti Boys ambao tunawapongeza sasa, huwezi ukaona successful plan ambayo inaandaa wengine. Inatokea tu kwamba ni bahati, vipaji vimekusanywa kwa wakati mmoja hasa kupitia wenzetu hawa wa Airtel Rising Star. Kwa hiyo, naomba kwamba lazima tuweke mkakati ambao utasaidia tuanze kuandaa vijana wengine. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sambamba na kuandaa vijana wengine, tuandae sasa hii ndio iwe dira yetu ya Timu ya Taifa inayokuja. Hawa vijana tutakapomaliza mashindano haya na tukawaacha wakaingia kwenye vilabu hivi vya Kitanzania ambavyo tunajua namna ambavyo wanawalea wachezaji, tutawaharibu. Kwa hiyo, nitoe rai kwa Mheshimiwa Waziri kwa kushirikiana na TFF tuhakikishe kwamba vijana hawa tunawatunza vizuri, tutafute Mawakala wazuri wa Kimataifa, vijana hawa waweze kupata exposure ya kwenda kucheza soka nje ya nchi ili baadaye waweze kuja kusaidia Taifa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sambamba na hilo, uendeshaji wa mpira wa miguu bado una wasiwasi mwingi. Baada ya kuondoka Rais aliyepita, Leonard Chila Tenga sasa hivi TFF pameyumba sana. Maamuzi mengi yanafanyika kwa upendeleo, kwa hila; ni hivi juzi tu hapa timu ya Simba imenyang’anywa points zake tatu nzuri kabisa. Sasa sheria ziko wazi kwamba mchezaji akiwa na kadi za njano zaidi ya tatu, haruhusiwi kucheza mchezo unaofuata. Matokeo yake yametoka maamuzi mengine bila kugusia kwamba: Je, kadi ilikuwepo ama haikuwepo? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, naomba Mheshimiwa Waziri, tuwaangalie TFF kwa jicho la karibu hasa ukizingatiwa kwamba FIFA ya wakati huu inaruhusu Serikali kuanza kuingilia kuangalia maendeleo katika nyanja hizo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na hilo, Mheshimiwa Waziri amezungumza hapa kwamba timu ya Everton inakuja kucheza na miongoni mwa timu moja ya Tanzania. Nataka niseme wazi kwamba Simba Sport Club ndiyo timu pekee inayoweza ikatoa uwakilishi mzuri. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, huwezi kuishindanisha Simba na Timu ambayo imefungwa na Mbao FC.

Kwa hiyo, naombe sana Mheshimiwa Waziri kwamba hakuna haja ya kushindanisha, Simba Sport Club ndiyo wanatutoa kimasomaso kwenye mashindano ya Kimataifa, hii ni nafasi pekee.