Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 – Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo

Hon. Mariamu Nassoro Kisangi

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 – Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo

MHE. MARIAM N. KISANGI: Mheshimiwa Spika, naunga mkono hoja ya Mheshimiwa Waziri wa Habari na Utamaduni kwa asilimia mia moja. Nampongeza Mheshimiwa Waziri, Naibu Waziri, Katibu Mkuu na Watendaji wote wa Wizara. Napongeza Utendaji mzuri wa Wizara na kwa kweli wanafanya kazi nzuri kwa kipindi kifupi.

Mheshimiwa Spika, mchango wangu utajikita katika Utamaduni wa Mtanzania. Utamaduni wa Mtanzania unapotea kwa kuwa kizazi chetu kinafurahia sana tamaduni za kizungu kuliko zetu. Vifaa vyetu vya asili kama mundu, kinu, mchi, kisagio, mtungi, kata, vibuyu na kadhalika vyote vinapotea na hakuna wa kuvirudisha. Je, Serikali ina mkakati gani wa kulinda utamaduni wetu wa asili kwa kuvilinda vifaa vyetu vya asili.

Mheshimiwa Spika, vile vile kwa mazao yetu pia, kwa kuwa shule nyingi ziko maeneo ya mijini utakuta wanafunzi wanashindwa kujua hata mmea wa mahindi ukoje? Naomba Serikali waweke mpango mahsusi wa kuandaa maeneo maalum ya kitamaduni kama vile Kijitonyama kuweka sehemu ya vitalu vya kuonyesha utamaduni wa mazao mbalimbali.

Mheshimiwa Spika, hiyo itasaidia katika kukuza na kuendeleza utamaduni wetu. Sambamba na hiyo ni mavazi yetu ya asili kama kaniki, kanzu, migolole, shanga, vibwaya na kadhalika. Vifaa hivyo vitunzwe kwa kumbukumbu kwa kuwa vinatoweka sasa.

Mheshimiwa Spika, Sanaa; wachezaji muziki walio wengi wanaume wanavaa nguo vizuri sana lakini wanawake wanavaa nusu uchi. Hali hiyo inatudhalilisha sana wanawake na inatuharibia kizazi chetu kipya kwa kuiga mavazi ya utamaduni ambao si sahihi sana. Serikali itoe kauli kwa wanawake wanaocheza muziki wavae mavazi yao ya heshima pasipo kuwadhalilisha wanawake wenzao.

Mheshimiwa Spika, Mapambo; utamaduni wa kusuka nywele, tumeona watoto wanakua kwa kukazwa nywele na kumfanya mtoto ashindwe kupumua na kupoteza maisha. Serikali itoe angalizo kwa akinamama wenye watoto waangalie watoto wao na wawasuke nywele za kawaida za utamaduni za mikono kwa kuwasaidia watoto mpaka watimie umri wa miaka 12 kwenda juu umri huo mtoto anaelewa baya na zuri.

Mheshimiwa Spika, TBC; ijengewe uwezo iweze kuwa na mitambo mizuri na shughuli za Kiserikali ikiwemo shughuli za Wabunge Majimboni watumie TBC Radio na TV itasaidia hata kuongeza kipato. TBC wajitahidi wawe na mawasiliano katika mikoa yetu ya Tanzania Bara na Zanzibar ili wananchi wetu wafaidi matunda ya Television yetu na Radio yetu ya Taifa.

Mheshimiwa Spika, naunga mkono hoja kwa asilimia mia moja.