Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 – Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo

Hon. Grace Victor Tendega

Sex

Female

Party

CHADEMA

Constituent

Special Seats

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 – Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo

MHE. GRACE V. TENDEGA: Mheshimiwa Spika, napenda kuchangia katika Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, maadili na utamaduni wa Mtanzania; maadili na utamaduni wa Mtanzania yameendelea kuporomoka siku hadi siku kutokana na mambo mengi ikiwemo ukuaji wa teknolojia. Watu walio wengi, hasa vijana, wamekuwa wakikosa maadili mema kwa kuangalia au kuiga mila na tamaduni za nje ya nchi. Baadhi ya watoto wamekosa heshima kwa wakubwa.

Mheshimiwa Spika, naishauri Serikali kutunza mila nzuri na tamaduni zetu kwa kuchukua hatua pale panapotokea ukiukwaji wa mila na desturi, wazazi pia wanapaswa kuangalia maadili ya watoto wao. Elimu kuhusu utunzaji wa mila na desturi itolewe katika jamii. Tunahitaji Tanzania yenye Watanzania walio na maadili mema.

Mheshimiwa Spika, uboreshaji wa viwanja vya michezo; viwanja vingi katika mikoa mbalimbali havikidhi vigezo vya kuwa viwanja vya michezo, hasa vile vinavyomilikiwa na CCM. Katika Mkoa wa Iringa, Uwanja wa Samora Machel umejengwa maghala ndani yake na kusababisha uharibifu pamoja na kuharibu lengo la kuwa na uwanja huo. Napendekeza kuwa Serikali, kupitia Wizara, iwashirikishe Sekta Binafsi ili kuendeleza viwanja hivyo hasa Uwanja wa Samora Machel Mjini Iringa ili kuweza kuinua kiwango cha michezo. Serikali pia ijenge viwanja vipya vya michezo.

Mheshimiwa Spika, Chuo cha Sanaa Bagamoyo; wananchi walio wengi, hasa vijana, wamekuwa wakijishughulisha na sanaa. TASUBA ni chuo kinachotoa mafunzo ya sanaa lakini miundombinu yake haikidhi mahitaji. Katika fedha waliyotengewa Bajeti 2016/2017, milioni 300, wamepata milioni 100 tu, sawa na 5.6%. Nashauri Serikali iweze kuwamalizia kiasi cha fedha kilichobakia kwani chuo hiki ni tegemeo la vijana wengi kupata ujuzi ili wajitegemee kimaisha.

Mheshimiwa Spika, uhuru wa kupata habari; kwa mujibu wa Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania inasisitiza kuwa wananchi wanao uhuru wa kupata habari, Serikali imezuia wananchi kupata habari za Bunge Live. Naishauri Serikali isiwe na woga wa kukosolewa kwani ni afya kwa Taifa na watajipanga kuweza kutekeleza majukumu yao. Niiombe Serikali iruhusu uhuru wa vyombo vya habari ili wananchi wapate haki yao.