Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 – Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo

Hon. Hamoud Abuu Jumaa

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kibaha Vijijini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 – Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo

MHE. HAMOUD A. JUMAA: Mheshimiwa Spika, awali ya yote, nichukue fursa hii kumshukuru Mwenyezi Mungu mwingi wa rehema kwa kuniwezesha kuwepo mahali hapa nami niweze kuchangia bajeti hii ya Wizara husika kwa mwaka 2017/2018. Nimpongeze Mheshimiwa Waziri kwa kuteuliwa katika Wizara hii. Pia nimpongeze Waziri pamoja na wataalam wake kwa kuandaa bajeti nzuri yenye mwelekeo chanya, bajeti hii ni utekelezaji wa Ilani ya Chama cha Mapinduzi.

Mheshimiwa Spika, kwanza niipongeze timu yetu ya Serengeti Boys kwa kuonesha mfano wa kufanya vizuri katika mechi zake zote, hii ni alama tosha na kuikumbusha Serikali kuwa mchezo wowote unahitaji uwekezaji kuanzia chini kwa maana ya kuanzisha vituo vya michezo na kukuza vipaji. Utaratibu huu umekuwa ukifanywa na nchi mbalimbali kama Ulaya, Amerika, Asia na Afrika ingawa sisi hatukuliona jambo hili kwa miaka ya hivi karibuni ukilinganisha na miaka ya nyuma.

Mheshimiwa Spika, michezo hivi sasa ni ajira ambapo imeajiri vijana wengi sana na wamekuwa wakinufaika kama akina Mbwana Samata ambaye anaiwakilisha nchi vizuri sana huko Ulaya. Hivyo, niishauri Serikali bado hatujachelewa tuwekeze katika michezo kwani kuna faida nyingi sana ambazo zitakwenda kutatua changamoto kwa mfano za ajira.

Mheshimiwa Spika, baadhi ya vyombo vya habari vimekuwa havifuati taratibu na sheria zilizowekwa. Hata Mheshimiwa Rais aliwahi kulisema hili kuwa baadhi ya vyombo vya habari vimekuwa vikivuka mipaka. Habari au uandishi kwa kuzungumzia hapa tunaweza kuona ni vitu vya kawaida tu lakini uandishi wa habari wa aina hasi unaweza kuliingiza Taifa katika machafuko makubwa sana. Mifano iko mingi sana ambayo vyanzo vya machafuko ni vyombo vya habari. Habari zinaenea kwa urahisi sana kuliko kitu chochote na sumu yake ni kali sana.

Mheshimiwa Spika, hivyo, tunahitaji kuwa makini sana na vyombo vyetu vya habari ambavyo habari zake ziko katika malengo hasi, habari zake si za kujenga nchi, wala za kimaendeleo, tuviangalie vyombo ambavyo vinatoa kipaumbele kwa habari binafsi ambazo hazina tija kwa Taifa. Serikali sasa kupitia Wizara ni wakati wa kuchukua hatua kali bila woga wala aibu kwa chombo chochote cha habari ama iwe redio, magazeti au televisheni ambacho kinakiuka taratibu na sheria zilizowekwa. Vinginevyo tukivionea haya na nchi ikaingia katika machafuko kutokana na vyombo vya habari basi ni sisi viongozi ndiyo tutakuwa wa kulaumiwa kwa sababu tulipewa dhamana ya kuvisimamia lakini kwa utashi wetu tukashindwa.

Mheshimiwa Spika, tunapozungumzia utamaduni huwa tunazungumzia tamaduni ya nchi au mahali husika. Sisi kama Taifa tuna tamaduni mbalimbali lakini tamaduni hizi tumekuwa tukiziona tu katika maadhimisho mbalimbali vikundi vikikaribishwa kucheza ngoma na kadhalika lakini hakuna mkakati madhubuti uliowekwa wa kuhakikisha tamaduni zetu zinadumishwa kwa namna yoyote na kuzitangaza. Tamaduni zetu ni fursa kama tukizitumia vizuri kwa sababu wageni watakuja kuziangalia na sisi tumejaliwa kuwa na makabila zaidi ya 100, hivyo tamaduni tunazo nyingi sana. Naishauri Serikali sasa kuchukua hatua katika sekta hii pia ili kuiwezesha kukua na kuleta manufaa kwa Taifa.

Mheshimiwa Spika, juzi Jijini Dar es Salaam wasanii wetu wa Bongo Movie waliandamana na dhumuni lao ni kuzuia filamu za nje kutokuuzwa nchini na kuzipa kipaumbele filamu za kwao. Nina ushauri mzuri kupitia Wizara hii naamini utawafikia. Kuzuia filamu za nje sio utatuzi bali wasanii wetu wanatakiwa kuangalia ni wapi walipokosea mpaka soko lao likashuka. Bila kujua walipokosea na kujirekebisha haitakuwa suluhisho kwao kwani hata wakizuia hizo filamu za nje na zikabaki za kwao tu pia soko halitakuwa zuri.

Mheshimiwa Spika, wananchi wamekuwa wakilalamika sana kuhusu ubora wa filamu za ndani kuanzia kwa waigizaji, vifaa wanavyotumia na matukio katika filamu zao. Ninavyofahamu, filamu haiwezi kutengenezwa kwa miezi miwili halafu ikawa tayari sokoni, ni ngumu kuingia katika ushindani wa soko la filamu hata tu la Afrika Mashariki. Hatuwezi ndugu zangu ni lazima tuishi kwa kujifunza, asiyetaka kujifunza lazima atakuwa na mawazo mgando.

Mheshimiwa Spika, hivyo tuwape elimu vijana wetu wa Bongo Movie kuacha kuharakisha filamu kwa miezi miwili au mitatu kuitoa sokoni huku ubora ukiwa finyu. Hakika wakibadilika watauza kwani hapo nyuma walikuwa wakifanya vizuri katika soko hili hili la filamu. Kama nilivyosema hapo awali ni wakati wao kujiuliza ni wapi walipokosea na kujipanga.

Mheshimiwa Spika, naunga mkono hoja.