Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 – Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo

Hon. Anastazia James Wambura

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 – Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo

NAIBU WAZIRI WA HABARI, UTAMADUNI, SANAA NA MICHEZO: Mheshimiwa Mwenyekiti, awali ya yote, naomba nianze kwa kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa kutujalia afya njema na kutupa fursa hii ya kuweza kujadili masuala yanayohusu maendeleo ya nchi yetu kwa muktadha wa uendelezaji wa Sekta za Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naungana na Watanzania wenzangu wote kutoa pole kwa msiba huu uliotupata na Mungu atupe faraja kama wazazi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nitumie fursa hii kumpongeza sana Rais, Mheshimiwa Dkt. John Pombe Magufuli, Makamu wa Rais Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan, Waziri Mkuu, Mheshimiwa Kassim Majaliwa kwa kusimamia vizuri Serikali na hasa kwa upande wa mapato na matumizi hadi kupelekea Wizara yetu kuongezewa bajeti kwa asilimia 19 kwa mwaka wa fedha 2017/2018.

Pia nimpongeze Mheshimiwa Spika, Naibu Spika na Wenyeviti kwa kuliongoza Bunge kwa weledi, lakini pia Waheshimiwa Wabunge wote kwa umoja na ushirikiano walionao katika kuwatetea wananchi na kuboresha bajeti ya Wizara.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nichukue nafasi hii ya kipekee kumpongeza Mheshimiwa Dkt. Harrison Mwakyembe, Waziri wangu, kwa hotuba nzuri ya Bajeti ya Wizara aliyoitoa tarehe 5 Mei, 2017 ambayo utekelezaji wake utaleta matokeo na mageuzi makubwa katika kuimarisha sekta za habari, utamaduni, sanaa na michezo nchini. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kutoa shukrani zangu za dhati kwa Mheshimiwa Waziri wangu kwa ukarimu wake mkubwa kwangu, Katibu Mkuu, Naibu Katibu Mkuu, Wakuu wa Idara na Taasisi pamoja na watumishi wa Wizara yangu kwa ushirikiano wanaonipa katika kazi zangu za Naibu Waziri. Niwashukuru wanawake wote wa UWT wa Mkoa wa Mtwara kwa kuendelea kushirikiana na mimi na kuniombea pia. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa namna ya pekee nasema ahsante kwa familia yangu inayoongozwa na mume wangu mpenzi Laurent Werema, kwa kunivumilia, kunitia moyo na kuniombea. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja hii, naomba na mimi nichangie kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, nianzie na sekta ya habari. Katika sekta hii tuna kundi la kwanza ambalo ni TBC ambapo Kamati iliitaka Serikali kulipa shirika uwezo wa kujiendesha. Wizara na TBC tayari zimelifanyia kazi suala la tozo ya visimbuzi (ving’amuzi) na andiko kuhusu tozo hii mpya linafanyiwa kazi na Wizara ya Fedha na liko katika hatua nzuri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala lingine la Kamati ni kwamba TBC ijenge studio ya kisasa Makao Makuu Dodoma. Fedha za kuboresha studio za TBC Dodoma zimetengwa katika bajeti ya mwaka 2017/2018. Tukiangalia ukurasa wa 79 katika hotuba ya Mheshimiwa Waziri fedha hizi zinaonekana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Kamati pamoja na baadhi ya Waheshimiwa Wabunge wameitaka Serikali kuimarisha usikivu wa TBC na utendaji, lakini pia kuboresha maslahi ya wafanyakazi. Ni kweli kwamba TBC inakabiliwa na changamoto ya uchakavu wa mitambo lakini hata hivyo Serikali imeanza kuchukua hatua zifuatazo katika kutatua kwa awamu changamoto za shirika. Katika mwaka ujao wa fedha 2017/2018, Serikali imetenga fedha za matumizi ya kawaida na bajeti ya maendeleo kutoka shilingi za Kitanzania bilioni moja hadi shilingi bilioni tatu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, shilingi bilioni moja kwa mwaka 2016/2017 imeshapatikana na hii ni kwa ajili ya kuboresha usikivu katika maeneo matano ya mipakani na moja ni Kakonko (Kibondo), Mheshimiwa Kasuku kama yupo amelipigia sana kelele suala hili kwa hiyo awaambie watu wake wakae mkao wa kula. Pia katika Wilaya za Nyasa, Longido, Rombo, Tarime na leo pia nimesikia Mheshimiwa Ngonyani akilipigia kelele, kwa hiyo, wananchi wa Nyasa nao wakae tayari kwa ajili ya usikivu wa TBC. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna suala la Kamati pia ambalo linaitaka Wizara ihamishe mashine ya zamani ya TSN ya kuchapia magazeti ifungwe Dodoma ili kurahisisha upatikanaji wa magazeti. Wizara itafunga mtambo mpya Dodoma na hii ni kwa sababu kitaalam mtambo wa zamani ukifunguliwa na kuhamishiwa Dodoma unaweza kuharibika zaidi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sekta ya utamaduni; Kambi Rasmi ya Upinzani iliitaka Serikali kukuza utalii wa kiutamaduni na majibu yake ni kwamba Serikali imeendelea kuratibu, kusimamia na kutangaza bidhaa za utamaduni na kufanya maonesho na matamasha ya fani mbalimbali za utamaduni ndani na nje ya nchi kwa ajili ya kuvutia utalii na kuingiza mapato.

Mheshimiwa Spika, kuna mchangiaji mmoja pia alipendekeza kwamba kila mkoa kuwe na makumbusho lakini hili ni suala la Wizara ya Maliasili na Utalii chini ya Kitengo cha Malikale.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna suala la kudhibiti mmomonyoko wa maadili ambalo limechangiwa na Wabunge kadhaa. Maadili ni mwenendo unaokubalika na wengi katika utendaji kazi au uendeshaji wa maisha. Kwa hiyo, suala hili ni la watu wote na inatakiwa lianzie katika familia hadi katika taasisi. Hata hivyo, Wizara inaendelea kutoa elimu kuhusu uzingatiaji wa maadili ya Mtanzania na kuchukua hatua mbalimbali za kisheria pale panapotokea ukiukwaji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika maendeleo ya sekta ya sanaa, Kamati imeitaka Wizara iendelee kupambana na wizi wa kazi za wasanii. Wizara inaishukuru Kamati kwa kuunga mkono jitihada za Wizara na pia kwa kutoa msimamo wake kwa kuwataka wote wanaohusika na uharamia wa kazi hizo kuacha mara moja. Aidha, Wizara inakubaliana na ushauri wa Kamati kuhusu uboreshaji wa kazi hizo na itaendelea kushirikiana na wadau kuwajengea uwezo ili kuboresha kazi zao ili waweze kuendana na maendeleo ya teknolojia na kushindana katika soko la ndani na la nje.

Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile Kamati imehimiza uboreshaji wa filamu za ndani na wananchi pia kununua kazi za ndani. Ushauri huo wa Kamati umepokelewa na utafanyiwa kazi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna suala la Kambi ya Upinzani katika sekta ya sanaa kwamba matumizi ya stempu za TRA kutofanya kazi vizuri kutokana na teknolojia ya mtandao. Stempu hizo hutumika kubandikwa katika DVD na CD ambazo kwa sasa ndiyo mfumo unaotumika kusambaza kazi hizi hapa nchini. Kutokana na ukuaji wa teknolojia tayari taratibu za kutengeneza stempu katika nakala laini zinaendelea na stempu hizi toka zimeanza kutumika zimefanikisha kubaini na kukamata kazi zisizo halali zenye thamani ya shilingi bilioni 5.1.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Kambi Rasmi ya Upinzani pia ilionesha kwamba kuzuia kazi za nje ya nchi sio kinga ya wizi wa kazi za filamu na muziki. Serikali haijazuia filamu za nje bali inazitaka kufuata sheria, kanuni na taratibu. Kwa hiyo, dhana hii kwamba tunazuia kazi za nje si kweli, tunataka utaratibu ufuatwe na sheria vilevile zizingatiwe. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sera ya Wizara ni kulinda mila na desturi zetu na kulinda kazi za wasanii na hatutakubali ukiukwaji wa utamaduni wetu na hatutakubali pia kazi za nje ziingie katika nchi yetu bila kufuata utaratibu. Wizara yangu iliwasilisha barua TAMISEMI kuwaomba wawasiliane na mikoa yote ili kuona namna bora ya kuondokana na filamu zisizofuata utaratibu. Kwa hiyo, utekelezaji wa maelekezo ya Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam ni kwa nchi nzima. Kwa hiyo, tusichukulie kwamba kwa kuwa yeye ametekeleza kwamba ni uamuzi wake.

Mheshimiwa Spika, nimeshasema kwamba Wizara iliandika barua TAMISEMI na kuomba wawasiliane na mikoa yote ili kuona namna bora ya kuondokana na filamu zisizofuata utaratibu, kwa hiyo, mikoa yote inatakiwa kufuata na kuzingatia agizo hili.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna suala la upatikanaji wa Vazi la Taifa ambalo nalo limechangiwa na Wabunge kadhaa. Suala hili lilifikia katika ngazi ya Baraza la Mawaziri na uamuzi ulikuwa kwamba Vazi la Taifa litokane na kuamuliwa na wananchi wenyewe. Nikitoa mifano tu ni kwamba hata kipindi cha zamani ilikuwa inatokea mama zetu tulikuwa tukiwasikia wanasema leo tuvae Kitaifa, lakini hapa katikati pia lilizuka vazi fulani ambalo linatokana na kitambaa cha kitenge (makenzi) likaenda mpaka kutaka kuwa kama Vazi la Taifa. Kwa hiyo, ni vyema wananchi wakaamua sasa tuvae vazi gani kama ndiyo Vazi la Taifa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna suala la kuboresha soko la ndani la tasnia ya filamu na kusimamia mapato ambapo tayari wapo watayarishaji wa filamu ambao wameendelea kutengeneza filamu nzuri zilizoweza kuingia kwenye soko la ushindani la ndani na nje ya nchi. Hata hivyo, hoja ya uwepo wa filamu za nje zisizofuata taratibu zimefanya soko la ndani kukumbwa na ushindani mkubwa na Serikali na wadau husika kukosa mapato. Serikali katika kuboresha soko la ndani imeendelea kuwajengea uwezo watayarishaji na wazalishaji wa filamu ili kufanya kazi zao kwa weledi na kwa ubora wa hali ya juu kama inavyoelekezwa kwa kina katika hotuba ya Mheshimiwa Waziri ukurasa wa 32.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna suala la uboreshaji wa tasnia ya ulimwende ambalo limechangiwa na wachangiaji kama wawili hivi. Tasnia ya ulimwende imeendelea kuendeshwa nchini kutoka mwaka 1994 na imeendelea kuwa na mafanikio makubwa hasa katika kuitangaza nchi na vivutio vyake ndani na nje ya mipaka ya Tanzania. Baadhi ya maeneo yaliyofanyiwa kazi ni pamoja na waandaaji kurekebisha dosari mbalimbali zilizojitokeza na kuwa na mfumo bora na uwazi wa uendeshaji wa mashindano mbalimbali ya ulimwende.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa upande wa Miss Tanzania, Wizara katika kulinda hadhi ya shindano hilo imetoa maagizo yafuatayo kwa waandaaji wa shindano hilo (Lino International Agency). Lino International Agency ihakikishe kwamba Kamati ya Miss Tanzania inatoa zawadi ya gari kwa mshindi wa Miss Tanzania 2016 na washiriki wengine wote wanaodai zawadi zao ndani ya mwaka huu kabla ya Juni, 2017 na endapo wakikaidi ama wakishindwa kutoa zawadi katika muda huo watakuwa wamejitoa wenyewe kwenye biashara hii na sheria itachukua mkondo wake.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna suala la kuitaka Serikali ikamilishe utungwaji wa Sera ya Filamu. Tayari maandalizi ya Sera ya Taifa ya Maendeleo ya Filamu yamefikia hatua ya kupata rasimu ya sera. Wadau mbalimbali wametoa maoni na rasimu hiyo itawasilishwa katika ngazi za maamuzi mwishoni mwa mwezi Juni, 2017. Rasimu hiyo ya sera imezingatia pamoja na mambo mengine umuhimu wa kuanzishwa kwa shule ya filamu (film school).

Mheshimiwa Mwenyekiti, maendeleo ya michezo. Katika sekta ya maendeleo ya michezo kuna hoja iliyojitokeza ya CCM kurejesha viwanja vyake Serikalini. Hili suala limetolewa ufafanuzi mara kadhaa hapa Bungeni lakini hata hivyo niendelee kusema tu tena kwamba viwanja hivi ni vya CCM kwa sababu hatimiliki ni ya CCM. Niseme tu tena kwamba haipo hati ambayo inaonesha kwamba kuna kiwanja kilikuwa cha mmiliki mmoja kikahamishiwa kwa CCM, kwa hiyo tuelewe wazi kwamba hivi viwanja ni vya CCM. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Waheshimiwa Wabunge wameitaka Serikali ijenge na kulinda viwanja na maeneo ya wazi. Kwa mujibu wa Sera ya Maendeleo ya Michezo ya Mwaka 1995 inaelekeza kuwa jukumu la ujenzi wa viwanja linashirikisha wadau wote ikiwemo Serikali na wadau wengine. Serikali katika juhudi zake za kuboresha miundombinu ya michezo inashirikiana na wadau mbalimbali wa ndani na nje kujenga miundombinu kwa ajili ya matumizi ya michezo.

Mheshimiwa Spika, katika kufanikisha azma hiyo, Serikali imejenga Viwanja vya Taifa na Uhuru na sasa inajiandaa kujenga Uwanja wa Dodoma. Aidha, mamlaka mbalimbali na wadau nchini wanahamasishwa kushiriki kama walivyoanza baadhi kama vile Azam, Halmashauri ya Bukoba Mjini, Liwale, Lindi na kadhalika na taasisi nyingine.

Mheshimiwa Mwenyekiti, natoa wito kwa wadau mbalimbali wa michezo wakiwemo Waheshimiwa Wabunge kuhakikisha kuwa halmashauri zao zinatenga maeneo na bajeti kwa ajili ya ujenzi wa viwanja vya michezo. Aidha, natoa wito kwa mamlaka zinazohusika kuhakikisha kuwa viwanja vyote vilivyovamiwa katika maeneo yao vinarejeshwa ili viweze kutumika kwa shughuli za michezo na burudani.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini napenda kuliarifu Bunge lako Tukufu kwamba yupo mdau mmoja muhimu sana katika kuendeleza viwanja vya michezo ambaye ni TFF. Kwa taarifa ni kwamba kwa sasa ule Uwanja wa Tanga uko mbioni kuanza kujengwa mwaka huu, wanasubiri tu bajeti ipitishwe ili waweze kuujenga. Vilevile kama nilivyosema hapo awali, viwanja vya Lindi na Memorial Moshi viko kwenye list ya ukarabati. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo, niseme tena naunga mkono hoja, ahsanteni.