Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa mwaka wa Fedha 2017/2018 – Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi

Hon. Khamis Mtumwa Ali

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kiwengwa

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa mwaka wa Fedha 2017/2018 – Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi

MHE. KHAMIS MTUMWA ALI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nami napenda kumshukuru Mwenyezi Mungu, muumba mbingu na ardhi kwa kuniwezesha kuwa mzima wa afya na kuweza kuchangia hotuba ya Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza kabisa, napenda kuchukua nafasi hii kumpongeza Rais wetu, Mheshimiwa Dkt. John Pombe Magufuli na Mama Samia Suluhu Hassan kwa kufanya kazi nzuri ya kusimamia Taifa letu hili. Pia napenda kuchukua fursa hii kumpongeza Mheshimiwa Waziri na Naibu Waziri kwa kazi nzuri wanazozifanya katika kusimamia amani ya nchi hii. Kwa kweli bila amani hatuwezi kufanya jambo lolote. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Jeshi la Polisi linakabiliwa na changamoto mbalimbali nitaanza kuzungumzia makazi ya askari. Kwa kweli makazi ya askari ni duni sana pamoja na Mheshimiwa Waziri kuelezea kwamba wana mpango mzuri wa kujenga nyumba za askari. Hata hivyo, kiuhalisia ukiangalia zile nyumba za askari ambazo zipo hivi sasa zinatisha. Ukienda central tu hapo utakuta nyumba za askari zina mabati, ndani hazina ceiling board hata yule askari akinunua mayai akayaweka ndani baada ya wiki utaona yameshatoa watoto yaani zile nyumba zimegeuka incubator. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hizo hizo nyumba za askari zilizopo ambazo hazina hata ceiling board, zimejegwa kwa udongo ambapo siku za mvua ukipata maji zinaporomoka. Kwa kweli Mheshimiwa Waziri ni lazima aangalie hali hii kwani mazingira wanayoishi askari wetu si mazuri. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ikifika wakati wa usiku baridi iliyokuwemo ndani ya nyumba zile ni kama wapo katika mafriji. Wale ni binadamu, wanataka nyumba nzuri ili waishi kama binadamu wengine ili waweze kufanya kazi vizuri. Naomba sana Serikali kupitia Wizara hii waweze kuangalia hizi nyumba wanazojenga na hizi ambazo zipo ili kuziboresha zaidi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kuongelea posho za askari wetu hawa. Kwa kweli inasikitisha sana, askari wadogo hawapati posho stahiki na kwa wakati na hali hii inapelekea kuwa na imani potofu na duni. Ikiwa kama kuna matabaka ya kupata hizi posho stahiki au kucheleweshewa kupelekwa posho hizi kwa wakati itapelekea askari hawa kuvunjika moyo na hatimaye kutofanya kazi zao vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwaka jana hapa wakati wa bajeti tulimwambia Mheshimiwa Waziri kwamba askari wanalipia umeme kwenye mifuko yao wenyewe kutoka katika mishahara yao. Mheshimiwa Waziri akasema hili atalisimamia lakini inafika hatua wanastaafu pesa za umeme ambazo wametumia kutoka kwenye mifuko yako hawajalipwa hadi sasa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, namwomba sana sana Mheshimiwa Waziri na hili aliangalie aweze kuhakikisha askari hawa wanapewa posho zao straight kama ilivyo kwa Jeshi la Wananchi (JW). Kwa sababu wakipewa hivyo itapunguza malalamiko wakati wa kustaafu ya kutopewa posho au pesa ambazo wanazitumia kwa ajili ya kulipia nyumba au umeme. Namwomba sana Mheshimiwa Waziri atakapokuja aweze kutuelezea vizuri mkakati huu kafikia wapi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa nizungumzie kuhusu mafunzo mbalimbali ya Jeshi la Polisi. Ni ukweIi usiopingika kwamba bila mafunzo Jeshi la Polisi haliwezi likafanya kazi vizuri. Ikiwa mafunzo haya yanatolewa kwa askari wa headquarter tu bila kuwashirikisha wale askari wadogo wadogo waliopo mikoani itakuwa ni vigumu askari hawa kufanya kazi kwa weledi zaidi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, namwomba sana Mheshimiwa Waziri aweze kuhakikisha kwamba askari wadogo nao wanakwenda mafunzo siyo waliopo headquarter tu mikoani mafunzo hamna, hivi sasa mafunzo yamepungua kabisa. Kama kutakuwa na upungufu wa bajeti basi Serikali ipeleke fedha kikamilifu ili mafunzo haya yaweze kupatikana vizuri zaidi kwa askari wetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu ujenzi wa Vituo vya Polisi kama alivyosema Mhesimiwa Raza pale vipo katika hali ngumu. Katika Jimbo langu kuna Kituo cha Polisi kimoja tu, unapotokea uhalifu inakuwa ni shida sana. Namwomba sana Mheshimiwa Waziri kwamba katika Shehia yangu ya Kilombero tungepata Kituo kimoja cha Polisi kwa sababu anapotokea mhalifu inakuwa ni vigumu kumfikisha Kituo cha Mahonda ambapo ni mbali zaidi kutoka eneo husika. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Waziri amekuja hapa akasema kwamba viatu vyake vizuri sana kuliko vya wengine, ni kweli. Hata hivyo, askari wake viatu wanavyotumia ni vile vya UN! Namwomba sana Mheshimiwa Waziri ajitahidi viatu vya askari wake viwe kama vyake.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya hapo naunga mkono hoja. Ahsante sana.