Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 - Wizari ya Maji na Umwagiliaji

Hon. Edward Franz Mwalongo

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Njombe Mjini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 - Wizari ya Maji na Umwagiliaji

MHE. EDWARD F. MWALONGO: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kunikumbuka na kunipa nafasi hii ili niweze kuchangia hoja iliyopo mbele yetu. Kutokana na ufinyu wa muda nianze kwa kusema kwanza kabisa naunga mkono hoja. Pili, nitoe mapendekezo yangu juu ya masuala ya maji.

Mheshimiwa Naibu Spika, bajeti yetu ya maji imepungua sana, licha ya kupungua na hata ile bajeti ambayo imekwenda ni asilimia 19 tu, na mimi naungana na wale wote wanaosema tuongeze kwenye tozo ya mafuta ili tuweze kupata fedha zaidi ili tupate maji zaidi kwa ajili ya vijiji vyetu huko Majimboni.

Mheshimiwa Naibu Spika, ninaiomba sana Serikali tutakapokubaliana kwamba tunaongeza tozo kwenye mafuta angalau kwa shilingi 50/= kwa lita basi mgawanyo wa fedha hizi uende sawa, isionekane tu kwamba upande fulani wa nchi ama upande fulani wa Majimbo ndio unapata fedha nyingi zaidi kuliko mwingine, kwa sababu tutakaolipia fedha kwenye mafuta ni Watanzania wote. Kwa hiyo, tupate kwa usawa, miradi yote ya maji igawiwe fedha kwa usawa.(Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Rais katika masuala ya maji anataka kumtua ndoo Mama wa Kitanzania na kasi ya Mheshimiwa Rais wako ambao hawaijui na wasioijua kasi Mheshimiwa Rais juu ya kumtua mama ndoo ni Wahandisi wa Maji walioko kwenye Halmashauri zetu, vilevile watu wa Idara ya Manunuzi wakiongozwa na Idara ya Manunuzi ya Halmashauri ya Mji wa Njombe pamoja na Mhandisi wa Idara ya Maji Njombe, hawana habari kabisa kwamba Mheshimiwa Rais anataka kumtua ndoo mama wa Kitanzania.

Mheshimiwa Naibu Spika, miradi ya maji ya Njombe haiendi, haiendi kwa sababu hawa watu wawili yaani Idara ya Manunuzi na Idara ya Maji hawana habari kabisa kama kuna kumtua mama wa Kitanzania ndoo ya maji kichwani.

Mheshimiwa Naibu Spika, ninaomba sana kwa kuwa, Idara hizi mbili Idara Manunuzi na Idara ya Uhandisi zipo chini ya TAMISEMI, TAMISEMI waziangalie Idara hizi ili kusudi waweze kufanya kazi vizuri.

Mheshimiwa Naibu Spika, Wizara ya Maji kaka yangu Mheshimiwa Lwenge ni Injinia na kaka yangu Mheshimiwa Kamwelwe pia ni Injinia. Kadri tunavyofahamu teknolojia ya maji ilivyo rahisi haikupaswa sisi tukose maji, tunakosa maji kwa sababu ya uzembe wa wahandisi walioko kwenye Idara ya Maji huko kwenye Halmashauri zetu.

Mheshimiwa Naibu Spika, Halmashauri ya Mji Njombe pamoja na Idara ya Manunuzi wanafanya manunuzi mwaka nzima, wanahangaika kufanya manunuzi, sielewi wananunua kitu gani.

Mheshimiwa Naibu Spika, ipo miradi ya maji ya Igongwe imeshindikana kutekelezwa ndani ya Halmashauri ya Mji Njombe kwa sababu tu kwamba Idara ile ya Manunuzi imesimamia utaratibu wa manunuzi mwaka mzima, mpaka leo naongea hivi bado mkandarasi hajakabidhiwa mradi, bado anahangaika na taratibu za manunuzi. Mara sijui tusaini hiki, mara tusaini hiki.

Ninaomba sana kwa kuwa ndugu yangu Mheshimiwa Simbachawene wanaokufahamu sasa wanakujua wewe ni Mwanasheria, lakini mimi ninayekufahamu zaidi najua wewe ni fundi, tulisoma chuo kimoja. Walioko kule wanahitajika Technician ili wafanya ile kazi, Engineer ni mtu ambaye kwa kweli hana uwezo kabisa wa kushughulika na maji vijijini.

Mheshimiwa Naibu Spika, ninaomba sana tuweke vijana ambao wana moyo wa kushughulikia matatizo ya wananchi na wana uwezo mkubwa. Injinia kwanza anajisikia, kwenda kwenye mabonde yale ya maji na uinjinia wake anaweza kuona ni matatizo.

Kwa hiyo, ninaomba sana kwamba tuweke technician, vijana wadogo ambao wako tayari kuhakikisha kwamba maji yanapatikana.

Mheshimiwa Naibu Spika, katika miradi ya maji kule Njombe tuna shida sana ya miradi miwili ya maji, Mradi wa Lugenge na Mradi wa Ngalanga. Miradi hii imeathirika vibaya sana. Serikali imetoa fedha ndiyo, hata kama imetoa kwa kuchelewa lakini jinsi miradi inavyotekelezwa inatia huruma, mradi wa Lugenge ulikuwa ni mradi wa mwaka 2012 na ulikuwa ni mradi wa miezi tisa, leo hii ni miaka mitano mradi haujakamilika.

Mheshimiwa Naibu Spika, ukiutembelea mradi unatia huruma, wananchi wale wanasikitika sana, mabomba yameachwa porini, mitaro imechimbwa na maji zaidi ya pale walipochimba. Intake zimejengwa hazijakamilika, Mhandisi yupo Mhandisi Mwelekezi yupo, Mhandisi wa Mkoa yupo, watu wote hao lakini mradi hauendi. (Makofi)

Ukiuliza Wizarani Mheshimiwa Waziri anasema fedha ipo walete certificate. Mkandarasi anatengeneza certificate anampelekea Mhandisi, Mhandisi anatoa copy certificate analeta ile copy wizarani, nani atalipa kwa malipo ya copy? Kwa hiyo, huu ni uzembe wa dhahiri kabisa na uzembe wa makusudi, wanasababisha wananchi wakose huduma bila sababu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa niombe Wizara ya Maji mtusaidie hasa huu mradi wa Lugenge, naomba mje muukague na mtusaidie kwa sababu huu mradi umeshapitisha miaka mitano. Leo hii mkisema bei ya mradi huu utekelezwe kwa gharama zilezile haiwezekani, hata kama utaratibu hauruhusu, lakini vifaa vilivyokuwa vinanunuliwa miaka mitano iliyopita vikinunuliwa leo bei zimebadilika. Niwaombe sana Wizara ya Maji mtusaidie, mje muangalie mradi wa Lugenge ili kusudi tuweze kuurekebisha, kwasababu wananchi wale wanashindwa kuielewa Serikali, na tumekuwa tukiwashawishi mara zote kwamba maji yenu mtapata. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, walishatengenezewa mabomba mitaani, mabomba hayana hata maji lakini intake hazijajengwa na mabomba hayajalazwa ya kukamilika. Kwa hiyo niombe sana Wizara sasa itusaidie, ituletee mtaalam aje afanye ukaguzi na atoe ushauri tufanye nini na mradi huu kwa sababu sasa hivi tunaona hata mkandarasi naye anasua sua.

Mheshimiwa Naibu Spika, vilevile mradi wa Ngalanga nao unaonekana kama umekosewa kufanyiwa designing kwa sababu wenyeji wanasema chanzo hakina maji kabisa na wanashangaa mabomba yanalazwa watapeleka nini? Kwa hiyo niombe sana miradi hii miwili ya Njombe ikaguliwe. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, mimi ni Mjumbe wa Kamati ya LAAC, katika Kamati yetu tulitembelea baadhi ya miradi ya umwagiliaji, kwa kweli inasikitisha. Unakwenda pale Halmashauri ya Lindi kuna mradi unaitwa Ngongo mpaka CAG amesema mradi unakosa umeme. Tumetembelea mradi hakuna dalili ya mradi kuanza leo wala kesho, ni pori. Sasa unajiuliza mpaka CAG anasema bado umeme halafu kuna pori hakuna maji, hawajalima wala nini lakini unaambiwa bado tu umeme. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini mradi wa maji tulitembelea pale Tabora nao ni hivyo hivyo, bwawa limekauka, fedha nyingi imetumika. Kwa hiyo, niombe sana kama kuna uwezekano kwenye miradi ya umwagiliaji nchi hii, kama tunaamini itatuokoa basi hiyo idara ya umwagiliaji huko wizarani ifanyiwe maboresho kwa sababu designing zao zimeonyesha kwamba miradi ile haina tija kabisa wala haifanyi kazi na wala haielekei kwamba inaweza kufanya kazi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, la mwisho, gharama za maji. Yuko mjumbe hapa jana ameongea kwamba hivi haya maji ni huduma au ni biashara? Ni kweli watumia maji wanapaswa kulipia gharama za maji lakini gharama zenyewe angalau ziwe zinaendana. Mji wa Njombe gharama ya maji ni juu sana, unit moja ya maji Njombe ni shilingi 855, na katika hiyo bei unalipa tena na service charge ya shilingi 2,000. Lakini maji tunayopata katika Mji wa Njombe ni maji ya mtiririko, mitaro ile tulichimba sisi wenyewe. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, halafu Njombe maji yetu yale pamoja na kwamba ni ya mtiririko hayana mtambo wa kuyasafisha wala nini, yanavyotiririka huko toka Mungu alivyoyaumba basi mpaka ndani ya nyumba zetu. Sasa gharama hii inavyokuwa kubwa namna hii wananchi wa Njombe wanalalamika na kusema kwamba hii inakuwaje?

Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Waziri Mkuu alivyofika aliambiwa jambo hili lakini akatoa maelekezo. Kwa hiyo, naomba tena idara ya maji, lifuatilie jambo hili. Ni kweli EWURA walikuja lakini je, unampambanisha EWURA na mwananchi wa kawaida? EWURA wale ni wataalam, mwananchi wa kawaida anaelewa nini? Haiwezekani kabisa kama anataka kulinda haki za wananchi wetu tuwapambanishe eti EWURA kwa sababu EWURA wanakaa wanaongea na mlaji. Mlaji anamsikiliza mtaalam wa idara ya maji anachosema, mtaalam wa Idara ya Maji ameshapiga hesabu zake pale. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini pamoja na hayo haiwezekani upandishe bei ya maji kutoka unit moja kutoka shilingi 395 mpaka shilingi 855 kwa mara moja? Una sababu gani na unakimbilia wapi? Umebanwa na nini cha pekee mpaka uamue kupandisha maji kwa gharama kubwa namna hii? Haiwezekani kwa sababu kama ninavyosema maji ya Mji wa Njombe ni maji ya mtiririko na gharama yake sehemu kubwa tulifanya wenyewe wananchi kwa kuchimba mitaro na wenyewe Idara ya Maji wamekuja wamekuta ule mradi upo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, niombe sana na kama haiwezekani kupunguza maji basi Mamlaka ya Maji ya Mji wa Njombe iondolewe, Idara ya Maji irudishwe Halmashauri kusudi ishughulikiwe na Halmashauri kusudi ishughulikiwe na isimamiwe na Halmashauri. Tunaamini kwamba gharama za maji zitapungua. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, tunapoiendea miradi hii ya maji niendelee kusisitiza kwamba tuombe sana mhandisi, idara ya maji ya Halmashauri ya Mji wa Njombe ije iangaliwe upya kwa maana ya watalaam wake na ikiwezekana…

(Hapa kengele ililia kuashiria kuisha kwa muda wa mzungumzaji)

MHE. EDWARD F. MWALONGO: Mheshimiwa Naibu Spika, naunga mkono hoja, asante sana.