Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 - Wizari ya Maji na Umwagiliaji

Hon. Leah Jeremiah Komanya

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Meatu

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 - Wizari ya Maji na Umwagiliaji

MHE. LEAH J. KOMANYA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kunipatia nafasi hii jioni ya leo na mimi niweze kuchangia hotuba ya Wizara ya Maji. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza napenda niwapongeze Mheshimiwa Waziri na Naibu wake kwa namna wanavyojituma. Muda mwingi nimekuwa nikifuatilia na kuwaona wako field. Kwa maana hiyo, wamekuwa wakifuatilia kuangalia namna miradi ya maji inavyotekelezwa na kuona changamoto zinavyojitokeza katika utekelezaji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba niungane na Mheshimiwa Chenge Mbunge wa Bariadi kuhusu kuboresha huduma ya maji katika Mji wa Bariadi, nami niongeze mambo mawili kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, Mji wa Bariadi ni Makao Makuu ya Mkoa wa Simiyu. Hivyo, ongezeko la watu limekuwa likiongezeka kila siku. Mji umekuwa ukipanuka kila siku na mradi huu umekuwa ni wa muda mrefu.

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba basi wakati wanakamilisha utekelezaji, waweze kufanya tathmini tena, waweze kuona ongezeko la watu na ongezeko la makaazi ya watu lilivyoongezeka ili waweze kuendelea kuupanua mradi huu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo lingine, naomba niungane na Mheshimiwa Chenge kuhusu Serikali katika utekelezaji, iweze kukumbuka yale makubaliano kwamba wakati wa utekelezaji wa huo mradi maji yatatengwa kwa ajili ya mifugo na kilimo.

Mheshimiwa Naibu Spika, naamini soko la Bariadi lina mahitaji makubwa, lina mahitaji ya mboga za majani, matunda na kadhalika. Angalau wanawake waweze kujipatia sehemu ya kuuza, kwa kulima mboga mboga na mazao mengine ambayo watapata soko lao katika Mji wa Bariadi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba pia nichangie upande wa programu ndogo ya maji na usafi wa mazingira. Programu hii imekuwa mkombozi kwa wananchi waishio vijijini. Programu hii ilianza mwaka 2006 hadi 2016, sasa yapata miaka kumi.

Mheshimiwa Naibu Spika, nikiwa Mtendaji nimeshuhudia kwa namna gani imeweza kusaidia upatikanaji wa maji vijijini. Nitoe masikitiko yangu; ukiangalia Kifungu 4001 - Maji Vijijini; Kifungu kidogo cha 3280 ambayo ni Maji na Usafi wa Mazingira, mwaka wa fedha wa 2016/ 2017 zilitengwa shilingi bilioni 310.7, lakini mwaka huu wa fedha wa 2017/2018 zimepungua hadi shilingi bilioni 158.5, zimepungua kwa zaidi ya asilimia 50.

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba fungu hili liongezewe fedha. Kwa kuwa bajeti kuu imeongezeka basi na kifungu hiki kiongezewe fedha. Kwa sababu ukiangalia sehemu kubwa ya nchi ni vijijini. Kwa mfano, nikiongelea mradi wa maji wa kutoka Ziwa Victoria kwa Mkoa wa Simiyu, kutoka Busega na maeneo yake. Mradi huu tu uta-cover vijiji 253. Ukiangalia vijiji ambavyo havitafikiwa na mradi viko zaidi ya asilimia 50.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa mfano, nikiangalia Jimbo la Maswa Magharibi, Jimbo zima hakuna kijiji kitakachofikiwa na mradi huu. Kwa hiyo, bado ipo changamoto ya uhitaji wa mradi wa maji vijijini, uongezewe bajeti. Kwa mfano, kuna Vijiji vya Kinamgulu, Mwabayanda, Ilamata na Mwandu. Vijiji hivi vipatiwe hata visima virefu kwa sababu kule mradi hautapitia hata kijiji kimoja. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba pia niungane na Wabunge wengine kwamba sasa shilingi 100 ziweze kukatwa katika bei ya petroli na diesel. Ziongezwe shilingi 50/= kwa sababu hii itaongeza bajeti ya maji vijijini. Nashauri asilimia 70 ielekee vijijini kwa sababu huko kuna changamoto ya upatikanaji wa vyanzo vya maji. Nashauri pia awepo Wakala wa kusimamia fedha hizi zitakapopatikana ili ziweze kuratibiwa kikamilifu.

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kuchangia kuhusu Bwawa la Mwanjolo lililopo Wilaya ya Meatu, Jimbo la Meatu. Mwaka 2016 mwezi wa Tano Mheshimiwa Waziri mwenyewe aliniahidi kwamba litafanyiwa tathmini ili liweze kukamilishwa, lakini hakuna utekelezaji ulioendelea. Bwawa hili lilianzishwa 2009, wananchi walitoa eneo wenyewe lakini sasa hivi limeanza kuwa kero kwao, limesababisha mmomonyoko wa udongo, wananchi waliacha kufanya shughuli zao kwa ajili ya mradi huo, lakini utekelezaji hakuna. Naomba sasa utekelezaji wake ukamilike. (Makofi)

Pia nichangie kuhusu Mamlaka ya Maji Mjini Mwanhuzi. Tunategemea maji kutoka Ziwa Victoria, lakini Wilaya ya Meatu itakuwa awamu ya pili. Ukiangalia bwawa lile, limejaa matope, nina wasiwasi kama maji yatafika hata mwezi wa Kumi. Mji mdogo wa Mwandoya, chanzo kilichopo cha Igobe kimezidiwa. Nashauri basi uwepo mpango wa dharura ili kuweza kuinusuru Wilaya ya Meatu, Mji mdogo wa Mwandoya pamoja na maji mjini. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, maji haya pia yanaweza yakapatikana kutoka Mto Sem ambayo itasaidia kupitiwa Kijiji cha Mwagila, Sem, Isengwa, Manyahina na Busia, Busia ambako tenki lipo pale lakini wananchi wa pale hawapati maji. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nichangie pia kuhusu dhana ya mradi wa vijiji kumi. Katika WSDP 1 dhana ya mradi wa vijiji kumi niliona kila kijiji kilikuwa kikitafuta chanzo cha maji. Nashauri katika WSDP 2 kama ni vijiji viwili au vitatu kinaweza kikapatikana chanzo kimoja, mtindo huo utumike ili kuweza kuokoa fedha. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, mimi ni Mjumbe wa Kamati ya LAAC; wakati wa ufuatiliaji miradi RWSSP katika ile component ya sanitation utekelezaji wake haufanyiki vizuri, kwa sababu unapofanyika mradi wa maji lazima kijengwe choo. Ukiangalia mradi wa maji wenye mabilioni umekamilika, lakini kipengele cha usafi na mazingira kujenga choo, yaani hela kidogo tu miradi hiyo haijatekelezwa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kuunga mkono hoja kwa asilimia mia.