Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 - Wizari ya Maji na Umwagiliaji

Hon. Yosepher Ferdinand Komba

Sex

Female

Party

CHADEMA

Constituent

Special Seats

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 - Wizari ya Maji na Umwagiliaji

MHE. YOSEPHER F. KOMBA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Kwanza kabisa, naomba niwape pole wafiwa wote wa ajali ya watoto kule Arusha, lakini pia niwape pole wananchi wa Mkoa wa Tanga, hasa maeneo ya Muheza, Korogwe, Tanga Mjini, Pangani ambao wamepata madhara makubwa kutokana na mvua zinazoendelea. Vile vile, niwape pole familia ya mtoto wa miaka 12 pale Kata ya Genge-Muheza ambaye alifariki juzi kwa kudondokewa na ukuta. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nichangie machache kwenye Wizara hii ya Maji. Ukiangalia kwenye Kitabu cha Waziri, ukiangalia yaliyoandikwa humu, bado hawajawa serious kuhakikisha kwamba wanamtua mama ndoo kichwani. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nilikuwa najaribu kufikiria msemo wenu wa kumtua mama ndoo kichwani, sidhani kama mnamaanisha. Kwa sababu, kwa Kiswahili cha kawaida, huwezi kutua kitu ambacho hakipo. Kwa hiyo, mnataka kusema mwanamke aendelee kubeba ndoo.

Mheshimiwa Naibu Spika, ninachotaka kuwaambia na kuwaomba, nchi ilipofikia tangu tupate uhuru hatutaki kusikia ndoo kichwani, tunataka kusikia mama anabeba maji si zaidi ya mita 400, tunataka kusikia mtoto wa kike anaenda shule bila kufikiria maji, tunataka kusikia watoto wa chini ya miaka mitano hawafi kwa magonjwa yanayotokana na shida za maji, tunataka kusikia akinamama wajawazito wanapoenda kujifungua hawaendi na ndoo za maji hospitalini, tunataka kusikia na kuona mnafanya mambo ambayo yanaendana na umri wa nchi hii. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nchi zilizoendelea sasa hivi wame-advance kutengeneza ATM za maji, Tanzania bado tunafikiria ndoo za maji vichwani, ni aibu! Nimepitia bajeti ya maendeleo mmezidi kuipunguza kutoka shilingi bilioni 900 mpaka shilingi bilioni 600, sijui lengo lenu ni nini? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini naomba nichangie kidogo kuhusu Mfuko wa Maji. Tunajua faida zinazotokana na mfuko huu ambao mliutengeneza kwa sheria hapa Bungeni mkiamini kwamba tozo ya shilingi 50 kwenye mafuta itasaidia kwenye miradi ya maji. Cha kushangaza tozo imeenda vizuri lakini matumizi mmeanza ku-diverge. Matumizi mengi ya mfuko huu yameonekana yameenda kwenye administration kuliko kwenye miradi halisi. Niwaombe muongeze shilingi 50 kwenye mfuko huu iwe shilingi 100 ili miradi ya maji iweze kutekelezwa kwa kiwango kinachotakiwa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini pia naunga mkono huu Mfuko wa Maji uendelee kuongezwa hela kwa sababu, kwenye Wilaya ya Muheza tuna Mradi wa Zigi - Pongwe ambao ni almost shilingi bilioni 2.7 na mfuko huu ndiyo chanzo kikubwa cha fedha kwenye huu mradi na fedha zimeanza kutolewa. Kuna miradi mingi inaanzishwa lakini inashia katikati, niendelee kuwaomba Serikali muutendee haki mradi huu kwa sababu hali ya maji Muheza ni mbaya. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, tunaomba mtutendee haki katika mradi huu kwa sababu mpaka ninavyoongea Muheza Mjini ambapo tumeshaanza kuanzisha Mamlaka ya Mji Mdogo tuna asilimia isiyozidi 25 ya wananchi wanaopata maji safi na salama. Niwaombe sana muutendee haki mradi huu kupitia mfuko huu kwa kuongeza Sh.50/= ili iwe Sh.100/= ili angalau 70% iende vijijini, 30% ibakie mjini. Pia kwa kutengeneza mfuko haitoshi, tunaomba kuwe na utaratibu mzuri wa kusambaza hela hizi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini kitu kingine naomba niongelee ukosefu waemergency plan. Tumeona kuna mafuriko yanaendelea maeneo mbalimbali ya nchi lakini hakuna plan yoyote ya Wizara ya Maji kwa ajili ya ku-control hali hii. Mafuriko yanatokea mabomba yanaziba, hivi sasa
ninavyoongea maji ya Mkoa wa Tanga katika maeneo mengi, Tanga Mjini, Muheza, Korogwe na maeneo mengine ni kama chai ya rangi, lakini kama mngekuwa na emergency plan, treatment plan na strainer za kuchuja maji ingesaidia sana inapotokea mvua na mambo mengine. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini pia miundombinu ya maji kwenye nchi hii imechakaa.