Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 – Wizara ya Maliasili na Utalii

Hon. Amb Dr. Diodorus Buberwa Kamala

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Nkenge

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 – Wizara ya Maliasili na Utalii

MHE. BALOZI. DKT. DIODORUS B. KAMALA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa kunipa fursa hii ya kuchangia hoja muhimu iliyo mbele yetu. Hoja ya kwanza niliyonayo leo ni kuhusu Wakala wa Huduma za Misitu. Wakala huyu anajitahidi kufanya kazi yake na kwa kweli tatizo kubwa linalojitokeza ni kwamba kwa muda mrefu alikuwa likizo lakini baada ya kuhimizwa na baada ya Wakala huyu kwenye mipango yake kuona kwamba ni muhimu sasa waanze kuweka mipaka ya kuonyesha eneo lao lakini kubwa linalojitokeza hapa ni mabadiliko ya tabianchi, lazima sote tukubali.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Wilayani Misenyi kwa muda mrefu sana hali ya hewa ilikuwa nzuri. Hakuna mtu aliyefikiria kuna sababu ya kwenda kulima kwenye maeneo ya matingatinga, hata hawa wenzetu wa huduma za misitu hawakuona umuhimu wa kubainisha mipaka kwa sababu kila mtu alikuwa na eneo la kutosha, kwa hiyo kulikuwa hakuna tatizo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kutokana na mabadiliko ya tabia nchi na mahitaji ya maeneo kuongezeka, sasa kila mmoja anajitahidi kuweka mipaka yake. Watu wa hifadhi wanajitahidi kubainisha mipaka ya maeneo yao kuonesha wanaanzia wapi na wanaishia wapi lakini na wananchi pia wangependa wawe na maeneo ya kutosha ya kuchungia mifugo yao. Wananchi wanafuata maelekezo ya viongozi ambapo tumezoea inapokuja wakati wa ukame wanawahimiza waende kulima kwenye maeneo ya matingatinga.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa mfano, ukiangalia pale Wilayani Misenyi, kuna hifadhi inaitwa Lusina; hii inagusa Kata za Bugandika na Bugorora; kuna hifadhi inaitwa Kikuru; hii inagusa Kata za Buyango na Ruzinga, lakini pia kuna hifadhi nyingine kubwa tu inaitwa Minziro. Hifadhi zote hizi zina changamoto ya mabadiliko ya tabia nchi na changamoto ya hawa wenzetu wa hifadhi kuanza kubainisha maeneo ya hifadhi zao na kwa kufanya hivyo unakuta wananchi wanaona wameingiliwa maeneo yao.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukisoma taarifa ya Mheshimiwa Waziri utagundua kuna kipengele kinasema kuna vijiji 228, hii ni kwa nchi nzima na maeneo mengine, vipo ndani ya hifadhi na vijiji 157 vimeshasajiliwa. Sasa kama kwenye kitabu chake cha hotuba Mheshimiwa Waziri anatambua vipo vijiji 228 ndani ya hifadhi katika maeneo mbalimbali Tanzania na anabainisha kwamba vijiji 157 vimeshasajiliwa maana yake alichokuwa anajaribu kutueleza Mheshimiwa Waziri ni kwamba kuna migogoro hapa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, migogoro ikishatokea kinachotakiwa ni kuitafutia ufumbuzi. Hatuwezi kuacha migogoro hii ikaendelea kwa sababu ukiacha na wewe unakuwa sehemu ya mgogoro. Kwa hiyo, nimwombe Profesa najua amebobea katika masuala haya, najua ana nia nzuri, najua wataalam wake kupitia hizi hifadhi za misitu wana nia nzuri pia basi tushirikiane kuhakikisha kwamba migogoro hii tunaipatia ufumbuzi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nichukue nafasi hii nishukuru wenzetu wa TANAPA kwa sababu nilipoteuliwa mara ya kwanza kuwa Balozi, maana kazi nyingine hizi hujasomea, nakumbuka baada ya kuteuliwa Mheshimiwa Rais akatuambia Ubalozi husomei nenda tu mtafanya kazi. Nikauliza wenzangu pale tunaanzia wapi? Tutakubaliana kwamba hebu tuwaombe TANAPA ambao wanasimamia hizi hifadhi watupe angalau mafunzo kidogo, tukienda nje huko basi tuweze kuitangaza Tanzania kwa sababu huwezi ukatangaza kitu usichokijua. TANAPA wakatupangia safari nzuri, tukaenda Northern circuit lakini pia wakatupeleka Southern circuit, tukatembelea Ruaha ni nzuri kweli kweli, tukaenda Katavi kule tukajifunza mambo mengi. Nakumbuka tulikuwa na Mabalozi mbalimbali, Mheshimiwa Balozi Batilda, Mheshimiwa Balozi Marmo, Balozi aliyeenda Msumbiji, Misri na Mabalozi wengine, kwa kweli tulijifunza vitu vingi kutokana na ziara hizi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tulipoenda kwenye vituo vya kazi tukajikuta kumbe kazi yetu kubwa ni kuitangaza Tanzania lakini huwezi kuitangaza Tanzania usiyoijua, ziara ile kwa kweli ilitusaidia sana. Nachukua nafasi hii kuwashukuru TANAPA na kumshukuru Mheshimiwa Waziri na Mheshimiwa Kijazi kwa sababu nilikuwa sijapata nafasi ya kurudi katika Bunge hili kushukuru. Kwa hiyo, nilienda, nilifanya kazi, nilijifunza na nimerudi na nawashukuru sana kwa kutupeleka maeneo hayo ya utalii. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jedwali Na.3 la kitabu cha Mheshimiwa Waziri linaonyesha estimates za maduhuli kwa mwaka 2015/2016 ni shilingi bilioni 25 lakini ukiangalia estimates za mwaka uliofuata ni sifuri. Sasa sijui ni makosa ya uchapaji, huwezi ukawa na makisio sifuri sijui nini kilitokea. Pia ukiangalia hata maduhuli upande wa wanyamapori ni shilingi bilioni 13 kwa 2015/2016, lakini ukiangalia mwaka unaofuata estimate ni sifuri. Nimwombe Mheshimiwa Waziri na watalam wapitie ili waweke rekodi vizuri ili vitabu viweze kueleweka isije ikaonekana kwamba mwaka huu unapata shilingi bilioni 25 mwaka unaofuata unapata sifuri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia nichukue nafasi hii kuwapongeza kwa kazi ambayo wanaifanya najua kutangaza utalii ni kazi ngumu. Niseme jambo moja, nimesikiliza kwa makini hotuba ya wenzetu wa upinzani, hili suala la Loliondo limechukua muda mrefu na naomba niseme tusipoangalia, hatutapata ufumbuzi kwa sababu kuna wadau wengi wanaoshiriki kwenye changamoto ile lakini nzuri na mbaya zaidi kuna na hela nyingi pia. Sehemu yoyote ikishakuwa na hela nyingi zinazunguka, usipokuwa makini huwezi kupata ufumbuzi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukiangalia OBC inaongelewa sana lakini nyuma ya OBC kuna wadau wengine pia ambao na wao wanachochea mgogoro huu. Ukitumia nguvu nyingi kuzungumzia OBC ukasahau wengine kama Wamarekani na watu wengine, ndugu zangu ule mgogoro wa Loliondo utaendelea miaka mingi kwa sababu kuna hela zinazunguka na watu hela wanazihitaji na hakuna anayependa kusema kwamba kuna hela. Kwa hiyo, ule mgogoro tusipokuwa makini utaendelea miaka nenda miaka rudi, watakuja Mawaziri hapa, tutawawajibisha, tutasema Waziri hapa umechukua mlungura ondoka, tutafanya kile na kile lakini Loliondo itaendelea kuwa Loliondo miaka nenda, miaka rudi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nikiwa pale Brussels, ndani ya Bunge la Jumuiya ya Ulaya ilitolewa hoja nzito na Tanzania wakatuazimia pia, hoja ile ilikuwa inahusu land grabbing. Land grabbing ni hoja mpya na ya kisasa ambayo wanasema unamnyang’anya mtu ardhi unaenda kutumia kwa maslahi yako au kwa vitu vingine.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hoja ile ya land grabbing ilipokuja, Bunge la Jumuiya ya Ulaya likaiazimia, likaleta hoja, likasema Mheshimiwa Balozi jibu. Balozi kazi yako ya kwanza lazima utetee nchi yako, kwa hiyo, unapoambiwa jibu, majibu unayotakiwa kutoa ni yale ya kutetea nchi yako siyo jibu lingine. Nilipopitia zile hoja zilizotolewa ambazo ni nyingi sana kuzipitia kwa sababu hapa Tanzania tuna zaidi ya mashirika 70 yote yako Loliondo na kila shirika lina taarifa na kila shirika linaongelea kivyake kuhusu masuala ya land grabbing.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, tukiacha tatizo tunaloliona Loliondo ndiyo wanasema kuna Loliondo nyingine kubwa inatengenezwa na Bunge la Ulaya limeshapitisha azimio. Tusipojipanga sasa, siku azimio likirindima ndani ya Bunge hili, ndugu zangu hatutaweza kupata majibu, tutaanza kutafutana mchawi ni nani, ndiyo maana nasema mapema ili tujipange. Yale majibu niliyotoa nikiwa Balozi, ukiwa Balozi unazungumza kama Balozi, nikija humu siwezi kuzungumza kama Balozi, nitazungumza kama Mbunge na hiyo itakuwa lugha tofauti kabisa, ndiyo maana nawaombeni ndugu zangu…

(Hapa kengele ililia kuashiria kuisha kwa muda wa mzungumzaji)

MHE. BALOZI. DKT. DIODORUS B. KAMALA: Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja.