Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 – Wizara ya Maliasili na Utalii

Hon. Zuberi Mohamedi Kuchauka

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Liwale

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 – Wizara ya Maliasili na Utalii

MHE. ZUBERI M. KUCHAUKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi hii jioni ya leo nami nitoe mchango wangu katika Wizara ya Maliasili. Kwa imani yangu ni kwamba Mawaziri wa Wizara hii ni wasikivu, basi haya nitakayoyashauri hapa, pengine yakawa na tija kwao na kwa Taifa kwa ujumla. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nianze mchango wangu kwa kujielekeza kwenye Hifadhi ya Selous. Kama ambavyo alivyotangulia kusema mama yangu pale, kwamba asilimia 60 ya Selous iko Liwale. Nami nataka kuwapa historia ya Selous pengine Wabunge wenzetu hamuelewi hii ilikuwa kuwaje. Founder wa hii hifadhi ya Selous alikuwa ni Fedrick Selous mnamo mwaka 1879. Mwaka 1905 ndipo hili eneo la Selous likatengwa kama eneo la uwindaji. Siyo hivyo tu mwaka 1922 ndipo eneo hili likahifadhiwa kama game reserve. Mpaka mwaka 1982 UNESCO waliitambua hii kama Hifadhi ya Dunia, hiyo ni historia fupi ya Selous.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na sifa hizi zote zilizonazo Selous lakini lango la kuingilia Selous liko Morogoro. Kwa maana ya kwamba ukanda mzima ule wa Kusini kuanzia Rufiji mpaka Lindi hakuna lango la kuingilia Selous. Sasa wana Selous wale walioko Liwale ambao ndiyo
wahifadhi wa kwanza, mimi naamini kwamba wahifadhi wa kwanza wa hifadhi yoyote ile ni wale wanaozunguka hifadhi. Kwa hiyo, Wanaliwale au Wanalindi kwa ujumla wake ndiyo wahifadhi wa kwanza lakini hakuna lango la kuingilia Selous, kwa maana hiyo basi hakuna manufaa yoyote ambayo wanapata wale ya direct kwa watu waliopo pale Selous.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba Mheshimiwa Waziri hebu aiangalie Selous na aangalie Kusini, mpaka leo hii Kusini hatuna hoteli ya kitalii wala hata barabara ya kufika kwenye hii hifadhi hatuna. Kama mpaka hata Wazungu nao wenzetu wanaithamini kwa kiwango hicho tunawezaje kushindwa hata kuweka barabara ya kuifikia hiyo Selous? Hili ni jambo la kusikitisha sana hasa kwa watu wa Kusini tunaoizunguka hii Selous. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile nijielekeze sasa kwenye mamlaka ya Uvunaji wa Mali za Misitu (TFS). TFS ilivyoundwa na lengo lake na inavyofanya kazi, mimi kwa upande wangu naona ni kinyume chake. Katika Halmashauri ya Wilaya ya Liwale tuna misitu ya aina mbili, kuna msitu wa Nyera Kipelele huu msitu tumeurithi kutoka kwa wakoloni, kuna msitu wa Hangai, huu ni msitu wa vijiji. Msitu huu ni msitu ambao umechangiwa na vijiji kadhaa moja ya vijiji vichache ambavyo vimechangia msitu huu ni Kijiji cha Ngongowele, Mpigamiti, Mikunya, Lilombe, Kitogoro, Mtawango, Mtawatawa, Mitawa, Namakololo, Makirikiti na Kipule.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hawa wote wamechangia kuhifadhi hii misitu lakini kinachoshangaza kwenye Kamati ya uvunaji wa misitu hii, Mwenyekiti ni Mkuu wa Mkoa, Mwenyekiti wa Halmashauri hayumo kwenye Kamati ya Uvunaji, Mbunge wa Jimbo husika hayumo kwenye Kamati ya Uvunaji waliopo kwenye Kamati hii ni Mkuu wa Mkoa, Mkuu wa Wilaya, Mkurugenzi wa Halmashauri, OCD na watu wengine.

Mheshimiwa Mwenyekiti, misitu hii imehifadhiwa na wanavijiji nami kama mwakilishi wa wanavijiji simo kwenye Kamati ya Uvunaji, uvunaji huu unakwendaje? Namwomba sana Mheshimiwa Waziri hebu afikirie muundo wa hii Taasisi ya TFS na uvunaji wa TFS.

Mheshimiwa Mwenyekiti, siyo hivyo tu, kwenye TFS Halmashauri tunapata asilimia tano ya kile kinachovunwa pale Halmashauri. Naomba sana hata wakati nachangia kwenye hotuba ya Waziri Mkuu nilisema naomba Mheshimiwa Waziri turejeshe hapa hiyo sera ya uundwaji wa TFS ili tuongeze angalau tufike hata asilimia 20 ili tunaozungukwa na ile misitu tuweze kunufaika na ile misitu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti katika nafasi hiyo ya TFS, elimu kwa sababu kuna Kamati za Vijiji ndiyo wanashughulika na mambo ya uvunaji wa hii misitu, lakini wale wanavijiji hawajapata elimu yoyote na wala hakuna semina yoyote inayowafikia. Matokeo yake kinachofanyika sasa mtu anapata leseni, anaenda kuvuna cubic meter 100 na anakata mti akikuta huo mti una pango anauacha, ili uweze kukamilisha mzigo wake maana yake unaacha jangwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, wanavijiji wale wanasaidiwa vipi? Hakuna elimu yoyote wanayoipata kujua kwamba madhara yanayotokana na ile miti ambayo yule mwekezaji haitaki, ile miti anailipiaje, Halmashauri inapata nini? Matokeo yake Halmashauri tunapata jangwa tu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, msitu wa Nyera Kipelele ni msitu tumeurithi kutoka kwa wakoloni, mpaka leo hii harvesting plan ya msitu ule haijatoka. Nimekwenda pale nimepata kitabu cha mwongozo kinaitwa kitabu cha mwongozo wa uvunaji endelevu. Kitabu hicho kwenye Halmashauri kipo kimoja tu na nimekutajia vijiji zaidi ya 20 ambavyo vina hifadhi lakini kitabu cha mwongozo wa uvunaji endelevu kipo kimoja kwenye Halmashauri. Msitu wa Nyera Kipelele mpaka leo hauna harversting plan maana yake ni kwamba huu msitu haujaanza uvunaji, tumeurithi kutoka kwa wakoloni. Sasa hawa ambao wanazungukwa na huu msitu wananufaika na nini?

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya hapo naomba nijielekeze kwenye Mamlaka ya Usimamizi wa Wanyamapori (TAWA). Hii taasisi haina ushirikiano na Halmashauri zetu, kwa sababu leo hii wanasema asilimia 25 ya mapato ya uwindaji wa kitalii yanaenda kwenye Halmashauri, huu ni mwaka wa tatu, mwaka wa nne, kila tukifungua kwenye Halmashauri pale kwenye mapato yetu haimo, hili pato haliingi. Nimefuatilia mpaka TAWA, nikawauliza kwanza nilitaka nijue hii asilimia 25 ni ya nini? Sijapata majibu mpaka leo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kama hawa watu wa TAWA hawawezi kutoa ushirikiano, tena nilienda pale wakaniambia kwamba hii sisi siyo Wasemaji wa TAWA nenda kwa Katibu Mkuu. Nimefika kwa Katibu Mkuu wa Wizara sijapata majibu mpaka leo. Tunapata asilimia 25, asilimia 25 ya nini?(Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile katika mambo ya utalii; utalii kwenye Halmashauri ya Liwale kuna boma la Mjerumani nilishalisema hapa, lile boma la Mjerumani ni moja ya kivutio cha utalii. Kwa sababu kumbukumbu yote ya vita ya Maji Maji ukitaka kuongelea leo lazima utalikumbuka lile jengo la vita ya Maji Maji. Vilevile tuna kivutio cha utalii kwenye kaburi la Mfaransa, watalii wanakuja kutoka Ujerumani wanakuja kuangalia pale, kila mwaka wanakuja kuhiji, lakini sisi wenyewe tumelala. Kuna kaburi la Bimkubwa wangu mmoja pale Ndapata, watu wanakwenda kuhiji pale lakini sisi wenyewe tumelala hivi vyote ni vivutio.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hivi Tanzania tupewe nini na Mwenyezi Mungu ili tuone kwamba tuko duniani. Kama watu wa nje wanaweza kutambua vivutio vyetu vya utalii sisi wenyewe tusivitambue. Mheshimiwa Waziri, najua ni msikivu najua hili ninalolisema atalisikia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwisho kabisa naomba niongelee mgogoro wa Hifadhi ya Selous na Kijiji cha Kikulyungu. Mgogoro huu sasa hivi una zaidi ya miaka 10 na umeshapoteza maisha ya watu wanne, namwomba Mheshimiwa Waziri afanye analoliweza, afike Kikulyungu atumalizie huu mgogoro kati yetu na wahifadhi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nijielekeze sasa katika mchango wa maendeleo unaotokana na hifadhi ya misitu. Mchango wa maendeleo pale kwetu wanasema kwamba ubao mmoja wana utoza sh. 400 kwenye Halmashauri ya Kijiji, gogo moja sh. 1000, hebu fikiria msitu ule unaohamishwa pale, sisi tunaambulia sh. 400! Kwa kweli Mheshimiwa Waziri hizi sheria tunaomba...

(Hapa kengele ililia kuashiria kuisha kwa muda wa mzungumzaji)

MWENYEKITI: Ahsante.