Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 – Wizara ya Maliasili na Utalii

Hon. Nape Moses Nnauye

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mtama

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 – Wizara ya Maliasili na Utalii

MHE. NAPE M. NNAUYE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi na mimi nichangie na nianze kwa kupongeza kazi nzuri inayofanywa na Serikali ya Awamu ya Tano hasa katika eneo hili la maliasili na utalii, ziko juhudi kadhaa zimefanyika na kwa kweli zinaonekana kwamba zinaweza kuzaa matunda mazuri. Ninaamini kwamba yako mambo yakiboreshwa tutapata matokeo mazuri zaidi, na nimefurahi leo nimemsikia rafiki yangu Musukuma akichangia hapa kwa ukali kidogo na nadhani ukali ule alioutumia ndio ukali tulikuwa tukiutumia hapa kuchangia kwenye maji na maeneo mengine na bahati mbaya wakati mwingine ukichangia kwa kueleza hisia za wapigakura wako unaonekana kama unashambulia Serikali hivi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini hapa tupo kuboresha, kinacholetwa hapa kinaletwa mapendekezo ya Serikali, tunapochangia lengo ni kuboresha ili tutoke na kitu kizuri zaidi kwa faida ya Watanzania, bila kujali mitazamo mbalimbali iliyoko hapa ndani. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, la kwanza ni suala hili la migogoro ya hifadhi na wananchi wanaozunguka maeneo hayo. Hili limekuwa tatizo la muda mrefu sana na limekuwa likizungumzwa sana na kunaonyeshwa nia ya Serikali ya kulimaliza, lakini likiendelea kutolea kwa ahadi kama ambavyo limekuwa likitolewa halitakwisha.

Ushauri wangu Mheshimiwa Waziri hebu njooni na time frame ya kushughulika na tatizo hili kwa sababu liko mahali kwingi na limeumiza watu sana. Na ukisoma kwenye hotuba humu wanazungumza habari ya kuweka zile beacons, mimi nadhani badala ya kuendelea na utaratibu huo na kwa sababu hifadhi nyingi hizi ziliwekwa miaka ya 1974 wakati population yetu ilikuwa ndogo sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukienda leo ene la Mkoa kama Tabora karibu eneo zima ni hifadhi, watu wameongezeka sana, sasa mkiendelea kuweka mipaka kwa kufuata uamuzi huo huo wa mwaka 1974 nadhani tutakuwa hatutendi haki kwenye jambo hili. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo ushauri wangu mimi nilidhani sitisheni utaratibu wa kuweka mipaka fanyeni tathimini kama kweli bado tunahitaji kutunza eneo kubwa kiasi hicho katika mazingira ambayo population imeongezeka sana, halafu tukishafikia uamuzi ndio tuweke mipaka ambayo itatupeleka kwa miaka mingine mingi zaidi mbele na katika hili pamoja na time frame mmekuwa mnaweka utaratibu wa task forces mbalimbali za kushughulikia matatizo kama haya. Mimi nilidhani katika hili kama nia ya dhati ya Serikali ni kulimaliza kwanza tuweke time frame lakini tutengeneze task force ipewe muda maalumu iende ikalimalize tatizo hili.

Mheshimiwa Mwenyekiti, la pili ni suala la biashara la kusafirisha viumbe hai. Kwenye hotuba ya Mheshimiwa Waziri ambaye nakiri anafanya kazi nzuri amesema wazi kwamba walisitisha biashara hii kwa miaka mitatu. Naanakiri kwamba baada ya kusitisha imefanyika tathimini kwenye mazizi ya wale ambao walishakusanya hawa viumbe hai na mwishoni anazungumza kwamba tathimini hiyo lengo lake ni kutoa kifuta jasho kwa wafanyabiashara walioathirika na katazo hilo. Sasa kwanza kitendo cha Serikali kukiri kwamba wamefanya tathimini na wana nia ya kutoa kifuta jasho maana yake ni kukiri kwamba yako makosa katika uamauzi huu, ambao mimi nadhani ni jambo la kiungwana kwamba kuna watu wameathirika hawakustahili kuathirika lakini wameathirika na uamuzi huo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa ushauri wangu mimi nilidhani la kwanza hawa watu wasisubiri hiyo miaka mitatu iishe, Serikali iruhusu hawa watu wasafirishe viumbe hai hawa ambao walishawakamata na waliwakamata wakawaweka kwenye mazizi yao kwa kufuata utaratibu, wamepata lesini, wamelipia kodi na wengine wamechukua mikopo kwenye mabenki na wengine walishalipwa pesa za utangulizi kabla ya kupeleka hawa viumbe kule nje. Kwa hiyo, mimi nilidhani badala ya kuzungumza habari ya kivuta jasho hapa izungumzwe habari ya fidia. Kwa sababu hawa watu wamepata hasara kutokana na uamuzi huu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini la pili uamuzi huu utenguliwe na Mheshimiwa Waziri mimi niko tayari kukamata shilingi yako leo hapa utengue huu uamuzi, hawa watu ambao kwa kweli hawakustahili kuadhibiwa nilikuwa naangalia zinapokiukwa sheria, kulikuwa na matatizo hapa katika uwindaji, kuna baadhi ya makampuni yalikiuka sheria hatukuwaadhibu wote walioshughulika na uwindaji, tuliwaadhibu wale waliokiuka sheria. Kwa hiyo, hata katika hili mimi sikuona sababu ya kuwaadhibu wote waliokuwa wanafanya biashara hii. Kwa hiyo, ushauri wangu ni kwamba walioathirika wapate fidia, lakini uamuzi huu sasa ufutwe na waruhusiwe kupeleka wanyama wao. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa sababu Mheshimiwa Waziri kwanza tumepoteza masoko, tumepoteza imani ya wale ambao walikuwa wanaamini kwamba biashara hii ingeendelea lakini kwa takwimu inaonekana hata wanyama wanaopelekwa ni kidogo sana, lakini mwisho wa yote Mheshimiwa Waziri nyuma ya jambo hili kuna harufu ya rushwa. Pengine inawezekana wasaidizi wako hawakwambii lakini kunahalufu ya rushwa na inazungumzwa wazi wazi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo la kwanza nilidhani uamuzi huu tusizungumze habari ya kifuta jasho, tuzungumze habari ya kufidia, la pili, tusiendelee na uamuzi huu hasa kwa wale ambao kwa kweli hatuna shida nao wale ambao tayari walishakamata wanyama, wamekopa mikopo, wanawafanyakazi wao, lakini walishachukua advance payment za kusafirisha hawa viumbe kuwapeleka nje. Tubadilishe kwenye hili na tukifanya hivi tutakuwa tumewaokoa na kwa sababu sheria ilishabadilishwa biashara hii ifanywa na wazawa. Kuna mikono ya wageni, lakini biashara hii inafanywa na wazawa, mimi nilidhani tuisimamie na tuwasaidie Watanzania hawa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lingine nchi yetu ina utajiri mkubwa wa utamaduni tuna makabila karibu 126 mimi nadhani umefika wakati sasa kwa kushirikiana na Wizara ya Utamaduni tuende tukawekeze kwenye utalii wa utamaduni wetu. Na mimi nadhani tukiwekeza huko tutapata faida kubwa, huu utamaduni usipowekezwa kitalii ukaanza kutuingizia pesa utaanza kupotea taratibu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nenda kaangalie leo tamaduni kama za Wamasai, Wamakonde, Wasukuma, Waha ni tamaduni ambazo zinaweza kuvutia utalii na uwekezaji wake sio mkubwa sana, uwekezaji wake mdogo sana ni kuutengeneza tu utamaduni ule ukae katika mazingira ambayo mtu akija anaweza akajifunza, anaweza akafanya utalii wake na wapo ambao watafanya tafiti mbalimbali katika utamaduni wetu. (Makofi)

Sasa mimi nazani tukiwaachia Wizara ya Utamaduni peke yake hawataweza, lakini sisi Wizara ya Maliasili na Utalii tunaweza tukawekeza katika utajiri huo wa utamaduni ambao tunao wenzetu wakaja wakajifunza. Mimi nimekwenda Bujora pale, pana mkusanyiko wa utamaduni mkubwa sana wa Wasukuma, lakini nenda Kusini Wayao, Wamakonde...

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa mzungumzaji)

MHE. NAPE M. NNAUYE: Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja.