Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 – Wizara ya Maliasili na Utalii

Hon. Constantine John Kanyasu

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Geita Mjini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 – Wizara ya Maliasili na Utalii

MHE. CONSTANTINE J. KANYASU: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana na kwa sababu ya muda naomba nizungumze mambo machache tu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la kwanza, Mheshimiwa Waziri anafahamu kwamba Geita Mjini tulipopata bahati ya kuwa Makao Makuu ya Mkoa wa Geita karibu nusu ya eneo la upande wa Mashariki miaka ya 1954 lilikuwa declared kwamba ni hifadhi, hakuna msitu wowote kuna bushes. Nilimwandikia barua na kumuomba kwamba wananchi wa Geita ule mkoa hauwezi kutanuka kuelekea Kaskazini wala kuelekea Magharibi kwa sababu ni eneo ambalo limepewa mgodi, eneo pekee la kutanuka ni kuelekea Kusini, na Mkoa kupitia RCC wameomba katika vikao tangu mwaka 2012 kuomba eneo la Msitu wa Usindakwe na eneo ambalo lilikuwa Msitu wa Geita (Usindakwe) liwe eneo ambalo Mkoa uruhusiwe kutoa maeneo ya makazi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hivi ninavyozungumza karibu nusu ya Mji wa Geita ni eneo ambalo zamani lilikuwa declared kwamba ni hifadhi, sasa nilikuomba Mheshimiwa Waziri kwa maandishi lakini sasa ni karibu miezi sita naomba leo uniambie ni hatua gani zimefikiwa? Sababu moja ni kwamba mpaka leo watu wa TFS wanazunguka, wanaweka alama kwenye nyumba, wana-disturb watu, lakini hakuna mti, hakuna chochote. Katika maeneo ya Nyakabale na Mgusu wananchi katikati ya kijiji kuna vigingi na katikati ya eneo la vijiji hivyo tayari mgodi umepewa eneo hilo, hivyo, wanashindwa kufanya chochote kwa sababu eneo hilo linaonekana kama ni hifadhi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la pili ni TFS katika Mkoa wa Geita, limetoka tangazo kupitia kwa Waziri kwamba ni marufuku kutumia pikipiki, baiskeli kubeba mkaa wala kubeba chochote. Vijiji vyetu vyote ambako wananchi wanakaa hakuna magari, hakuna chochote, kwa hiyo matokeo yake watu wa TFS wamerundika pikipiki na baiskeli Makao Makuu ya Ofisi zao na wanategemea kuzipiga mnada. Baiskeli ambayo imenunuliwa shilingi 150,000 inauzwa shilingi 10,000.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Waziri jambo hili ni uonevu mkubwa kwa sababu wananchi katika maeneo hayo ya vijiji hawana usafiri mwingine wowote mbadala zaidi ya baiskeli. Sasa sheria inaposema kwamba ni lazima tutumie magari, kusafirisha mkaa, hivi wananchi kwenye vijiji wanapata wapi magari? Kwa sababu inavyonekana ni kama mkakati wa kuwadhulumu wananchi baiskeli zao, ananunua mtu baiskeli, anakamatwa anakimbizwa porini ananyanganywa na sasa hivi watu wa TFS wanakwenda kwenye masoko kusubiria watu. (Makofi)
Mimi nafikiri TFS wamesahau core function yao. Core function yao ni kulinda misitu, wanachokifanya sasa siyo kulinda misitu tena, ni kusubiri barabarani waendasha baiskeli na pikipiki. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hebu tuambie na tangaza leo hawa wananchi wanatumia nishati gani? Tuambie tu mimi niko tayari kuwaambia wananchi sasa acheni, ni nishati gani mbadala ambayo Wizara yako imeandaa kwamba sasa hii ndiyo itakuwa nishati mbadala? Kinachoendelea sasa hivi na kwa wananchi ni kwamba wananchi wanalazimishwa sasa waanze kulala njaa kwa sababu mkaa unakamatwa sokoni, unakamatwa barabarani, anakamatwa mwenye baiskeli, pikipiki, gari haijulikani utaratibu huu sasa unatupeleka wapi.

Mheshimiwa Waziri inawezekana wewe huna taarifa, nguvu inayotumika kwenye suala hili kule kwenye maeneo ya wananchi ni kubwa kuliko hata thamani ya kitu kinachoenda kuzuiwa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninataka nikushauri Mheshimiwa Waziri, kwa nini unapata tatizo kubwa sana la kulinda misitu yako, unapata shida ya kulinda hifadhi? Kwa sababu ya mahusiano mabaya sana ya TFS na vijiji. Watu wa samaki walibuni kitu kinaitwa Beach Management Unit (BMU) kwa sababu wananchi wanatakiwa wajisimamie wenyewe. Ninyi mnatumia nguvu kubwa, amesema Mheshimiwa Mbunge asubuhi…

(Hapa kengele ililia kuashiria kuisha kwa muda wa mzungumzaji)

MWENYEKITI: Ahsante.