Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 – Wizara ya Maliasili na Utalii

Hon. Janet Zebedayo Mbene

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Ileje

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 – Wizara ya Maliasili na Utalii

MHE. JANET Z. MBENE: Mheshimiwa Mwenyekiti, ninashukuru kwa kunipa fursa ya kuchangia kwenye hotuba hii muhimu. Ninamshukuru Mungu kwa fursa ya kuwa katika Bunge hili Tukufu. Ninawapongeza Mheshimiwa Waziri Profesa Jumanne Maghembe na Naibu Waziri wake Engineer Ramo Makani na watendaji wa Wizara hii.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninaomba kuchangia kwenye maeneo machache nikianza na hati za kumiliki misitu. Ninaomba kwa Wilaya na Mikoa yenye misitu mingi ya asili na ya kibiashara watu wakatiwe vitalu vya misitu kama watu wanavyopata hati za ardhi ili wawekeze kwenye upandaji miti na watumie hati hizo za vitalu vya miti kukopa kwa ajili ya kuendeleza misitu, ufugaji nyuki na viwanda vidogo vya mbao na samani za ujenzi na za taasisi na za majumbani.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kuishauri Serikali kuzidisha juhudi na mikakati ya kulinda antiques za nchi hii hususani za kitamaduni zilizopo vijijini ambazo huondolewa kwa sababu ya umaskini na kutokuwa na uelewa. Wanachi wengi wamekuwa wakirubuniwa na wageni wanosaidiwa na wajanja wachache kuwashawishi kuuza antiques hizo za kihistoria za makabila na jamii mbalimbali. Kwa mfano kulinda antiques za fimbo, vigoda, mavazi ya machifu na viongozi mbalimbali wa kimila, samani, vyombo vilivyotumika kulima, kusaga nafaka, kuhifadhi chakula, kuwinda na uhunzi. Mavazi ya sherehe mbalimbali vyote vinapotea na kupoteza historia muhimu ya Taifa letu na jamii mbalimbali. Serikali ilitupie macho na kuweka mikakati ya kuzilinda na kuzihifadhi na kuziwekea kumbukumbu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukataji wa miti kwa matumizi ya mkaa umeongezeka sana hasa maeneo yenye ukame ambako misitu ni michache, na wakati huo huo matumizi ya gesi na umeme pamoja na majiko sanifu vimeongezeka. Ninaitaka Serikali kutoa takwimu za gharama ya kukata miti kwa kila gunia la mkaa na uharibifu wa mazingira. Tulinganishe uharibifu huu na gharama ya mbadala kama matumizi ya gesi, majiko sanifu na umeme tutaona jinsi gani matumizi mbadala ya nishati ni nafuu huko tunakoelekea. Gharama ya gesi ukishanunua mtungi ni rahisi kuliko mkaa. Kwa wastani mkaa unauzwa kwa familia ya kawaida ni gunia nne kwa mwezi 70,000 x 4 = 280,000/=; lakini gesi kwa mwezi ni mitungi miwili ya shilingi 90,000/= ukiongeza gharama ya mtungi 100,000 ni 190,000/=; ni dhahiri gesi ni nafuu. Kuhusu mkaa tutoe ulinganisho mkaa na gesi na tuwaelimishe wananchi gesi ni bora.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunaitaka Serikali itafute njia ya kutoa elimu kwa mapana yake ili matumizi ya mkaa yaachwe kidogo kidogo. Serikali ianze kuwatoza wote wanaokata miti kwa mkaa wa kuuzwa ili walipie gharama ya kupanda miti hii, tusilionee haya hili, tutajuta baadae.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwisho naomba kutoa ushauri kwa Serikali juu ya utalii wa fukwe. Utalii huu ni mojawapo ya eneo linalovutia sana watalii nchini na kwa hali hiyo kuna haja ya kuwekeza kwa kiwango kikubwa kwenye vivutio vya utalii wa fukwe.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tuna changamoto kubwa ya upungufu wa mahoteli ya kutosha kwa ajili ya watalii wanotaka kuja Tanzania. Nataka kupendekeza kuwa Serikali iboreshe mazingira ya uwekezaji kwenye ujenzi wa hoteli nyingi kwenye fukwe zetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali itoe msamaha wa ushuru wa vifaa vyote vya ujenzi wakati wa ujenzi wa hoteli hizi ili kwa miaka miwii au mitatu wawekezaji wajenge hoteli za viwango vya kimataifa na baada ya hapo tozo na kodi zote zihusike. Hii imefanyika Zambia na Mozambique na imewezesha utalii kukua sana. Wizara hii itumie wataalam kufanya benefit cost analysis ya wazo hili na nina hakika wataona kuwa kodi na ushuru tunaokosa sasa kutafidiwa kwenye mapato mengi ya utalii baadae. Wawekezaji wa ndani watahitaji kuwekeza. Serikali ipime maeneo kwenye ufukwe wa Bahari ya Hindi kuanzia Tanga hadi Mtwara.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ipo dhana kuwa makaa ya mawe yanaweza kuwa mbadala wa mkaa wa miti, naomba Serikali ifahamishe wanachi juu ya hili. Makaa ya mawe yanahitaji majiko na tanuru maalum kabla ya kutumia kwa hiyo haitakuwa automatic.

Mheshimiwa Mwenyekiti, maeneo yetu mengi hasa ya pembezoni kama Songwe na Ileje yana misitu, mabonde, mito mingi inayofaa kwa utalii wa utamaduni, wa kupiga picha na wa camp sites na kupanda milima. Lakini hatuna wataalam kabisa wa kuendeleza hayo. Tunaiomba Serikali itufikirie. Naunga mkono hoja.