Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 – Wizara ya Maliasili na Utalii

Hon. Omary Tebweta Mgumba

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Morogoro Kusini Mashariki

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 – Wizara ya Maliasili na Utalii

MHE. OMARY T. MGUMBA Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa kupata nafasi hii ya kutoa mchango wangu katika Wizara ya Maliasili na Utalii.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nichukue nafasi hii kuwapongeza Mheshimiwa Rais Dkt. John Joseph Pombe Magufuli kwa uamuzi wake wa kununua ndege na kuimarisha Shirika letu la Ndege ili kuinua utalii wa ndani na nje kwa ujumla.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia nampongeza Mheshimiwa Waziri, Naibu Waziri na timu nzima ya wataalam kwa wasilisho zuri la hotuba yao ya uchapaji kazi wao katika Wizara hii. Baada ya utangulizi huo, naomba kutoa mchango na ushauri wangu kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu zuio la mkaa; zaidi ya asilimia 90 ya Watanzania wanategemea matumizi ya mkaa na kuni katika maisha yao ya kila siku, kwa mfano vijijini. Kwa kuwa nishati mbadala mpaka sasa haijasambaa nchi nzima hasa kwa maeneo ya vijijini katika Jimbo langu la Morogoro Kusini Mashariki ambako zaidi ya asilimia 70 ya vijiji umeme haujafika na hata gesi hakuna na wananchi hutegemea kuni na mkaa kama nishati ya kupikia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia ni kwa kuwa wananchi wengi vipato vyao ni vidogo kumudu gharama ya umeme ukizingatia umeme wenyewe ni mdogo ambao haukidhi mahitaji ya nchi na kwamba anayetumia zaidi analipa zaidi na gharama kubwa sana ambazo wananchi hawawezi kumudu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kushauri Serikali kusitisha zoezi la katazo la matumizi ya mkaa kusafirisha sehemu moja kwenda nyingine mpaka pale Serikali itakapokuwa na uwezo wa kuzalisha na kusambaza nishati mbadala nchi nzima kwa wananchi na pia kupata maandalizi ya kutosha katika kutoa elimu kwa wananchi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la pili ni kuhusu ahadi ya Serikali ya kutupatia ardhi ya kulima kutoka katika msitu wa Mkulazi ulio karibu na Kijiji kipya Bwila Juu walikohamia watu waliopisha ujenzi wa bwawa la Kidunda. Watu waliopisha ujenzi wa bwawa kutoka Kidunda Kitongoji cha Manyanyu na vingine walikuwa na nyumba zao pamoja na mashamba katika maeneo hayo kama ilivyo kawaida sehemu za vijijini. Lakini Serikali aliwapa wananchi hawa katika eneo jipya viwanja tu vya kujenga nyumba bila ardhi ya kilimo ili kujitegemea kiuchumi kama eneo la awali lilivyo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kuzingatia changamoto hiyo na umuhimu wa kilimo na uchumi wa wananchi hao, Serikali kupitia Mkuu wa Mkoa wa Morogoro Dkt. Rajabu Lutengwe ilisema itawapa wananchi hawa ardhi yenye ukubwa wa ekari 50,000 iliyo karibu na vijiji vipya ili wananchi waweze kuhamia pale na kuendeleza shughuli zao za kilimo na kiuchumi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba Serikali kutimiza ahadi hii haraka ili wananchi waweze kuendeleza shughuli za kiuchumi na kuepuka mambo kama yale yaliyotokea mwaka 1973 katika operation vijiji. Ni lini Serikali itatoa ardhi hii kwa wananchi?

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la tatu ni mamba katika Mto Ruvu. Wakati wa kiangazi tunapata maafa mengi hasa katika Kata ya Tunanguo kutokana na mauaji yanayosababishwa na mamba wanaotoka katika Mto Ruvu. Ombi langu kwa Serikali, kwanza kuvuna mamba hawa kutoka Mto Ruvu kwa sababu wamekuwa wengi na pili kulipa fidia na matibabu kwa wananchi walioathirika na mamba. Pia Serikali kulipa wananchi wangu walioathirika na tembo miaka saba iliyopita katika kata ya Kidugala, Ngerengere, Mkulazi na Matuti.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja.